Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msifu Yehova ‘Katikati ya Kutaniko’

Msifu Yehova ‘Katikati ya Kutaniko’

Msifu Yehova ‘Katikati ya Kutaniko’

MIKUTANO ya Kikristo ni mpango wa Yehova wa kuwasaidia watu wake waendelee kuwa na nguvu kiroho. Tunapohudhuria mikutano kwa ukawaida, tunaonyesha kwamba tunathamini mipango hiyo ya Yehova. Zaidi ya hayo, mikutano hutuwezesha ‘kuwachochea ndugu zetu kwenye upendo na kazi zilizo bora,’ ambako ni njia muhimu ya kuonyeshana upendo. (Waebrania 10:24; Yohana 13:35) Hata hivyo, tunaweza kuwachocheaje ndugu zetu kwenye mikutano?

Tangaza Hadharani

Mfalme Daudi aliandika hivi kujihusu: “Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu, katikati ya kusanyiko [“kutaniko,” NW] nitakusifu. Kwako zinatoka sifa zangu katika kusanyiko [“kutaniko,” NW] kubwa.” “Nitakushukuru katika kusanyiko [“kutaniko,” NW] kubwa; nitakusifu kati ya watu wengi.” “Nimehubiri habari za haki katika kusanyiko [“kutaniko,” NW] kubwa. Sikuizuia midomo yangu.”—Zaburi 22:22, 25; 35:18; 40:9.

Katika siku za mtume Paulo, Wakristo walipokusanyika kwa ajili ya ibada, wao pia walitangaza kuhusu imani yao katika Yehova na kuhusu utukufu wake. Kwa njia hiyo, walitiana moyo na kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora. Katika siku zetu, karne nyingi baada ya Daudi na Paulo, sisi kwa kweli ‘tunaiona siku ya Yehova ikikaribia.’ (Waebrania 10:24, 25) Mfumo wa mambo wa Shetani unayumba-yumba kuelekea uharibifu, na matatizo yanazidi kuongezeka. ‘Tunahitaji uvumilivu’ sasa, kuliko wakati mwingine wowote. (Waebrania 10:36) Ni nani atakayetutia moyo tuvumilie ikiwa si ndugu zetu?

Leo, kama vile ilivyokuwa nyakati za kale, mipango hufanywa ili waamini mmoja-mmoja watangaze imani yao “katikati ya kutaniko.” Wote wana nafasi ya kutoa maelezo wanapojibu maswali ambayo wasikilizaji huulizwa katika mikutano ya kutaniko. Usipuuze kamwe manufaa ya kutoa maelezo kwenye mikutano. Kwa mfano, maelezo yanayoonyesha jinsi ya kushinda au kuepuka matatizo huimarisha azimio la ndugu zetu la kufuata kanuni za Biblia. Ndugu wanapotoa maelezo kuhusu maandiko ya Biblia ambayo hayajanukuliwa, au wanapotaja habari ambayo wamejifunza kutokana na utafiti wao, wanaweza kuwatia moyo wengine wasitawishe mazoea mazuri ya kujifunza.

Kujua kwamba sisi na wengine hunufaika tunapotoa maelezo kwenye mikutano kunapaswa kuwachochea Mashahidi wote wa Yehova washinde woga. Ni muhimu hasa kwa wazee na watumishi wa huduma kutoa maelezo kwenye mikutano kwa sababu wanapaswa kuwa mfano mzuri katika kutoa maelezo na kuhudhuria mikutano. Hata hivyo, mtu anawezaje kufanya maendeleo anapoona ni vigumu kushiriki katika utendaji huu wa Kikristo?

Madokezo ya Jinsi ya Kufanya Maendeleo

Kumbuka kwamba Yehova anahusika. Dada mmoja Mkristo anayeishi Ujerumani anaeleza maoni yake kuhusu kutoa maelezo. “Mimi huona maelezo yangu kuwa jibu langu kwa Shetani ambaye hujaribu kuwazuia watu wa Mungu wasitangaze imani yao.” Ndugu mmoja wa kutaniko hilohilo aliyebatizwa hivi karibuni anasema: “Mimi husali sana ninapotaka kutoa maelezo.”

Jitayarishe vizuri. Usipojifunza mapema habari itakayozungumziwa, utaona vigumu kutoa maelezo, na maelezo yako hayatakuwa na matokeo sana. Madokezo ya jinsi ya kutoa maelezo kwenye mikutano ya kutaniko yanapatikana katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 70. *

Weka mradi wa kutoa maelezo angalau mara moja kwenye kila mkutano. Hii inamaanisha kwamba tutayarishe majibu kadhaa, kwa kuwa kuna uwezekano mkubwa kwa ndugu anayeongoza kutuita tunapoinua mkono mara nyingi. Hata unaweza kumweleza mapema maswali ambayo umejitayarisha kujibu. Kufanya hivyo kutafaa hasa ikiwa wewe ni mpya. Kwa kuwa huenda ukasita kuinua mkono “katika kutaniko kubwa,” utatiwa moyo kutoa maelezo unapojua kwamba umejitayarisha kujibu fungu hilo na kwamba ndugu anayeongoza mkutano atakuwa akitafuta mkono wako.

Toa maelezo katika mafungu ya kwanza-kwanza. Kazi ngumu haiwi rahisi kwa kuiahirisha. Kutoa maelezo katika mafungu ya kwanza-kwanza kutakusaidia. Unaposhinda kizuizi cha kwanza, utaona jinsi ilivyo rahisi kutoa maelezo mara ya pili au ya tatu.

Chagua kuketi mahali panapofaa. Wengine huona ni rahisi kutoa maelezo wanapoketi kwenye viti vya mbele vya Jumba la Ufalme. Sehemu hiyo haina vikengeusha-fikira vingi na mwenye kuongoza anaweza kuwaona kwa urahisi. Ukiketi kwenye viti hivyo, kumbuka kuzungumza kwa sauti kubwa ili wote wasikie, hasa ikiwa kutaniko halina vikuza-sauti kwa ajili ya wasikilizaji.

Sikiliza kwa makini. Kufanya hivyo kutakusaidia uepuke kurudia jambo ambalo limesemwa na mtu mwingine. Pia, huenda maelezo yanayotolewa na wengine yakakukumbusha andiko au jambo fulani ambalo unaweza kuongezea kwa yale ambayo yamesemwa. Pindi kwa pindi, jambo fupi lililoonwa linaweza kufafanua habari inayozungumziwa. Maelezo hayo yanafaa sana.

Jifunze kujibu kwa maneno yako mwenyewe. Kusoma maelezo kutoka katika kichapo kunaweza kuonyesha kwamba umepata jibu sahihi na ni njia nzuri ya kuanza kutoa maelezo. Lakini unapofanya maendeleo na kujibu kwa maneno yako mwenyewe unaonyesha kwamba umeelewa habari hiyo. Si lazima unukuu vichapo vyetu neno kwa neno. Mashahidi wa Yehova hawarudii tu yale ambayo vichapo vyao husema.

Toa maelezo yanayohusiana na habari inayozungumziwa. Haifai kutoa maelezo yasiyohusiana na habari inayozungumziwa au yanayokengeusha watu kutoka kwenye mawazo makuu. Hii inamaanisha kwamba maelezo yako yanapaswa kuhusiana na habari inayozungumziwa. Ukitoa maelezo kama hayo, utafanya habari iwe yenye kujenga kiroho.

Lengo lako liwe kuwatia moyo wengine. Kwa kuwa sababu moja kuu ya kutoa maelezo ni kuwatia moyo wengine, tunapaswa kuepuka kusema mambo yanayoweza kuwavunja moyo. Pia, hatupaswi kujibu kila jambo kwenye fungu bila kuwaachia wengine jambo la kusema. Majibu marefu na yenye kutatanisha yanaweza kuficha maana. Majibu mafupi yenye maneno machache yanaweza kuwa na matokeo sana, na yatawatia moyo wapya kutoa maelezo yao mafupi.

Daraka la Wale Wanaoongoza Mikutano

Ndugu anayeongoza mikutano ana daraka kubwa la kuwatia moyo wengine. Yeye huonyesha kwamba anapendezwa kikweli na maelezo yote yanayotolewa kwa kusikiliza kwa makini na kumwangalia yule anayetoa maelezo badala ya kujishughulisha na mambo mengine. Haingefaa hata kidogo ikiwa angerudia yale ambayo yamesemwa au kuuliza swali ambalo tayari limejibiwa kwa sababu hakuwa akisikiliza kwa makini!

Pia lingekuwa jambo la kuvunja moyo ikiwa mara kwa mara anayeongoza angerudia maelezo yaliyotolewa kwa maneno yake mwenyewe kana kwamba maelezo hayo hayakutosha. Kwa upande mwingine, ni jambo lenye kutia moyo wakati maelezo yanapoendeleza jambo kuu linalozungumziwa. Maswali yafuatayo yanaweza kuwatia moyo wasikilizaji washiriki katika kutoa maelezo yenye kujenga: ‘Tunawezaje kutumia habari hii katika kutaniko letu?’ au, ‘Ni andiko gani katika fungu linalounga mkono maelezo ambayo yametolewa?’

Bila shaka, wapya au watu wenye haya wanapaswa kupongezwa hasa wanapotoa maelezo. Jambo hilo linaweza kufanywa faraghani baada ya funzo ili kuepuka kumwaibisha, na kumpa kiongozi nafasi ya kutoa madokezo inapofaa.

Katika mazungumzo ya kawaida, mtu ambaye hutawala mazungumzo huwavunja moyo wengine. Wasikilizaji wake watahisi kwamba hakuna haja ya kujieleza. Wanalazimika kumsikiliza shingo upande. Jambo kama hilo linaweza kutokea ikiwa yule anayeongoza anatawala mazungumzo kwa kutoa maelezo mara nyingi. Hata hivyo, mara kwa mara, yule anayeongoza anaweza kuwachochea wahudhuriaji wafikirie habari inayozungumziwa na kutoa maelezo kwa kuuliza maswali ya ziada. Maswali hayo hayapaswi kuulizwa kila mara.

Si lazima yule anayeongoza amwite mtu wa kwanza kuinua mkono. Kufanya hivyo kunaweza kuwavunja moyo wale ambao wanahitaji muda ili kufikiria wanayotaka kusema. Kwa kungoja kidogo, atampa nafasi yule ambaye hajajibu kujibu. Pia ataonyesha busara kwa kutowachagua watoto wachanga wajibu maswali yanayohusu habari wasiyoweza kuelewa.

Namna gani mtu akitoa jibu ambalo si sahihi? Yule anayeongoza anapaswa kuepuka kumwaibisha mtu aliyetoa jibu hilo. Mara nyingi, hata kama jibu si sahihi lina ukweli fulani. Kwa kukazia kwa busara jambo ambalo huenda likawa sahihi, au kwa kuuliza swali kwa njia nyingine, au kwa kuuliza swali la ziada, mwenye kuongoza anaweza kusahihisha jibu pasipo kumwaibisha yeyote.

Ili kuwatia moyo wahudhuriaji watoe maelezo, yule anayeongoza mkutano anapaswa kuepuka kuuliza maswali ya ujumla kama vile, ‘Je, kuna mtu mwingine anayetaka kutoa maelezo?’ Huenda yule anayeongoza akawa na nia nzuri anapouliza, ‘Ni nani ambaye bado hajatoa maelezo? Hii ndiyo nafasi yako ya mwisho!’ lakini kufanya hivyo hakuwatii watu moyo kutoa maelezo. Ndugu hawapaswi kufanywa wahisi hatia kwa kuwa hawakutoa maelezo katika mafungu ya kwanza-kwanza wakati wa funzo. Badala yake, wanapaswa kutiwa moyo waeleze wanayojua kwa sababu kufanya hivyo ni wonyesho wa upendo. Zaidi ya hayo, yule anayeongoza anapomwita mtu atoe maelezo, haingefaa kusema, “Baada yake, tutasikia maelezo ya Ndugu Fulani, kisha Dada Fulani.” Yule anayeongoza anapaswa kwanza kusikiliza maelezo, kisha aamue ikiwa maelezo ya ziada yanahitajiwa.

Ni Pendeleo Kutoa Maelezo

Kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni jambo muhimu kiroho; ni pendeleo kutoa maelezo kwenye mikutano hiyo. Kadiri tunavyoshiriki kumsifu Yehova katika njia hii ya pekee “katikati ya kutaniko,” ndivyo tunavyofuata kielelezo cha Daudi na kutii shauri la Paulo. Tunapotoa maelezo kwenye mikutano, tunathibitisha kwamba tunawapenda ndugu zetu na kwamba sisi ni sehemu ya kutaniko kubwa la Yehova. Ungependa kuwa wapi pengine ‘unapoona siku ikikaribia’?—Waebrania 10:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ni muhimu kusikiliza na kutoa maelezo kwenye mikutano ya Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yule anayeongoza huonyesha kwamba anapendezwa kikweli na maelezo yote yanayotolewa