Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hutujali Sikuzote

Yehova Hutujali Sikuzote

Simulizi la Maisha

Yehova Hutujali Sikuzote

LIMESIMULIWA NA ENELESI MZANGA

Ilikuwa mwaka wa 1972. Vijana kumi, wanachama wa Chama cha Vijana cha Malawi, walivunja nyumba yetu na kuingia, wakanikamata na kunikokota hadi kwenye shamba la miwa lililokuwa karibu. Hapo, walinipiga na kuniacha karibu kufa.

Mashahidi wengi wa Yehova nchini Malawi walipatwa na mashambulio makali kama hili lililonipata. Kwa nini walinyanyaswa? Ni nini kilichowasaidia kuvumilia? Tafadhali acha nikusimulie kuhusu familia yangu.

NILIZALIWA Desemba 31, 1921, katika familia ya kidini. Baba yangu alikuwa mchungaji wa Kanisa la Kipresibiteri la Afrika ya Kati. Nililelewa huko Nkhoma, mji mdogo karibu na Lilongwe, jiji kuu la Malawi. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, niliolewa na Emmas Mzanga.

Siku moja, rafiki ya baba yangu, ambaye pia alikuwa mchungaji, alitutembelea. Alikuwa ameona kwamba Mashahidi wa Yehova waliishi karibu na nyumbani kwetu, naye akatuonya tusijihusishe nao. Alituambia kwamba Mashahidi walikuwa na roho waovu na tusipojihadhari, sisi pia tunaweza kupagawa na roho waovu. Onyo hilo lilitushtua sana hivi kwamba tulihamia kijiji kingine, ambapo Emmas alipata kazi ya kuuza dukani. Lakini punde si punde, tukagundua pia kwamba makao yetu mapya yalikuwa karibu na Mashahidi wa Yehova!

Hata hivyo, baada ya muda mfupi, Emmas ambaye aliipenda sana Biblia, alichochewa kusema na mmoja wa Mashahidi hao. Baada ya kupata majibu yenye kusadikisha kwa maswali yake mengi, Emmas alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi. Mwanzoni, funzo hilo la Biblia lilifanyiwa dukani alikofanya kazi, lakini baadaye funzo hilo la kila juma lilifanyiwa nyumbani mwetu. Kila mara Mashahidi wa Yehova walipokuja, niliondoka nyumbani kwa sababu niliwaogopa. Hata hivyo, Emmas aliendelea kujifunza Biblia. Baada ya kujifunza kwa miezi sita hivi, alibatizwa mnamo Aprili 1951. Ingawa hivyo, hakuniambia kuhusu jambo hilo kwa sababu aliogopa kwamba habari hizo zingevunja ndoa yetu.

Majuma Yenye Matatizo

Hata hivyo, siku moja, rafiki yangu Ellen Kadzalero aliniambia kwamba mume wangu alikuwa amebatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilijawa na hasira! Tangu siku hiyo na kuendelea, sikusema naye wala kumpikia chakula. Niliacha pia kuteka na kumchemshia maji ya kuoga, kazi ambayo kulingana na desturi yetu huonwa kuwa ni daraka la mke.

Baada ya kuvumilia kutendewa hivyo kwa majuma matatu, Emmas aliniomba kwa fadhili niketi, kisha akanieleza kwa nini aliamua kuwa Shahidi. Alisoma na kufafanua maandiko kadhaa kama vile 1 Wakorintho 9:16. Nilichochewa sana na nikahisi kwamba mimi pia ninahitaji kushiriki katika kuhubiri habari njema. Kwa hiyo, niliamua kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Jioni hiyohiyo nilimpikia mume wangu mpendwa chakula kitamu, naye akafurahi sana.

Nawahubiria Ukweli Watu wa Familia na Marafiki

Wazazi wetu waliposikia kwamba tunashirikiana na Mashahidi wa Yehova, walitupinga vikali. Familia yangu ilituandikia barua na kutuambia tusiwatembelee tena. Hatua hiyo ilitusikitisha sana, lakini tuliitumaini ahadi ya Yesu kwamba tungekuwa na ndugu, dada, baba, na mama wengi wa kiroho.—Mathayo 19:29.

Nilifanya maendeleo ya haraka katika kujifunza Biblia, nami nikabatizwa mnamo Agosti 1951, miezi mitatu na nusu tu baada ya mume wangu kubatizwa. Niliona nina wajibu wa kumhubiria ukweli rafiki yangu Ellen. Nilifurahi alipokubali funzo la Biblia. Ellen alibatizwa Mei 1952, akawa dada yangu wa kiroho, jambo ambalo liliimarisha urafiki wetu. Leo tungali marafiki wakubwa sana.

Katika mwaka wa 1954, Emmas alipewa mgawo wa kutembelea makutaniko akiwa mwangalizi wa mzunguko. Kufikia wakati huo, tayari tulikuwa na watoto sita. Siku hizo, mwangalizi asafiriye aliyekuwa na familia alitumia juma moja kutembelea kutaniko, kisha alikaa nyumbani pamoja na mke na watoto wake juma lililofuata. Hata hivyo, Emmas alipokuwa safarini, sikuzote alihakikisha kwamba niliongoza funzo la Biblia la familia yetu. Tulijaribu kufanya funzo pamoja na watoto wetu lifurahishe. Pia tulisema kwa usadikisho wa kutoka moyoni kuhusu upendo wetu kwa Yehova na kweli ya Neno lake, na tulishiriki katika kazi ya kuhubiri tukiwa familia. Mpango huo wa mazoezi ya kiroho uliimarisha imani ya watoto wetu, nao uliwatayarisha kwa ajili ya mnyanyaso uliokuwa karibu kutupata.

Mnyanyaso wa Kidini Waanza

Malawi ilikuwa taifa huru mwaka wa 1964. Maofisa wa chama kinachotawala walipojua msimamo wetu wa kutokuwamo kisiasa, walijaribu kutulazimisha tununue kadi za uanachama. * Kwa kuwa mimi na Emmas tulikataa kununua kadi hizo, wanachama wa Chama cha Vijana waliharibu shamba letu la mahindi ambayo yalikuwa tegemeo letu la chakula la mwaka uliofuata. Wanachama wa Chama hicho cha Vijana waliimba hivi wakikata mahindi hayo: “Wale wote wanaokataa kununua kadi ya Kamuzu [Rais Banda], mchwa watakula mahindi yao mabichi na watu hao watayalilia.” Ijapokuwa tulipoteza chakula chetu, hatukukata tamaa. Yehova alitujali. Alituimarisha kwa upendo.—Wafilipi 4:12, 13.

Usiku mmoja mnamo Agosti 1964, nilikuwa nyumbani mimi peke yangu na watoto. Tulikuwa tumelala, lakini niliamshwa na sauti za nyimbo zilizosikika kwa mbali. Zilikuwa sauti za Gulewamkulu, kikundi cha siri cha wacheza-dansi za kikabila walioogopewa sana, ambao waliwashambulia watu na kujifanya kuwa roho za mababu waliokufa. Chama cha Vijana kilikuwa kimewatuma Gulewamkulu watushambulie. Niliwaamsha watoto haraka, kisha tukakimbilia kichakani kabla washambuliaji hao kufika nyumbani kwetu.

Tukiwa mafichoni, tuliona nuru nyangavu. Gulewamkulu walikuwa wameiwasha moto nyumba yetu iliyokuwa imeezekwa kwa nyasi. Iliteketea kabisa pamoja na vitu vyetu vyote. Washambuliaji hao walipokuwa wakiondoka kwenye mabaki ya nyumba yetu yaliyokuwa bado yakiungua polepole, tuliwasikia wakisema, “Tumemwashia Shahidi yule moto mzuri wa kuota.” Tulimshukuru sana Yehova kwa kutusaidia kukimbilia usalama. Ni kweli kwamba waliharibu mali yetu, lakini hawakuharibu azimio letu la kumtumaini Yehova badala ya wanadamu.—Zaburi 118:8.

Baadaye tulisikia kwamba Gulewamkulu walikuwa wamezitendea familia nyingine tano za Mashahidi wa Yehova ukatili huohuo katika eneo letu. Tulifurahi na kushukuru sana wakati ndugu kutoka makutaniko jirani walipokuja kutusaidia. Walijenga upya nyumba zetu na kutupa chakula kwa majuma kadhaa.

Mnyanyaso Wazidi

Mnamo Septemba 1967, kulikuwa na kampeni ya kuwakusanya Mashahidi wote wa Yehova nchini. Ili kutukamata, wanachama wakatili na wajeuri wa Chama cha Vijana na wale wa Chama Chipukizi cha Malawi waliojihami kwa mapanga, waliwasaka Mashahidi nyumba kwa nyumba. Walipowapata, walijaribu kuwauzia kadi za chama cha kisiasa.

Walipofika nyumbani kwetu, walituuliza ikiwa tulikuwa na kadi ya chama. Nilijibu: “La, sijainunua. Sitainunua sasa, wala sitainunua wakati ujao.” Kisha wakanikamata mimi na mume wangu na kutupeleka kwenye kituo cha polisi, na hawakuturuhusu tubebe chochote. Watoto wetu wachanga walipotoka shuleni, hawakutupata, hivyo wakawa na wasiwasi sana. Jambo la kufurahisha ni kwamba Daniel, mwana wetu mkubwa, alifika nyumbani muda mfupi baadaye na kuelezwa na jirani yaliyotukia. Aliwachukua ndugu zake wachanga mara moja na kwenda kwenye kituo cha polisi. Walipofika kwenye kituo hicho, polisi walikuwa wakitutupa kwenye malori yao ili kutupeleka Lilongwe. Watoto wetu waliambatana nasi.

Jijini Lilongwe, tulifikishwa mbele ya mahakama bandia kwenye makao makuu ya polisi. Maofisa hao walituuliza, “Je, mtaendelea kuwa Mashahidi wa Yehova?” Tukajibu, “Ndiyo!” ingawa jibu hilo lilimaanisha kifungo cha miaka saba gerezani. Wale “waliosimamia” tengenezo walihukumiwa kifungo cha miaka 14.

Baada ya kukaa usiku mmoja bila kulala na bila chakula, polisi walitupeleka kwenye Gereza la Maula. Seli zilikuwa zimesongamana watu na hatukuweza kupata hata mahali pa kulala kwenye sakafu! Kulikuwa na ndoo moja tu iliyotumiwa kama choo katika kila seli iliyosongamana watu. Chakula kilikuwa kidogo na hakikupikwa vizuri. Baada ya majuma mawili, maofisa wa gereza walitambua kwamba sisi ni watu wenye amani, hivyo walituruhusu tutumie uwanja wa nje wa kufanyia mazoezi wa gereza hilo. Kwa kuwa tulikuwa Mashahidi wengi mahali pamoja, kila siku tulipata nafasi za kutiana moyo na kuwatolea ushahidi mzuri wafungwa wengine. Kwa kushangaza, baada ya kutumikia kifungo cha miezi mitatu hivi, tuliachiliwa kwa sababu serikali ya Malawi ilishinikizwa na mataifa mbalimbali.

Maofisa wa polisi walituhimiza turudi nyumbani kwetu, lakini walituambia pia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku nchini Malawi. Marufuku hiyo ilichukua karibu miaka 26, kuanzia Oktoba 20, 1967, hadi Agosti 12, 1993. Miaka hiyo ilikuwa yenye magumu, lakini kwa msaada wa Yehova tuliweza kudumisha msimamo wetu thabiti wa kutokuwamo.

Tuliwindwa Kama Wanyama

Mnamo Oktoba 1972, amri iliyotolewa na serikali ilianzisha wimbi jingine la mnyanyaso mkali. Amri hiyo iliwataka Mashahidi wote wa Yehova wafutwe kazi na pia Mashahidi wote walioishi vijijini wafukuzwe kutoka nyumbani kwao. Mashahidi waliwindwa kama wanyama.

Wakati huo, kijana mmoja Mkristo alikuja nyumbani kwetu na kumletea Emmas ujumbe huu wa dharura, ‘Chama cha Vijana kinapanga kukukata kichwa na kukiweka kwenye mti, kisha wakipeleke kwa machifu.’ Baada ya kufanya mipango tumfuate haraka iwezekanavyo, Emmas aliondoka nyumbani upesi. Kwa haraka, niliwaambia watoto waende. Kisha nilipokaribia kuondoka, wanachama kumi wa Chama cha Vijana walitokea wakimtafuta Emmas. Walivunja nyumba yetu lakini wakagundua kwamba Emmas alikuwa ameondoka. Kwa hasira, wanaume hao walinikokota hadi kwenye shamba la miwa lililokuwa karibu, ambapo walinipiga kwa mateke na kwa miwa. Kisha wakaniacha karibu kufa. Baada ya kupata fahamu, nilijikokota hadi nyumbani.

Usiku huo, baada ya giza kuingia, Emmas alihatarisha maisha yake kwa kurudi nyumbani kunitafuta. Aliponikuta nikiwa nimepigwa vibaya, Emmas na rafiki yake ambaye alikuwa na gari walinibeba polepole na kuniingiza kwenye gari hilo. Kisha tukaenda hadi kwenye nyumba ya ndugu mmoja jijini Lilongwe, ambapo nilianza kupata nafuu polepole kutokana na majeraha ya shambulizi hilo, naye Emmas akaanza kufanya mipango ya kukimbia kutoka nchini.

Wakimbizi Wasiokuwa na Mahali pa Kwenda

Binti yetu Dinesi na mume wake walikuwa na lori lenye uzito wa tani tano. Walimwajiri dereva ambaye hapo zamani alikuwa mwanachama wa Chama Chipukizi cha Malawi ambaye alituhurumia. Alijitolea kutusaidia sisi na Mashahidi wengine. Kwa jioni kadhaa, dereva huyo aliwabeba Mashahidi kutoka mahali palipopangwa mafichoni. Kisha akavaa mavazi yake ya Chama Chipukizi cha Malawi na kuendesha lori hilo lililojaa watu kupitia vizuizi kadhaa vilivyowekwa na polisi barabarani. Alijihatarisha sana ili kuwasaidia mamia ya Mashahidi kuvuka mpaka na kuingia Zambia.

Baada ya miezi michache, serikali ya Zambia iliturudisha Malawi; lakini bado hatungeweza kurudi kwenye vijiji vyetu. Mali zetu zote zilizobaki zilikuwa zimeibiwa. Hata mabati ya nyumba zetu yalikuwa yameng’olewa. Kwa kuwa hatukuwa na mahali pa kwenda, tulikimbilia Msumbiji na kukaa katika kambi ya wakimbizi ya Mlangeni kwa miaka miwili na nusu. Hata hivyo, mnamo Juni 1975, serikali mpya nchini Msumbiji ilifunga kambi hiyo na kutulazimisha kurudi Malawi, ambapo hali zilikuwa bado ni mbaya kwa watu wa Yehova. Hatukuwa na la kufanya ila kukimbilia Zambia mara ya pili. Tulifika kwenye kambi ya wakimbizi ya Chigumukire.

Miezi miwili baadaye, msafara wa mabasi na malori ya kijeshi yaliegeshwa kando ya barabara kuu, na mamia ya wanajeshi wa Zambia wenye silaha kali wakaivamia kambi. Walituambia kwamba tulikuwa tumejengewa nyumba nzuri mahali fulani na walikuja kutusaidia kuhamia huko. Tulijua kwamba hawakuwa wakituambia ukweli. Wanajeshi hao walianza kuwasukuma kwa fujo watu waingie kwenye malori na mabasi na kukawa na hofu kubwa. Wanajeshi walianza kufyatua risasi hewani wakitumia bunduki zao za rashasha, na maelfu ya ndugu na dada zetu wakatawanyika kwa hofu.

Wakati wa mvurugo huo, Emmas aliangushwa na watu wakamkanyaga, lakini ndugu mmoja akamsaidia kusimama. Tulifikiri kwamba dhiki kubwa ilikuwa imeanza. Wakimbizi wote walikimbia kuelekea Malawi. Tulipokuwa tungali Zambia, tulifika kwenye mto fulani na akina ndugu wakashikana mikono ili kusaidia kila mtu avuke salama. Hata hivyo, tulipofika ng’ambo, tulizingirwa na wanajeshi wa Zambia na kurudishwa Malawi kwa nguvu.

Tuliporudi Malawi tena, hatukujua twende wapi. Tulipata habari kwamba watu walikuwa wameonywa kwenye mikutano ya kisiasa na magazetini wajihadhari na “nyuso mpya,” yaani Mashahidi wa Yehova waliokuwa wakiingia vijijini. Hivyo tuliamua kwenda katika jiji kuu, ambapo hatungejulikana kwa urahisi kama vijijini. Tulifanikiwa kupanga nyumba ndogo, na Emmas akaanza tena kutembelea makutaniko kisiri akiwa mwangalizi asafiriye.

Kuhudhuria Mikutano ya Kutaniko

Ni nini kilichotusaidia tubaki waaminifu? Mikutano ya kutaniko! Tukiwa kwenye kambi za wakimbizi huko Msumbiji na Zambia, tulikutanika kwa uhuru kwenye Majumba ya Ufalme yaliyoezekwa kwa nyasi. Ilikuwa vigumu na pia hatari kukusanyika kwa ajili ya mikutano nchini Malawi. Hata hivyo, sikuzote tulinufaika kwa kufanya hivyo. Ili tusigunduliwe, kwa kawaida tulifanya mikutano yetu usiku katika sehemu zilizokuwa mbali. Ili watu wasijue mahali tulipofanyia mikutano yetu, hatukumpigia msemaji makofi ya shukrani bali tulisugua tu mikono yetu.

Ubatizo ulifanywa usiku. Mwana wetu, Abiyudi, alibatizwa usiku. Baada ya hotuba ya ubatizo, yeye pamoja na wengine waliotaka kubatizwa walitembezwa gizani hadi mahali penye matope ambapo palikuwa pamechimbwa shimo dogo. Walibatizwa ndani ya shimo hilo.

Nyumba Yetu Ndogo—Mahali Salama

Miaka ya baadaye ya marufuku hiyo ya serikali, nyumba yetu jijini Lilongwe ilitumiwa kama mahali salama pa kuhifadhi vitu. Barua na vichapo kutoka ofisi ya tawi ya Zambia vililetwa kwa siri hadi nyumbani kwetu. Ndugu waliopeleka barua kwa kutumia baiskeli walikuja nyumbani kwetu na kuchukua mizigo iliyotoka Zambia, kisha wakasafirisha barua na vichapo hadi sehemu zote za Malawi. Magazeti ya Mnara wa Mlinzi yaliyopelekwa sehemu hizo zote yalikuwa membamba kwa sababu yalichapishwa kwenye makaratasi membamba yanayotumiwa kuchapisha Biblia. Jambo hilo liliwawezesha ndugu hao kubeba idadi mara mbili ya magazeti ambayo wangebeba ikiwa yangechapishwa kwenye karatasi ya kawaida. Ndugu hao pia walipeleka magazeti madogo ya Mnara wa Mlinzi yaliyokuwa tu na makala za funzo. Ilikuwa rahisi kuficha gazeti dogo kwenye mfuko wa shati kwa sababu lilikuwa na ukurasa mmoja tu.

Ndugu hao walihatarisha uhuru na maisha yao walipokuwa wakiendesha baiskeli zao kupitia vichakani, wakati mwingine katika usiku wenye giza, huku wakiwa wamebeba makatoni mengi ya vichapo vilivyopigwa marufuku. Ijapokuwa kulikuwa na vizuizi vya polisi barabarani na hatari nyinginezo, walisafiri mamia ya kilometa bila kujali hali ya hewa ili kuwapelekea ndugu zao chakula cha kiroho. Ndugu hao wapendwa walikuwa na ujasiri mkubwa.

Yehova Huwajali Wajane

Mnamo Desemba 1992, Emmas alipatwa na ugonjwa wa kiharusi alipokuwa akitoa hotuba kwenye kutaniko moja la mzunguko wake. Baada ya hapo, hakuweza kuzungumza tena. Muda fulani baadaye, alipatwa tena na kiharusi na upande mmoja wa mwili wake ukapooza. Ingawa ilikuwa vigumu sana kwake kukabiliana na ugonjwa huo, msaada wa upendo tuliopokea kutoka kwenye kutaniko ulifanya nisikate tamaa. Nilimtunza mume wangu nyumbani hadi alipokufa Novemba 1994, akiwa na umri wa miaka 76. Tulikuwa tumeoana kwa miaka 57, na Emmas aliona marufuku ikiondolewa kabla ya kifo chake. Lakini bado ninaomboleza kifo cha rafiki yangu mwaminifu.

Baada ya mimi kuwa mjane, mwana-mkwe wangu alijitwalia daraka la kunitunza mimi pamoja na mke na watoto wake watano. Kwa kuhuzunisha, alikufa Agosti 2000, baada ya kuugua kwa muda mfupi. Binti yangu angepataje chakula na makao kwa ajili yetu? Kwa mara nyingine tena, niliona kwamba Yehova anatujali, naye kwa kweli ni “baba wa yatima na mwamuzi wa wajane.” (Zaburi 68:5) Kupitia watumishi wake duniani, Yehova alituandalia nyumba mpya nzuri. Jinsi gani? Ndugu na dada zetu kutanikoni walipoona shida yetu, walitujengea nyumba kwa majuma matano tu! Ndugu kutoka makutaniko mengine ambao ni mafundi wa matofali walikuja kutusaidia. Tulifurahi sana kwa sababu ya upendo na fadhili ambazo Mashahidi hao walituonyesha kwa kuwa walitujengea nyumba bora kuliko nyumba ambazo wengi wao wanaishi. Upendo huo ambao kutaniko lilionyesha ulikuwa ushahidi mzuri sana kwa jirani zetu. Ninapolala usiku, mimi huhisi kana kwamba niko katika Paradiso! Naam, nyumba yetu mpya nzuri imejengwa kwa matofali na saruji, lakini kama vile ambavyo wengi wamesema, ni nyumba ambayo kwa kweli ilijengwa kwa upendo.—Wagalatia 6:10.

Yehova Anaendelea Kutujali

Ingawa nyakati nyingine nimekaribia kukata tamaa kabisa, Yehova amekuwa mwema kwangu. Kati ya watoto wangu tisa, saba wangali hai, na familia yangu sasa ina washiriki 123. Jinsi ninavyoshukuru kwamba wengi wao wanamtumikia Yehova kwa uaminifu!

Nina umri wa miaka 82 sasa, na ninafurahi sana kuona yale ambayo roho ya Mungu imetimiza nchini Malawi. Katika muda wa miaka minne iliyopita, nimeona idadi ya Majumba ya Ufalme ikiongezeka kutoka jumba moja hadi zaidi ya majumba 600. Pia sasa tuna ofisi mpya ya tawi jijini Lilongwe, nasi tunafurahi kupata mtiririko usiokatizwa wa chakula cha kiroho chenye kutia nguvu. Kwa kweli ninahisi kwamba nimeona utimizo wa ahadi ya Mungu inayopatikana kwenye Isaya 54:17 ambapo tunahakikishiwa hivi: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa.” Baada ya kumtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 50, ninasadiki kwamba hata tukabili majaribu gani, Yehova anatujali sikuzote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ili kupata habari zaidi kuhusu historia ya Mashahidi wa Yehova huko Malawi, ona 1999 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 149-223, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mume wangu, Emmas, alibatizwa Aprili 1951

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kikundi cha ndugu jasiri waliopeleka barua

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nyumba iliyojengwa kwa upendo