Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuimarisha Ndoa Yako

Jinsi ya Kuimarisha Ndoa Yako

Jinsi ya Kuimarisha Ndoa Yako

WAZIA nyumba ambayo imeachiliwa bila kutunzwa. Rangi imebambuka, paa limeharibika, na hata nyasi haijakatwa. Bila shaka, nyumba hiyo imepigwa na dhoruba kali kwa miaka mingi nayo imechakaa. Je, ibomolewe? Si lazima, kwa sababu ikiwa msingi wake ni imara na muundo wake ni thabiti, nyumba hiyo inaweza kurekebishwa.

Je, hali ya nyumba hiyo inakukumbusha ndoa yako? Kwa miaka mingi, huenda dhoruba kali za mfano zimeathiri ndoa yako. Inawezekana mmoja wenu au nyote wawili mmeiachilia ndoa yenu kwa kadiri fulani. Huenda ukahisi kama Sandy ambaye alisema hivi baada ya miaka 15 ya maisha ya ndoa: “Hatukushirikiana katika jambo lolote ila tu kwamba tulikuwa tumeoana. Na hiyo haitoshi.”

Hata kama hali katika ndoa yako iko hivyo, usikate kauli haraka kwamba inapaswa kuvunjwa. Ndoa yako inaweza kurekebishwa. Mengi yanategemea kadiri wewe na mwenzi wako mnavyotimiza wajibu wenu katika ndoa. Kufanya hivyo kunaweza kuimarisha ndoa yenu wakati wa majaribu. Lakini wajibu katika ndoa ni nini? Nayo Biblia inaweza kukusaidiaje kuuimarisha?

Wajibu Hutia Ndani Daraka

Wajibu katika ndoa humaanisha kulazimika kutimiza jambo fulani au kujiwekea masharti. Wakati mwingine neno hilo hutumika kuhusu mikataba mingine kama vile makubaliano ya kibiashara. Kwa mfano, mjenzi anaweza kuhisi analazimika kutimiza matakwa ya mkataba wa kujenga nyumba ambao alitia sahihi. Huenda yeye hamjui mtu aliyeagiza kazi hiyo ifanywe. Hata hivyo, anahisi ni sharti atimize ahadi yake.

Ingawa ndoa si kama mkataba wa kibiashara, wajibu katika ndoa unatia ndani masharti fulani. Yaelekea wewe na mwenzi wako wa ndoa mliweka nadhiri nzito mbele za Mungu na watu kwamba mtaishi pamoja, chini ya hali zozote zile. Yesu alisema: “Yeye aliyewaumba wao [mwanamume na mwanamke] kutoka mwanzo aliwafanya wa kiume na wa kike na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mtu ataacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.’” Yesu aliongezea: “Kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.” (Mathayo 19:4-6) Matatizo yanapotokea, basi wewe na mwenzi wako wa ndoa mnapaswa kuazimia kabisa kutimiza ahadi mlizotoa. * Mke mmoja anasema: “Mambo yalianza kuwa mazuri tulipoacha kufikiria talaka.”

Lakini kuna mengi zaidi yanayohusika katika ndoa kuliko tu kutimiza wajibu. Ni mambo gani hayo?

Ushirikiano Huimarisha Wajibu Katika Ndoa

Wajibu katika ndoa haumaanishi kwamba wenzi wa ndoa hawatagombana kamwe. Wanapogombana, wanapaswa kujitahidi sana kutatua tatizo hilo, si kwa sababu ya nadhiri walizofanya bali kwa sababu wanapendana. Yesu alisema hivi kuhusu mume na mke: “Wao si wawili tena, bali mwili mmoja.”

Inamaanisha nini kuwa “mwili mmoja” na mwenzi wako? Mtume Paulo aliandika kwamba “waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28, 29) Hivyo basi, kuwa “mwili mmoja” humaanisha kwamba unahangaikia hali njema ya mwenzi wako kama unavyohangaikia hali yako mwenyewe. Wenzi wa ndoa wanahitaji kubadili mtazamo wao, na badala ya kufikiria mambo kama waseja, wayafikirie kama watu waliooana. Mshauri mmoja aliandika: “Wenzi wa ndoa wanapaswa kuacha kujiona kama waseja, na badala yake wajione kuwa watu waliofunga ndoa.

Je, wewe na mwenzi wako mnajiona kuwa watu waliofunga ndoa? Inawezekana kuishi pamoja kwa miaka mingi na bado msiwe “mwili mmoja.” Naam, jambo hilo linaweza kutokea, lakini kitabu Giving Time a Chance kinasema: “Ndoa humaanisha kushirikiana maishani, na kadiri watu wawili wanavyoshirikiana ndivyo ndoa yao inavyositawi.”

Wenzi fulani wa ndoa huendelea kuishi pamoja bila furaha kwa sababu tu ya watoto wao au usalama wa kifedha. Wengine huvumilia kwa sababu wanaona talaka kuwa jambo lisilofaa kiadili au wanaogopa jinsi wengine watakavyowaona ikiwa watatalikiana. Ingawa ni jambo zuri kwamba ndoa hizo hazivunjiki, kumbuka kwamba lengo lenu ni kuwa na uhusiano wenye upendo bali si wenye kudumu tu.

Kutokuwa na Ubinafsi Huimarisha Wajibu Katika Ndoa

Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho,” watu watakuwa “wenye kujipenda wenyewe.” (2 Timotheo 3:1, 2) Kama unabii huo unavyosema, inaonekana leo watu hujifikiria mno. Katika ndoa nyingi, kujitoa kumfanyia mwenzi wako jambo fulani bila kuwa na hakika kwamba atakufanyia vivyo hivyo, huonwa kuwa udhaifu. Hata hivyo, katika ndoa zilizofanikiwa, wenzi wote wawili huonyesha roho ya kujidhabihu. Unawezaje kufanya hivyo?

Badala ya kufikiria tu swali hili, ‘Ninafaidikaje na ndoa hii?’ jiulize, ‘Mimi mwenyewe ninafanya nini ili kuimarisha ndoa yangu?’ Biblia inasema kwamba Wakristo wanapaswa ‘kufuliza kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yao wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi ya wengine.’ (Wafilipi 2:4) Unapotafakari kanuni hiyo ya Biblia changanua matendo yako ya juma lililopita. Ni mara ngapi ulimtendea mwenzi wako kwa fadhili kwa sababu tu ulitaka kumnufaisha? Mwenzi wako alipotaka kuzungumza, je, ulimsikiliza—hata ingawa hukutaka kuongea? Ni mambo mangapi uliyotenda ambayo yalimpendeza mwenzi wako zaidi ya vile yalivyokupendeza?

Unapochanganua maswali hayo, usiwe na wasiwasi kwamba matendo yako mema yatapuuzwa au yakose kuthawabishwa. Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema, “Katika mahusiano mengi, mtu anapomtendea mwenzake mema, yeye hutendewa vivyo hivyo, kwa hiyo fanya yote uwezayo kumtia moyo mwenzi wako atende mema kwa kutenda mema wewe mwenyewe.” Matendo ya kujidhabihu huimarisha ndoa yako kwa sababu yanaonyesha kwamba unaithamini na unataka idumu.

Ni Muhimu Kuiona Ndoa Kuwa Mpango wa Kudumu

Yehova Mungu huthamini sana ushikamanifu. Naam, Biblia husema: ‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’ (2 Samweli 22:26NW) Kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu humaanisha pia kuendelea kuwa mshikamanifu kwa mpango wa ndoa alioanzisha.—Mwanzo 2:24.

Ikiwa wewe na mwenzi wako ni washikamanifu, mnaweza kufurahia muungano wenye kudumu. Mnapofikiria miezi, miaka, na makumi ya miaka inayokuja, mnajiona mkiwa pamoja bado. Wazo la kwamba hamngekuwa mmeoana haliingii akilini hata kidogo, na mtazamo huo hufanya ndoa yenu iwe salama. Mke mmoja anasema: “Hata ninapomkasirikia [mume wangu] na kuudhiwa na jinsi mambo yalivyo kati yetu, mimi sihangaiki eti ndoa yetu itavunjika. Jambo linalonihangaisha ni jinsi tutakavyorudia uhusiano tuliokuwa nao kabla ya mambo kuharibika. Mimi huwa sina shaka hata kidogo kwamba tutatatua tatizo hilo, ingawa wakati huo sijui jinsi ya kufanya hivyo.”

Kuwa na maoni kwamba ndoa ni mpango wa kudumu ni jambo muhimu katika kutimiza wajibu wako kwa mwenzi wako. Hata hivyo, inasikitisha kwamba sivyo ilivyo katika ndoa nyingi. Mnapogombana vikali, mmoja wenu anaweza kusema hivi kwa hasira, “Nitakuacha!” au “Nitatafuta mtu mwingine anayenithamini kikweli!” Ni kweli kwamba mara nyingi maneno hayo hayamaanishi kuwa mwenzi huyo atafanya hivyo. Lakini Biblia husema kwamba ulimi “umejaa sumu yenye kuleta kifo.” (Yakobo 3:8) Unapotoa vitisho na maonyo ni kana kwamba unasema hivi: ‘Sioni ndoa yetu kuwa yenye kudumu. Ninaweza kukuacha wakati wowote.’ Kutumia maneno kama hayo kunaweza kuharibu ndoa.

Unapokuwa na maoni kwamba ndoa ni mpango wa kudumu, unatumaini kuishi na mwenzi wako chini ya hali zozote. Jambo hilo linaleta manufaa zaidi. Litafanya iwe rahisi zaidi kwako na mwenzi wako kukubali kasoro na makosa yenu na kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari. (Wakolosai 3:13) Kijitabu kimoja kinasema kwamba “katika ndoa nzuri, nyote wawili mnaweza kukosea, na bado ndoa isivunjike.”

Siku ya arusi yako, ulifanya ahadi kwa mwenzi wako bali si kwa mpango wa ndoa. Jambo hilo linapaswa kuathiri jinsi unavyofikiri na kutenda ukiwa mwenzi wa ndoa. Je, hukubali kwamba unapaswa kuendelea kuishi na mwenzi wako si kwa sababu tu una imani thabiti katika utakatifu wa ndoa bali pia kwa sababu unampenda mwenzi wako?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Hali zinapokuwa ngumu kupita kiasi wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na sababu halali ya kutengana. (1 Wakorintho 7:10, 11; ona kitabu, Siri ya Kupata Furaha ya Familia, ukurasa wa 160-161, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.) Zaidi ya hayo, Biblia huruhusu talaka kwa sababu ya uasherati.—Mathayo 19:9.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Yale Unayoweza Kufanya Sasa

Unatimiza wajibu wako kadiri gani katika ndoa? Labda unaona kwamba kuna mambo unayohitaji kufanyia maendeleo. Ili kuwajibika zaidi katika ndoa yenu, jaribu kufanya mambo yafuatayo:

● Jichunguze na ujiulize: ‘Je, mimi hujiona kuwa mtu aliyefunga ndoa au bado ninafikiri na kutenda kama mseja?’ Kuhusiana na hilo, mwulize mwenzi wako ana maoni gani kukuhusu.

● Soma makala hii pamoja na mwenzi wako. Kisha, kwa utulivu mzungumzie jinsi mnavyoweza kuwajibika zaidi katika ndoa yenu.

● Nyote wawili, fanyeni mambo yanayoimarisha uwajibikaji wenu. Kwa mfano: Tazameni picha za arusi yenu na matukio mengine yenye kuvutia. Fanyeni mambo mliyofurahia wakati wa uchumba wenu au katika miaka ya mapema ya ndoa yenu. Someni pamoja makala zinazotegemea Biblia katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo zinazungumzia ndoa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Wajibu Katika Ndoa Huhusisha...

Daraka “Tekeleza ulichoahidi. Ni afadhali kutoweka nadhiri kuliko kuweka nadhiri kisha usiitimize.”—Mhubiri 5:4, 5, Biblia Habari Njema.

Kushirikiana “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja . . . Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake.”—Mhubiri 4:9, 10.

Kujidhabihu “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Kuwa na Maoni Kwamba Ndoa Ni Mpango wa Kudumu “Upendo . . . huvumilia mambo yote.”—1 Wakorintho 13:4, 7.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, wewe humsikiliza mwenzi wako anapotaka kuzungumza?