Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kabla na Baadaye—Jinsi Biblia Ilivyombadili Mtu Huyu

Kabla na Baadaye—Jinsi Biblia Ilivyombadili Mtu Huyu

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Kabla na Baadaye—Jinsi Biblia Ilivyombadili Mtu Huyu

MUZIKI ulikuwa muhimu sana katika maisha ya Rolf-Michael. Alipenda sana dawa za kulevya. Akiwa kijana huko Ujerumani alitumia sana pombe na dawa mbalimbali za kulevya, ambazo baadhi yake zilimwathiri akili.

Alipokuwa akijaribu kuingiza kimagendo dawa za kulevya katika nchi moja ya Afrika, Rolf-Michael alikamatwa na kufungwa gerezani kwa miezi 13. Kipindi alichokaa gerezani kilimsaidia kufikiria kusudi halisi la maisha.

Rolf-Michael na mke wake, Ursula, walitafuta sana kujua kweli na kusudi la maisha. Ingawa walikatishwa tamaa na makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, walitamani sana kumjua Mungu. Lakini walikuwa na maswali ambayo dini mbalimbali hazikuweza kuwajibu kwa njia yenye kuridhisha. Isitoshe, dini hizo hazikuwapa kichocheo chenye nguvu ili kubadili maisha yao.

Mwishowe, Rolf-Michael na Ursula walikutana na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuanza kujifunza Biblia, Rolf-Michael aliguswa moyo sana na shauri hili: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Aliazimia ‘kuweka mbali utu wa zamani uliofuatana na njia yake ya kwanza ya mwenendo na kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’—Waefeso 4:22-24.

Rolf-Michael angewezaje kuvaa utu mpya? Alionyeshwa katika Biblia, kwamba “kupitia ujuzi sahihi” utu wa mtu unaweza ‘kufanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba,’ yaani, Yehova Mungu.—Wakolosai 3:9-11.

Alipoendelea kutwaa ujuzi sahihi, Rolf-Michael alijitahidi kupatanisha maisha yake na viwango vya Neno la Mungu. (Yohana 17:3) Ingawa ilikuwa vigumu kuacha kutumia dawa za kulevya, Rolf-Michael aliona umuhimu wa kumkaribia Yehova katika sala na kupata msaada wake. (1 Yohana 5:14, 15) Alipata msaada zaidi kwa kushirikiana kwa ukaribu na Mashahidi wa Yehova ambao hujitahidi kufanya mapenzi ya Mungu.

Kujua kwamba ulimwengu unapitilia mbali na kwamba wale wanaofanya mapenzi ya Mungu watadumu milele pia kulimsaidia Rolf-Michael. Jambo hilo lilimsaidia kuchagua baraka za milele zinazotokana na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu mwenye upendo, Yehova, badala ya kupenda vitu vya muda vya ulimwengu huu. (1 Yohana 2:15-17) Rolf-Michael aliguswa moyo sana na maneno haya ya Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Anasema hivi kwa uthamini: “Mstari huo unaonyesha upendo mwingi wa Yehova, kwa kuwa yeye huwapa wanadamu nafasi ya kuufurahisha moyo wake.”

Kama Rolf-Michael, mke wake, na watoto wao watatu, watu wengi sana hufaidika kwa kufuata kanuni za Biblia. Watu hao wanaweza kupatikana katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni kote. Inasikitisha kwamba katika nchi fulani Mashahidi hushitakiwa kwa uwongo kuwa madhehebu hatari ambayo huvunja familia. Mambo yaliyompata Rolf-Michael yanaonyesha kuwa jambo hilo si kweli.—Waebrania 4:12.

Rolf-Michael anasema kwamba andiko la Mathayo 6:33, linalotuhimiza tutangulize mambo ya kiroho linaongoza familia yake kwa njia ifaayo. Yeye na familia yake wanamshukuru sana Yehova kwa kuwa na maisha ya familia yenye furaha wakiwa Wakristo. Wanakubaliana na hisia za mtunga-zaburi aliyeimba: “Nimrudishie BWANA nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?”—Zaburi 116:12.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Mungu huwapa wanadamu nafasi ya kuufurahisha moyo wake

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kanuni za Biblia Zinazofanya Kazi

Zifuatazo ni baadhi ya kanuni za Biblia ambazo zimewachochea wengi kuacha kutumia dawa za kulevya zinazoweza kuhatarisha maisha:

“Enyi mmpendao BWANA, uchukieni uovu.” (Zaburi 97:10) Inakuwa rahisi kwa mtu kufanya yanayompendeza Mungu baada ya kusadikishwa kwamba mazoea fulani ni mabaya na yanaweza kuleta kifo, na pia kusitawisha chuki kuyaelekea.

“Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Ili kukataa dawa za kulevya na vitu vingine vinavyolewesha, mtu anahitaji kuchagua kwa makini watu anaoshirikiana nao. Inanufaisha kwelikweli kusitawisha urafiki na Wakristo watakaomsaidia akatae dawa za kulevya.

“Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani hiyo ya moyo na akili haiwezi kupatikana kwa kutumia dawa za kulevya. Kumtegemea Mungu kwa sala kunaweza kumsaidia mtu kutatua matatizo maishani bila kutumia dawa za kulevya.