Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tusali Bila Kukoma?

Kwa Nini Tusali Bila Kukoma?

Kwa Nini Tusali Bila Kukoma?

“Salini bila kukoma. Kuhusiana na kila jambo toeni shukrani.”—1 WATHESALONIKE 5:17, 18.

1, 2. Danieli alionyeshaje kwamba alithamini pendeleo la sala, na hilo lilikuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wake pamoja na Mungu?

NABII Danieli alikuwa na desturi ya kusali kwa Mungu mara tatu kwa siku. Alikuwa akipiga magoti kando ya dirisha la chumba chake cha juu lililoelekea jiji la Yerusalemu, na kusali. (1 Wafalme 8:46-49; Danieli 6:10) Hata wakati amri ya kifalme ilipokataza kusali kwa mtu mwingine yeyote isipokuwa Dario, mfalme wa Umedi, Danieli hakuyumbayumba hata kidogo. Mwanamume huyo aliyependa kusali alimsihi Yehova bila kukoma hata kama kufanya hivyo kulihatarisha uhai wake au la.

2 Yehova alimwonaje Danieli? Malaika Gabrieli alipokuja kujibu moja ya sala za Danieli, alimtaja nabii huyo kuwa ‘mtu anayependwa sana.’ (Danieli 9:20-23) Katika unabii wa Ezekieli, Yehova alimtaja Danieli kuwa mwanamume mwenye haki. (Ezekieli 14:14, 20) Bila shaka, sala za Danieli ziliimarisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wake muda wote wa maisha yake, jambo ambalo hata Dario alitambua.—Danieli 6:16.

3. Sala inawezaje kutusaidia kudumisha uaminifu-maadili kama inavyoonyeshwa na mambo yaliyompata mishonari mmoja?

3 Sala za ukawaida zinaweza pia kutusaidia kukabiliana na majaribu makali. Kwa mfano, fikiria kisa cha Harold King, aliyekuwa mishonari huko China ambaye alihukumiwa kifungo cha upweke cha miaka mitano. Kuhusiana na yaliyompata, Ndugu King alisema: “Ninaweza kuwa nimetengwa na wanadamu wenzangu, lakini hakuna mtu anayeweza kunitenga na Mungu. . . . Hivyo, kwa kuwa mtu yeyote anayepita angeweza kuniona nikiwa katika chumba changu gerezani, nilipiga magoti mara tatu kwa siku nikasali kwa sauti ndani ya chumba changu, nikimkumbuka Danieli, anayetajwa na Biblia. . . . Ilionekana kwamba katika pindi hizo roho ya Mungu iliongoza akili yangu kwa mambo yenye faida zaidi nami nikahisi nimetulia. Sala iliniimarisha kiroho na kunifariji kama nini!”

4. Ni maswali gani kuhusu sala tutakayochunguza katika makala hii?

4 Biblia inasema: “Salini bila kukoma. Kuhusiana na kila jambo toeni shukrani.” (1 Wathesalonike 5:17, 18) Kulingana na shauri hilo, tuchunguze maswali yafuatayo: Kwa nini tunapaswa kufikiria sala zetu kwa uzito? Tuna sababu gani za kumkaribia Yehova daima? Na tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahisi hatustahili kusali kwa Mungu kwa sababu ya udhaifu wetu?

Jenga Urafiki Kupitia Sala

5. Sala hutusaidia tuwe na urafiki gani wa pekee?

5 Je, ungependa Yehova akuone kama rafiki yake? Alisema kwamba mzee wa ukoo Abrahamu ni rafiki yake. (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Yehova anataka tukuze urafiki wa aina hiyo pamoja naye. Kwa kweli anatualika tumkaribie. (Yakobo 4:8) Je, mwaliko huo hautufanyi tufikirie kwa uzito uandalizi wa pekee wa sala? Ni vigumu sana kupata nafasi ya kuzungumza na afisa mkuu wa serikali, sembuse kuwa rafiki yake. Lakini Muumba wa ulimwengu anatutia moyo tuwe huru kumkaribia katika sala, wakati wowote tunapotaka au tunapohitaji kufanya hivyo. (Zaburi 37:5) Kusali bila kukoma hutusaidia kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova.

6. Kielelezo cha Yesu kinatufunza nini kuhusu uhitaji wa “kusali kwa kuendelea”?

6 Hata hivyo, inaweza kuwa rahisi kupuuza sala. Kushughulika tu na mikazo ya kila siku kunaweza kukengeusha fikira zetu tusijitahidi kuzungumza na Mungu. Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake ‘wasali kwa kuendelea,’ naye mwenyewe alifanya hivyo. (Mathayo 26:41) Ingawa alikuwa na shughuli nyingi mchana kutwa, alitenga wakati wa kuzungumza na Baba yake wa mbinguni. Wakati mwingine, Yesu aliamka “mapema asubuhi, kulipokuwa bado kuna giza,” ili asali. (Marko 1:35) Pindi nyingine, alienda mahali pasipo na watu jioni, ili asali kwa Yehova. (Mathayo 14:23) Kila mara Yesu alitenga wakati wa kusali, nasi pia tunapaswa kufanya hivyo.—1 Petro 2:21.

7. Ni hali gani zinazopaswa kutuchochea kuzungumza na Baba yetu wa mbinguni kila siku?

7 Kila siku tunapata nafasi nyingi zinazofaa kusali faraghani tunapokabili matatizo, vishawishi, au tunapofanya maamuzi. (Waefeso 6:18) Tunapotafuta uongozi wa Mungu katika hali zote za maisha, tunakuwa na uhakika kwamba urafiki wetu pamoja naye utakua. Ikiwa marafiki wawili wanakabili matatizo pamoja, urafiki wao unaimarika zaidi. (Mithali 17:17) Itakuwa hivyo tunapomtegemea Yehova na kupata msaada wake.—2 Mambo ya Nyakati 14:11.

8. Tunajifunza nini kuhusu urefu wa sala zetu za kibinafsi kutokana na vielelezo vya Nehemia, Yesu, na Hana?

8 Tunafurahi kama nini kwamba Mungu hatuwekei mipaka kuhusu urefu wa sala au mara ambazo tunaweza kuzungumza naye katika sala! Nehemia alitoa sala fupi kimya-kimya kabla ya kutoa ombi lake kwa mfalme wa Uajemi. (Nehemia 2:4, 5) Yesu pia alitoa sala fupi alipomwomba Yehova ampe nguvu za kumfufua Lazaro. (Yohana 11:41, 42) Kwa upande mwingine, Hana ‘alidumu kuomba mbele za BWANA’ alipomweleza yote yaliyokuwa moyoni mwake. (1 Samweli 1:12, 15, 16) Sala zetu za kibinafsi zinaweza kuwa fupi au ndefu kulingana na uhitaji na hali.

9. Kwa nini sala zetu zinapaswa kutia ndani sifa na shukrani kwa Yehova kwa yote anayotufanyia?

9 Sala nyingi katika Biblia zinaonyesha uthamini unaotoka moyoni kwa ajili ya cheo kikuu cha Yehova na kazi zake za ajabu. (Kutoka 15:1-19; 1 Mambo ya Nyakati 16:7-36; Zaburi 145) Katika maono, mtume Yohana anaona wazee 24, yaani, hesabu kamili ya Wakristo watiwa-mafuta katika cheo chao cha kimbingu, wakimsifu Yehova, wakisema: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufunuo 4:10, 11) Sisi pia tuna sababu ya kumsifu Muumba kwa ukawaida. Wazazi hufurahi sana wakati mtoto wao anapowashukuru kutoka moyoni kwa jambo ambalo wamemfanyia. Kufikiria kwa uthamini fadhili za Yehova na kuonyesha shukrani zetu za kutoka moyoni ni njia nzuri ya kuboresha sala zetu.

Kwa Nini ‘Tusali Bila Kukoma?’

10. Sala inatimiza sehemu gani katika kuimarisha imani yetu?

10 Kusali kwa ukawaida ni muhimu kwa imani yetu. Baada ya kuonyesha uhitaji wa ‘kusali sikuzote badala ya kukata tamaa,’ Yesu aliuliza: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?” (Luka 18:1-8) Sala ya bidii na ya kutoka moyoni hujenga imani. Kwa kuwa Mzee wa ukoo Abrahamu alikuwa anaendelea kuzeeka na alikuwa bado hajapata mtoto, alizungumza na Mungu kuhusu jambo hilo. Kwa kumjibu, Yehova alimwomba kwanza atazame mbinguni na kuhesabu nyota, kama angeweza kufanya hivyo. Ndipo Mungu akamhakikishia Abrahamu hivi: “Ndivyo itakavyokuwa uzao wako.” Ikawaje? Abrahamu ‘alimwamini BWANA, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki.’ (Mwanzo 15:5, 6) Yehova ataimarisha imani yetu ikiwa tunamweleza yote yaliyo moyoni katika sala, kukubali ahadi zake katika Biblia, na kumtii.

11. Sala inawezaje kutusaidia kutatua matatizo?

11 Sala inaweza pia kutusaidia kutatua matatizo. Je, maisha yetu ni yenye kulemea na tunakabili hali ngumu kuvumilia? Biblia inasema: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Tunapokabili maamuzi mazito, tunaweza kuiga kielelezo cha Yesu. Alisali faraghani usiku kucha kabla ya kuwachagua mitume wake 12. (Luka 6:12-16) Na usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alisali kwa juhudi nyingi sana hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka kwenye ardhi.” (Luka 22:44) Ikawaje? ‘Alisikiwa kwa kupendelewa kwa sababu ya hofu yake ya kimungu.’ (Waebrania 5:7) Tutapata msaada wa kukabiliana na hali ngumu na majaribu makali tukisali kwa bidii na bila kukoma.

12. Sala inaonyeshaje kwamba Yehova anapendezwa nasi?

12 Sababu nyingine ya kumkaribia Yehova kwa njia ya sala ni kwamba yeye pia atatukaribia. (Yakobo 4:8) Tunapomweleza Yehova yote yaliyo moyoni katika sala, je, hatuhisi kwamba yeye anapendezwa na mahitaji yetu na anatujali kwa wororo? Tunauona upendo wa Mungu katika njia ya pekee sana. Yehova hajampa yeyote yule daraka la kusikiliza sala ambazo watumishi wake wanamtolea akiwa Baba yao wa mbinguni. (Zaburi 66:19, 20; Luka 11:2) Naye anatualika ‘tutupe hangaiko letu lote juu yake, kwa sababu yeye hutujali.’—1 Petro 5:6, 7.

13, 14. Tuna sababu gani za kusali bila kukoma?

13 Sala inaweza kutusaidia kuwa na bidii zaidi katika kazi ya kuhubiri na hutuimarisha wakati ambapo ubaridi au upinzani waweza kutufanya tukate tamaa. (Matendo 4:23-31) Sala inaweza pia kutulinda na “mbinu za Ibilisi.” (Waefeso 6:11, 17, 18) Tunapojitahidi kukabiliana na majaribu ya kila siku, tunaweza kumwomba Mungu bila kukoma ili atutie nguvu. Katika sala ya Yesu ya kielelezo alimwomba Yehova ‘atukomboe kutokana na yule mwovu,’ Shetani Ibilisi.—Mathayo 6:13.

14 Tukiendelea kusali ili tupate msaada wa kudhibiti maelekeo yetu yenye dhambi, Yehova atatusaidia. Tuna uhakika huu: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:13) Yehova alimtia nguvu mtume Paulo katika hali mbalimbali. Alisema: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:13; 2 Wakorintho 11:23-29.

Tudumu Katika Sala Ingawa Tuna Udhaifu

15. Ni nini kinachoweza kutokea tunapokosa kufuata viwango vya Mungu katika mwenendo wetu?

15 Ili sala zetu zikubaliwe, hatupaswi kukataa shauri la Neno la Mungu. Mtume Yohana aliandika, “Chochote kile tuombacho twapokea kutoka kwake kwa sababu tunashika amri zake na kufanya mambo yanayopendeza machoni pake.” (1 Yohana 3:22) Hata hivyo, ni nini kinachoweza kutokea tunapokosa kufuata viwango vya Mungu katika mwenendo wetu? Adamu na Hawa walijificha baada ya kufanya dhambi katika bustani ya Edeni. Sisi pia tunaweza kuwa na mwelekeo wa kujificha ‘BWANA Mungu asituone’ na kuacha kusali. (Mwanzo 3:8) Klaus, mwangalizi asafiriye mwenye uzoefu anasema: “Nimetambua kwamba mara nyingi kuacha kusali ndiyo hatua ya kwanza yenye kosa inayochukuliwa na wale wanaojitenga na Yehova na tengenezo lake.” (Waebrania 2:1) Ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha José Ángel. Anasema: “Kwa karibu miaka minane, nilisali mara chache sana kwa Yehova. Nilihisi kwamba sikustahili kuzungumza naye, ingawa bado nilimwona kuwa Baba yangu wa mbinguni.”

16, 17. Toa mifano ya jinsi sala za ukawaida zinavyoweza kutusaidia kushinda udhaifu wa kiroho.

16 Huenda baadhi yetu tukahisi kuwa hatufai kusali kwa sababu ya udhaifu wetu wa kiroho au kwa sababu tumetumbukia katika kosa. Lakini huo ndio wakati tunaopaswa kuthamini zaidi manufaa ya sala. Yona alikimbia mgawo wake. Lakini, ‘alipomlilia BWANA kwa sababu ya shida yake, Yeye alimwitikia. Katika tumbo la kuzimu aliomba, naye BWANA akasikia sauti yake.’ (Yona 2:2) Yona aliposali, Yehova alijibu sala yake, naye akarudia hali nzuri ya kiroho.

17 José Ángel pia alisali kwa bidii ili kupata msaada. Anakumbuka: “Nilimweleza Mungu yote yaliyokuwa moyoni na kumwomba anisamehe. Naye alinisaidia. Sidhani kama ningerudia kweli bila msaada wa sala. Sasa ninasali kwa ukawaida kila siku, nami hutazamia kwa hamu pindi hizo.” Tunapaswa kujihisi huru kuzungumza na Mungu waziwazi juu ya makosa yetu na kumwomba kwa unyenyekevu atusamehe. Mfalme Daudi alipotubu makosa yake, Yehova alimsamehe dhambi zake. (Zaburi 32:3-5) Yehova anataka kutusaidia, wala si kutuhukumu. (1 Yohana 3:19, 20) Sala za wazee wa kutaniko zinaweza kutusaidia kiroho, kwa kuwa zina “kani nyingi.”—Yakobo 5:13-16.

18. Watumishi wa Mungu wanaweza kuwa na uhakika gani hata kama wamekosea kwa kadiri gani?

18 Ni baba gani anayeweza kukataa kumsikiliza mwana anayemwendea kwa unyenyekevu ili kumwomba msaada na shauri baada ya kufanya kosa? Mfano wa mwana mpotevu huonyesha kwamba Baba yetu wa mbinguni hufurahi tunapomrudia hata kama tumekosea kwa kadiri gani. (Luka 15:21, 22, 32) Yehova anawasihi wote wanaofanya makosa wamwite ‘kwa kuwa atawasamehe kabisa.’ (Isaya 55:6, 7) Ingawa Daudi alitenda dhambi nzito kadhaa, alimwomba Yehova, akisema: “Ee, Mungu uisikilize sala yangu, wala usijifiche nikuombapo rehema.” Alisema pia: “Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua, naye [Yehova] atasikia sauti yangu.” (Zaburi 55:1, 17) Jambo hilo linatoa uhakikisho ulioje!

19. Kwa nini hatupaswi kukata kauli kwamba sala ambazo zinaonekana kuwa hazijibiwi ni uthibitisho wa kutokubaliwa na Mungu?

19 Namna gani ikiwa sala yetu haijibiwi mara moja? Basi, tunapaswa kuhakikisha kwamba tunaomba kupatana na mapenzi ya Yehova na kupitia jina la Yesu. (Yohana 16:23; 1 Yohana 5:14) Mwanafunzi Yakobo alitaja Wakristo fulani ambao sala zao hazikujibiwa kwa sababu ‘waliomba kwa kusudi baya.’ (Yakobo 4:3) Kwa upande mwingine, hatupaswi kukata kauli kwamba sala ambazo zinaonekana kuwa hazijibiwi ni uthibitisho wa kutokubaliwa na Mungu. Huenda wakati mwingine Yehova akaruhusu waabudu waaminifu waendelee kusali kwa muda juu ya jambo fulani kabla ya kuwajibu. Yesu alisema, “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa.” (Mathayo 7:7) Hivyo, tunahitaji ‘kudumu katika sala.’—Waroma 12:12.

Sali kwa Ukawaida

20, 21. (a) Kwa nini tunahitaji kusali bila kukoma katika ‘siku hizi za mwisho’? (b) Tutapata nini tunapokaribia kila siku kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa cha Yehova?

20 Mikazo na matatizo yanaendelea kuongezeka katika ‘siku hizi za mwisho,’ zinazotiwa alama na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Ni rahisi kuanza kufikiria tu majaribu yanayotupata. Hata hivyo, kusali bila kukoma kutatusaidia kuendelea kukazia fikira mambo ya kiroho licha ya matatizo, majaribu, na kuvunjika moyo. Tunaweza kupata msaada muhimu tunaohitaji kwa kusali kwa Yehova kila siku.

21 Yehova ni “Msikiaji wa sala,” na hawezi kamwe kuwa na shughuli nyingi sana asiweze kutusikiliza. (Zaburi 65:2; NW) Nasi tusiwe kamwe wenye shughuli nyingi sana tusiweze kuzungumza naye. Urafiki wetu pamoja na Mungu ndilo jambo lenye thamani zaidi kwetu. Kamwe na tusiuchukulie urafiki huo kivivi hivi tu. “Acheni tukaribie kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa, ili tuweze kupokea rehema na kupata fadhili isiyostahiliwa kwa msaada katika wakati ufaao.”—Waebrania 4:16.

Ungejibuje?

• Tunajifunza nini kuhusu umuhimu wa sala kutoka kwa nabii Danieli?

• Tunaweza kuimarishaje urafiki wetu pamoja na Yehova?

• Kwa nini tunapaswa kusali bila kukoma?

• Kwa nini hisia za kwamba hatufai hazipaswi kutuzuia kusali kwa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nehemia alitoa sala fupi kimya-kimya kabla ya kuzungumza na mfalme

[Picha katika ukurasa wa 17]

Hana ‘alidumu kuomba mbele za BWANA’

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alisali usiku kucha kabla ya kuwachagua mitume wake 12

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tunapata nafasi mbalimbali za kusali katika siku