Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazungumzo ya Kiroho Hujenga

Mazungumzo ya Kiroho Hujenga

Mazungumzo ya Kiroho Hujenga

“Msiache usemi uliooza utoke kinywani mwenu, bali usemi wowote ule ulio mwema kwa ajili ya kujenga kama vile kuwezavyo kuwa na uhitaji, ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.”—WAEFESO 4:29.

1, 2. (a) Usemi wa kibinadamu ni wenye thamani kadiri gani? (b) Watumishi wa Yehova hutamani kutumia ulimi wao jinsi gani?

“USEMI wa binadamu ni siri; ni zawadi kutoka kwa Mungu, ni muujiza.” Ndivyo alivyoandika mtungaji wa kamusi Ludwig Koehler. Huenda tunachukulia zawadi hii ya Mungu kivivi hivi tu. (Yakobo 1:17) Lakini fikiria ile hasara inayotokea wakati ugonjwa wa kupooza unapofanya mpendwa wako asiweze kusema mambo yenye kueleweka. Joan ambaye mume wake alipatwa na ugonjwa wa kupooza anaeleza hivi: “Tulikuwa na mawasiliano mazuri sana yaliyoimarisha uhusiano wetu. Jinsi ninavyoyakosa mazungumzo yetu!”

2 Mazungumzo yanaweza kuimarisha urafiki, kusuluhisha kutoelewana, kutia moyo wenye huzuni, kuimarisha imani, kuboresha maisha—lakini mambo hayo yanahitaji jitihada. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Tukiwa watumishi wa Yehova, tunataka mazungumzo yetu yawe yenye afya na yenye kujenga badala ya kuumiza na kubomoa. Tunatamani pia kutumia ulimi wetu kumsifu Yehova katika huduma na katika mazungumzo ya faraghani. Mtunga-zaburi aliimba: “Tumejisifia Mungu mchana kutwa, na jina lako tutalishukuru milele.”—Zaburi 44:8.

3, 4. (a) Sote tunakabili tatizo gani kuhusiana na usemi wetu? (b) Kwa nini tufikirie usemi wetu?

3 Mwanafunzi Yakobo anaonya kwamba, “ulimi, hakuna hata mmoja kati ya wanadamu awezaye kuufuga.” Anatukumbusha: “Sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2, 8) Hakuna mmoja wetu aliye mkamilifu. Ingawa tunakusudia kutumia usemi wetu vizuri, mara nyingi haujengi wengine wala kumletea Muumba sifa. Kwa hiyo, ni lazima tujifunze kuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema. Isitoshe, Yesu alisema: “Kila usemi usio na faida ambao watu husema, watatoa hesabu kuhusu huo Siku ya Hukumu; kwa maana kwa maneno yako wewe utatangazwa kuwa mwadilifu, na kwa maneno yako utahukumiwa.” (Mathayo 12:36, 37) Bila shaka, Mungu wa kweli atatutoza hesabu kwa yale tunayosema.

4 Njia moja bora zaidi ya kuepuka usemi wenye kuumiza ni kujizoeza kuzungumzia mambo ya kiroho. Makala hii itachunguza jinsi tunavyoweza kutenda hivyo, mambo tunayoweza kuzungumzia, na faida tunazoweza kupata kutokana na usemi wenye kujenga.

Kazia Uangalifu Yaliyo Moyoni

5. Moyo hutimizaje sehemu muhimu katika mazungumzo yenye kujenga?

5 Ili kujizoeza kuzungumza kwa njia yenye kujenga, ni lazima kwanza tutambue kwamba usemi wetu huonyesha yaliyo moyoni. Yesu alisema: “Kutoka katika wingi wa moyo kinywa husema.” (Mathayo 12:34) Kwa kawaida, sisi huzungumzia mambo yaliyo muhimu kwetu. Kwa hiyo, tunahitaji kujiuliza: ‘Mazungumzo yangu yanafunua nini kuhusu hali ya moyo wangu? Ninapokuwa pamoja na familia yangu au waamini wenzangu, je mimi huzungumzia zaidi mambo ya kiroho au wakati wote huzungumzia michezo, mavazi, sinema, chakula, vitu nilivyonunua hivi karibuni, au mambo fulani yasiyo muhimu?’ Huenda bila kujua tukawa tumeanza kukazia fikira mambo yasiyo muhimu sana maishani. Kutanguliza mambo yanayofaa kutaboresha mazungumzo na pia maisha yetu.—Wafilipi 1:10.

6. Kutafakari kunatimiza sehemu gani katika mazungumzo yetu?

6 Njia nyingine ya kuboresha jinsi tunavyosema ni kutafakari tukiwa na kusudi fulani. Tukijitahidi kufikiria mambo ya kiroho, itakuwa rahisi kuyazungumzia. Mfalme Daudi aliona jinsi mambo hayo yanavyohusiana. Aliimba hivi: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA.” (Zaburi 19:14) Naye mtunga-zaburi Asafu alisema: “Nitaitafakari kazi yako [Mungu] yote; nitaziwaza habari za matendo yako.” (Zaburi 77:12) Bila shaka, moyo na akili zinazohangaikia sana kweli za Neno la Mungu zitafurika semi zenye kusifika. Yeremia hangeweza kujizuia kusema mambo ambayo Yehova alimfundisha. (Yeremia 20:9) Inaweza kuwa vivyo hivyo kwa upande wetu ikiwa tunatafakari mambo ya kiroho kwa ukawaida.—1 Timotheo 4:15.

7, 8. Ni habari gani zinazofaa kwa mazungumzo yenye kujenga?

7 Tukiwa na mazoea mazuri ya kiroho tutakuwa na mambo mengi yenye kujenga katika mazungumzo yetu. (Wafilipi 3:16) Makusanyiko, mikutano ya kutaniko, vichapo vya hivi karibuni, na kuchunguza andiko kila siku na maelezo yaliyochapishwa, yote hayo yanatuandalia mambo mazuri ya kiroho tunayoweza kuzungumza na wengine. (Mathayo 13:52) Mambo tunayoona katika huduma ya Kikristo yanaweza kuwa yenye kusisimua kiroho kama nini!

8 Mfalme Sulemani alivutiwa sana na aina mbalimbali za miti, wanyama, ndege, na samaki aliowaona huko Israeli. (1 Wafalme 4:33) Alifurahia kuzungumzia kazi ya uumbaji ya Mungu. Tunaweza kufanya vivyo hivyo. Watumishi wa Yehova hufurahia kuongea kuhusu habari mbalimbali, lakini wakati wote kuzungumzia habari za kiroho huboresha mazungumzo ya watu wa kiroho.—1 Wakorintho 2:13.

“Endeleeni Kufikiria Mambo Haya”

9. Paulo alitoa shauri gani kwa Wafilipi?

9 Hata iwe tunazungumzia habari gani, mazungumzo yetu yatawajenga wengine ikiwa tunashikamana na shauri la mtume Paulo kwa kutaniko la Filipi. Aliandika: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa likiwako, endeleeni kufikiria mambo haya.” (Wafilipi 4:8) Mambo yanayotajwa na Paulo ni muhimu sana hivi kwamba anasema “endeleeni kufikiria mambo haya.” Tunapaswa kujaza akili na mioyo yetu mambo hayo. Basi na tuone jinsi kutoa uangalifu kwa kila moja ya mambo hayo manane yanayotajwa na Paulo kunavyoweza kutusaidia katika mazungumzo yetu.

10. Mazungumzo yetu yanawezaje kuhusisha mambo yaliyo ya kweli?

10 Yale yaliyo kweli yanatia ndani mengi zaidi ya habari zilizo sahihi na zisizo za uwongo. Yanahusu mambo yaliyo manyoofu na yenye kutumainika, kama vile kweli ya Neno la Mungu. Hivyo, tunapozungumza na wengine kuhusu kweli za Biblia zilizotufurahisha, hotuba zilizotutia moyo, au mashauri ya Kimaandiko yaliyotusaidia, tunafikiria mambo yaliyo ya kweli. Kwa upande mwingine, tunakataa ule ‘unaoitwa “ujuzi” isivyo kweli’ ambao huonekana tu kwa nje kuwa ukweli. (1 Timotheo 6:20) Nasi huepuka kueneza porojo au mambo yasiyo ya hakika ambayo hatuwezi kuthibitisha.

11. Ni mambo gani ya hangaikio zito tunayoweza kuzungumzia?

11 Mambo ya hangaikio zito ni habari zenye kuheshimika na muhimu, si upuuzi tu. Zinatia ndani mambo muhimu kuhusu huduma yetu ya Kikristo, nyakati za hatari tunamoishi, na uhitaji wetu wa kudumisha mwenendo mzuri. Tunapozungumzia mambo hayo mazito, tunaimarisha azimio letu la kubaki macho kiroho, tunadumisha uaminifu-maadili wetu, na tunaendelea kuhubiri habari njema. Kwa kweli, mambo yenye kupendeza tunayoona katika huduma yetu na matukio ya hivi karibuni yanayotukumbusha kwamba tunaishi katika siku za mwisho, yanatuandalia habari mbalimbali kwa ajili ya mazungumzo yenye kusisimua.—Matendo 14:27; 2 Timotheo 3:1-5.

12. Kulingana na shauri la Paulo kuhusu kufikiria mambo yaliyo ya uadilifu na yaliyo safi kiadili, ni mambo gani yanayopaswa kuepukwa?

12 Neno uadilifu linamaanisha kuwa mwenye haki machoni pa Mungu, yaani, kutimiza viwango vyake. Mambo yaliyo safi kiadili yanatoa wazo la utakato katika mawazo na mwenendo. Uchongezi, mizaha michafu, au kusema kwa mafumbo habari za ngono ni mambo yasiyofaa kabisa katika mazungumzo yetu. (Waefeso 5:3; Wakolosai 3:8) Wanapokuwa kazini au shuleni, kwa hekima Wakristo huondoka mazungumzo yanapoanza kuhusisha mambo ya namna hiyo.

13. Taja mifano ya mazungumzo yanayokazia mambo yenye kupendeka na kusemwa vema.

13 Paulo anapopendekeza kufikiria mambo yenye kupendeka, anazungumzia mambo yenye kupendeza na mazuri au yanayochochea upendo, badala ya yale yanayoamsha chuki, uchungu, au ugomvi. Mambo yenye kusemwa vema yanahusu habari nzuri au zinazofaa. Habari hizo nzuri ambazo hupatikana kwa ukawaida katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinatia ndani masimulizi ya maisha ya akina ndugu na dada waaminifu. Mbona usiwaambie wengine maoni yako baada ya kusoma makala hizo zenye kuimarisha imani? Inatia moyo kama nini kusikia mambo ya kiroho ambayo wengine wametimiza! Mazungumzo kama hayo yatakuza upendo na umoja kutanikoni.

14. (a) Tunahitaji nini ili kuonyesha wema wa kiadili? (b) Mazungumzo yetu yanawezaje kutia ndani mambo yanayostahili sifa?

14 Paulo anazungumzia “wema wa adili wowote ulioko.” Wema wa adili humaanisha wema au ubora wa kiadili. Tunapaswa kuangalia kwamba usemi wetu unaongozwa na kanuni za Kimaandiko na kwamba haukengeuki kutoka kwa mambo yaliyo ya adili, safi na mema kiadili. Lolote la kustahili sifa humaanisha “jambo lenye kusifika.” Ukisikia hotuba nzuri au ukiona mtu mwenye mfano mzuri wa uaminifu kutanikoni, taja jambo hilo, kwa mtu huyo na kwa wengine pia. Mara nyingi mtume Paulo aliwasifu waabudu wenzake waliokuwa na sifa nzuri. (Waroma 16:12; Wafilipi 2:19-22; Filemoni 4-7) Na bila shaka, kazi ya mikono ya Muumba wetu inastahili sifa. Katika uumbaji tunapata habari nyingi kwa ajili ya mazungumzo yenye kujenga.—Mithali 6:6-8; 20:12; 26:2.

Shiriki Katika Mazungumzo Yenye Kujenga

15. Ni amri gani ya Kimaandiko inayoonyesha kwamba wazazi wanapaswa kuwa na mazungumzo yanayofaa pamoja na watoto wao?

15 Andiko la Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 linasema: “Maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Bila shaka, amri hii inaonyesha kwamba wazazi wanapaswa kuwa na mazungumzo yanayofaa na ya kiroho pamoja na watoto wao.

16, 17. Wazazi Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na vielelezo vya Yehova na Abrahamu?

16 Tunaweza kuwazia mazungumzo marefu ambayo Yesu alikuwa nayo pamoja na Baba yake wa mbinguni kuhusu mgawo wake duniani. “Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu lile la kunena na lile la kusema.” (Yohana 12:49; Kumbukumbu la Torati 18:18) Ni lazima Abrahamu mzee wa ukoo alitumia muda mrefu kuzungumza na mwanaye Isaka kuhusu jinsi Yehova alivyowabariki wao na babu zao. Kwa hakika, mazungumzo kama hayo yaliwasaidia Yesu na Isaka kujitiisha kwa unyenyekevu chini ya mapenzi ya Mungu.—Mwanzo 22:7-9; Mathayo 26:39.

17 Watoto wetu pia wanahitaji mazungumzo yenye kujenga. Ni lazima wazazi watafute wakati katika ratiba yao yenye shughuli nyingi ili kuzungumza na watoto wao. Ikiwezekana, kwa nini msipange kula pamoja mkiwa familia angalau mara moja kwa siku? Mnapokula na baada ya hapo, mtakuwa na nafasi nyingi za kuzungumzia mambo yenye kujenga yanayoweza kuboresha sana hali ya kiroho ya familia.

18. Eleza jambo linaloonyesha faida ya mawasiliano mazuri kati ya wazazi na watoto.

18 Alejandro, ambaye ni painia mwenye umri wa miaka 20 na kitu, anakumbuka shaka alizokuwa nazo akiwa na umri wa miaka 14. Anasema: “Kwa sababu ya uvutano wa wanashule na walimu, nilikuwa na shaka juu ya kuwapo kwa Mungu na juu ya usahihi wa Biblia. Wazazi wangu walitumia wakati mwingi kujadiliana nami kwa subira. Mazungumzo hayo yalinisaidia kushinda shaka zangu wakati huo wa magumu na pia kufanya maamuzi mazuri maishani mwangu.” Namna gani sasa? Alejandro anaendelea: “Bado ninaishi nyumbani. Lakini kwa sababu tuna shughuli nyingi, si rahisi mimi na baba yangu kuzungumza faraghani. Kwa hiyo, sisi wawili hula pamoja mara moja kwa juma kazini kwake. Ninathamini sana mazungumzo hayo.”

19. Kwa nini sote tunahitaji mazungumzo ya kiroho?

19 Je, sisi pia hatuthamini kuwa na nafasi za mazungumzo ya kiroho yenye kuthawabisha pamoja na waamini wenzetu? Tunapata nafasi hizo kwenye mikutano, katika utumishi wa shambani, katika vikusanyiko vya kirafiki, na tunaposafiri. Paulo alikuwa na hamu nyingi ya kuzungumza na Wakristo huko Roma. Aliwaandikia hivi: “Nina hamu sana ya kuwaona nyinyi, kwamba kupate kuwa na badilishano la kitia-moyo miongoni mwenu, kwa kila mmoja kupitia imani ya mwingine, yenu na yangu pia.” (Waroma 1:11, 12) Johannes mzee Mkristo anasema, “mazungumzo ya kiroho pamoja na Wakristo wenzetu hutimiza uhitaji muhimu. Huchangamsha moyo na kupunguza mahangaiko ya kila siku. Mara nyingi mimi huwauliza walio wazee waniambie juu ya maisha yao na kinachowawezesha kuendelea kuwa waaminifu. Kwa miaka mingi nimezungumza na wengi, na nimepata hekima na ujuzi kutoka kwa kila mmoja wao ambao umeyaboresha maisha yangu.”

20. Tunaweza kufanya nini ikiwa tutakutana na mtu mwenye haya?

20 Namna gani ikiwa mtu anaonekana hapendezwi unapotaka kuzungumzia habari za kiroho? Usikate tamaa. Labda unaweza kutafuta wakati unaofaa baadaye. Sulemani alisema: “Neno linenwalo wakati wa kufaa, ni kama machungwa katika vyano vya fedha.” (Mithali 25:11) Wajali wenye haya. “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” * (Mithali 20:5) Zaidi ya yote, usiruhusu kamwe mitazamo ya wengine ikuzuie kuzungumzia mambo yanayokugusa moyo.

Mazungumzo ya Kiroho Huthawabisha

21, 22. Tunapata faida gani tunaposhiriki katika mazungumzo ya kiroho?

21 Paulo alishauri: “Msiache usemi uliooza utoke kinywani mwenu, bali usemi wowote ule ulio mwema kwa ajili ya kujenga kama vile kuwezavyo kuwa na uhitaji, ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.” (Waefeso 4:29; Waroma 10:10) Huenda ikahitaji jitihada kubadili mazungumzo na kuzungumzia mambo yafaayo, lakini kuna manufaa nyingi kufanya hivyo. Mazungumzo ya kiroho hutuwezesha kuwaeleza wengine imani yetu na kuwajenga ndugu zetu.

22 Basi na tutumie zawadi ya usemi kuwaimarisha wengine na kumsifu Mungu. Mazungumzo kama hayo yataturidhisha na kuwatia moyo wengine. Zaidi ya yote, yatafurahisha moyo wa Yehova kwa sababu yeye husikiliza mazungumzo yetu naye hufurahi tunapotumia ulimi wetu kwa njia inayofaa. (Zaburi 139:4; Mithali 27:11) Mazungumzo yetu yanapokuwa ya kiroho, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatatusahau. Biblia inasema hivi inapozungumzia wale wanaomtumikia Yehova leo: “Ndipo wale waliomcha BWANA waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha BWANA, na kulitafakari jina lake.” (Malaki 3:16; 4:5) Ni muhimu kama nini kwamba mazungumzo yetu yawe yenye kujenga kiroho!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Visima fulani huko Israeli vilikuwa virefu sana. Huko Gibeoni waakiolojia waligundua tangi kubwa lenye urefu wa meta 25 hivi. Lilikuwa na ngazi iliyowawezesha watu kuteremka mpaka chini ili kuteka maji.

Ungejibuje?

• Mazungumzo yetu hufunua nini kutuhusu?

• Tunaweza kuzungumzia mambo gani yenye kujenga?

• Mazungumzo yanatimiza sehemu gani muhimu katika familia na katika kutaniko la Kikristo?

• Mazungumzo yenye kujenga yanaleta faida gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mazungumzo yenye kujenga hukazia  . . .

“mambo yoyote yaliyo ya kweli”

“mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito”

“jambo lolote la kustahili sifa likiwako”

“mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema”

[Picha zimeandaliwa]

Video cover, Stalin: U.S. Army photo; Creator book cover, Eagle Nebula: J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakati wa chakula hutoa nafasi nzuri sana ya kuwa na mazungumzo ya kiroho