Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ahadi Zitakapotimizwa

Wakati Ahadi Zitakapotimizwa

Wakati Ahadi Zitakapotimizwa

HISTORIA imejaa ahadi nyingi ambazo hazikutimizwa. Mara nyingi mataifa yameshindwa kutimiza mikataba mizito ya kutoshambuliana, na hivyo kuwafanya watu wao wapigane vita vibaya. Wakati mmoja Napoleon alisema: “Serikali hutimiza ahadi zao zinapolazimishwa kufanya hivyo, au ikiwa zenyewe zitanufaika.”

Namna gani ahadi zinazofanywa na watu mmoja-mmoja? Inavunja moyo kama nini mtu anaposhindwa kutimiza ahadi aliyotoa! Inakuwa hivyo hasa ikiwa unamjua na kumtumaini mtu huyo. Bila shaka, inaonekana watu wameshindwa au hawataki kutimiza ahadi zao.

Ahadi za wanadamu na za Mungu zinatofautiana kama nini! Ahadi za Mungu zinategemeka na kutumainika kabisa. Ahadi yoyote iliyotolewa na Yehova Mungu ni lazima itimie. Likizungumzia Neno la Mungu ambalo halikosi kutimia, andiko la Isaya 55:11 linasema: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”

Hivyo basi, tunapaswa kuzionaje ahadi za Mungu zilizo katika Biblia? Bila shaka tunaweza kuzitegemea. Kwa mfano, mtume Yohana aliandika: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Unaweza kupata baraka hizo ukitenda kupatana na maneno haya ya Yesu: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.