Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu

Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu

Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu

“Wenye furaha ni wale ambao wamenyanyaswa kwa ajili ya uadilifu.”—MATHAYO 5:10.

1. Kwa nini Yesu alikuwa mbele ya Pontio Pilato, naye alisema nini?

“KWA ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu alisema maneno hayo akiwa mbele ya Pontio Pilato, Gavana Mroma wa Yudea. Yeye hakuwa hapo kwa mwaliko wa Pilato au kwa sababu alikuwa ameamua kwenda hapo. Lakini, Yesu alijikuta hapo kwa sababu viongozi wa dini ya Kiyahudi walikuwa wamemshtaki kwa uwongo kuwa mkosaji aliyestahili kifo.—Yohana 18:29-31.

2. Yesu alichukua hatua gani, na matokeo yakawaje?

2 Yesu alijua vizuri sana kwamba Pilato alikuwa na mamlaka ya kumwachilia au kumuua. (Yohana 19:10) Lakini jambo hilo halikumzuia asizungumze na Pilato kwa ujasiri kuhusu Ufalme. Ingawa maisha ya Yesu yalikuwa hatarini, alitumia nafasi hiyo kumtolea ushahidi mtu aliyekuwa na mamlaka kubwa zaidi ya kiserikali katika eneo hilo. Ijapokuwa alitoa ushahidi huo, Yesu alihukumiwa na kuuawa. Aliuawa kifo chenye maumivu makali kwenye mti wa mateso kwa ajili ya imani yake.—Mathayo 27:24-26; Marko 15:15; Luka 23:24, 25; Yohana 19:13-16.

Shahidi au Mfia-Imani?

3. Neno “mfia-imani” lilimaanisha nini nyakati za Biblia, lakini linamaanisha nini leo?

3 Leo watu wengi humwona mfia-imani kuwa mtu aliye na imani kali au msimamo mkali kuhusu dini. Mara nyingi watu walio tayari kufa kwa ajili ya imani yao, hasa imani ya kidini, hutuhumiwa kuwa magaidi au watu hatari katika jamii. Hata hivyo, nyakati za Biblia neno la Kigiriki (marʹtys) ambalo linatafsiriwa mfia-imani lilimaanisha “shahidi,” yaani, mtu ambaye hutoa ushuhuda, labda katika kesi ya mahakama, kuhusu yale anayoamini kuwa kweli. Hata hivyo, baadaye neno hilo lilitumiwa kumaanisha “mtu ambaye hutoa uhai wake kwa sababu ya kutoa ushahidi,” au hata kufa ili atoe ushahidi.

4. Neno la Kigiriki marʹtys lilitumiwa hasa katika maana gani kumhusu Yesu?

4 Kumhusu Yesu, neno la Kigiriki marʹtys lilitumiwa hasa kumaanisha mtu anayetoa ushahidi. Yesu alimwambia Pilato kwamba alikuja ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ Watu waliitikia ushahidi wake kwa njia mbalimbali. Baadhi ya watu wa kawaida waliguswa moyo sana na mambo waliyosikia na kuona, na hivyo wakamwamini Yesu. (Yohana 2:23; 8:30) Watu kwa ujumla na hasa viongozi wa kidini waliitikia ujumbe kwa njia isiyofaa kwa kuupinga vikali. Yesu aliwaambia hivi jamaa zake wasioamini: “Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia nyinyi, lakini huo wanichukia mimi, kwa sababu natoa ushahidi kuhusu huo kwamba kazi zao ni mbovu.” (Yohana 7:7) Yesu alichukiwa na kuuawa na viongozi wa taifa kwa sababu ya kutoa ushahidi kuhusu kweli. Naam, alikuwa “shahidi mwaminifu na wa kweli (marʹtys).”—Ufunuo 3:14.

“Mtakuwa Vitu vya Kuchukiwa”

5. Mapema katika huduma yake, Yesu alisema nini kuhusu mnyanyaso?

5 Yesu mwenyewe alinyanyaswa vikali naye aliwaonya wafuasi wake kwamba wangenyanyaswa pia. Mapema katika huduma yake, Yesu aliwaambia hivi wasikilizaji wake katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale ambao wamenyanyaswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao. Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa katika mbingu.”—Mathayo 5:10-12.

6. Yesu alitoa onyo gani alipowatuma wale mitume 12?

6 Baadaye, alipowatuma mitume 12, Yesu aliwaambia hivi: “Jilindeni dhidi ya watu; kwa maana watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” Lakini wanafunzi wa Yesu hawangenyanyaswa tu na viongozi wa kidini. Yesu pia alisema: “Ndugu atakabidhi ndugu kwenye kifo, na baba mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe. Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 10:17, 18, 21, 22) Mambo yaliyowapata Wakristo wa karne ya kwanza yanathibitisha kwamba maneno hayo ni kweli.

Habari Kuhusu Watu Waliovumilia kwa Uaminifu

7. Ni nini kilichofanya Stefano afe kwa ajili ya imani?

7 Muda mfupi baada ya Yesu kufa, Stefano ndiye aliyekuwa Mkristo wa kwanza kufa kwa sababu ya kutoa ushahidi kuhusu kweli. Alikuwa “mwenye kujaa wema na nguvu, [na] alikuwa akifanya mambo makubwa ya ajabu na ishara miongoni mwa watu.” Maadui wake wa kidini “hawakuweza kufaulu katika pambano dhidi ya hekima na roho aliyokuwa akisema kwayo.” (Matendo 6:8, 10) Kwa kujawa na wivu, walimburuta Stefano mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Kiyahudi ambapo alikabili watu waliomshtaki kwa uwongo na kuwatolea ushahidi wenye nguvu. Hata hivyo, mwishowe maadui wa Stefano walimuua shahidi huyo mwaminifu.—Matendo 7:59, 60.

8. Wanafunzi waliokuwa Yerusalemu walitendaje waliponyanyaswa baada ya Stefano kuuawa?

8 Baada ya Stefano kuuawa, “mnyanyaso mkubwa ulitokea dhidi ya kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu; wote isipokuwa mitume walitawanywa kotekote katika mikoa ya Yudea na Samaria.” (Matendo 8:1) Je, mnyanyaso ulikomesha kazi ya Kikristo ya kutoa ushahidi? La, kwa kuwa tunaelezwa kwamba “wale waliokuwa wametawanywa walipita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:4) Bila shaka, walihisi kama mtume Petro alivyohisi aliposema hivi awali: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Ijapokuwa walinyanyaswa, wanafunzi hao waaminifu na wenye ujasiri waliendelea na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu kweli, hata ingawa walijua kwamba wangepatwa na magumu zaidi kwa kufanya hivyo.—Matendo 11:19-21.

9. Wafuasi wa Yesu waliendelea kupatwa na mnyanyaso gani?

9 Bila shaka, wanafunzi hao waliendelea kupatwa na magumu. Kwanza, tunaona kwamba Sauli, aliyeshuhudia na kuunga mkono wakati Stefano alipokuwa akipigwa mawe, alikuwa ‘bado anapumua tisho na uuaji-kimakusudi dhidi ya wanafunzi wa Bwana, alipomwendea kuhani wa cheo cha juu na kumwomba barua za kwenda kwenye masinagogi katika Damasko, ili apate kuwaleta hadi Yerusalemu wakiwa wamefungwa wowote ambao angewapata walio wa Ile Njia, wanaume na pia wanawake.’ (Matendo 9:1, 2) Kisha, yapata mwaka wa 44 W.K., “Herode mfalme alitumia mikono yake kutenda vibaya baadhi ya wale wa kutaniko. Alimmaliza Yakobo ndugu ya Yohana kwa upanga.”—Matendo 12:1, 2.

10. Tunapata habari gani kuhusu mnyanyaso katika kitabu cha Matendo na Ufunuo?

10 Sura zilizosalia za kitabu cha Matendo zina habari zisizoweza kusahaulika kuhusu majaribu, vifungo vya gerezani, na mnyanyaso uliowapata watu waaminifu kama vile Paulo, ambaye hapo awali alikuwa mnyanyasaji kabla ya kuwa mtume. Yaelekea mwaka wa 65 W.K. hivi, Maliki Mroma Nero, aliamuru mtume huyo auawe kwa ajili ya imani yake. (2 Wakorintho 11:23-27; 2 Timotheo 4:6-8) Mwishowe, katika kitabu cha Ufunuo kilichoandikwa karne ya kwanza ikikaribia kwisha, tunaona kwamba mtume Yohana aliyekuwa mzee alifungwa kwenye kisiwa cha kuadhibia wafungwa cha Patmosi “kwa ajili ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” Kitabu cha Ufunuo pia kinamtaja “Antipasi, shahidi wangu, aliye mwaminifu, aliyeuawa” huko Pergamamu.—Ufunuo 1:9; 2:13.

11. Maisha ya Wakristo wa mapema yalithibitishaje ukweli wa maneno ya Yesu kuhusu mnyanyaso?

11 Minyanyaso hiyo yote ilithibitisha ukweli wa maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” (Yohana 15:20) Wakristo waaminifu wa mapema walikuwa tayari kukabiliana na jaribu kuu zaidi ambalo ni kuuawa—kwa kuteswa, kutupiwa wanyama, au kwa njia nyinginezo—ili kufanya kazi hii ambayo Bwana Yesu Kristo aliwapa: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.

12. Kwa nini kunyanyaswa kwa Wakristo si jambo lililotokea wakati wa zamani tu?

12 Mtu yeyote akifikiri kwamba wafuasi wa Yesu walinyanyaswa kikatili wakati wa zamani tu, atakuwa amekosea sana. Paulo, ambaye kama tulivyoona alivumilia magumu, aliandika hivi: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Petro alisema hivi kuhusu mnyanyaso: “Kwa kweli, kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Tangu wakati huo hadi ‘siku hizi za mwisho’ za mfumo huu wa mambo, watu wa Yehova wanaendelea kuwa vitu vya kuchukiwa na kuonyeshwa uadui. (2 Timotheo 3:1) Katika sehemu zote za dunia, Mashahidi wa Yehova wamenyanyaswa wakati fulani chini ya utawala wa kimabavu na katika nchi za kidemokrasia wakiwa mtu mmoja-mmoja au kikundi.

Kwa Nini Wanachukiwa na Kunyanyaswa?

13. Watumishi wa Yehova wa sasa wanapaswa kukumbuka nini kuhusu mnyanyaso?

13 Hata ingawa wengi wetu leo tunafurahia uhuru wa kadiri wa kuhubiri na kukutana pamoja kwa amani, lazima tusikilize kikumbusho cha Biblia kwamba “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31) Mambo yanaweza kubadilika kwa ghafula hivi kwamba tusipojitayarisha kiakili, kihisia, na kiroho, tunaweza kukwazwa kwa urahisi. Kwa hiyo, tunapaswa kufanya nini ili kujilinda? Njia nzuri zaidi ya kujilinda ni kukumbuka sababu inayofanya Wakristo wanaopenda amani na kutii sheria wachukiwe na kunyanyaswa.

14. Petro alisema Wakristo walinyanyaswa kwa sababu gani?

14 Mtume Petro alizungumzia jambo hilo katika barua yake ya kwanza aliyoandika yapata mwaka wa 62-64 W.K., wakati Wakristo katika Milki yote ya Roma walipokuwa wakikabili majaribu na mnyanyaso. Alisema: “Wapendwa, msitatanishwe juu ya kuwaka miongoni mwenu, ambako kunatukia kwenu kuwa jaribu, kama kwamba jambo geni linawapata.” Ili kufafanua jambo alilokuwa akizungumzia, Petro aliendelea kusema: “Acheni mmoja wenu asiteseke akiwa muuaji-kimakusudi au mwizi au mtenda-maovu au akiwa mjishughulishaji katika mambo ya watu wengine. Lakini ikiwa ateseka akiwa Mkristo, acheni asione aibu, bali acheni afulize kumtukuza Mungu katika jina hili.” Petro alisema kwamba waliteseka kwa sababu walikuwa Wakristo wala si kwa sababu walitenda makosa yoyote. Kama wangalikuwa wamejitia katika “dimbwi lilelile la chini la ufasiki” kama watu waliowazunguka, basi wangekubalika kwa watu hao. Lakini ukweli ni kwamba waliteseka kwa sababu walijitahidi kutimiza daraka lao wakiwa wafuasi wa Kristo. Hali ya Wakristo wa kweli leo inafanana na hiyo.—1 Petro 4:4, 12, 15, 16.

15. Kwa nini leo Mashahidi wa Yehova hupigwa marufuku na kudhulumiwa ingawa wana mwenendo mzuri?

15 Katika sehemu nyingi duniani, Mashahidi wa Yehova husifiwa hadharani kwa umoja na muungano wanaoonyesha kwenye makusanyiko yao na kwenye miradi ya ujenzi, kwa unyoofu na bidii yao, kwa maadili yao na maisha mazuri ya familia, na hata kwa mavazi na mwenendo wao mzuri. * Kwa upande mwingine, wakati makala hii ilipoandikwa, bado kulikuwa na marufuku au vizuizi katika nchi 28, na Mashahidi wengi wanadhulumiwa na kupoteza mali yao kwa ajili ya imani yao. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hupigwa marufuku na kudhulumiwa ingawa wana mwenendo mzuri? Na kwa nini Mungu huruhusu jambo hilo?

16. Sababu kuu ambayo humfanya Mungu aruhusu watu wake wanyanyaswe ni gani?

16 Tunapaswa kukumbuka hasa maneno ya Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Naam, tunanyanyaswa kwa sababu ya suala lililozushwa zamani linalohusu enzi kuu ya ulimwengu wote. Ingawa ushuhuda mwingi sana umetolewa na wote walioshika uaminifu-maadili kwa Yehova katika karne zilizopita, bado Shetani anaendelea kumdhihaki Yehova kama alivyofanya siku za Ayubu mwadilifu. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Bila shaka, Shetani amekuwa na pirikapirika nyingi zaidi katika jitihada yake ya mwisho ya kuthibitisha dai lake, kwa kuwa sasa Ufalme wa Mungu umesimamishwa imara, nao una raia waaminifu na wawakilishi duniani pote. Je, raia hao wataendelea kuwa waaminifu kwa Mungu hata wakipatwa na matatizo na magumu? Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujibu kibinafsi swali hilo.—Ufunuo 12:12, 17.

17. Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba “itageuka kwenu kuwa ushahidi”?

17 Alipowaambia wanafunzi wake mambo ambayo yangetukia wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alionyesha sababu nyingine inayomfanya Yehova aruhusu watumishi wake wanyanyaswe. Aliwaambia hivi: ‘Mtaburutwa mbele ya wafalme na magavana kwa ajili ya jina langu. Itageuka kwenu kuwa ushahidi.’ (Mathayo 24:3, 9; Luka 21:12, 13) Yesu mwenyewe alitoa ushahidi mbele ya Herode na Pontio Pilato. Mtume Paulo pia ‘aliburutwa mbele ya wafalme na magavana.’ Kwa mwongozo wa Bwana Yesu Kristo, Paulo alitafuta njia ya kumtolea ushahidi mtawala aliyekuwa na mamlaka kuu zaidi wakati huo aliposema: “Mimi nakata rufani kwa Kaisari!” (Matendo 23:11; 25:8-12) Vivyo hivyo leo, mara nyingi hali ngumu zimefanya iwezekane kuwatolea ushahidi maofisa na watu kwa ujumla kwa njia nzuri. *

18, 19. (a) Kuvumilia majaribu kunaweza kutunufaishaje? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?

18 Kwa kumalizia, tunaweza kunufaika kwa kuvumilia majaribu na dhiki. Jinsi gani? Mwanafunzi Yakobo aliwakumbusha Wakristo wenzake hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.” Ndiyo, mnyanyaso unaweza kuboresha imani yetu na kufanya tuwe na uvumilivu zaidi. Hivyo, hatuogopi mnyanyaso, wala hatutafuti njia zisizo za Kimaandiko ili kuuepuka au kuukomesha. Badala yake, tunatii shauri la Yakobo: “Acheni uvumilivu uwe na kazi yao ikiwa kamili, ili nyinyi mpate kuwa kamili na timamu katika mambo yote, bila ukosefu katika kitu chochote.”—Yakobo 1:2-4.

19 Hata ingawa Neno la Mungu hutusaidia kuelewa kwa nini watumishi waaminifu wa Mungu hunyanyaswa na kwa nini Yehova huruhusu mnyanyaso, jambo hilo halifanyi iwe rahisi kuvumilia. Ni nini kinachoweza kutuimarisha ili kuuvumilia? Tunaweza kufanya nini tunaponyanyaswa? Tutazungumzia mambo hayo muhimu katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1995, ukurasa wa 27-29; Aprili 15, 1994, ukurasa wa 16-17; na Amkeni! la Desemba 22, 1993, ukurasa wa 6-13.

Je, Unaweza Kueleza?

• Neno la Kigiriki marʹtys lilitumiwa hasa katika maana gani kumhusu Yesu?

• Mnyanyaso uliwaathirije Wakristo katika karne ya kwanza?

• Kama Petro alivyoeleza, kwa nini Wakristo wa kweli walinyanyaswa?

• Ni sababu gani ambazo hufanya Yehova aruhusu watumishi wake wanyanyaswe?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Wakristo wa karne ya kwanza waliteseka, kwa sababu walikuwa Wakristo wala si kwa sababu walitenda makosa yoyote

PAULO

YOHANA

ANTIPASI

YAKOBO

STEFANO