Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa

Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa

Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa

“Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.”—1 PETRO 2:20.

1. Kwa kuwa Wakristo wa kweli wanahangaikia kuishi kupatana na wakfu wao, ni swali gani linalopaswa kufikiriwa?

WAKRISTO wamejiweka wakfu kwa Yehova nao wanataka kufanya mapenzi yake. Ili kuishi kupatana na wakfu wao, wao hujitahidi kadiri wawezavyo kufuata hatua za Yesu Kristo aliye Kielelezo chao, na hutoa ushahidi kuhusu kweli. (Mathayo 16:24; Yohana 18:37; 1 Petro 2:21) Hata hivyo, Yesu na watu wengine waaminifu walikufa kwa ajili ya imani yao. Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo wote watarajie kufa kwa ajili ya imani yao?

2. Wakristo huyaonaje majaribu na mateso?

2 Tukiwa Wakristo tunahimizwa tuwe waaminifu mpaka kifo, lakini si lazima tufe kwa ajili ya imani. (2 Timotheo 4:7; Ufunuo 2:10) Hilo linamaanisha kwamba hatungependa kufa hata ingawa tuko tayari kuteseka—na ikiwa lazima, kufa—kwa ajili ya imani yetu. Hatufurahii kuteseka wala hatufurahii kupatwa na maumivu na kufedheheshwa. Hata hivyo, kwa kuwa tunatarajia majaribu na mnyanyaso, tunahitaji kufikiria kwa makini jinsi tunavyoweza kutenda tunapopatwa na mambo hayo.

Waaminifu Chini ya Jaribu

3. Unaweza kusimulia mifano ya watu gani katika Biblia ambao walikabiliana na mnyanyaso? (Ona sanduku “Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso,” kwenye ukurasa unaofuata.)

3 Katika Biblia, tunapata masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi watumishi wa Mungu wa zamani walivyotenda walipokabili hali zilizohatarisha maisha yao. Watumishi hao walitenda kwa njia mbalimbali ambazo zinaweza kuwasaidia Wakristo leo wakipatwa na hali kama hizo. Soma masimulizi mbalimbali kwenye sanduku lenye kichwa “Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso,” na uone ni mambo gani unayoweza kujifunza kutokana nayo.

4. Tunaweza kusema nini kuhusu jinsi Yesu na watumishi wengine waaminifu walivyotenda walipopatwa na majaribu?

4 Waliponyanyaswa, Yesu na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walitenda kwa njia mbalimbali ikitegemea hali. Lakini ni wazi kwamba hawakuhatarisha maisha yao isivyo lazima. Walipojikuta katika hali hatari, walikuwa jasiri lakini wenye kujihadhari. (Mathayo 10:16, 23) Walikuwa na lengo la kuendelea kuhubiri na kudumisha uaminifu-maadili wao kwa Yehova. Matendo yao katika hali mbalimbali ni mfano mzuri kwa Wakristo ambao leo wanakabiliana na majaribu na minyanyaso.

5. Ni mnyanyaso gani uliotokea Malawi miaka ya 1960, nao Mashahidi wa nchi hiyo walitendaje?

5 Leo, mara nyingi watu wa Yehova hujikuta katika hali ngumu sana na umaskini kwa sababu ya vita, marufuku, au kunyanyaswa. Kwa mfano katika miaka ya 1960 Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa kikatili nchini Malawi. Majumba yao ya Ufalme, nyumba, vyakula, na biashara zao, yaani, vitu vyote walivyokuwa navyo viliharibiwa. Walipigwa na kutendewa mambo mengine yenye kusikitisha. Ndugu hao walitendaje? Maelfu walikimbia vijiji vyao. Wengi walikimbilia msituni, huku wengine wakihamia nchi jirani ya Msumbiji kwa muda. Ingawa ndugu wengi waaminifu walikufa, wengine waliamua kukimbia eneo lenye hatari, hatua ambayo yaonekana ilifaa kuchukuliwa katika hali hizo. Kwa kufanya hivyo, ndugu hao waliiga kielelezo cha Yesu na Paulo.

6. Ni nini ambacho Mashahidi wa Malawi hawakuacha kufanya kujapokuwa mnyanyaso mkali?

6 Hata ingawa ndugu wa Malawi walilazimika kuhama au kujificha, walitafuta na kufuata mwongozo wa kiroho nao waliendelea kufanya kazi ya Kikristo kisiri kadiri walivyoweza. Ikawaje? Kulikuwa na kilele cha watangazaji wa Ufalme 18,519 kabla tu ya marufuku iliyotokea mwaka wa 1967. Kufikia mwaka wa 1972 kulikuwa na kilele kipya cha watangazaji 23,398 ingawa marufuku ilikuwa bado haijaondolewa na wengi walikuwa wamekimbilia Msumbiji. Walihubiri kwa wastani wa saa zaidi ya 16 kila mwezi. Bila shaka, walimletea Yehova sifa kwa jinsi walivyotenda, naye aliwabariki ndugu hao waaminifu wakati huo mgumu sana. *

7, 8. Ni kwa sababu gani wengine huamua kutokimbia, hata ingawa upinzani unaleta matatizo?

7 Kwa upande mwingine, katika nchi ambako upinzani unaleta matatizo, huenda baadhi ya akina ndugu wakaamua wasikimbie, hata ingawa wanaweza kufanya hivyo. Huenda kukimbia kukatatua matatizo fulani, lakini kunaweza kusababisha magumu mengine. Kwa mfano, je, wataweza kudumisha mawasiliano na ndugu zao Wakristo na wasitengwe nao kiroho? Je, wataweza kuendelea na programu yao ya kawaida ya mambo ya kiroho huku wakijitahidi kuanza maisha mapya, labda katika nchi tajiri au nchi ambako wanaweza kujipatia vitu vingi vya kimwili?—1 Timotheo 6:9.

8 Wengine huamua kutokimbia kwa sababu wanajali hali ya kiroho ya ndugu zao. Wao huamua kubaki na kukabiliana na hali ili waendelee kuhubiri katika maeneo ya kwao na kuwatia moyo waabudu wenzao. (Wafilipi 1:14) Kwa kuamua kufanya hivyo, mwishowe wengine wameweza kuchangia kushinda kesi kadhaa katika nchi zao. *

9. Mtu anapaswa kufikiria mambo gani anapoamua kama atabaki au atakimbia kwa sababu ya mnyanyaso?

9 Kwa kweli uamuzi wa kukimbia au kubaki ni wa mtu binafsi. Bila shaka, maamuzi hayo yanapaswa kufanywa baada ya kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala. Lakini, hata tuamue kufanya nini, tunapaswa kukumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Kama tulivyoona awali, Yehova anataka kila mmoja wa watumishi wake aendelee kuwa mwaminifu katika hali zote. Leo, baadhi ya watumishi wake wanapatwa na majaribu na mnyanyaso na huenda wengine wakapatwa na mambo hayo baadaye. Wote watajaribiwa kwa njia moja au nyingine, na hakuna yeyote anayepaswa kufikiri kwamba hawezi kupatwa na majaribu. (Yohana 15:19, 20) Tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu hatuwezi kuepuka lile suala la ulimwenguni pote linalohusu kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi yake kuu.—Ezekieli 38:23; Mathayo 6:9, 10.

“Msirudishe Ovu kwa Ovu kwa Yeyote”

10. Yesu na mitume wake walituwekea kielelezo gani muhimu katika kukabiliana na mikazo na upinzani?

10 Kanuni nyingine muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi Yesu na mitume walivyotenda chini ya mkazo ni kwamba hatupaswi kulipiza kisasi dhidi ya watu wanaotunyanyasa. Biblia haisemi popote kwamba Yesu na wafuasi wake waliunda kikundi fulani cha upinzani au kutumia jeuri ili kupambana na watu waliowanyanyasa. Kinyume cha hilo, mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. . . . Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’” Isitoshe, “usijiache mwenyewe ushindwe na lililo ovu, bali fuliza kushinda lililo ovu kwa lililo jema.”—Waroma 12:17-21; Zaburi 37:1-4; Mithali 20:22.

11. Mwanahistoria mmoja anasema nini kuhusu mtazamo wa Wakristo wa mapema kuelekea Serikali?

11 Wakristo wa mapema walitii shauri hilo. Katika kitabu chake The Early Church and the World, mwanahistoria Cecil J. Cadoux anaeleza mtazamo wa Wakristo kuelekea Serikali katika miaka ya 30-70 W.K. Anaandika hivi: “Hatuna uthibitisho wowote kwamba wakati huo Wakristo walitumia jeuri ili kupinga mnyanyaso. Jambo ambalo Wakristo walifanya ni kuwashutumu tu watawala au kuwatatanisha kwa kukimbia. Kwa kawaida Wakristo walikataa kwa upole lakini kwa uthabiti kutii maagizo ya serikali ambayo waliamini yalipingana na utii wao kwa Kristo.”

12. Kwa nini inafaa kuvumilia mateso kuliko kulipiza kisasi?

12 Je, ni jambo la hekima kwa Wakristo kuvumilia tu mateso bila kujitetea? Je, kutojitetea hakungefanya iwe rahisi kwa wale walio na nia ya kuwaangamiza Wakristo wafanye hivyo? Je, halingekuwa jambo la hekima kujitetea? Huenda jambo hilo likaonekana kuwa la hekima kulingana na maoni ya mwanadamu. Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Yehova tuna hakika kwamba njia iliyo bora zaidi ni kufuata mwongozo wa Yehova katika mambo yote. Sisi hukumbuka maneno haya ya Petro: “Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.” (1 Petro 2:20) Tuna hakika kwamba Yehova anajua vizuri hali ilivyo naye hatairuhusu iendelee milele. Tunawezaje kuwa na hakika kuhusu jambo hilo? Yehova aliwaambia hivi watu wake waliokuwa utumwani Babiloni: ‘Yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho langu.’ (Zekaria 2:8) Hakuna mtu awezaye kuruhusu mboni ya jicho lake iguswe kwa muda mrefu. Yehova ataleta kitulizo wakati unaofaa. Hatuna shaka lolote kwamba atafanya hivyo.—2 Wathesalonike 1:5-8.

13. Kwa nini Yesu aliwaruhusu maadui wake wamkamate bila kuchukua hatua yoyote?

13 Kuhusu hilo, tunaweza kumwiga Yesu ambaye ni kielelezo chetu. Ingawa Yesu angeweza kujitetea, aliruhusu maadui wake wamkamate katika bustani ya Gethsemane. Hata aliwaambia hivi wanafunzi wake: ‘Mnafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika? Katika kisa hicho, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?’ (Mathayo 26:53, 54) Yesu aliona kutimizwa kwa mapenzi ya Yehova kuwa jambo muhimu zaidi, hata ingawa angeteseka kwa kufanya hivyo. Aliyaamini kabisa maneno ya unabii wa zaburi hii ya Daudi: “Hutakuachia kuzimu nafsi yangu, wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu.” (Zaburi 16:10) Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alisema hivi kumhusu Yesu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:2.

Shangwe ya Kulitakasa Jina la Yehova

14. Ni shangwe gani iliyomtegemeza Yesu wakati wa majaribu yake yote?

14 Ni shangwe gani iliyomtegemeza Yesu wakati alipopatwa na jaribu kali sana? Kati ya watumishi wote wa Yehova, Yesu, Mwana mpendwa wa Mungu, ndiye kwa kweli aliyekuwa shabaha kuu zaidi ya Shetani. Kwa hiyo, kwa kudumisha uaminifu-maadili chini ya jaribu, Yesu angetoa jibu bora kabisa kwa dhihaka za Shetani dhidi ya Yehova. (Mithali 27:11) Je, unaweza kuwazia shangwe na uradhi ambao Yesu alipata alipofufuliwa? Ni lazima awe alifurahi sana kutambua kwamba alikuwa ametimiza jukumu alilopewa akiwa mwanadamu mkamilifu la kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina Lake. Isitoshe, hapana shaka kwamba kuketi “kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu” ni pendeleo zuri ambalo humletea Yesu shangwe kuu sana.—Zaburi 110:1, 2; 1 Timotheo 6:15, 16.

15, 16. Ni mnyanyaso gani wa kikatili uliowapata Mashahidi huko Sachsenhausen, na walipata wapi nguvu za kuvumilia?

15 Vivyo hivyo, Wakristo hupata shangwe kushiriki katika kulitakasa jina la Yehova kwa kuvumilia majaribu na mnyanyaso, wakiiga kielelezo cha Yesu. Mfano mzuri unahusu Mashahidi walioteseka kwenye kambi yenye sifa mbaya ya Sachsenhausen na kunusurika ule msafara wa kifo wenye kuchosha mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wakati wa msafara huo, maelfu ya wafungwa walikufa kwa sababu ya baridi kali, ugonjwa, au njaa au waliuawa kikatili barabarani na kikosi maalumu cha walinzi wa Hitler. Mashahidi wote 230 walinusurika kwa kukaa karibu-karibu na kusaidiana ingawa kufanya hivyo kulihatarisha maisha yao.

16 Mashahidi hao walipata wapi nguvu za kuvumilia mnyanyaso huo wa kikatili? Mara tu walipofika mahali salama, walionyesha shangwe na shukrani zao kwa Yehova katika hati yenye kichwa, “Azimio la Mashahidi wa Yehova 230 kutoka mataifa sita waliokusanyika msituni karibu na Schwerin huko Mecklenburg.” Katika hati hiyo walisema: “Kipindi kirefu cha majaribu kimeisha, na wale walionusurika, ambao waliponea chupuchupu, hawakuathiriwa na majaribu yaliyowapata. (Ona Danieli 3:27.) Badala yake, wanajawa na nguvu na uwezo kutoka kwa Yehova na wanangojea kwa hamu maagizo mapya kutoka kwa Mfalme ili kuendeleza mambo yanayohusu Ufalme.” *

17. Leo watu wa Mungu wanakabili majaribu ya aina gani?

17 Kama Mashahidi hao waaminifu 230, imani yetu pia inaweza kujaribiwa, hata ingawa bado ‘hatujakinza kamwe hadi damu.’ (Waebrania 12:4) Lakini majaribu yanaweza kuwa ya namna mbalimbali. Huenda yakawa dhihaka kutoka kwa wanadarasa, au kushawishiwa kufanya uasherati na mambo mengine mabaya. Isitoshe, mara kwa mara uamuzi wa kujiepusha na damu, kufunga ndoa katika Bwana tu, au kulea watoto wanaomwamini Mungu katika familia iliyogawanyika kidini kunaweza kusababisha mikazo na majaribu makali.—Matendo 15:29; 1 Wakorintho 7:39; Waefeso 6:4; 1 Petro 3:1, 2.

18. Tuna uhakikisho gani kwamba tunaweza kuvumilia hata jaribu kali sana?

18 Lakini, hata tupatwe na majaribu gani, tunajua kwamba tunateseka kwa sababu ya kumtanguliza Yehova na Ufalme wake, nasi huona kufanya hivyo kuwa pendeleo kubwa na pia jambo linaloleta shangwe. Tunapata ujasiri kutokana na maneno haya ya Petro yanayotoa uhakikisho: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, nyinyi ni wenye furaha, kwa sababu roho ya utukufu, naam, roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:14) Roho ya Yehova hutupa nguvu ya kuvumilia hata majaribu makali sana, na hivyo kumletea utukufu na sifa.—2 Wakorintho 4:7; Waefeso 3:16; Wafilipi 4:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Matukio ya miaka ya 1960 yalikuwa mwanzo tu wa mfululizo wa mnyanyaso wa kikatili ambao ungewapata Mashahidi nchini Malawi kwa miaka karibu thelathini. Kwa habari kamili, ona kitabu 1999 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 171-212.

^ fu. 8 Ona makala “Mahakama Kuu Yatetea Ibada ya Kweli Katika ‘Nchi ya Ararati’” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2003, ukurasa wa 11-14.

^ fu. 16 Kwa habari kamili kuhusu azimio hilo, ona kitabu 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 208-209. Mtu mmoja aliyenusurika msafara huo anaeleza yaliyompata kwenye toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1998, ukurasa wa 25-29.

Je, Unaweza Kueleza?

• Wakristo huyaonaje mateso na mnyanyaso?

• Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu na watu wengine waaminifu walivyotenda chini ya majaribu?

• Kwa nini si jambo la hekima kulipiza kisasi tunaponyanyaswa?

• Ni shangwe ya aina gani iliyomsaidia Yesu kuvumilia majaribu yaliyompata, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na hayo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso

• Kwa mwongozo wa malaika, Yosefu na Maria walimchukua mtoto Yesu na kukimbilia Misri kabla askari wa Herode kufika Bethlehemu ili kuwaua watoto wote wa kiume waliokuwa na umri wa miaka miwili na chini.—Mathayo 2:13-16.

• Wakati wa huduma yake, maadui wa Yesu walijaribu mara nyingi kumuua kwa sababu ya ushahidi wake wenye nguvu. Yesu aliwakwepa kila mara walipojaribu kufanya hivyo.—Mathayo 21:45, 46; Luka 4:28-30; Yohana 8:57-59.

• Wakati askari na maofisa walipokuja katika bustani ya Gethsemane kumkamata Yesu, alijitambulisha kwao waziwazi na kuwaambia hivi mara mbili: “Mimi ndiye.” Hata aliwazuia wafuasi wake wasipigane nao naye akawaruhusu watu hao wenye ghasia wamkamate na kwenda naye.—Yohana 18:3-12.

• Huko Yerusalemu, Petro na wengine walikamatwa, wakapigwa viboko, na kuamriwa waache kuzungumza juu ya Yesu. Lakini walipoachiliwa ‘walishika njia yao na kila siku katika hekalu na kutoka nyumba hadi nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’—Matendo 5:40-42.

• Wakati Sauli, aliyekuja kuwa mtume Paulo, alipojua kwamba Wayahudi huko Damasko walikuwa wamepanga njama ya kumuua, akina ndugu walimtia ndani ya kikapu na kumteremsha usiku kupitia mwanya fulani kwenye ukuta wa jiji, naye akatoroka.—Matendo 9:22-25.

• Miaka kadhaa baadaye, Paulo aliamua kukata rufani kwa Kaisari, hata ingawa Gavana Festo na Mfalme Agripa hawakuona “lolote linalostahili kifo au vifungo” kumhusu.—Matendo 25:10-12, 24-27; 26:30-32.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Ingawa maelfu ya Mashahidi waaminifu wa Malawi walilazimika kukimbia mnyanyaso mkali, wao waliendelea na utumishi wao wa Ufalme kwa furaha

[Picha katika ukurasa wa 17]

Shangwe waliyopata ya kutakasa jina la Yehova iliwategemeza waaminifu hawa kwenye kambi za mateso na wakati wa ule msafara wa kifo wa Nazi

[Hisani]

Death march: KZ-Gedenkstätte Dachau, courtesy of the USHMM Photo Archives

[Picha katika ukurasa wa 18]

Majaribu na mikazo yanaweza kuwa ya namna mbalimbali