Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Mengi—Majibu Machache Yenye Kuridhisha

Maswali Mengi—Majibu Machache Yenye Kuridhisha

Maswali Mengi—Majibu Machache Yenye Kuridhisha

ASUBUHI moja, Novemba 1, 1755, tetemeko kubwa la ardhi lilitokea katika jiji la Lisbon wakati wakaaji wengi walipokuwa kanisani asubuhi wakiadhimisha Siku ya Watakatifu Wote. Majengo mengi sana yaliporomoka, na watu wengi sana wakafa.

Muda mfupi baada ya msiba huo kutokea, Voltaire, mwandishi Mfaransa, alichapisha shairi lake lenye kichwa Poème sur le désastre de Lisbonne (Shairi Kuhusu Msiba wa Lisbon), ambalo lilikanusha dai la kwamba msiba huo ulisababishwa na Mungu ili awaadhibu watu kwa sababu ya dhambi zao. Akidai kwamba wanadamu hawawezi kuelewa wala kueleza kinachosababisha misiba hiyo, Voltaire aliandika:

Uumbaji hauwezi kuzungumza, hauwezi kujibu maswali yetu;

Tunahitaji Mungu anayewasiliana na wanadamu.

Bila shaka, Voltaire hakuwa mtu wa kwanza kuzusha maswali kumhusu Mungu. Katika historia yote ya wanadamu, misiba imefanya watu wajiulize maswali mbalimbali. Miaka ipatayo 3,600 iliyopita mzee wa ukoo Ayubu, aliyekuwa amefiwa na watoto wake wote na aliyekuwa anaugua ugonjwa mbaya, aliuliza: “Mbona yeye aliye mashakani kupewa mwanga, na hao wenye uchungu rohoni kupewa uhai [na Mungu]?” (Ayubu 3:20) Leo, wengi hawaelewi ni kwa nini Mungu mwenye upendo na mwema anaonekana kutojishughulisha ingawa kuna mateso na ukosefu mwingi wa haki.

Watu wengi wanapopatwa na njaa, vita, ugonjwa, na kifo, wao hukataa kabisa kuwa kuna Muumba anayewajali wanadamu. Mwanafalsafa mmoja asiyeamini kuwa kuna Mungu alisema: “Mungu hana sababu yoyote ya kuruhusu watoto wateseke, . . . isipokuwa tu awe hayupo.” Misiba mikubwa kama vile yale Maangamizi Makubwa yaliyotokea katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, hufanya wengi wawe na maoni kama hayo. Ona maneno haya ya mwandikaji Myahudi katika gazeti moja: “Mateso yaliyotokea huko Auschwitz yanaonyesha kwamba hakuna Mungu anayeweza kuingilia kati shughuli za wanadamu.” Kulingana na uchunguzi uliofanywa mwaka wa 1997 katika nchi ya Ufaransa ambayo ina Wakatoliki wengi, asilimia 40 hivi ya watu waliohojiwa wanatilia shaka kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya mauaji ya watu wengi, kama yale yaliyotokea nchini Rwanda mwaka wa 1994.

Kizuizi kwa Imani

Kwa nini Mungu haingilii kati kuzuia misiba isitokee? Mkatoliki mmoja aliye mwandikaji wa matukio katika historia anadai kwamba kwa watu wengi swali hilo ni “kizuizi kikubwa kwa imani.” Anauliza hivi: “Je, kweli inawezekana kumwamini Mungu ambaye hutazama tu bila kufanya lolote huku mamilioni ya watu wasio na hatia wakifa na wengine wakiuawa kwa wingi ulimwenguni?”

Pia tahariri moja katika gazeti la Wakatoliki, La Croix, inasema: “Iwe ni misiba iliyotokea zamani, misiba inayosababishwa na maendeleo ya kiteknolojia, misiba ya kiasili, magenge ya wahalifu, au kifo cha mpendwa, watu humgeukia Mungu kwa hofu wakitaka kuelezwa ni kwa nini mambo hayo hutukia. Mungu yuko wapi? Wanataka kujibiwa. Je, yeye si Mungu Mkuu Asiyejali, Mungu Mkuu Asiyejishughulisha na wanadamu?”

Papa John-Paul wa Pili alizungumzia suala hilo katika barua yake Salvifici Doloris ya mwaka wa 1984. Aliandika hivi: “Kuwapo kwa ulimwengu humsaidia mwanadamu aelewe kwamba kuna Mungu mwenye hekima, uwezo, na ukuu. Lakini yaonekana uovu na kuteseka hufanya watu wasitambue kabisa sifa hizo za Mungu, hasa inapoonekana kwamba wengi wanateseka isivyo haki kila siku, huku wengine wakifanya makosa bila kuadhibiwa ifaavyo.”

Ikiwa kuna Mungu mwenye upendo na nguvu zote, kama Biblia inavyosema, je, anaweza kuruhusu wanadamu wateseke? Je, yeye huingilia kati ili kuzuia misiba isitokee? Je, yeye hufanya jambo lolote kwa ajili yetu leo? Kwa kumnukuu Voltaire, je, kuna “Mungu anayewasiliana na wanadamu” ili kujibu maswali hayo? Tafadhali soma makala inayofuata ili upate jibu.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Uharibifu wa Lisbon mwaka wa 1755 ulimchochea Voltaire kudai kwamba wanadamu hawawezi kuelewa matukio hayo

[Hisani]

Voltaire: From the book Great Men and Famous Women; Lisbon: J.P. Le Bas, Praça da Patriarcal depois do terramoto de 1755. Foto: Museu da Cidade/Lisboa

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wengi hutilia shaka kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya maafa yanayotokana na mauaji ya watu wengi kama yale ya Rwanda

[Hisani]

AFP PHOTO

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

COVER, children: USHMM, courtesy of Main Commission for the Prosecution of the Crimes against the Polish Nation