Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?

Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?

Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?

KATIKA karne ya nane K.W.K., Mfalme Hezekia wa Yuda mwenye umri wa miaka 39 alipata habari kwamba alikuwa na ugonjwa ambao ungemuua. Hezekia alivunjwa moyo na habari hizo naye akamsihi Mungu amponye. Mungu alimjibu hivi kupitia nabii wake: “Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano.”—Isaya 38:1-5.

Kwa nini Mungu aliingilia kati pindi hiyo? Karne kadhaa mapema, Mungu alikuwa amemwahidi hivi Mfalme Daudi mwadilifu: “Nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.” Pia, Mungu alifunua kwamba Mesiya angezaliwa katika ukoo wa Daudi. (2 Samweli 7:16; Zaburi 89:20, 26-29; Isaya 11:1) Hezekia alipougua, alikuwa bado hajapata mtoto wa kiume. Hivyo, ukoo wa kifalme wa Daudi ulikuwa katika hatari ya kukatizwa. Katika kisa cha Hezekia, Mungu aliingilia kati akiwa na kusudi hususa la kuhifadhi ukoo ambao ungetokeza Mesiya.

Katika kipindi chote kilichotangulia Ukristo, mara nyingi Yehova aliamua kuingilia kati kwa ajili ya watu wake ili atimize ahadi zake. Musa alisema hivi kuhusu kukombolewa kwa Waisraeli kutoka utumwani Misri: “Kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu.”—Kumbukumbu la Torati 7:8.

Pia katika karne ya kwanza, Mungu aliingilia kati ili kutimiza makusudi yake. Kwa mfano, wakati Myahudi mmoja aitwaye Sauli alipokuwa njiani kwenda Damasko, alipata maono kimuujiza ili kumzuia asiendelee kuwanyanyasa wanafunzi wa Kristo. Mtu huyo aliyegeuzwa imani na kuwa mtume Paulo, alichangia sana kuenezwa kwa habari njema kati ya mataifa.—Matendo 9:1-16; Waroma 11:13.

Je, Ilikuwa Kawaida ya Mungu Kuingilia Kati?

Je, ilikuwa kawaida ya Mungu kuingilia kati? Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba hilo halikuwa jambo la kawaida hata kidogo. Ingawa Mungu aliwakomboa wale vijana Waebrania watatu wasiuawe katika tanuru ya moto na kumkomboa nabii Danieli kutoka katika shimo la simba, hakuchukua hatua ya kuwakomboa manabii wengine wasife. (2 Mambo ya Nyakati 24:20, 21; Danieli 3:21-27; 6:16-22; Waebrania 11:37) Petro alikombolewa kimuujiza kutoka gerezani baada ya Herode Agripa wa Kwanza kumtia humo. Hata hivyo, mfalme huyohuyo aliagiza mtume Yakobo auawe, naye Mungu hakuingilia kati ili kuzuia mauaji hayo. (Matendo 12:1-11) Ingawa Mungu aliwapa mitume uwezo wa kuponya wagonjwa na hata kufufua wafu, hakukubali kuuondoa “mwiba katika mwili” uliomsumbua mtume Paulo, ambao huenda ulikuwa ugonjwa fulani.—2 Wakorintho 12:7-9; Matendo 9:32-41; 1 Wakorintho 12:28.

Mungu hakuingilia kati kuzuia mnyanyaso mkubwa dhidi ya wanafunzi wa Kristo uliotekelezwa na Nero, Maliki Mroma. Wakristo waliteswa, wakateketezwa kwa moto wakiwa hai, na kutupiwa wanyama. Hata hivyo, Wakristo wa mapema hawakushangazwa na upinzani huo wala haukudhoofisha imani yao kuwa kuna Mungu, kwa kuwa Yesu alikuwa amewaonya wanafunzi wake kwamba wangepelekwa mahakamani na wangepaswa kuwa tayari kuteseka na hata kufa kwa ajili ya imani yao.—Mathayo 10:17-22.

Bila shaka, leo Mungu anaweza kuwakomboa watumishi wake kutoka katika hatari kama alivyofanya zamani, na hatupaswi kuwachambua wale wanaohisi kwamba Mungu amewalinda katika hali fulani. Lakini katika visa hivyo, ni vigumu kusema kwa uhakika kabisa kama Mungu aliingilia kati au la. Watumishi waaminifu kadhaa wa Yehova walijeruhiwa katika mlipuko uliotokea Toulouse, na Wakristo wengi waaminifu walikufa katika kambi za Nazi na za Wakomunisti au katika misiba mingine bila Mungu kuingilia kati ili kuizuia. Kwa nini Mungu haingilii kati kila mara kwa ajili ya wote walio na kibali chake?—Danieli 3:17, 18.

“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”

Msiba unapotokea, unaweza kumpata yeyote hata kama mtu huyo ni mwaminifu kwa Mungu. Mlipuko ulipotokea jijini Toulouse, Alain na Liliane walinusurika, lakini watu 30 walikufa na mamia wakajeruhiwa, hata ingawa halikuwa kosa lao. Kwa kiwango kikubwa, makumi ya maelfu ya watu huathiriwa na uhalifu, kuendesha gari bila kujali, au vita, na hatuwezi kumlaumu Mungu kwa misiba hiyo. Biblia inatukumbusha kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata” wote.—Mhubiri 9:11, NW.

Zaidi ya hayo, wanadamu hupatwa na magonjwa, huzeeka, na kufa. Hata baadhi ya watu ambao walifikiri kwamba Mungu aliwakomboa kimuujiza au kuwaponya bila kutazamia, mwishowe walikufa. Kuondolewa kwa magonjwa na kifo, na ‘kufutwa kabisa kwa kila chozi’ katika macho ya wanadamu kutatokea wakati ujao.—Ufunuo 21:1-4.

Ili jambo hilo litokee, hatua kubwa na muhimu inahitaji kuchukuliwa badala ya kuingilia kati pindi kwa pindi. Biblia inazungumza juu ya “siku ya BWANA iliyo kuu.” (Sefania 1:14) Wakati Mungu atakapochukua hatua hiyo kubwa, ataondoa uovu wote. Wanadamu watapewa nafasi ya kuishi milele katika hali kamilifu, ambapo “mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Hata wafu watafufuliwa, na hivyo kubatilisha mojawapo ya misiba mikubwa zaidi inayowapata wanadamu. (Yohana 5:28, 29) Wakati huo Mungu mwenye wema na upendo mwingi atakuwa ametatua kabisa matatizo ya wanadamu.

Jinsi Mungu Huingilia Kati Leo

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wakati huu Mungu hutazama tu bila kufanya jambo lolote huku uumbaji ukiteseka. Leo, Mungu anawatolea wanadamu wote nafasi ya kumjua na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye bila kujali kabila lao au jamii yao. (1 Timotheo 2:3, 4) Yesu alifafanua jambo hilo aliposema hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Mungu huwavuta watu wenye mioyo minyoofu kupitia ujumbe wa Ufalme unaotangazwa na watumishi wake ulimwenguni kote.

Isitoshe, Mungu huhusika moja kwa moja katika maisha ya wale walio tayari kuongozwa naye. Kupitia roho yake takatifu, Mungu ‘anafungua mioyo yao’ ili waelewe mapenzi yake na kutimiza matakwa yake. (Matendo 16:14) Naam, kwa kuwatolea wanadamu nafasi ya kumjua, kujua Neno lake, na makusudi yake, Mungu huthibitisha kwamba anapendezwa na kila mmoja wetu.—Yohana 17:3.

Mwishowe, leo Mungu huwasaidia watumishi wake, si kwa kuwakomboa kimuujiza, bali kwa kuwapa roho yake takatifu na “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kukabiliana na hali yoyote ile. (2 Wakorintho 4:7) Mtume Paulo aliandika: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye [Yehova Mungu] anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.

Kwa hiyo tuna kila sababu kumshukuru Mungu kila siku kwa ajili ya uhai na tumaini analotupatia la kuishi milele katika ulimwengu usio na mateso yoyote. “Nimrudishie BWANA nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?” mtunga-zaburi mmoja akauliza. “Nitakipokea kikombe cha wokovu; na kulitangaza jina la BWANA.” (Zaburi 116:12, 13) Ukisoma gazeti hili kwa ukawaida litakusaidia uelewe yale ambayo Mungu amefanya, anayofanya, na atakayofanya. Mambo hayo yanaweza kukuletea furaha sasa na tumaini hakika la wakati ujao.—1 Timotheo 4:8.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17

[Picha katika ukurasa wa 5]

Katika nyakati za Biblia, Yehova hakuzuia Zekaria asipigwe mawe . . .

wala hakumzuia Herode kuwaua watu wengi wasio na hatia

[Picha katika ukurasa wa 7]

Hivi karibuni kuteseka kutakoma; na hata wafu wataishi tena