Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!

Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!

Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!

“Kila mtu anayeshiriki katika shindano hutumia kujidhibiti katika mambo yote.”—1 WAKORINTHO 9:25.

1. Kupatana na andiko la Waefeso 4:22-24, watu wengi wamekubali jinsi gani kufanya mapenzi ya Yehova?

IKIWA ulibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ulitangaza hadharani kwamba ulikuwa tayari kushiriki katika pambano ambalo tuzo lake ni uhai wa milele. Ulikubali kufanya mapenzi ya Yehova. Kabla ya kujiweka wakfu kwa Yehova, wengi wetu tulifanya mabadiliko makubwa ili wakfu wetu uwe wa kweli na wenye kukubaliwa na Mungu. Tulifuata shauri hili la mtume Paulo kwa Wakristo: “Mweke mbali utu wa hapo zamani unaofuatana na njia yenu ya kwanza ya mwenendo na ambao unafisidiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu . . . Mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” (Waefeso 4:22-24) Yaani, kabla ya kujiweka wakfu kwa Mungu, ilitubidi kuacha mwenendo wa zamani usiofaa.

2, 3. Andiko la 1 Wakorintho 6:9-12 linaonyeshaje kwamba mabadiliko ya aina mbili yanapaswa kufanywa ili kupata kibali cha Mungu?

2 Baadhi ya tabia za utu wa kale ambazo watu wanaotaka kuwa Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuacha zinashutumiwa waziwazi na Neno la Mungu. Paulo aliorodhesha baadhi ya tabia hizo katika barua yake kwa Wakorintho, akisema: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” Kisha akaonyesha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walifanya mabadiliko mbalimbali kuhusiana na utu wao, na kuendelea kusema: “Hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” Ona kwamba Wakristo hao walikuwa hivyo, lakini wakabadilika.1 Wakorintho 6:9-11.

3 Paulo alidokeza kwamba huenda pia ikawa lazima kufanya mabadiliko zaidi, kwa kuwa aliendelea kusema: “Mambo yote yaruhusika kisheria kwangu; lakini si mambo yote yenye faida.” (1 Wakorintho 6:12) Hivyo, leo wengi ambao hutamani kuwa Mashahidi wa Yehova huona uhitaji wa kukataa kabisa hata mambo ambayo, ingawa yanaruhusika kisheria, hayana faida au hayana thamani ya kudumu. Mambo hayo yanaweza kuwapotezea wakati na kuwakengeusha wasifuatie mambo yaliyo muhimu zaidi.

4. Wakristo waliojiweka wakfu wanakubaliana na Paulo katika jambo gani?

4 Mtu hujiweka wakfu kwa Mungu kwa hiari, na si shingo upande kana kwamba kufanya hivyo ni kujidhabihu sana. Wakristo waliojiweka wakfu wanakubaliana na Paulo ambaye alisema hivi baada ya kuwa mfuasi wa Kristo: “Kwa sababu yake [Yesu] nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kupata Kristo.” (Wafilipi 3:8) Paulo alikataa kabisa kwa hiari mambo yasiyo na thamani ili aweze kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu.

5. Paulo alishiriki kwa mafanikio katika shindano gani, nasi tunawezaje kufanya hivyo?

5 Paulo alionyesha sifa ya kujidhibiti alipokuwa akikimbia katika shindano lake la kiroho na mwishowe aliweza kusema: “Nimepigana pigano bora, nimekimbia mwendo hadi mwisho, nimeshika imani. Tangu wakati huu na kuendelea kumewekwa akiba kwa ajili yangu taji la uadilifu, ambalo Bwana, aliye hakimu mwadilifu, atanipa kuwa zawadi katika siku ile, lakini si mimi tu, bali pia wale wote ambao wamependa udhihirisho wake.” (2 Timotheo 4:7, 8) Je, siku moja tutaweza kusema kama yeye? Tutafanya hivyo ikiwa kwa imani tunaonyesha sifa ya kujidhibiti tunapokimbia katika shindano letu la Kikristo mpaka mwisho bila kuacha.

Kujidhibiti Kunahitajiwa ili Kufanya Mema

6. Kujidhibiti ni nini, na tunapaswa kuonyesha sifa hiyo katika njia gani mbili?

6 Maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotafsiriwa “kujidhibiti” katika Biblia, kihalisi yanamaanisha kwamba mtu ana uwezo wa kujizuia. Mara nyingi maneno hayo yanadokeza wazo la kujizuia usifanye mabaya. Lakini ni wazi kwamba kujidhibiti kwa kadiri fulani kunahitajiwa pia ikiwa tutafanikiwa kutumia miili yetu kufanya kazi njema. Kwa kawaida wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kufanya mabaya, kwa hiyo tuna mapambano ya aina mbili. (Mhubiri 7:29; 8:11) Tunapojizuia kufanya mabaya, inatubidi pia tujilazimishe kufanya mema. Kwa kweli, kudhibiti mwili wetu ili kufanya mema ni mojawapo kati ya njia bora zaidi za kuepuka kufanya mabaya.

7. (a) Kama Daudi, tunapaswa kusali kwa ajili ya nini? (b) Tunaweza kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kadiri kubwa kwa kutafakari mambo gani?

7 Bila shaka kujidhibiti ni muhimu ili kutimiza wakfu wetu kwa Mungu. Tunapaswa kusali kama Daudi: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.” (Zaburi 51:10) Tunaweza kutafakari manufaa ya kuepuka mambo yasiyo maadilifu au yanayotudhoofisha kimwili. Fikiria madhara unayoweza kupata kwa kutoepuka mambo hayo: matatizo mabaya ya afya, mahusiano yaliyoharibika, na hata kifo cha mapema. Kwa upande mwingine, fikiria faida nyingi za kufuata njia ya maisha ambayo Yehova hupendekeza. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba moyo wetu ni mdanganyifu. (Yeremia 17:9) Ni lazima tuazimie kutoruhusu moyo wetu upunguze uzito wa kufuata viwango vya Yehova.

8. Tumejifunza nini kutokana na mambo yaliyotupata? Toa mfano.

8 Kutokana na mambo yaliyotupata, wengi wetu tunajua kwamba mara nyingi mwili usio na nia ya kufanya mema hupunguza bidii na nia yetu ya kufanya yaliyo mema. Kwa mfano, fikiria kazi ya kuhubiri Ufalme. Yehova hupendezwa na nia ya wanadamu ya kutaka kufanya mema kwa kushiriki katika kazi hii inayotoa uhai. (Zaburi 110:3; Mathayo 24:14) Haikuwa rahisi kwa wengi wetu kujifunza kuhubiri hadharani. Tulihitaji na labda bado tunahitaji kudhibiti mwili wetu, ‘kuupiga-piga’ na “kuuongoza kama mtumwa,” badala ya kuuruhusu utuzuie kuhubiri.—1 Wakorintho 9:16, 27; 1 Wathesalonike 2:2.

“Katika Mambo Yote”?

9, 10. Ni nini kinachohusika katika kuonyesha sifa ya “kujidhibiti katika mambo yote”?

9 Shauri la Biblia kuhusu “kujidhibiti katika mambo yote” linaonyesha kwamba kuna mengi zaidi yanayohusika kuliko kudhibiti tu hasira yetu na kujiepusha na mwenendo usio mwadilifu. Huenda tukahisi kwamba tumejidhibiti katika mambo hayo, na ikiwa ndivyo, tunaweza kufurahi kwelikweli. Hata hivyo, namna gani sehemu nyingine za maisha ambazo huenda isionekane waziwazi kwamba tunahitaji kuonyesha sifa ya kujidhibiti? Kwa mfano, tuseme tunaishi katika nchi ambayo ni tajiri kwa kadiri fulani na yenye kiwango cha juu cha maisha. Je, halitakuwa jambo la hekima kujifunza kutotumia pesa kwa vitu visivyo vya lazima? Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kutonunua kitu chochote wanachoona kwa sababu tu kinapatikana, kinavutia, au wana pesa za kukinunua. Bila shaka, ili mafundisho hayo yawe yenye matokeo, lazima wazazi waweke mfano mzuri.—Luka 10:38-42.

10 Kujifunza kuishi bila kitu fulani tunachotaka kunaweza kuimarisha azimio letu. Pia kunaweza kufanya tuthamini vitu tulivyo navyo na kuwahurumia zaidi wale wasiokuwa na vitu hivyo, si kwa kupenda kwao, bali kwa sababu hawana pesa za kuvinunua. Naam, kuishi maisha sahili ni kinyume kabisa na maoni ya watu wengi kwamba lazima watu wajijali kupita kiasi au kuona kwamba wao ndio wanaostahili vitu bora zaidi. Wanabiashara huchochea tamaa ya kujitosheleza papo hapo, lakini wao hufanya hivyo ili wapate faida. Huenda hali hiyo ikazuia jitihada zetu za kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Hivi karibuni, gazeti moja la nchi fulani tajiri ya Ulaya lilisema hivi: “Ikiwa wale wanaoishi chini ya hali ngumu sana za umaskini wanahitaji kujitahidi ili kudhibiti tamaa zisizofaa, basi wale wanaoishi katika nchi tajiri wanahitaji kujitahidi hata zaidi katika jamii ya leo yenye utajiri!”

11. Kwa nini kuna manufaa ya kujifunza kuishi bila vitu fulani, na ni nini hufanya jambo hilo liwe gumu?

11 Ikiwa ni vigumu kwetu kutofautisha kati ya vitu tunavyotaka na mahitaji halisi, huenda ikafaa kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba hatutendi bila kufikiri. Kwa mfano, ikiwa tunataka kujizuia tusitumie pesa ovyoovyo, huenda tukaazimia kutonunua vitu kwa mkopo, au kuchukua kiasi hususa cha pesa tunapoenda kununua vitu. Kumbuka kwamba Paulo alisema ‘ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu’ ni “njia ya kupata faida kubwa.” Alitoa hoja hii: “Hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” (1 Timotheo 6:6-8) Je, tunaridhika? Kujifunza kuishi maisha sahili, bila kujiingiza katika mambo yanayoweza kutuzuia kufanya mambo yaliyo ya lazima—hata yawe ni nini—huhitaji tuazimie na kujidhibiti. Hata hivyo, kuna manufaa ya kujifunza kufanya hivyo.

12, 13. (a) Mikutano ya Kikristo inahusishaje sifa ya kujidhibiti? (b) Tunapaswa kusitawisha sifa ya kujidhibiti katika sehemu gani nyingine?

12 Kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na makusanyiko kunahusisha kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa njia fulani hususa. Kwa mfano, sifa hiyo ni muhimu ili kuzuia akili yetu isitangetange wakati programu inapoendelea. (Mithali 1:5) Huenda sifa ya kujidhibiti ikahitajiwa ili tusiwasumbue wengine kwa kuwanong’onezea wale walioketi karibu nasi badala ya kumsikiliza msemaji kwa makini. Huenda tukahitaji sifa ya kujidhibiti ili turekebishe ratiba yetu na kufika mapema. Isitoshe, huenda tukahitaji kuonyesha sifa ya kujidhibiti ili kutenga wakati wa kutayarisha na kushiriki katika mikutano.

13 Kuonyesha sifa ya kujidhibiti katika mambo madogo huimarisha uwezo wetu wa kuonyesha sifa hiyo katika mambo makubwa. (Luka 16:10) Kwa hiyo, ni jambo zuri kujitia nidhamu ili kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu na vichapo vinavyozungumzia Biblia, kujifunza na kutafakari mambo tunayojifunza. Ni jambo la hekima kama nini kujitia nidhamu kuhusu kazi zisizofaa, urafiki, mitazamo, na tabia fulani au kujitia nidhamu ili kukataa kabisa mambo yanayoweza kutupotezea wakati wenye thamani wa kumtumikia Mungu! Bila shaka, kuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova hutulinda dhidi ya mambo yanayoweza kutuondoa katika paradiso ya kiroho ya kutaniko la Yehova la ulimwenguni pote.

Iweni Wakomavu kwa Kujidhibiti

14. (a) Watoto wanapaswa kujifunzaje kuonyesha sifa ya kujidhibiti? (b) Watoto wanaweza kupata manufaa gani wanapojifunza kuonyesha sifa hiyo mapema maishani?

14 Mtoto mchanga hawezi kujidhibiti. Kijitabu kimoja cha wataalamu wa tabia ya watoto kinasema: “Sifa ya kujidhibiti haitokei tu bila jitihada yoyote. Watoto wanahitaji mwongozo na msaada wa wazazi ili waanze kujifunza kuwa na sifa ya kujidhibiti. . . . Wazazi wanapowafunza, watoto huanza kusitawisha sifa ya kujidhibiti na kuendelea kuionyesha miaka yote wanapokuwa shuleni.” Uchunguzi uliofanywa kuhusu watoto wenye umri wa miaka minne ulionyesha kwamba wale waliojifunza kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kadiri fulani “kwa ujumla walikua wakawa vijana wenye nidhamu, wenye kupendeza, wajasiri, wenye uhakika na wenye kutegemeka.” Wale ambao hawakuwa wameanza kujifunza sifa hiyo, “yaelekea walikuwa wapweke, wenye kukasirika kwa urahisi, na wakaidi. Walishindwa na mkazo na hawakutaka kukabili magumu.” Bila shaka, ni lazima mtoto ajifunze kuonyesha sifa ya kujidhibiti ili atakapokuwa mtu mzima awe na nidhamu.

15. Kutojidhibiti huonyesha nini, na kunatofautianaje na lengo linalotajwa katika Biblia?

15 Vivyo hivyo, ili tuwe Wakristo waliokomaa, lazima tujifunze jinsi ya kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Kutojidhibiti huonyesha kwamba bado sisi ni watoto kiroho. Biblia inatushauri ‘tuwe watu wazima katika nguvu za kuelewa.’ (1 Wakorintho 14:20) Lengo letu ni ‘kuufikia umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu, kufikia kuwa mwanamume aliyekua kabisa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujao wa Kristo.’ Kwa nini? “Ili tusiwe tena vitoto, tukirushwa huku na huku kama vile na mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kwa njia ya mbinu ya hadaa ya watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Waefeso 4:13, 14) Ni wazi kwamba kujifunza kuonyesha sifa ya kujidhibiti ni muhimu kwa hali yetu ya kiroho.

Kusitawisha Sifa ya Kujidhibiti

16. Yehova hutoaje msaada?

16 Ili kusitawisha sifa ya kujidhibiti, tunahitaji msaada wa Mungu, nao unapatikana. Neno la Mungu ambalo ni kama kioo, hutuonyesha mahali tunapohitaji kufanya marekebisho ya kibinafsi, nalo hutoa shauri la jinsi ya kufanya hivyo. (Yakobo 1:22-25) Pia ndugu zetu wenye upendo ulimwenguni pote wana nia ya kutusaidia. Wazee Wakristo huonyesha kwamba wanaelewa hali za wengine wanapotoa msaada. Yehova mwenyewe hutupatia roho yake takatifu kwa hiari ikiwa tunaiomba katika sala. (Luka 11:13; Waroma 8:26) Kwa hiyo, na tutumie maandalizi hayo kwa furaha. Madokezo kwenye ukurasa wa 21 yanaweza kusaidia.

17. Andiko la Mithali 24:16 linatupa kitia moyo gani?

17 Ni jambo lenye kufariji kama nini kujua kwamba Yehova huthamini jitihada zetu tunapojaribu kumpendeza! Hilo lapaswa kutuchochea kuendelea kujitahidi ili tuzidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Hata tujikwae mara nyingi kadiri gani, hatupaswi kamwe kuacha kujitahidi. “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” (Mithali 24:16, NW) Kila mara tunapofanikiwa kumpendeza Yehova, tunakuwa na sababu ya kufurahi. Pia tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anapendezwa nasi. Shahidi mmoja anasema kwamba kabla hajajiweka wakfu kwa Yehova, kila mara alipojidhibiti kutovuta sigara kwa juma moja, alijithawabisha mwenyewe kwa kununua kitu kizuri akitumia pesa ambazo angetumia kununua sigara.

18. (a) Pambano letu la kusitawisha sifa ya kujidhibiti linahusisha nini? (b) Yehova anatuhakikishia nini?

18 Zaidi ya yote, tunapaswa kukumbuka kwamba kujidhibiti kunahusisha akili na hisia. Tunaweza kuona jambo hilo kutokana na maneno haya ya Yesu: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28; Yakobo 1:14, 15) Mtu ambaye amejifunza kudhibiti akili na hisia zake, ataona ni rahisi pia kudhibiti mwili wake wote. Kwa hiyo, acheni tuimarishe azimio letu la kutofanya mabaya na pia kutoyafikiria. Mawazo mabaya yakitokea, yakatae papo hapo. Tunaweza kukimbia kishawishi kwa kusali huku tukimkazia Yesu macho yetu. (1 Timotheo 6:11; 2 Timotheo 2:22; Waebrania 4:15, 16) Tunapojitahidi kufanya yote tuwezayo, tutakuwa tukitii shauri linalopatikana katika Zaburi 55:22: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”

Je, Unakumbuka?

• Tunapaswa kusitawisha sifa ya kujidhibiti katika njia gani mbili?

• Inamaanisha nini kusitawisha sifa ya “kujidhibiti katika mambo yote”?

• Ni madokezo gani mazuri ya kusitawisha sifa ya kujidhibiti yaliyokupendeza hasa katika funzo letu?

• Sifa ya kujidhibiti huanzia wapi?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

Jinsi ya Kuimarisha Sifa ya Kujidhibiti

• Isitawishe hata katika mambo madogo

• Tafakari manufaa ya sasa na ya wakati ujao ya sifa hiyo

• Epuka kufanya mambo ambayo Mungu anakataa na utendee yale anayotaka

• Kataa mawazo mabaya papo hapo

• Jaza akili yako mawazo ya kiroho yenye kujenga

• Kubali msaada unaoweza kupewa na Wakristo wenzako wakomavu

• Epuka hali zenye kushawishi

• Sali ili upate msaada wa Mungu wakati wa vishawishi

[Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Sifa ya kujidhibiti hutuchochea tufanye mema