Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu Kujidhibiti

Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu Kujidhibiti

Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu Kujidhibiti

“Jazeni . . . kwenye ujuzi wenu kujidhibiti.”—2 PETRO 1:5-8.

1. Matatizo mengi ya wanadamu yanasababishwa na kutoweza kufanya nini?

WAKATI wa kampeni kubwa ya kupinga matumizi ya dawa za kulevya, vijana nchini Marekani walishauriwa hivi: “Kataeni kabisa.” Hali zingekuwa nzuri kama nini iwapo kila mtu angekataa kabisa dawa za kulevya, ulevi, maisha ya kutojali au yasiyo maadilifu, mazoea ya kibiashara yasiyo manyoofu, na “tamaa za mwili”! (Waroma 13:14) Hata hivyo, si rahisi kukataa kabisa mambo hayo.

2. (a) Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kwamba ilikuwa vigumu hata kwa watu wa zamani kukataa kabisa mambo fulani? (b) Mifano hiyo inapaswa kututia moyo kufanya nini?

2 Kwa kuwa si rahisi kwa wanadamu wote wasio wakamilifu kuonyesha sifa ya kujidhibiti, tunapaswa kutamani kujua jinsi tunavyoweza kushinda udhaifu wowote tulio nao. Biblia hutueleza kuhusu watu wa zamani waliojitahidi kumtumikia Mungu, ingawa wakati mwingine ilikuwa vigumu kwao kukataa kabisa mambo fulani. Kumbuka Daudi na dhambi ya uzinzi aliyofanya pamoja na Bath-sheba. Dhambi hiyo ilisababisha kifo cha watu wawili wasio na hatia, mtoto wao aliyezaliwa kwa uzinzi na pia mume wa Bath-sheba. (2 Samweli 11:1-27; 12:15-18) Au fikiria mtume Paulo, ambaye alikiri hivi waziwazi: “Kwa maana lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” (Waroma 7:19) Je, nyakati nyingine unahisi umekata tamaa kama yeye? Paulo aliendelea kusema: “Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” (Waroma 7:22-24) Mifano inayotajwa katika Biblia inapaswa kuimarisha azimio letu la kuendelea na pambano letu la kuwa wenye kujidhibiti zaidi.

Tunapaswa Kujifunza Jinsi ya Kujidhibiti

3. Eleza kwa nini si rahisi kuonyesha sifa ya kujidhibiti.

3 Sifa ya kujidhibiti, ambayo inatia ndani uwezo wa kukataa kabisa mambo fulani, inatajwa kwenye 2 Petro 1:5-7 pamoja na imani, wema wa adili, ujuzi, uvumilivu, ujitoaji-kimungu, shauku ya kidugu, na upendo. Hakuna mtu anayezaliwa akiwa amesitawisha kabisa sifa hizo nyingine zenye kupendeza. Ni lazima zisitawishwe. Tunahitaji kujitahidi sana ili kuzionyesha kwa kadiri kubwa na ndivyo ilivyo na sifa ya kujidhibiti.

4. Kwa nini watu wengi huhisi kwamba hawana tatizo la kuonyesha sifa ya kujidhibiti, lakini jambo hilo linaonyesha nini?

4 Kwa kweli, huenda watu wengi wakahisi hawana tatizo la kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Wao hufanya watakavyo maishani, na kwa kujua au bila kujua, wao hujiendesha kupatana na mwili wao usio mkamilifu bila kujali jinsi wao au watu wengine watakavyoathiriwa na matokeo ya matendo yao. (Yuda 10) Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wengi wanashindwa au hawataki kukataa kabisa mambo fulani. Kwa kweli, hiyo inaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ambazo Paulo alizungumzia alipotabiri hivi: “Nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, . . . wasio na hali ya kujidhibiti.”—2 Timotheo 3:1-3.

5. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na habari inayohusu kujidhibiti, na ni shauri gani linalofaa hata leo?

5 Mashahidi wa Yehova wanajua vizuri sana ni vigumu kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Kama Paulo, wanatambua pambano kati ya tamaa ya kumpendeza Mungu kwa kuishi kupatana na viwango vyake, na mwenendo ambao huenda mwili wao usio mkamilifu ukawachochea kuufuata. Kwa sababu hiyo, kwa muda mrefu wametaka kujua jinsi ya kushinda pambano hilo. Mnamo mwaka wa 1916, toleo la mapema la gazeti unalosoma sasa lilizungumzia “njia inayofaa kufuata ili tujidhibiti wenyewe, mawazo yetu, maneno na mwenendo wetu.” Lilidokeza tukumbuke maneno ya andiko la Wafilipi 4:8. Shauri la Mungu katika andiko hilo linafaa hata leo, ingawa liliandikwa miaka 2,000 hivi iliyopita na labda ni vigumu zaidi kulitii sasa kuliko ilivyokuwa wakati huo au katika mwaka wa 1916. Hata hivyo, Wakristo hujitahidi sana kukataa kabisa tamaa za ulimwengu, huku wakitambua kwamba wanapofanya hivyo wanakubali kufanya mapenzi ya Muumba wao.

6. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa tunapositawisha sifa ya kujidhibiti?

6 Sifa ya kujidhibiti inatajwa katika andiko la Wagalatia 5:22, 23 kama sehemu ya “matunda ya roho [takatifu].” Tukionyesha sifa hii pamoja na “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, [na] upole,” tutanufaika sana. Kama Petro anavyosema, kufanya hivyo kutatuzuia tusiwe “ama wasiotenda ama wasiozaa matunda” katika utumishi wetu kwa Mungu. (2 Petro 1:8) Lakini hatupaswi kukata tamaa au kujilaumu tunaposhindwa kuonyesha sifa hizo haraka na kwa ukamili kama vile ambavyo tungependa. Labda umeona kwamba shuleni mwanafunzi fulani hujifunza mambo haraka zaidi kuliko mwingine. Au kazini mtu fulani hujifunza kazi haraka zaidi kuliko wafanyakazi wenzake. Vivyo hivyo, watu fulani hujifunza na kuonyesha sifa za Kikristo haraka zaidi kuliko wengine. Hata hivyo, jambo lililo muhimu ni kuendelea kusitawisha sifa za kimungu kadiri tuwezavyo. Tunaweza kufanya hivyo kwa kujinufaisha kikamili na msaada ambao Yehova hutoa kupitia Neno na kutaniko lake. Kuazimia kwa bidii kufanya maendeleo ndilo jambo muhimu zaidi kuliko kufikia mradi wetu haraka.

7. Ni nini kinachoonyesha kwamba sifa ya kujidhibiti ni muhimu?

7 Ingawa sifa ya kujidhibiti ndiyo inayotajwa mwisho katika orodha ya matunda ya roho, hiyo haimaanishi kwamba sifa hiyo si muhimu sana kama sifa zile nyingine. Tunapaswa kukumbuka kwamba tunaweza kuepuka ‘kazi zote za mwili’ kama tungeweza kujidhibiti kikamili. Hata hivyo, wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kufanya baadhi ya “kazi za mwili . . . uasherati, ukosefu wa usafi, mwenendo mlegevu, ibada ya sanamu, zoea la uwasiliani-roho, uadui, zogo, wivu, hasira za ghafula, magomvi, migawanyiko, mafarakano.” (Wagalatia 5:19, 20) Kwa hiyo, lazima tuendelee kushindana daima, na kuazimia kuondoa kabisa mielekeo isiyofaa kutoka katika akili na moyo.

Ni Vigumu Zaidi kwa Wengine Kuonyesha Sifa ya Kujidhibiti

8. Ni mambo gani ambayo hufanya iwe vigumu kwa wengine kuonyesha sifa ya kujidhibiti?

8 Ni vigumu zaidi kwa Wakristo fulani kuonyesha sifa ya kujidhibiti kuliko wengine. Kwa nini? Huenda ikawa vigumu kwao kuonyesha sifa hiyo kwa sababu ya malezi au mambo yaliyowapata zamani. Tunapaswa kufurahi ikiwa hatuna tatizo la kusitawisha na kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Lakini bila shaka tunapaswa kuwa na huruma na kuelewa hali tunaposhughulika na wale ambao ni vigumu kwao kuonyesha sifa ya kujidhibiti, hata ikiwa tunaumia wanapokosa kuionyesha. Kwa kuwa sisi pia si wakamilifu, ni nani kati yetu aliye na sababu ya kujiona kuwa mwadilifu?—Waroma 3:23; Waefeso 4:2.

9. Wengine wana udhaifu gani, nao udhaifu huo utaondolewa kabisa wakati gani?

9 Kwa mfano: Huenda tunajua kwamba nyakati nyingine baadhi ya Wakristo wenzetu ambao wameacha kutumia tumbaku au dawa za “kujiburudisha” wanaweza bado kuwa na tamaa kubwa ya kutumia vitu hivyo. Au wengine huona ni vigumu kupunguza kiasi cha chakula wanachokula au kileo wanachotumia. Wengine wana shida ya kudhibiti ulimi wao, kwa hiyo mara nyingi wao hujikwaa katika maneno. Tunahitaji kujitahidi sana kusitawisha sifa ya kujidhibiti ili kushughulika na udhaifu huo. Kwa nini? Andiko la Yakobo 3:2 linakiri hivi kwa kufaa: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” Hata hivyo, wengine wana tamaa kubwa ya kucheza kamari. Au huenda ikawa vigumu kwao kudhibiti hasira yao. Huenda ikachukua muda kujua jinsi unavyoweza kufanikiwa kukabiliana na udhaifu huo au udhaifu mwingine kama huo. Ingawa tunaweza kufanya maendeleo makubwa sasa, tamaa mbaya zitaondolewa kabisa tutakapofikia ukamilifu. Wakati huu, kujitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kutatusaidia tusirudie maisha ya dhambi. Pambano hilo linapoendelea, na tusaidiane ili tusife moyo.—Matendo 14:21, 22.

10. (a) Kwa nini ni vigumu kwa wengine sana kujidhibiti katika mambo ya ngono? (b) Ndugu mmoja alifanya badiliko gani kubwa? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 16.)

10 Sehemu nyingine ambayo wengine wana tatizo la kujidhibiti inahusu mambo ya ngono. Yehova Mungu alituumba tukiwa na hamu ya ngono. Hata hivyo, wengine huona ni vigumu sana kujidhibiti kuhusiana na ngono, kupatana na viwango vya Mungu. Inaweza kuwa vigumu zaidi kwao kwa sababu wana hamu kubwa ya ngono isivyo kawaida. Tunaishi katika ulimwengu ulio na kichaa cha ngono ambao huchochea tamaa hizo katika njia mbalimbali. Hiyo inaweza kufanya iwe vigumu sana kwa Wakristo wanaotaka kubaki waseja—angalau kwa muda—ili kumtumikia Mungu bila vikengeusha-fikira vinavyosababishwa na ndoa. (1 Wakorintho 7:32, 33, 37, 38) Lakini kupatana na amri ya Kimaandiko kwamba “ni bora kuoa na kuolewa kuliko kuwashwa na harara,” huenda wakaamua kufunga ndoa, jambo ambalo bila shaka linaheshimika. Wakati huohuo wameazimia kufunga ndoa “katika Bwana tu,” kama Maandiko yanavyoshauri. (1 Wakorintho 7:9, 39) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hufurahia kuona tamaa yao ya kufuata kanuni zake za uadilifu. Wakristo wenzao hufurahi kushirikiana na waabudu wa kweli wanaofuata viwango vya juu vya maadili na uaminifu-maadili.

11. Tunaweza kumsaidiaje ndugu au dada ambaye anataka kufunga ndoa lakini hajaweza kufanya hivyo?

11 Namna gani ikiwa mtu hawezi kupata mwenzi anayefaa? Wazia jinsi mtu anavyoweza kuvunjika moyo ikiwa anataka kufunga ndoa lakini hajaweza kufanya hivyo! Huenda akaona marafiki wake wakifunga ndoa na kupata furaha ya kadiri fulani, huku akiwa bado anatafuta mwenzi anayefaa. Huenda wengine walio katika hali hiyo wakawa na tatizo la kudumu la kupiga punyeto. Kwa vyovyote vile, hakuna Mkristo yeyote ambaye angependa kumvunja moyo bila kujua Mkristo mwenzake anayejitahidi kudumisha usafi wa kiadili. Huenda tukawavunja wengine moyo bila kukusudia ikiwa tutawauliza swali kama hili bila kufikiri, “Utafunga ndoa wakati gani?” Huenda mtu akauliza hivyo bila nia mbaya, lakini ingekuwa vema sana kama tungejidhibiti kwa kulinda ulimi wetu! (Zaburi 39:1) Tunapaswa kuwapongeza sana waseja walio kati yetu ambao wanadumisha usafi wa kiadili. Badala ya kusema mambo yanayoweza kuwavunja moyo tunaweza kujitahidi kuwatia moyo. Kwa mfano, tunaweza kujitahidi kuwaalika waseja wakati kikundi kidogo cha Wakristo waliokomaa wanapokutana kula pamoja au kufurahia ushirika wa Kikristo unaofaa.

Kujidhibiti Katika Ndoa

12. Kwa nini hata wale waliofunga ndoa wanahitaji kujidhibiti kwa kadiri fulani?

12 Hata kama umefunga ndoa, hiyo haimaanishi kwamba hutahitaji kujidhibiti kuhusiana na ngono. Kwa mfano, huenda mahitaji ya ngono ya mume na mke yakatofautiana sana. Au huenda nyakati nyingine hali ya mwenzi mmoja ikafanya iwe vigumu au isiwezekane kuwa na uhusiano wa ngono. Labda kwa sababu ya mambo yaliyotukia zamani, huenda ikawa vigumu kwa mwenzi mmoja kutii amri hii: “Acha mume ampe mke wake haki yake; lakini acha mke pia afanye hivyohivyo kwa mume wake.” Katika hali kama hiyo, huenda mwenzi yule mwingine akahitaji kujidhibiti zaidi. Lakini wote wawili wanapaswa kukumbuka shauri la Paulo lenye upendo kwa Wakristo waliofunga ndoa: “Msiwe mkinyimana hiyo, ila kwa makubaliano kwa wakati uliowekwa rasmi, ili mpate kutumia wakati kwa sala na mpate kuja pamoja tena, ili Shetani asipate kufuliza kuwashawishi kwa sababu ya kukosa kwenu kujirekebisha.”—1 Wakorintho 7:3, 5.

13. Tunaweza kufanya nini kwa niaba ya wale wanaojitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti?

13 Wale waliofunga ndoa wanaweza kufurahi sana ikiwa wote wawili wamejifunza kujidhibiti ifaavyo katika uhusiano huo ulio wa karibu sana. Wakati huohuo, wanapaswa kuelewa hali za waabudu wenzao ambao bado wanajitahidi kuonyesha sifa hiyo kuhusiana na ngono. Hatupaswi kamwe kusahau kusali kwa Yehova ili awapatie ndugu zetu wa kiroho ufahamu, ujasiri, na nia ya kuendelea na pambano lao la kuonyesha sifa ya kujidhibiti na kuchukua hatua kushinda tamaa zisizofaa.—Wafilipi 4:6, 7.

Endeleeni Kusaidiana

14. Kwa nini tunapaswa kushughulika na Wakristo wenzetu kwa huruma na kwa kuelewa hali zao?

14 Nyakati nyingine, huenda ikawa vigumu kwetu kuelewa hali za Wakristo wenzetu ambao wanajitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kuhusiana na jambo fulani ambalo kwetu si tatizo. Lakini watu wanatofautiana kiasili. Baadhi yao huongozwa na hisia kwa urahisi; nao wengine huzidhibiti. Wengine huona ni rahisi kujidhibiti. Kwao hilo si tatizo kubwa. Wengine huona ni vigumu zaidi kujidhibiti. Hata hivyo, kumbuka kwamba mtu anayejitahidi si mbaya. Tunahitaji kuelewa hali za Wakristo wenzetu na kuwaonyesha huruma. Tunapata furaha tunapoendelea kuwaonyesha huruma wale ambao bado wanajitahidi kuonyesha sifa ya kujidhibiti kwa kiwango kikubwa zaidi. Tunaweza kuona jambo hilo katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:7.

15. Kwa nini maneno ya Zaburi 130:3 yanafariji kuhusiana na kujidhibiti?

15 Hatungependa kamwe kumwelewa vibaya Mkristo mwenzetu ambaye huenda pindi fulani akakosa kuonyesha utu wa Kikristo. Inatia moyo kama nini kujua kwamba mbali na kuona pindi moja ambapo labda tulishindwa kuonyesha sifa ya kujidhibiti, Yehova anaona pindi nyingi ambapo tulisimama imara hata ikiwa Wakristo wenzetu hawakuona jambo hilo! Inafariji sana kukumbuka maneno ya Zaburi 130:3: “BWANA, kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?”

16, 17. (a) Tunaweza kutumiaje andiko la Wagalatia 6:2, 5 kuhusiana na kujidhibiti? (b) Tutazungumzia mambo gani kuhusu kujidhibiti katika makala inayofuata?

16 Ili kumpendeza Yehova, lazima kila mmoja wetu asitawishe sifa ya kujidhibiti, lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba ndugu zetu Wakristo watatusaidia. Ingawa ni lazima kila mmoja wetu abebe mzigo wake wa daraka, tunahimizwa tusaidiane ili kukabiliana na udhaifu mbalimbali. (Wagalatia 6:2, 5) Tunaweza kumthamini sana mzazi, mwenzi wa ndoa, au rafiki anayetuzuia tusiende mahali tusipopaswa kwenda, kutazama vitu tusivyopaswa kutazama, au kufanya mambo tusiyopaswa kufanya. Anatusaidia kuonyesha sifa ya kujidhibiti, yaani uwezo wa kukataa kabisa mambo fulani.

17 Huenda Wakristo wengi wanakubaliana na mambo ambayo tumezungumzia kuhusu sifa ya kujidhibiti, lakini huenda wakahisi kwamba wanapaswa kufanya maendeleo zaidi. Wangependa kuonyesha sifa ya kujidhibiti kikamili zaidi, kwa kadiri ambavyo wanaona inawezekana kwa wanadamu wasio wakamilifu. Je, unahisi hivyo? Hivyo basi, unaweza kufanya nini ili kusitawisha sifa hii ambayo ni mojawapo ya matunda ya roho ya Mungu? Na kufanya hivyo kunaweza kukusaidiaje kutimiza miradi yako ya muda mrefu ukiwa Mkristo? Acheni tuone jambo hilo katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

 

• Kwa nini ni muhimu kwa Wakristo kusitawisha sifa ya kujidhibiti?

• Kwa nini ni vigumu hasa kwa wengine kuonyesha sifa ya kujidhibiti?

• Kwa nini sifa ya kujidhibiti ni muhimu katika ndoa?

• Kwa nini kujidhibiti ni sifa ambayo tunaweza kusaidiana kuisitawisha?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

Alijifunza Kukataa Kabisa

Mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeishi Ujerumani alikuwa ameajiriwa kama karani kwenye mitambo ya mawasiliano. Kazi yake ilitia ndani kuchunguza vipindi 30 vya televisheni na redio. Wakati hitilafu zilipotokea, ilimbidi kutazama kipindi kilichohusika ili kujua tatizo ni nini. Anasema: “Yaonekana nyakati zote hitilafu hizo zilitokea wakati usiofaa, wakati tu picha za jeuri au ngono zilipokuwa zikionyeshwa. Picha hizo mbaya zilibaki akilini mwangu kwa siku au majuma kadhaa, kana kwamba zilikuwa zimechapwa kwenye ubongo wangu.” Anakiri kwamba picha hizo ziliathiri hali yake ya kiroho: “Kwa kawaida mimi hukasirika upesi, kwa hiyo picha za jeuri zilifanya iwe vigumu kwangu kuonyesha sifa ya kujidhibiti. Picha za ngono zilisababisha hali ya kutoelewana kati yangu na mke wangu. Nilipambana kila siku na uvutano huo. Ili nisishindwe na uvutano huo, niliamua kutafuta kazi nyingine, hata kama ningelipwa mshahara mdogo zaidi. Hivi majuzi nilipata kazi nyingine. Tamaa yangu imetimizwa.”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ujuzi tunaopata kwa kujifunza Biblia hutusaidia kuonyesha sifa ya kujidhibiti