Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yehova alikuwa anamtaja nani kuwa “mmoja wetu” kwenye Mwanzo 3:22?

Yaonekana Yehova Mungu alikuwa anajitaja mwenyewe na Mwana wake mzaliwa wa pekee aliposema: “Huyu mtu amekuwa kama mmoja wetu, kwa kujua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:22) Acheni tuone ni kwa nini.

Yehova alisema maneno hayo baada ya kuwahukumu wanadamu wawili wa kwanza. Wengine wameelewa maneno “mmoja wetu” kuwa usemi unaotumiwa kwa namna ya wingi ili kuonyesha utukufu. Hata hivyo, msomi wa Biblia Donald E. Gowan anasema hivi kuhusu andiko la Mwanzo 1:26 na 3:22: “Agano la Kale haliungi mkono ufafanuzi mbalimbali unaodai kwamba neno la wingi ‘sisi’ linaonyesha utukufu . . . au linadokeza wingi kuhusiana na kuwepo kwa watu watatu katika Mungu mmoja. Hakuna mojawapo ya ufafanuzi huo unaotoa maana kamili ya andiko la Mwanzo 3:22, ambalo linataja ‘mmoja wetu.’”

Je, Yehova alikuwa akimtaja Shetani Ibilisi, aliyekuwa ameanza kuamua peke yake kuhusu “mema na mabaya,” na ambaye aliwashawishi wanadamu wa kwanza wafanye vivyo hivyo? Hilo si jambo linalopatana na akili. Hapa Yehova alitumia usemi “mmoja wetu.” (Italiki ni zetu.) Shetani hakuwa miongoni mwa kundi la malaika waaminifu wa Yehova, hivyo hangeweza kuwa mmoja wa wale ambao walikuwa upande wa Yehova.

Je, Mungu alikuwa anataja malaika waaminifu? Hatuwezi kuwa na hakika. Hata hivyo, ufanani uliopo kati ya andiko la Mwanzo 1:26 na 3:22 unatudokezea jambo fulani. Katika andiko la Mwanzo 1:26, tunasoma kwamba Yehova alisema: “Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” (Italiki ni zetu.) Alikuwa anazungumza na nani? Mtume Paulo alisema hivi kuhusu kiumbe wa roho Yesu, ambaye alikuwa mwanadamu mkamilifu: “Yeye ndio mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote; kwa sababu kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa katika mbingu na juu ya dunia.” (Wakolosai 1:15, 16) Naam, linaonekana kuwa jambo linalopatana na akili kwamba katika Mwanzo 1:26, Yehova alikuwa akizungumza na Mwana wake mzaliwa wa pekee, aliye “stadi wa kazi,” ambaye alikuwa kando yake alipokuwa akiumba mbingu na dunia. (Mithali 8:22-31) Ufanani wa usemi ulio katika Mwanzo 3:22 unadokeza kwamba Yehova alikuwa akizungumza tena na Mwana wake mzaliwa wa pekee aliye karibu sana naye.

Yaonekana Mwana mzaliwa pekee wa Mungu alijua “mema na mabaya.” Bila shaka, kwa kuwa alishirikiana kwa ukaribu na kwa muda mrefu na Yehova, Yesu alijua mawazo, kanuni, na viwango vya Baba yake. Kwa kuwa Yehova alikuwa na hakika kwamba Mwana wake alijua mambo hayo na alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kuyahusu, huenda alimpa uhuru wa kushughulikia mambo fulani moja kwa moja bila kushauriana Naye. Kwa hiyo, kufikia wakati huo, Mwana angeweza na alikuwa na mamlaka ya kuamua kati ya mema na mabaya. Hata hivyo, Yesu hakuweka kiwango cha mema na mabaya kilichopingana na cha Yehova kama vile Shetani, Adamu, na Hawa walivyofanya.