Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kufanya Maamuzi ya Hekima?

Unawezaje Kufanya Maamuzi ya Hekima?

Unawezaje Kufanya Maamuzi ya Hekima?

MFALME Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu.” Nyakati fulani wengi wetu tumefanya maamuzi yasiyo ya hekima kwa sababu tu tulikataa kusikiliza mashauri ya wengine.—Mithali 1:5.

Baadaye, maneno hayo ya Sulemani yaliandikwa katika Biblia, pamoja na ‘methali nyingine elfu tatu’ alizotunga. (1 Wafalme 4:32, Biblia Habari Njema) Je, tunaweza kunufaika kwa kujua na kutii maneno yake ya hekima? Ndiyo. Yanatusaidia “kujua hekima na adabu; kutambua maneno ya ufahamu; kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili.” (Mithali 1:2, 3) Acheni tuzungumzie kanuni tano zinazotegemea Biblia ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima.

Fikiria Matokeo ya Muda Mrefu

Maamuzi fulani yatakuwa na matokeo muhimu. Kwa hiyo, jaribu kujua mapema matokeo yatakavyokuwa. Uwe mwangalifu manufaa ya muda mfupi yasikupumbaze ukose kuona matokeo mabaya ya muda mrefu. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia,” linaonya andiko la Mithali 22:3.

Huenda ikafaa kuandika orodha ya matokeo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Huenda matokeo ya muda mfupi ya kuchagua kazi fulani yakawa mshahara mnono au kazi yenye kufurahisha. Lakini je, matokeo ya muda mrefu yanaweza kutia ndani kuwa na kazi ambayo haina matarajio mazuri ya baadaye? Je, huenda mwishowe kazi hiyo ikakufanya uhamie mahali pengine, labda mbali na marafiki au familia? Je, huenda ikakulazimu kukaa katika mazingira yasiyofaa au huenda isiwe yenye kupendeza na hivyo kukukatisha tamaa sana? Fikiria faida na madhara, kisha uamue utatanguliza nini.

Tumia Wakati wa Kutosha

Ni rahisi kufanya maamuzi yasiyo ya hekima ikiwa utayafanya haraka-haraka. Andiko la Mithali 21:5, NW, linaonya: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huulekea uhitaji.” Kwa mfano, vijana waliopumbazika kimahaba hawapaswi kuamua kufunga ndoa haraka-haraka. La sivyo, huenda wakakubaliana na maneno haya ya mwandishi Mwingereza wa michezo ya kuigiza, William Congreve, aliyeandika miaka ya mapema ya 1700: “Watu wanaofunga ndoa haraka-haraka huenda wakajuta kwa muda mrefu.”

Hata hivyo, kutumia wakati wa kutosha hakumaanishi kukawia-kawia. Maamuzi mengine ni muhimu sana hivi kwamba ni jambo la hekima kuyafanya haraka iwezekanavyo. Kukawia-kawia isivyofaa kunaweza kutuletea sisi au wengine hasara kubwa. Huenda kuahirisha kufanya uamuzi fulani, kukawa kwenyewe uamuzi mwingine, lakini hilo si jambo la hekima.

Kubali Mashauri

Kwa kuwa hali haziwezi kufanana kabisa, huenda watu wawili wakafanya maamuzi tofauti ingawa wanakabili matatizo yaleyale. Hata hivyo, inafaa kusikiliza jinsi wengine walivyoamua mambo katika hali zinazofanana na zetu. Waulize jinsi wanavyoyaona maamuzi yao sasa. Kwa mfano, unapochagua kufanya biashara fulani, waulize wale ambao tayari wanaifanya wakueleze faida na hasara za biashara hiyo. Wamepata manufaa gani kwa kuchagua kufanya biashara hiyo, na wamepata hasara gani au biashara hiyo inaweza kuwa na hatari gani?

Tunaonywa kwamba “pasipo mashauri makusudi hubatilika; bali kwa wingi wa washauri huthibitika.” (Mithali 15:22) Bila shaka, tunapotafuta mashauri na kujifunza kutokana na mambo yaliyowapata wengine, tunapaswa kutambua kabisa kwamba sisi wenyewe ndio tutakaofanya uamuzi wa mwisho na pia kuwajibika kwa uamuzi huo.—Wagalatia 6:4, 5.

Sikiliza Dhamiri Iliyozoezwa Vizuri

Dhamiri inaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayopatana na kanuni za msingi tunazochagua kufuata maishani. Kwa Mkristo, hilo linamaanisha kuzoeza dhamiri ili itende kupatana na mawazo ya Mungu. (Waroma 2:14, 15) Neno la Mungu linatuambia hivi: “Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:6) Bila shaka, katika hali fulani, huenda watu wawili—kila mmoja akiwa na dhamiri iliyozoezwa vizuri—wakafikia mikataa tofauti na hivyo kufanya maamuzi yaliyo tofauti.

Hata hivyo, dhamiri iliyozoezwa vizuri itamzuia mtu kuamua kutofanya mambo yanayoshutumiwa moja kwa moja na Neno la Mungu. Kwa mfano, huenda dhamiri ambayo haijazoezwa na kanuni za Biblia ikamruhusu mwanamume na mwanamke kuishi pamoja kabla ya kufunga ndoa ili kuona kama wanafaana. Huenda wakafikiri kwamba wamefanya uamuzi wa hekima, wakisema kwamba hatua hiyo itawazuia kufanya jambo lisilo la hekima la kufunga ndoa haraka-haraka. Huenda wasisumbuliwe na dhamiri yao. Lakini, yeyote aliye na maoni kama ya Mungu kuhusu ngono na ndoa hataamua kuchukua hatua hiyo ya muda na isiyo ya adili.—1 Wakorintho 6:18; 7:1, 2; Waebrania 13:4.

Jinsi Maamuzi Yako Yanavyowaathiri Wengine

Mara nyingi, huenda maamuzi yako yakawaathiri wengine. Kwa hiyo, usifanye kimakusudi maamuzi yasiyo ya hekima au hata ya kipumbavu ambayo yanaweza kuhatarisha uhusiano wako wenye thamani pamoja na marafiki na watu wa ukoo, na hasa pamoja na Mungu. Andiko la Mithali 10:1 linasema: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.”

Kwa upande mwingine, unapaswa kutambua kwamba nyakati nyingine utalazimikakuamua ni nani watakaokuwa marafiki wako. Kwa mfano, huenda ukaamua kukataa maoni ya kidini uliyokuwa nayo zamani kwa kuwa sasa unajua kwamba yanapingana na Maandiko. Au huenda ukaamua kufanya mabadiliko makubwa kuhusiana na utu wako kwa sababu unatamani kuishi kupatana na kanuni za Mungu ambazo sasa umekubali. Huenda baadhi ya marafiki au watu wa ukoo wasipendezwe na uamuzi wako, lakini uamuzi wowote unaompendeza Mungu ni wa hekima.

Fanya Uamuzi Ulio Mkuu Zaidi kwa Hekima

Kila mtu leo anakabili uamuzi kati ya uhai na kifo ingawa watu kwa ujumla hawajui jambo hilo. Waisraeli wa kale walikabili hali kama hiyo walipokuwa wamepiga kambi kwenye mpaka wa Nchi ya Ahadi mwaka wa 1473 K.W.K. Akiwa msemaji wa Mungu, Musa aliwaambia hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako, ili ukae katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo kwamba atawapa wao.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20, NW.

Unabii na matukio ya Biblia yanaonyesha kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” na kwamba “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (2 Timotheo 3:1; 1 Wakorintho 7:31) Badiliko lililotabiriwa litafikia upeo wakati mfumo wa wanadamu, ambao hauna lolote la thamani utakapoharibiwa na mahali pake kuchukuliwa na ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.

Tunakaribia sana kuingia katika ulimwengu huo mpya. Je, utaingia na kufurahia uhai wa milele duniani chini ya Ufalme wa Mungu? Au utaondolewa duniani wakati mfumo wa Shetani utakapoondolewa? (Zaburi 37:9-11; Mithali 2:21, 22) Wewe mwenyewe ndiye unayeamua hatua unayopaswa kuchukua sasa, na kwa kweli uamuzi wako unamaanisha uhai au kifo. Je, ungependa kusaidiwa kufanya uamuzi unaofaa na ulio wa hekima?

Ukiamua kufanya uamuzi wa kupata uhai, unahitaji kujifunza matakwa ya Mungu. Kwa kadiri kubwa, makanisa yameshindwa kueleza matakwa hayo kwa usahihi. Mara nyingi viongozi wao wamewapotosha watu kuamini uwongo na kufanya mambo yasiyompendeza Mungu. Wamepuuza kuwaeleza watu uhitaji wa kufanya uamuzi wa kibinafsi wa kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ndiyo sababu watu wengi hawafanyi hivyo. Lakini ona vile Yesu alivyosema: “Yeye asiyekuwa upande wangu yuko dhidi yangu, naye asiyekusanya pamoja nami hutawanya.”—Mathayo 12:30.

Mashahidi wa Yehova hufurahi kuwasaidia watu kulielewa vema zaidi Neno la Mungu. Wao huzungumzia masuala ya Biblia kwa ukawaida pamoja na watu mmoja-mmoja au vikundi, nao hufanya hivyo wakati na mahali panapowafaa watu hao. Wale ambao wangependa kunufaika na mpango huo wanapaswa kuwasiliana na Mashahidi walio katika eneo lao au kuwaandikia wachapishaji wa Mnara wa Mlinzi.

Bila shaka, huenda wengine tayari wanajua matakwa ya msingi ya Mungu. Huenda hata wanaamini kwamba Biblia ni ya kweli na yenye kutegemeka. Hata hivyo, baadhi yao wameahirisha uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Mungu. Kwa nini? Huenda wakawa na sababu kadhaa.

Labda hawajui umuhimu wa kufanya hivyo. Yesu alisema hivi waziwazi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbingu, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye katika mbingu ataingia.” (Mathayo 7:21) Kuijua Biblia peke yake hakutoshi; tunahitaji kuchukua hatua fulani. Kutaniko la Kikristo la mapema liliweka kielelezo. Tunasoma hivi kuhusu baadhi yao katika karne ya kwanza: “Walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo, waliendelea kubatizwa, wanaume na pia wanawake.” (Matendo 2:41; 8:12) Hivyo, ikiwa mtu amekubali Neno la Mungu kwa moyo wote, anaamini linavyosema, na anaishi kupatana na viwango vya Mungu, ni nini kitakachomzuia asibatizwe ili kuonyesha kwamba amejiweka wakfu? (Matendo 8:34-38) Bila shaka, ili akubaliwe na Mungu, anapaswa kuchukua hatua hiyo kwa hiari na kwa furaha.—2 Wakorintho 9:7.

Huenda wengine wakahisi kwamba hawana ujuzi wa kutosha kuweza kujiweka wakfu kwa Mungu. Lakini kila mtu anayeanza jambo jipya maishani huwa hana ujuzi mwingi. Hakuna mtaalamu anayeweza kudai kwamba alikuwa na ujuzi alio nao sasa wakati alipoanza kazi yake. Ili kuamua kumtumikia Mungu unahitaji tu ujuzi wa msingi kuhusu mafundisho na kanuni za Biblia pamoja na tamaa ya kweli ya kuishi kupatana na mambo hayo.

Je, wengine hukawia kufanya uamuzi wakiogopa kwamba huenda wakashindwa kuishi kupatana na uamuzi wao? Wanadamu huwa na wasiwasi wa kadiri fulani kuhusu kushindwa kutimiza wajibu mbalimbali. Huenda mtu anayeamua kufunga ndoa na kuwa na familia akahisi kwamba hawezi kutimiza daraka hilo, lakini uwajibikaji utamchochea kufanya yote awezayo. Vivyo hivyo, huenda kijana ambaye amepata leseni ya kuendesha gari hivi karibuni akaogopa kusababisha aksidenti, hasa ikiwa anajua kwamba madereva wengi vijana husababisha aksidenti nyingi zaidi kuliko watu wenye umri mkubwa. Hata hivyo, habari hiyo inaweza kumnufaisha na kumfanya aendeshe gari kwa uangalifu zaidi. Kukataa kuchukua leseni hakusuluhishi lolote!

Fanya Uamuzi wa Kupata Uhai!

Biblia inaonyesha kwamba hivi karibuni mfumo wa sasa wa kisiasa, kiuchumi, na kidini na wale wanaouunga mkono, utapitilia mbali. Lakini watu ambao wameamua kwa hekima kufuata njia ya uhai na wanaotenda kulingana na uamuzi huo watabaki. Wakiwa jamii ya kwanza katika ulimwengu mpya, watashiriki kuifanya dunia kuwa paradiso kama Mungu alivyokusudia. Je, wewe ungefurahia kushiriki katika kazi hiyo yenye kuleta furaha chini ya mwongozo wa Mungu?

Ikiwa ndivyo, amua kujifunza Neno la Mungu. Amua kujifunza matakwa ya Mungu ili kumpendeza. Amua kuyafuata. Zaidi ya yote, amua kuendelea kushikamana na uamuzi wako mpaka mwisho. Kwa ufupi, fanya uamuzi wa kupata uhai!

[Picha katika ukurasa wa 4]

Tumia wakati wa kutosha kufanya maamuzi mazito

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kubali mashauri unapochagua kazi utakayofanya

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wale wanaoamua kumtumikia Mungu leo watashiriki kazi ya kuifanya dunia iwe paradiso