Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Tembeeni kwa Kumstahili Yehova

Vijana, Tembeeni kwa Kumstahili Yehova

Vijana, Tembeeni kwa Kumstahili Yehova

VIJANA fulani Wakristo wamelazimika kuishi kwa muda mbali na familia zao na kutaniko lao la nyumbani. Baadhi yao wamefanya hivyo ili kupanua huduma yao. Wengine wamelazimika kuondoka nyumbani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo katika mambo ya ulimwengu huu. (Isaya 2:4; Yohana 17:16) Katika nchi fulani, “Kaisari” amewahukumu vijana wanaoshika uaminifu-maadili kufungwa gerezani au kufanya kazi ya jamii. *Marko 12:17; Tito 3:1, 2.

Wanapotumikia kifungo chao gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo, huenda vijana hao wakafungwa kwa muda mrefu pamoja na vijana wahalifu. Vijana wengine wameondoka nyumbani kwa sababu nyinginezo na hivyo kulazimika kufanya kazi katika mazingira yasiyofaa kiadili. Vijana hao Wakristo na watu wengine ambao wamelazimika kuishi katika hali hizo wanawezaje kufanikiwa kukabiliana na mikazo na magumu yanayowapata wanapojitahidi “kutembea kwa ustahili wa Mungu?” (1 Wathesalonike 2:12) Wazazi wao wanawezaje kuwasaidia wajitayarishe kukabiliana na hali zisizofaa zinazoweza kuwapata?—Mithali 22:3.

Magumu Yanayowapata Vijana Hao

“Lilikuwa jambo gumu na lenye kuogopesha kuwa mbali na ulinzi wa wazazi wangu na pia uangalizi wenye upendo wa wazee ambao walinijua vizuri,” anasema Tákis mwenye umri wa miaka 21, ambaye alilazimika kuishi mbali na nyumbani kwa miezi 37. * Anaendelea kusema: “Nyakati nyingine, nilihisi sina ulinzi wowote.” Pétros mwenye umri wa 21 alilazimika kuondoka nyumbani kwa zaidi ya miaka miwili. Anakiri hivi: “Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nililazimika kufanya maamuzi peke yangu kuhusu vitumbuizo na mashirika lakini maamuzi yangu hayakuwa ya hekima wakati wote.” Kisha anasema: “Nyakati nyingine nilikuwa na wasiwasi kuhusu majukumu yaliyoongezeka kwa sababu ya kuwa na uhuru zaidi.” Tássos, mzee Mkristo ambaye hukutana kwa ukawaida na vijana Wakristo katika hali hizo, alisema: “Vijana wasio na tahadhari na wasio na ulinzi wanaweza kuathiriwa na lugha chafu, uasi, na mwenendo wa jeuri wa vijana wenzao wasioamini.”

Vijana Wakristo wanapoishi na kufanya kazi na watu wasioheshimu kanuni za Biblia, wanapaswa kujihadhari wasishawishiwe kuiga mwenendo wa vijana wenzao usio wa adili na usiopatana na Maandiko. (Zaburi 1:1; 26:4; 119:9) Huenda ikaonekana kuwa vigumu kudumisha ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na kuhubiri. (Wafilipi 3:16) Huenda pia ikawa vigumu kujiwekea miradi ya kiroho na kuitimiza.

Bila shaka, vijana Wakristo walio waaminifu wangependa kumfurahisha Yehova kwa mwenendo na usemi wao. Wanajitahidi kwa uaminifu kutii mwaliko huu wenye kuvutia wa Baba yao wa mbinguni: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Wanatambua kwamba adabu na mwenendo wao huathiri maoni ya wengine kumhusu Yehova na watu wake.—1 Petro 2:12.

Ni jambo zuri kwamba vijana wengi hujitahidi wawezavyo kuwaiga ndugu zao wa karne ya kwanza ambao mtume Paulo alisali hivi kuwahusu: “Mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema . . . ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Wakolosai 1:9-11) Biblia inataja mifano kadhaa ya vijana waliomwogopa Mungu ambao walifanikiwa kutembea kwa kumstahili Mungu wakiwa katika mazingira ya kigeni, yenye uhasama, na ibada ya sanamu.—Wafilipi 2:15.

“Yehova Alikuwa Pamoja na Yosefu”

Alipokuwa mchanga, Yosefu, mwana mpendwa wa Yakobo na Raheli, alijikuta mbali sana na nyumbani ambapo alipata ulinzi wa baba yake mwenye kumwogopa Mungu. Alipouzwa utumwani huko Misri, Yosefu aliweka mfano mzuri sana wa kuwa kijana mwenye bidii, mwenye kutumainika, na mwenye maadili. Ingawa alimtumikia Potifa ambaye hakuwa mwabudu wa Yehova, Yosefu alikuwa makini na mwenye bidii hivi kwamba mwishowe bwana wake alimkabidhi mambo yote ya nyumbani. (Mwanzo 39:2-6) Yosefu alishika uaminifu-maadili wake kwa Yehova, na alipotupwa gerezani kwa sababu ya jambo hilo, yeye hakusema: “Kuna haja gani kushika uaminifu-maadili?” Hata alipokuwa gerezani alionyesha sifa nzuri, na baada ya muda mfupi akawa msimamizi wa kazi mbalimbali gerezani. (Mwanzo 39:17-22) Mungu alimbariki, na kama inavyotajwa kwenye Mwanzo 39:23, NW, “Yehova alikuwa pamoja na Yosefu.”

Ingalikuwa rahisi sana kwa Yosefu, ambaye alikuwa ametenganishwa na familia yake yenye kumwogopa Mungu, kufuata mwenendo wa wapagani ambao aliishi kati yao, na kuiga maisha ya Wamisri yasiyo na maadili. Lakini aliendelea kufuata kanuni za Mungu na kudumisha msimamo safi ingawa alikabili vishawishi vikali sana. Mke wa Potifa alipomsihi tena na tena afanye mapenzi naye, Yosefu alimjibu hivi kwa uthabiti: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?”—Mwanzo 39:7-9.

Leo, vijana Mashahidi wanahitaji kutii maonyo ya Biblia kuhusu mashirika yasiyofaa, vitumbuizo visivyo vya adili, ponografia, na muziki unaoshusha heshima. Wanatambua kwamba “Macho ya BWANA yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.”—Mithali 15:3.

Musa Alikataa ‘Mfurahio wa Dhambi’

Musa alikulia katika nyumba ya Farao ambako kulikuwa na ibada ya sanamu na watu waliopenda kujifurahisha. Biblia inasema hivi kumhusu: “Kwa imani Musa . . . alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akichagua kutendwa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kuwa na mfurahio wa muda wa dhambi.”—Waebrania 11:24, 25.

Urafiki na ulimwengu unaweza kuwa na manufaa fulani, lakini urafiki huo ni wa muda mfupi. Unaweza tu kudumu kwa muda ambao ulimwengu huu utaendelea kuwapo. (1 Yohana 2:15-17) Je, haingekuwa afadhali kufuata kielelezo cha Musa? Biblia inasema kwamba “aliendelea akiwa imara kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Alitafakari juu ya urithi wa kiroho wa mababu wake waliomwogopa Mungu. Aliamua kutenda kupatana na kusudi la Yehova maishani mwake, na kuweka mradi wa kufanya mapenzi yake.—Kutoka 2:11; Matendo 7:23, 25.

Vijana wenye kumwogopa Mungu wanapojikuta kati ya watu wasiomwogopa Mungu na wasio na urafiki, wanaweza kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova kupitia funzo la kibinafsi na hivyo kupata kumjua vizuri zaidi “Yeye asiyeonekana.” Kuwa na utendaji mwingi wa Kikristo, kutia ndani kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na kuhubiri, kutawasaidia vijana hao watafakari juu ya mambo ya kiroho. (Zaburi 63:6; 77:12) Wanapaswa kujitahidi kusitawisha imani na tumaini lenye nguvu kama la Musa. Wanapaswa kujitahidi kumzingatia Yehova katika mawazo na matendo yao na kufurahia kuwa marafiki wake.

Alitumia Ulimi Wake Kumsifu Mungu

Kijana mwingine aliyeweka kielelezo kizuri akiwa mbali na nyumbani ni msichana Mwisraeli aliyetekwa na Washami katika siku za nabii wa Mungu Elisha. Alikuwa kijakazi wa mke wa Naamani, mkuu wa jeshi la Washami, aliyekuwa na ukoma. Msichana huyo alimwambia hivi bimkubwa wake: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake.” Kwa sababu ya ushahidi wake, Naamani alienda kwa Elisha huko Israeli na kutakaswa ukoma wake. Isitoshe, Naamani alipata kuwa mwabudu wa Yehova.—2 Wafalme 5:1-3, 13-19.

Kielelezo cha msichana huyo kinakazia kwamba vijana wanahitaji kutumia ulimi wao katika njia inayomheshimu Mungu, hata wanapokuwa mbali na wazazi wao. Kama msichana huyo angalikuwa na mazoea ya ‘kuongea kipumbavu’ au ‘kufanya mizaha yenye aibu,’ je, ingalikuwa rahisi kwake kutumia ulimi wake kwa matokeo kama alivyofanya alipopata nafasi? (Waefeso 5:4; Mithali 15:2) Níkos, kijana mwenye umri wa miaka 20, ambaye alifungwa kwa sababu ya msimamo wake wa kutokuwamo anakumbuka: “Nilipokuwa na ndugu wengine vijana kwenye gereza la kilimo, mbali na usimamizi wa wazazi wangu na kutaniko, niliona kwamba usemi wetu ulizidi kuwa mbaya. Haukumletea Yehova sifa hata kidogo.” Ni jambo lenye kufurahisha kwamba Níkos na vijana wengine wamesaidiwa kutii shauri la Paulo kuhusu jambo hilo: “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu.”—Waefeso 5:3.

Yehova Alikuwa Halisi Kwao

Mambo yaliyowapata Waebrania watatu waliokuwa marafiki wa Danieli huko Babiloni ya kale, yanaonyesha ukweli wa kanuni iliyotajwa na Yesu kwamba kuwa mwaminifu katika mambo madogo hufanya uwe mwaminifu katika mambo makubwa. (Luka 16:10) Walipokabili tatizo la kula vyakula vilivyokatazwa na Sheria ya Musa, wangeweza kusema kwamba iliwabidi kula vyakula hivyo kwa kuwa walikuwa wafungwa katika nchi ya kigeni. Lakini walibarikiwa kama nini kwa kuchukua kwa uzito jambo ambalo huenda lilionekana kuwa dogo! Walikuwa wenye afya na wenye hekima zaidi kuliko mateka wengine wote walioendelea kula chakula kitamu cha mfalme. Bila shaka, uaminifu katika mambo hayo madogo uliwaimarisha sana hivi kwamba walipokabili jaribu kubwa zaidi la kuinamia sanamu, walikataa kufanya hivyo.—Danieli 1:3-21; 3:1-30.

Yehova alikuwa halisi kabisa kwa vijana hao watatu. Waliazimia kuendelea bila kutiwa doa na ulimwengu, ingawa walikuwa mbali na nchi yao na kituo cha ibada ya Mungu. (2 Petro 3:14) Uhusiano wao pamoja na Yehova ulikuwa wenye thamani sana hivi kwamba walikuwa tayari kudhabihu uhai wao.

Yehova Hatawaacha

Ni jambo linaloeleweka kwamba vijana wanaweza kuhisi kwamba hawana usalama, uhakika, au wakawa na wasiwasi wanapokuwa mbali na watu wanaopenda na kutumaini. Hata hivyo, wanaweza kukabili majaribu yao wakiwa na uhakika kamili kwamba “Yehova hatawaacha.” (Zaburi 94:14, NW) Ikiwa vijana hao ‘watateseka kwa ajili ya uadilifu,’ Yehova atawasaidia waendelee kutembea katika “njia ya haki.”—1 Petro 3:14; Mithali 8:20.

Yehova aliendelea kuwaimarisha na kuwathawabisha sana Yosefu, Musa, msichana mtumwa Mwisraeli, na wale vijana watatu Waebrania. Leo, anatumia roho yake takatifu, Neno lake, na tengenezo lake ili kuwategemeza wale ‘wanaopigana pigano bora la imani,” akiwawekea thawabu ya “uhai udumuo milele.” (1 Timotheo 6:11, 12) Naam, inawezekana kutembea kwa kumstahili Yehova na ni jambo la hekima kufanya hivyo.—Mithali 23:15, 19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1996, ukurasa wa 18-20.

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

WAZAZI—TAYARISHENI WATOTO WENU!

“Kama mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana ujanani.” (Zaburi 127:4) Mshale hauwezi kulenga shabaha yake bila kuelekezwa vizuri. Ni lazima uelekezwe kwa ustadi. Vivyo hivyo, watoto hawatakuwa tayari kukabiliana na hali halisi za maisha wakiwa mbali na nyumbani bila mwongozo unaofaa wa wazazi.—Mithali 22:6.

Vijana wana maelekeo ya kutenda bila kutafakari au kushindwa na “tamaa zenye kutukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Biblia inaonya: “Fimbo na maonyo hutia hekima; bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mithali 29:15) Ukishindwa kumwekea kijana mipaka kuhusiana na mwenendo wake, kijana huyo hatakuwa tayari kukabiliana na magumu na mikazo ya maisha atakapokuwa mbali na nyumbani.

Kwa njia iliyo wazi na thabiti, wazazi Wakristo wanapaswa kuwaeleza watoto wao matatizo, mikazo, na hali halisi za maisha katika mfumo huu wa mambo. Bila kuwa na maoni mabaya au yenye kuvunja moyo, wazazi wanaweza kumweleza kijana wao hali zisizo nzuri anazoweza kukabili anapoishi mbali na nyumbani. Mazoezi hayo, pamoja na hekima kutoka kwa Mungu, ‘yatawapa wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari.’—Mithali 1:4.

Wazazi wanaokazia kanuni za kimungu na za kiadili katika mioyo ya watoto wao huwasaidia wafanikiwe kukabiliana na matatizo ya maisha. Kujifunza Biblia kwa ukawaida, mazungumzo ya wazi, na kupendezwa kikweli na hali ya watoto wao, kunaweza kuwasaidia watoto wafanikiwe au washindwe na matatizo ya maisha. Wazazi wanapaswa kutoa mazoezi ya kimungu kwa njia yenye usawaziko na inayofaa, na hivyo kuwatayarisha watoto wao waweze kujitegemea baadaye maishani. Kupitia kielelezo chao wenyewe, wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao kwamba inawezekana kuwa katika ulimwengu na wasiwe sehemu yake.—Yohana 17:15, 16.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Vijana fulani Wakristo wamelazimika kuondoka nyumbani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kwa kupinga vishawishi, vijana wanaweza kumwiga Yosefu na kubaki wakiwa safi kiadili

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mwige msichana Mwisraeli aliyekuwa mtumwa, ambaye alitumia ulimi wake kumtukuza Yehova