Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunaweza Kumtumaini Yeyote?

Je, Tunaweza Kumtumaini Yeyote?

Je, Tunaweza Kumtumaini Yeyote?

BAADA ya Ukuta wa Berlin kuanguka mwaka wa 1989, mambo fulani yaliyokuwa yamewekwa siri yalifunuliwa. Kwa mfano, Lydia * aligundua kwamba wakati wa utawala wa Kisoshalisti huko Ujerumani Mashariki, Stasi, au Shirika la Usalama la Serikali, lilikuwa na faili iliyokuwa na habari kuhusu shughuli zake za kibinafsi. Ingawa Lydia alishangaa kusikia juu ya faili hiyo, alishtuka alipojua kwamba mume wake ndiye aliyetoa habari hizo kwa shirika hilo la usalama. Alikuwa amesalitiwa na mtu ambaye alipaswa kumtumaini kabisa.

Robert alikuwa mwanamume mzee ambaye “alimheshimu, kumpenda, na kumtumaini sana daktari wake,” laripoti gazeti la The Times la London. Daktari huyo alijulikana kuwa mwenye “fadhili na huruma.” Kisha Robert akafa ghafula. Je, alikufa kwa ugonjwa wa moyo au wa kiharusi? La. Wenye mamlaka waligundua kwamba wakati daktari huyo alipomtembelea Robert nyumbani kwake, alimdunga sindano ya sumu bila yeye wala familia yake kujua. Yaonekana Robert aliuawa na mtu aliyemtumaini kabisa.

Lydia na Robert walisalitiwa vibaya sana na matokeo yakawa mabaya sana. Katika visa vingine, matokeo huwa si mabaya hivyo. Hata hivyo, si ajabu kusalitiwa na mtu ambaye tunamtumaini. Ripoti moja iliyochapishwa na shirika mashuhuri la Ujerumani la kutafuta maoni, Allensbacher Jahrbuch der Demoskopie 1998-2002, ilionyesha katika uchunguzi mmoja kwamba, asilimia 86 ya watu waliohojiwa walisalitiwa na mtu fulani waliyekuwa wamemtumaini. Labda hata wewe umewahi kusalitiwa. Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa kwamba gazeti moja la Uswisi Neue Zürcher Zeitung liliripoti katika mwaka wa 2002 kwamba “katika nchi za Magharibi zilizoendelea kiviwanda, mahusiano kati ya nchi hizo yamezidi kuzorota kwa miaka mingi kwa sababu ya kutotumainiana.”

Husitawishwa Polepole, Huharibiwa Haraka

Inamaanisha nini kumtumaini mtu? Kuwatumaini wengine humaanisha kuamini kwamba wao ni wanyoofu na hawawezi kufanya kimakusudi jambo linaloweza kukuumiza. Imani husitawishwa polepole, lakini inaweza kuharibiwa haraka. Kwa kuwa watu wengi wanahisi kuwa wamesalitiwa, haishangazi kuona kwamba wao husita kuwatumaini wengine. Kulingana na uchunguzi uliochapishwa nchini Ujerumani mnamo mwaka wa 2002, “vijana wasiozidi 1 kati ya 3 ndio wanaoamini watu wengine kwa kiasi fulani.”

Huenda tukajiuliza: ‘Je, tunaweza kumtumaini yeyote? Je, inafaa kumtumaini iwapo kuna uwezekano wa kusalitiwa?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 86 ya watu waliohojiwa walisalitiwa na mtu fulani waliyekuwa wamemtumaini