Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha

Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha

Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha

KUCHAFUKA tumbo kwa sababu ya kula chakula kibaya ni jambo lenye kuudhi sana. Mtu anayechafuka tumbo mara kwa mara anahitaji kuwa mwangalifu kuhusu vitu anavyokula. Lakini si jambo la busara kuacha kula kabisa ili usichafuke tumbo. Kufanya hivyo hakungetatua tatizo hilo bali kungesababisha matatizo zaidi, kwa kuwa hakuna anayeweza kuishi kwa muda mrefu bila chakula.

Vivyo hivyo, mtu huumia sana anaposalitiwa. Kusalitiwa mara nyingi kunaweza kufanya tufikirie kwa makini kuhusu watu tunaochagua kushirikiana nao. Hata hivyo, hatuwezi kutatua tatizo hilo la kusalitiwa kwa kuepuka kabisa kushirikiana na watu. Kwa nini? Kwa sababu kutowatumaini wengine kunaweza kutukosesha furaha. Ili kuwa na maisha yenye kuridhisha, tunahitaji kuwa na uhusiano na wengine na kuwatumaini.

Kitabu Jugend 2002 kinasema, “Kuwatumaini wengine ni mojawapo ya mambo ya msingi yanayofanya iwe rahisi kushirikiana na wengine katika mambo ya kawaida.” Nalo gazeti Neue Zürcher Zeitung linasema kwamba “kila mtu hutamani atumainiwe.” “Kuwatumaini wengine huboresha maisha” sana hivi kwamba ‘ni muhimu kuwa na sifa hiyo ili kuendelea kuishi.’ Naam, gazeti hilo linaendelea kusema, “mtu hawezi kukabiliana na maisha” iwapo hawatumaini wengine.

Kwa kuwa tuna uhitaji wa msingi wa kumtumaini mtu fulani, ni nani tunayeweza kumtumaini bila kuogopa kusalitiwa?

Mtumaini Yehova kwa Moyo Wako Wote

Biblia hutuambia, “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote.” (Methali 3:5, Union Version) Kwa kweli, sikuzote Neno la Mungu hututia moyo tumtegemee Muumba wetu, Yehova Mungu.

Kwa nini tunaweza kumtumaini Mungu? Sababu moja ni kwamba Yehova Mungu ni mtakatifu. Nabii Isaya aliandika: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova.” (Isaya 6:3) Je, huvutiwi na wazo hilo la utakatifu? Linapaswa kukuvutia kwa sababu utakatifu wa Yehova humaanisha kwamba yeye ametakata, hawezi kutenda kosa lolote, na anategemeka kabisa. Hawezi kamwe kupotoka au kututendea vibaya, wala hawezi kutusaliti.

Isitoshe, tunaweza kumtumaini Mungu kwa sababu ya uwezo na tamaa yake ya kuwategemeza wale wanaomtumikia. Kwa mfano, nguvu zake kuu humwezesha kutenda. Yeye hutenda kupatana na haki na hekima yake kamilifu. Nao upendo wake usio na kifani humchochea kutenda. Mtume Yohana aliandika kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Mungu huchochewa na upendo katika yote afanyayo. Utakatifu wa Yehova na sifa zake mbalimbali za kipekee humfanya kuwa Baba bora, tunayeweza kumtumaini kabisa. Hakuna kitu wala mtu yeyote anayeweza kutumainika zaidi kuliko Yehova.

Mtumaini Yehova na Uwe Mwenye Furaha

Sababu nyingine nzuri ya kumtumaini Yehova ni kwamba yeye anatuelewa vizuri zaidi kuliko mtu mwingine yeyote. Yeye anajua kwamba kila mwanadamu ana uhitaji wa msingi wa kuwa na uhusiano salama, wa kudumu, na wa kutumainika pamoja na Muumba. Wale walio na uhusiano kama huo huhisi wakiwa salama zaidi. “Mwenye furaha ni mwanamume ambaye amemfanya Yehova kuwa tegemeo lake,” akasema Mfalme Daudi. (Zaburi 40:4) Watu wengi leo hukubaliana kwa moyo wote na maoni ya Daudi.

Fikiria mifano kadhaa. Doris ameishi Jamhuri ya Dominika, Ujerumani, Ugiriki, na Marekani. Yeye anasema: “Ninafurahi sana kumtumaini Yehova. Yeye anajua jinsi ya kunitunza kimwili, kiroho, na kihisia-moyo. Yeye ndiye rafiki bora zaidi ambaye mtu anaweza kuwa naye.” Wolfgang, mshauri wa kisheria, anasema: “Inafurahisha sana kuweza kumtegemea mtu anayekutakia mema, mtu anayeweza na atakayekufanyia yaliyo mema!” Ham aliyezaliwa barani Asia, na ambaye sasa anaishi Ulaya anasema: “Nina hakika kwamba Yehova anadhibiti mambo yote, naye hawezi kukosea, kwa hiyo ninafurahi kumtegemea.”

Bila shaka, kila mmoja wetu anahitaji kumtumaini Muumba wetu na pia watu wengine. Kwa hiyo, kwa kuwa Yehova ni rafiki mwenye hekima na uzoefu, yeye hutushauri kuhusu watu tunaopaswa kuwatumaini. Kwa kusoma Biblia kwa makini, tunaweza kufahamu shauri lake kuhusu jambo hilo.

Watu Tunaoweza Kuwatumaini

“Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake,” akaandika mtunga-zaburi. (Zaburi 146:3, UV) Andiko hilo lililoongozwa kwa roho ya Mungu hutusaidia kuona kwamba watu walio wengi hawastahili kutumainiwa. Hata sisi hatuwatumaini bila kufikiri watu wanaoheshimiwa sana na kuonwa kuwa “wakuu” wa ulimwengu huu, kama vile wataalamu wa elimu na wa taaluma mbalimbali. Mara nyingi wao hutoa mwongozo wenye kupotosha, na tunaweza kukata tamaa upesi tukiwatumaini “wakuu” hao.

Bila shaka, jambo hilo halipaswi kutuzuia tusimtumaini yeyote. Hata hivyo, ni wazi kwamba tunahitaji kuwa waangalifu tunapochagua watu tunaoweza kuwatumaini. Tunapaswa kutumia kanuni gani? Kuna mfano mmoja katika taifa la kale la Israeli unaoweza kutusaidia. Wakati Musa alipolazimika kuchagua watu ambao wangechukua daraka zito katika Israeli, alishauriwa ‘achague kutoka kati ya watu wote wanaume wenye uwezo, wanaomwogopa Mungu, wanaume wenye kutegemeka, wanaochukia faida isiyo ya haki.’ (Kutoka 18:21) Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

Wanaume hao walionyesha sifa fulani za kimungu kabla ya kuteuliwa kwenye vyeo vyenye kutumainika. Tayari walikuwa wamethibitisha kwamba wanamwogopa Mungu na kwamba walimheshimu Muumba ifaavyo na waliogopa kumchukiza. Ilikuwa wazi kwamba wanaume hao walifanya yote wawezayo kutegemeza viwango vya Mungu. Walichukia faida isiyo ya haki, jambo lililoonyesha kwamba walikuwa na nguvu za kiadili ambazo zingeweza kuwazuia wasipotoke kwa sababu ya kuwa na uwezo. Hawangetumia tumaini ambalo watu waliweka kwao kujinufaisha au kunufaisha jamaa zao au marafiki.

Je, halingekuwa jambo la hekima kutumia kanuni hiyohiyo leo tunapochagua watu tunaoweza kuwatumaini? Je, tunajua watu ambao mwenendo wao huonyesha kwamba wanamwogopa Mungu? Je, wameazimia kudumisha viwango vyake vya mwenendo? Je, wana sifa ya utimilifu inayoweza kuwasaidia waepuke kufanya mambo yasiyofaa? Je, wao ni wanyoofu hivi kwamba hawatumii hali fulani kujinufaisha au kupata wanachotaka? Bila shaka, tunastahili kuwatumaini wanaume na wanawake wanaoonyesha sifa hizo.

Usivunjike Moyo Unapokatishwa Tamaa Mara kwa Mara

Tunapaswa kuwa na subira tunapoamua ni nani tunayeweza kumtumaini kwa kuwa inachukua muda kuanza kumtumaini mtu. Ni jambo la busara kujenga tumaini letu katika mtu pole kwa pole, hatua kwa hatua. Jinsi gani? Tunaweza kuchunguza mwenendo wa mtu kwa muda fulani na kuona jinsi yeye hutenda katika hali fulani. Je, mtu huyo anaweza kutumainika katika mambo madogo? Kwa mfano, je, yeye hurudisha vitu alivyoazima kama alivyoahidi, na je, yeye hufika kwa wakati anapoahidi kuonana na mtu? Ikiwa ndivyo, huenda tukahisi kwamba inafaa kumtumaini katika mambo mazito zaidi. Hilo linapatana na kanuni hii: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi ni mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Kuwa waangalifu na wenye subira kunaweza kutusaidia kuepuka kukatishwa tamaa.

Lakini itakuwaje tukikatishwa tamaa na mtu fulani? Wanafunzi wa Biblia watakumbuka kwamba usiku ambao Yesu Kristo alikamatwa, mitume wake walimkatisha tamaa sana. Yuda Iskariote alimsaliti, nao wale wengine wakakimbia kwa woga. Hata Petro alimkana Yesu mara tatu. Lakini Yesu alitambua kwamba Yuda tu ndiye aliyetenda kimakusudi. Majuma kadhaa baadaye, Yesu aliwahakikishia mitume wake 11 kwamba aliwatumaini ingawa walikuwa wamemkatisha tamaa wakati huo muhimu. (Mathayo 26:45-47, 56, 69-75; 28:16-20) Vivyo hivyo, tunapohisi kwamba tumesalitiwa na mtu tunayemtumaini, tunapaswa kufikiria kama tendo hilo linaloonekana kuwa usaliti ni uthibitisho kwamba mtu huyo hawezi kutumainika au ni udhaifu tu wa muda wa mwili.

Je, Ninatumainika?

Mtu anayeamua kuwa mwangalifu kuhusu watu anaoweza kuwatumaini anapaswa kujiuliza hivi kwa unyoofu: ‘Je, ninatumainika? Ni viwango gani vinavyofaa kuhusu kutumainika ambavyo ninaweza kutazamia mimi na hata wengine watimize?’

Bila shaka, mtu anayetumainika husema kweli daima. (Waefeso 4:25) Yeye hajinufaishi kwa kupinda maneno yake ili yawafae wale wanaomsikiliza. Na anapoweka ahadi, mtu anayetumainika hufanya yote awezayo kutimiza ahadi yake. (Mathayo 5:37) Ikiwa mtu anamweleza jambo fulani la siri, mtu anayetumainika hutunza siri na hapigi porojo. Mtu mwenye kutegemeka ni mwaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa. Hatazami ponografia, hatumii wakati mwingi akiwaza-waza juu ya mambo yanayoamsha tamaa za mwili, naye hachezi-chezi na wengine kimapenzi. (Mathayo 5:27, 28) Mtu tunayeweza kumtumaini hujitahidi kujiruzuku na kuruzuku familia yake, naye hajaribu kujipatia pesa kwa njia rahisi kwa kuwatumia wengine vibaya. (1 Timotheo 5:8) Kukumbuka viwango hivyo vya Kimaandiko vinavyofaa kutatusaidia kutambua wale tunaoweza kuwatumaini. Isitoshe, kufuata viwango hivyo vya mwenendo kutatusaidia sote kuwa watu wanaoweza kutumainiwa na wengine.

Ingefurahisha sana kuishi katika ulimwengu ambapo watu wote wanaweza kutumainika na ambapo hawakati tamaa kwa sababu ya kusalitiwa! Je, hiyo ni ndoto tu? Watu wanaochukua ahadi za Biblia kwa uzito hawaoni hiyo kuwa ndoto kwa sababu Neno la Mungu linatabiri kuja kwa “dunia mpya” nzuri ambayo haitakuwa na udanganyifu, uwongo, kuwatumia watu vibaya, huzuni, ugonjwa, na hata kifo! (2 Petro 3:13; Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:3-5) Je, haingefaa kuchunguza zaidi kuhusu taraja hilo? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukupasha habari zaidi kuhusu jambo hilo na mambo mengine muhimu.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kutowatumaini wengine kunaweza kutukosesha furaha

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yehova ndiye tunayestahili kumtumaini kabisa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Sote tunahitaji kuwa na uhusiano na wengine na kuwatumaini