Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Roho ya Kutoa

Sitawisha Roho ya Kutoa

Sitawisha Roho ya Kutoa

HAKUNA mtu anayezaliwa akiwa na roho ya kutoa. Ni kawaida ya mtoto mchanga kutaka kutosheleza mahitaji yake, bila hata kujali masilahi ya wale wanaomtunza. Hata hivyo, baada ya muda mtoto hugundua kwamba si yeye tu aliye na mahitaji. Lazima afikirie wengine pia, na ajifunze kutoa na kushiriki vitu vyake na wengine bali si kupokea tu. Roho ya kutoa inahitaji kusitawishwa.

Si watu wote wanaotoa walio na roho ya kutoa, hata wale ambao hutoa kwa wingi. Huenda watu fulani wakatoa michango kwa mashirika ya kutoa misaada ili kuendeleza masilahi yao wenyewe. Huenda wengine wakatoa michango ili wasifiwe na watu. Wakristo wa kweli hutoa kwa sababu tofauti. Kwa hiyo, Neno la Mungu linatutia moyo tushiriki katika utoaji wa aina gani? Tutapata jibu kwa kuchunguza kwa ufupi utoaji wa Wakristo wa karne ya kwanza.

Mifano ya Utoaji wa Kikristo

Kama Biblia inavyoonyesha, kwa kawaida utoaji wa Kikristo ulihusisha “kushiriki vitu pamoja na wengine” waliokuwa na uhitaji wa kweli. (Waebrania 13:16; Waroma 15:26) Watu hawakupaswa kulazimishwa kutoa. Mtume Paulo aliandika: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Pia watu hawakutoa ili kujionyesha. Anania na Safira walifanya hivyo na matokeo yakawa mabaya sana.—Matendo 5:1-10.

Kulikuwa na uhitaji mkubwa wa kutoa wakati wageuzwa-imani na Wayahudi wengi kutoka sehemu za mbali walipokusanyika Yerusalemu kusherehekea sikukuu ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Hapo ndipo wafuasi wa Yesu ‘walipojazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti.’ Umati mkubwa ulikusanyika kuwazunguka nao ukasikia hotuba ya Petro yenye kusisimua kumhusu Yesu Kristo. Baadaye, watu hao waliona jinsi Petro na Yohana walivyomponya mtu aliyekuwa kilema kwenye mlango wa hekalu, nao wakamsikia Petro akizungumza tena kumhusu Yesu na uhitaji wa kutubu. Maelfu walitubu na kubatizwa kuwa wafuasi wa Kristo.—Matendo, sura ya 2 na 3.

Wageuzwa-imani hao wapya walitaka kubaki Yerusalemu ili waendelee kufundishwa na mitume wa Yesu. Lakini mitume wangewezaje kutosheleza mahitaji ya wageni hao wote? Biblia inatueleza hivi: ‘Wale wote waliokuwa na mashamba au nyumba walikuwa wakiviuza na kuleta thamani ya vitu vilivyouzwa nao walikuwa wakiviweka miguuni pa mitume. Na kila mmoja alikuwa akigawiwa, kulingana na uhitaji wake.’ (Matendo 4:33-35) Kwa kweli, kutaniko jipya la Yerusalemu lilikuwa na roho ya kutoa!

Baadaye, makutaniko mengine yalionyesha roho kama hiyo ya kutoa. Kwa mfano, ingawa Wakristo wa Makedonia walikuwa maskini, walitoa michango kupita uwezo wao ili kuwasaidia ndugu zao wenye uhitaji huko Yudea. (Waroma 15:26; 2 Wakorintho 8:1-7) Kutaniko la Wafilipi lilitegemeza huduma ya Paulo kwa njia ya pekee. (Wafilipi 4:15, 16) Kutaniko la Yerusalemu lenyewe liligawa chakula kila siku kwa wajane wenye uhitaji, nao mitume wakachagua wanaume saba wanaostahili ili kuhakikisha kwamba hakuna mjane yeyote mwenye uhitaji aliyepuuzwa.—Matendo 6:1-6.

Wakristo wa makutaniko ya mapema walitoa msaada mara moja hata walipotarajia kutokea kwa hali ngumu. Kwa mfano, wakati nabii Agabo alipotabiri kwamba kungetokea njaa kuu, wanafunzi wa kutaniko la Antiokia ya Siria ‘waliamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.’ (Matendo 11:28, 29) Walionyesha roho nzuri kama nini kwa kutambua mapema mahitaji ya wengine!

Ni nini kilichowachochea Wakristo wa mapema wawe wakarimu na wenye upendo hivyo? Naam, mtu husitawishaje roho ya kutoa? Tunaweza kujifunza mengi kwa kufikiria kwa ufupi kielelezo cha Mfalme Daudi.

Daudi Ategemeza Ibada ya Kweli kwa Ukarimu

Kwa miaka 500 hivi, sanduku la agano—sanduku takatifu lililowakilisha kuwapo kwa Yehova—halikuwa na mahali pa kudumu pa kuliweka. Liliwekwa ndani ya hema, au tabenakulo, lililobebwa kutoka eneo moja hadi lingine wakati Waisraeli walipokuwa wakitangatanga nyikani na walipoingia katika Nchi ya Ahadi. Mfalme Daudi alitamani sana kulitoa sanduku hilo takatifu katika hema ambapo liliwekwa na kumjengea Yehova nyumba inayofaa ambapo lingewekwa. Daudi alimwambia hivi nabii Nathani: “Tazama, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, lakini sanduku la agano la Yehova linakaa ndani ya vitambaa vya mahema.”—1 Mambo ya Nyakati 17:1.

Hata hivyo, Daudi alikuwa mtu wa vita. Kwa hiyo, Yehova akasema kwamba mwana wake Sulemani ndiye angejenga hekalu wakati wa utawala wenye amani, na kuliweka humo sanduku la agano. (1 Mambo ya Nyakati 22:7-10) Lakini jambo hilo halikumzuia Daudi asionyeshe roho ya kutoa. Baada ya kuwatayarisha wafanyakazi wengi, Daudi alianza kutoa vifaa vya ujenzi ambavyo vingetumiwa kujenga hekalu hilo. Baadaye alimwambia Sulemani hivi: “Nimetayarisha kwa ajili ya nyumba ya Yehova talanta mia moja elfu za dhahabu na talanta milioni moja za fedha, na hakuna namna ya kupima uzito wa shaba na chuma kwa sababu zimekuwa nyingi sana; nami nimetayarisha mbao na mawe.” (1 Mambo ya Nyakati 22:14) Daudi hakutosheka na utoaji huo, bali alichanga kutoka kwa hazina yake mwenyewe dhahabu na fedha ambayo sasa ina thamani ya zaidi ya dola 1,200,000,000. Isitoshe, wakuu pia walitoa kwa ukarimu. (1 Mambo ya Nyakati 29:3-9) Daudi alionyesha roho ya kutoa yenye ukarimu kama nini!

Ni nini kilichomchochea Daudi atoe kwa ukarimu hivyo? Alitambua kwamba alipata vyote alivyokuwa navyo na kutimiza yote aliyotimiza kwa baraka za Yehova. Alikiri hivi katika sala: “Ee Yehova, Mungu wetu, wingi huu wote ambao tumetayarisha ili kukujengea nyumba kwa ajili ya jina lako takatifu, umetoka mkononi mwako, nao wote ni mali yako. Nami ninajua vema, Ee Mungu wangu, kwamba wewe ni mchunguzaji wa moyo, nawe unafurahia unyoofu. Nami katika unyoofu wa moyo wangu, nimetoa kwa hiari vitu hivi vyote, na sasa watu wako waliopo hapa nimefurahi kuona wakikutolea matoleo kwa hiari.” (1 Mambo ya Nyakati 29:16, 17) Daudi alithamini sana uhusiano wake pamoja na Yehova. Alitambua kwamba alihitaji kumtumikia Mungu “kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe,” naye alifurahia kufanya hivyo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Sifa hizohizo ziliwachochea Wakristo wa mapema kuonyesha roho ya kutoa.

Yehova Ndiye Mtoaji Mkuu Zaidi

Yehova ndiye aliye kielelezo bora zaidi cha utoaji. Anatupenda na kutujali sana hivi kwamba “yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Yeye huwapa wanadamu wote “uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Naam, kama vile mwanafunzi Yakobo anavyosema, “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.”—Yakobo 1:17.

Zawadi kubwa zaidi ambayo Yehova ametupatia ni kumtuma “Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Hakuna anayeweza kudai kwamba anastahili kupokea zawadi hiyo “kwa maana wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23, 24; 1 Yohana 4:9, 10) Fidia ya Kristo ndiyo msingi na njia ya Mungu ya kutoa “zawadi yake ya bure isiyoelezeka,” yaani, ‘fadhili zake nyingi zaidi zisizostahiliwa.’ (2 Wakorintho 9:14, 15) Kwa kuthamini zawadi ya Mungu, Paulo aliamua “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu” kuwa kazi kuu maishani mwake. (Matendo 20:24) Alitambua kwamba yalikuwa mapenzi ya Mungu “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.

Leo, mapenzi ya Mungu yanatimizwa kupitia kazi kubwa ya kuhubiri na kufundisha ambayo sasa imepanuka na kutia ndani nchi 234 duniani pote. Yesu alitabiri mpanuko huo aliposema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Naam, “katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10) Mwaka jana zaidi ya watangazaji wa habari njema milioni sita walitumia muda wa saa 1,202,381,302 kufanya kazi hiyo nao wakaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 5,300,000. Mafundisho hayo ni muhimu sana kwa kuwa maisha ya watu yamo hatarini.—Waroma 10:13-15; 1 Wakorintho 1:21.

Ili kuwasaidia wale walio na njaa ya kuijua kweli ya Biblia, mamilioni ya vichapo, kutia ndani Biblia, vitabu, na broshua, huchapishwa kila mwaka. Isitoshe, zaidi ya nakala bilioni moja za gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! huchapishwa. Kadiri watu wanavyoitikia habari njema, ndivyo Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yanavyozidi kujengwa ili kutumiwa kama vituo vya kujifunzia Biblia. Makusanyiko ya mzunguko na makusanyiko ya pekee na vilevile makusanyiko ya wilaya hufanywa kila mwaka. Pia mishonari, waangalizi wasafirio, wazee, na watumishi wa huduma wanaendelea kuzoezwa. Tunamshukuru Yehova kwa maandalizi hayo yote tunayopata kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Tunafurahi sana kuonyesha shukrani zetu Kwake.

Kumshukuru Yehova

Maandalizi hayo yote hugharimiwa kwa michango ya hiari tu kama vile ujenzi wa hekalu na mahitaji ya Wakristo wa makutaniko ya mapema yalivyogharimiwa. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba hakuna mtu anayeweza kumtajirisha Yehova Mwenye vitu vyote. (1 Mambo ya Nyakati 29:14; Hagai 2:8) Kwa hiyo, tunapotoa michango tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova na tunatamani kuendeleza ibada ya kweli. Paulo anasema kwamba kuonyesha ukarimu kwa njia hiyo ni “wonyesho wa shukrani kwa Mungu.” (2 Wakorintho 9:8-13) Yehova hututia moyo tutoe kwa ukarimu kwa sababu utoaji huo huonyesha kwamba tuna roho ya kutoa na moyo mzuri kumwelekea. Wale ambao ni wakarimu na wanamtegemea Yehova watabarikiwa naye na watafanikiwa kiroho. (Kumbukumbu la Torati 11:13-15; Methali 3:9, 10; 11:25) Yesu alituhakikishia kwamba tutapata furaha kwa kufanya hivyo aliposema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Wakristo walio na roho ya kutoa hawangojei mpaka wakati wa uhitaji. Badala yake, wao hutafuta nafasi za ‘kuwatendea wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Wagalatia 6:10) Paulo aliandika hivi ili kututia moyo tuwe wakarimu kama Mungu: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:16) Yehova Mungu hufurahi sana tunapotumia mali zetu zinazotia ndani wakati, nguvu, na pesa, ili kuwasaidia wengine na kuendeleza ibada safi. Kwa kweli, yeye hupenda roho ya kutoa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Jinsi Ambavyo Wengine Hutoa Michango

MICHANGO KWA AJILI YA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi hutenga kiasi fulani cha pesa ambacho wao hutia katika masanduku ya michango yaliyoandikwa, “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.”

Kila mwezi, makutaniko hutuma pesa hizo kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi yao. Michango ya hiari ya pesa inaweza kutumwa moja kwa moja kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, c/o Office of the Secretary and Treasurer, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya nchi yenu. Cheki za benki zinapaswa kuonyesha kwamba zitalipwa kwa shirika la “Watch Tower.” Vito au vitu vingine vyenye thamani vinaweza kuchangwa vilevile. Barua fupi inayoonyesha kwamba vitu hivyo ni zawadi ya moja kwa moja inapaswa kuambatanishwa na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zinaweza kuchangwa kukiwa na mpango hususa wa kwamba iwapo mtoaji atazihitaji tena, anaweza kurudishiwa. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Ofisi ya Katibu na Mweka-Hazina kwa kutumia anwani iliyoonyeshwa hapa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za moja kwa moja za pesa au vitu vyenye thamani na michango yenye masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme duniani pote. Hizo zinatia ndani:

Bima: Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa hati ya bima ya maisha au wa malipo ya kustaafu kazi au ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akaunti za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zinaweza kuwekwa zikiwa amana, au kulipwa wakati wa kifo, kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki za kwenu.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Society zikiwa zawadi ya moja kwa moja.

Ardhi na Nyumba: Ardhi au nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kutolewa zikiwa zawadi ya moja kwa moja au zawadi yenye masharti, yaani, mtoaji anaweza kuendelea kuishi humo hadi kifo chake. Julisha ofisi ya tawi katika nchi yako kabla ya kuchanga ardhi au nyumba.

Malipo-Mwaka: Huo ni mpango wa kutoa pesa, hisa na amana, ziwe mali za Watch Tower Society. Yule anayetoa mchango huo, au mtu fulani aliyechaguliwa na mtoaji, hupata kiasi fulani cha pesa kila mwaka maishani mwake. Mtoaji hupunguziwa kodi ya serikali mwaka ule ambapo mpango huo unaanzishwa.

Wasia na Amana: Watch Tower Society inaweza kuachiwa urithi wa mali au pesa kwa njia ya wasia halali, au Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Kuwa na amana inayofaidi tengenezo la kidini kunaweza kupunguza kwa kiasi fulani kodi ambayo hutozwa na serikali.

Kama vile usemi “utoaji uliopangwa” unavyodokeza, michango ya aina hii kwa kawaida hutaka mtoaji afanye mipango hususa. Watch Tower Society imetayarisha broshua ya Kiingereza na Kihispania yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide, ili kuwasaidia watu wanaotamani kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa njia ya utoaji uliopangwa. Broshua hiyo iliandikwa ili kujibu maswali mengi yaliyopokewa kuhusu zawadi, wasia, na amana. Pia ina habari za ziada zenye manufaa juu ya mipango ya ardhi na nyumba, pesa, na kodi. Inawajulisha watu kuhusu njia mbalimbali za kutoa zawadi sasa au kama urithi mtu anapokufa. Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na washauri wao wa mambo ya sheria na kodi, na pia Charitable Planning Office, watu wengi wameweza kuwasaidia Mashahidi wa Yehova kotekote duniani, na wakati uleule wakapunguziwa kodi kwa sababu ya kufanya hivyo. Unaweza kupata broshua hiyo kwa kuiomba moja kwa moja kutoka kwenye Charitable Planning Office.

Kwa habari zaidi unaweza kuwasiliana na Charitable Planning Office, ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu, kwenye anwani iliyoonyeshwa hapa chini, ama kwenye ofisi ya tawi ya nchi yako.

Mashahidi wa Yehova

P.O. Box 47788

00100 GPO Nairobi

Kenya

Simu: (02) 573211

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ni nini kilichowachochea Wakristo wa mapema wawe wakarimu?