Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani

Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani

Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani

“Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.”—METHALI 31:30.

1. Maoni ya Yehova kuhusu urembo yanatofautianaje na ya ulimwengu?

ULIMWENGU hukazia sana sura ya nje, hasa kuhusiana na wanawake. Hata hivyo, Yehova hupendezwa hasa na utu wa ndani, ambao unaweza kuendelea kuwa wenye kuvutia kadiri mtu anavyozeeka. (Methali 16:31) Kwa hiyo, Biblia huwahimiza hivi wanawake: “Kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa nje na kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:3, 4.

2, 3. Wanawake walichangiaje kuenezwa kwa habari njema katika karne ya kwanza, na jambo hilo lilikuwa limetabiriwaje?

2 Roho hiyo inayostahili sifa ilionyeshwa na wanawake wengi wanaotajwa katika Biblia. Katika karne ya kwanza, baadhi ya wanawake hao walikuwa na pendeleo la kumhudumia Yesu na mitume wake. (Luka 8:1-3) Baadaye, wanawake Wakristo wakawa waeneza-injili wenye bidii; wengine wakatoa utegemezo muhimu kwa wanaume Wakristo wenye kuongoza, kutia ndani mtume Paulo; nao wengine wakaonyesha ukaribishaji-wageni wa kipekee na hata kutoa nyumba zao kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.

3 Maandiko yalitabiri kwamba Yehova angewatumia wanawake kwa njia kubwa sana katika kutimiza kusudi lake. Kwa mfano, andiko la Yoeli 2:28, 29 lilitabiri kwamba wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, wangepokea roho takatifu na kushiriki katika kueneza habari njema ya Ufalme. Unabii huo ulianza kutimizwa siku ya Pentekoste 33 W.K. (Matendo 2:1-4, 16-18) Wanawake fulani waliotiwa mafuta kwa roho walipewa zawadi za kufanya miujiza kama vile kutoa unabii. (Matendo 21:8, 9) Kwa sababu ya bidii yao katika huduma, jeshi hilo kubwa la kiroho la dada waaminifu lilichangia kuenea haraka kwa Ukristo katika karne ya kwanza. Kwa kweli, yapata mwaka wa 60 W.K., mtume Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23.

Wapongezwa kwa Ujasiri, Bidii, na Ukaribishaji-Wageni

4. Kwa nini Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kuwapongeza wanawake kadhaa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

4 Kwa mfano, mtume Paulo alithamini huduma iliyofanywa na wanawake fulani hususa—kama vile waangalizi Wakristo leo wanavyothamini huduma inayofanywa na wanawake wenye bidii. Kati ya wanawake ambao Paulo aliwataja kwa jina ni “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana” na “Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo alifanya kazi nyingi katika Bwana.” (Waroma 16:12) Paulo aliandika kwamba Euodia na Sintike walikuwa ‘wamekazana pamoja naye katika habari njema.’ (Wafilipi 4:2, 3) Prisila pamoja na mume wake Akila walitumikia pia pamoja na Paulo. Prisila na Akila hata ‘walihatarisha shingo zao’ kwa ajili ya Paulo, na hivyo kumchochea kuandika: “Si mimi tu bali pia makutaniko yote ya mataifa yanawashukuru.”—Waroma 16:3, 4; Matendo 18:2.

5, 6. Ni katika njia zipi Prisila aliwawekea dada mfano mzuri leo?

5 Ni nini kilichofanya Prisila awe mwenye bidii na ujasiri? Tunapata dokezo fulani kwenye Matendo 18:24-26, ambapo tunasoma kwamba alimuunga mkono mume wake kumsaidia Apolo, msemaji mwenye kipawa, afahamu habari za karibuni zaidi kuhusu kweli iliyofunuliwa. Basi, ni wazi kwamba Prisila alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu na mafundisho ya mitume. Kwa sababu hiyo, alisitawisha sifa nzuri zilizofanya awe mwenye thamani kwa Mungu na kwa mume wake na pia awe mshiriki mwenye thamani wa kutaniko la mapema. Leo, dada wengi Wakristo wenye bidii ambao hujifunza Biblia kwa bidii na pia kula chakula cha kiroho ambacho Yehova huandaa kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu,” ni wenye thamani pia.—Luka 12:42.

6 Akila na Prisila walikuwa wakaribishaji-wageni wa kipekee. Paulo alikaa nyumbani kwao alipofanya kazi pamoja nao katika biashara yao ya kutengeneza mahema huko Korintho. (Matendo 18:1-3) Wakati wenzi hao walipohamia Efeso na baadaye Roma, waliendelea kuonyesha sifa ya Kikristo ya ukaribishaji-wageni, na hata wakatoa nyumba yao itumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (Matendo 18:18, 19; 1 Wakorintho 16:8, 19) Vivyo hivyo, Nimfa na Maria mama ya Yohana Marko walitoa nyumba zao zitumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.—Matendo 12:12; Wakolosai 4:15.

Ni Wenye Thamani Sana Leo

7, 8. Leo wanawake wengi Wakristo wana sifa gani nzuri ya utumishi mtakatifu, nao wanaweza kuwa na uhakika wa jambo gani?

7 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo wanawake Wakristo waaminifu hutimiza fungu muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu hasa katika kazi ya kueneza injili. Dada hao wana sifa nzuri kama nini! Fikiria mfano wa Gwen, ambaye alimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa zaidi ya miaka 50 mpaka alipokufa mwaka wa 2002. Mume wake anasema, “Gwen alijulikana sana katika jiji letu kwa bidii yake ya kueneza injili. Aliwaona watu wote kuwa wanaweza kunufaika na upendo na ahadi za Yehova. Ushikamanifu wake kwa Mungu, tengenezo lake, na kwa familia yetu—pamoja na kitia-moyo chake chenye upendo wakati tulipokuwa tumeshuka moyo—ni mambo yaliyonitegemeza na kutegemeza watoto wetu sana katika kipindi tulichoishi pamoja naye ambacho kilikuwa chenye kuridhisha na kuthawabisha. Tunamkosa sana.” Gwen na mume wake walikuwa wameoana kwa miaka 61.

8 Wanawake wengi sana Wakristo, waseja na walioolewa, wanatumikia wakiwa wahudumu mapainia na mishonari, nao huridhika na mahitaji ya lazima ya maisha wanapoeneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo yanayotia ndani majiji yenye shughuli nyingi na pia maeneo ya mbali. (Matendo 1:8) Wengi wamejinyima kuwa na makao au watoto ili kumtumikia Yehova kwa ukamili zaidi. Kuna wale ambao huwaunga mkono kwa ushikamanifu waume zao wanaotumikia wakiwa waangalizi wasafirio, huku maelfu ya akina dada wengine wakitumika kwenye makao ya Betheli ulimwenguni pote. Bila shaka, wanawake hao wenye kujidhabihu wamo kati ya “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” ambavyo vinaijaza nyumba ya Yehova utukufu.—Hagai 2:7.

9, 10. Washiriki fulani wa familia wameonyeshaje kwamba wanathamini kielelezo kizuri kinachowekwa na wake na mama Wakristo?

9 Bila shaka, wanawake wengi Wakristo wana madaraka ya familia; hata hivyo wanatanguliza mambo ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Dada mmoja mseja ambaye ni painia aliandika: “Kielelezo kizuri cha mama na imani yake thabiti vilinisaidia sana kuwa painia wa kawaida. Hata alikuwa mmoja kati ya mapainia bora zaidi niliopata kushirikiana nao.” Mume mmoja anasema hivi kumhusu mke wake, mama ya binti watano ambao sasa ni watu wazima: “Nyumba yetu ilikuwa safi na nadhifu daima. Bonnie hakurundika vitu nyumbani, hivyo familia yetu iliweza kukazia fikira mambo ya kiroho. Kwa sababu alitumia pesa kwa uangalifu, niliweza kufanya kazi isiyo ya wakati wote kwa miaka 32, jambo lililonisaidia kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yetu na kushughulikia mambo ya kiroho. Mke wangu pia aliwafunza watoto umuhimu wa kuwa wenye bidii. Ninampongeza sana.” Leo, mume huyo na mke wake wanatumika kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova.

10 Mume mmoja anaandika hivi kuhusu mke wake, aliye mama ya watoto ambao sasa ni watu wazima: “Sifa za Susan zinazonivutia zaidi ni upendo wake mwingi kwa Mungu na kwa watu, na vilevile kuelewa hali za watu, huruma, na unyofu. Sikuzote alionelea kwamba tunapaswa kumpa Yehova yaliyo bora zaidi—kanuni ambayo anaifuata akiwa mtumishi wa Mungu na pia mama.” Kwa utegemezo wa mke wake, mume huyo ameweza kukubali mapendeleo kadhaa ya kiroho kutia ndani kutumikia akiwa mzee, painia, mwangalizi wa mzunguko wa badala, na pia mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali. Wanawake hao ni wenye thamani kama nini kwa waume zao, Wakristo wenzao, na zaidi ya yote, kwa Yehova!—Methali 31:28, 30.

Wanawake Wenye Thamani Wasio na Waume

11. (a) Yehova ameonyeshaje kwamba anawajali wanawake waaminifu, hasa wajane? (b) Wajane Wakristo na dada wengine waaminifu wasio na mume wanaweza kuwa na uhakika gani?

11 Mara nyingi Yehova alionyesha jinsi anavyowajali wajane. (Kumbukumbu la Torati 27:19; Zaburi 68:5; Isaya 10:1, 2) Yeye hakubadilika. Bado anawajali sana wajane, mama wasio na wenzi wa ndoa, na pia wanawake ambao wameamua kubaki waseja au wale ambao hawajapata mume Mkristo anayefaa. (Malaki 3:6; Yakobo 1:27) Ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu bila utegemezo wa mwenzi Mkristo, unaweza kuwa na hakika kwamba u mwenye thamani machoni pa Mungu.

12. (a) Dada fulani Wakristo wanaonyeshaje ushikamanifu wao kwa Yehova? (b) Baadhi ya dada zetu wanavumilia hisia za aina gani?

12 Kwa mfano, fikiria dada zetu Wakristo ambao hawajaolewa kwa sababu wanatii kwa ushikamanifu shauri la Yehova la kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; Methali 3:1) Neno la Mungu linawahakikishia hivi: ‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’ (2 Samweli 22:26) Lakini kwa wengi wao, si rahisi kubaki waseja. Dada mmoja anasema hivi: “Niliazimia kuolewa katika Bwana tu, lakini nimelia mara nyingi ninapoona marafiki wangu wakiolewa na wanaume wazuri Wakristo huku nikibaki mseja.” Dada mwingine anasema: “Nimemtumikia Yehova kwa miaka 25. Nimeazimia kubaki mshikamanifu kwake, lakini mara nyingi mimi huhuzunika kwa sababu ya upweke.” Anaendelea kusema: “Dada kama mimi hutamani sana kutiwa moyo.” Tunaweza kuwasaidiaje dada hao washikamanifu?

13. (a) Mfano uliowekwa na wale waliomtembelea binti Yeftha unatufunza nini? (b) Ni katika njia gani zaidi tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali dada waseja katika kutaniko letu?

13 Njia moja ni kwa kuiga mfano mmoja wa kale. Wakati binti ya Yeftha alipoachilia mbali nafasi yake ya kuwa na mume, watu walitambua kwamba alikuwa akijinyima. Alitiwaje moyo? “Mwaka baada ya mwaka binti za Israeli wakawa wakienda kumpongeza binti ya Yeftha Mgileadi, siku nne kwa mwaka.” (Waamuzi 11:30-40) Vivyo hivyo, tunapaswa kuwapongeza kutoka moyoni dada waseja wanaotii amri ya Mungu kwa ushikamanifu. * Ni katika njia gani nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali? Tunapotoa sala, tunapaswa kumsihi Yehova awategemeze dada hao wapendwa na waaminifu ili waendelee kumtumikia kwa ushikamanifu. Wanapaswa kuhakikishiwa kwamba wanapendwa na kuthaminiwa sana na Yehova na kutaniko lote la Kikristo.—Zaburi 37:28.

Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa Hufanikiwaje?

14, 15. (a) Kwa nini Wakristo ambao ni mama wasio na wenzi wa ndoa wanapaswa kumwomba Yehova awasaidie? (b) Wazazi wasio na wenzi wanawezaje kutenda kupatana na sala zao?

14 Wanawake Wakristo ambao ni wazazi wasio na wenzi wa ndoa pia hukabili magumu mengi. Hata hivyo, wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kulea watoto wao kupatana na kanuni za Biblia. Ni kweli kwamba ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, huwezi kutimiza kabisa-kabisa daraka la baba na mama. Hata hivyo, Yehova atakusaidia kutimiza majukumu yako mengi ukimwomba msaada wake kwa imani. Kwa mfano: Wazia kwamba unabeba mzigo mzito wa viazi kutoka shambani mwako kurudi nyumbani kwako ambako ni mbali sana. Je, ungeng’ang’ana kuubeba mzigo huo peke yako iwapo rafiki yako mwenye gari kubwa angetokea na kujitolea kukusaidia? La, hungefanya hivyo! Vivyo hivyo, usijaribu kubeba mizigo ya kihisia-moyo peke yako kwa kuwa unaweza kumwomba Yehova akusaidie. Hata anakutia moyo ufanye hivyo. Andiko la Zaburi 68:19 linasema: “Na abarikiwe Yehova, ambaye hutubebea mzigo wetu kila siku.” Vivyo hivyo, andiko la 1 Petro 5:7 linakutia moyo umtupie Yehova mahangaiko yako yote ‘kwa sababu yeye anakujali wewe.’ Kwa hiyo, unapolemewa na matatizo na mahangaiko, mtupie Baba yako wa mbinguni mizigo hiyo, ukifanya hivyo “bila kuacha.”—1 Wathesalonike 5:17; Zaburi 18:6; 55:22.

15 Kwa mfano, ikiwa wewe ni mama, bila shaka unahangaikia uvutano wa marika juu ya watoto wako shuleni au majaribu ya utimilifu ambayo huenda wakakabili. (1 Wakorintho 15:33) Hayo ni mahangaiko halali. Lakini unaweza pia kusali kuyahusu. Unaweza kusali kuhusu mambo hayo pamoja na watoto wako kabla ya kwenda shuleni, labda baada ya kuchunguza andiko la siku pamoja. Kusali kutoka moyoni na kutaja mambo hususa kunaweza kuwa na matokeo mazuri kwa watoto wako. Zaidi ya yote, Yehova atakubariki ukijitahidi kwa subira kuwafundisha watoto wako Neno lake. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Methali 22:6) Kumbuka, “macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.”—1 Petro 3:12; Wafilipi 4:6, 7.

16, 17. (a) Mwana mmoja alisema nini kuhusu upendo alioonyeshwa na mama yake? (b) Mtazamo wa kiroho wa mama huyo ulikuwa na matokeo gani juu ya watoto wake?

16 Fikiria mfano wa Olivia, mama ya watoto sita. Mume wake asiyeamini aliacha familia yake mara tu baada ya kitindamimba kuzaliwa. Lakini mara moja Olivia akachukua daraka la kuwalea watoto wake katika njia za Mungu. Mwana wa Olivia, Darren, ambaye sasa ni painia na mzee Mkristo mwenye umri wa miaka 31, alikuwa na umri wa miaka 5 hivi wakati huo. Mahangaiko ya Olivia yaliongezeka Darren aliposhikwa na ugonjwa mbaya ambao bado unamsumbua. Darren anaandika hivi anapokumbuka mambo yaliyotukia alipokuwa mtoto: “Bado ninakumbuka nikiketi juu ya kitanda changu hospitalini huku nikimsubiri Mama kwa hamu. Yeye angeketi kando yangu na kunisomea Biblia kila siku. Kisha angeimba wimbo wa Ufalme wenye kichwa ‘Asante, Yehova.’ * Ningali naupenda sana wimbo huo.”

17 Olivia alifanikiwa akiwa mama asiye na mwenzi wa ndoa kwa sababu alimtumaini na kumpenda Yehova. (Methali 3:5, 6) Mtazamo wake mzuri ulidhihirishwa katika miradi aliyowawekea watoto wake. “Sikuzote Mama alitutia moyo tufuatie mradi wa kuwa wahudumu wa wakati wote,” asema Darren. “Kwa sababu hiyo, mimi pamoja na wanne kati ya dada zangu watano ni wahudumu wa wakati wote. Hata hivyo, Mama hakuwa akijigamba kwa wengine kuhusu mafanikio hayo. Mimi hujitahidi sana kuiga sifa zake nzuri.” Ni kweli kwamba si watoto wote wanaokua na kumtumikia Mungu kama watoto wa Olivia. Lakini mama anapofanya yote awezayo kuishi kupatana na kanuni za Biblia, anaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atamwongoza na kumsaidia kwa upendo.—Zaburi 32:8.

18. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini uandalizi wa Yehova wa kutaniko la Kikristo?

18 Mungu hutoa msaada mwingi kupitia kutaniko la Kikristo lenye mpango wa kulisha watu kiroho kwa ukawaida, undugu wa Kikristo, na “zawadi katika wanadamu” ambao wamekomaa kiroho. (Waefeso 4:8) Wazee waaminifu hujitahidi kuwajenga wote kutanikoni, wakiwapa uangalifu wa kipekee “mayatima na wajane katika dhiki yao.” (Yakobo 1:27) Kwa hiyo, kaa karibu na watu wa Mungu na usijitenge kamwe.—Methali 18:1; Waroma 14:7.

Sifa Nzuri ya Ujitiisho

19. Kwa nini ujitiisho wa mke hauonyeshi kwamba yeye ni wa hali ya chini, na ni mfano gani katika Biblia unaounga mkono jambo hilo?

19 Yehova alimwumba mwanamke awe kikamilisho cha mwanamume. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, ujitiisho wa mke kwa mume wake hauonyeshi kwamba yeye ni wa hali ya chini. Badala yake, ujitiisho hufanya mwanamke aheshimiwe na humwezesha kutumia uwezo na vipawa vyake vingi kupatana na mapenzi ya Mungu. Methali sura ya 31 huzungumzia mambo mbalimbali ambayo mwanamke mwenye uwezo wa Israeli ya kale alifanya. Aliwasaidia wenye uhitaji, akapanda mashamba ya mizabibu, na kununua ardhi. Naam, ‘moyo wa mume wake ulimtegemea, wala hakuna faida iliyokosekana.’—Mstari wa 11, 16, 20.

20. (a) Mwanamke Mkristo anapaswa kuonaje uwezo, au vipawa alivyopewa na Mungu? (b) Esta alionyesha sifa gani nzuri, na kwa sababu hiyo Yehova alimtumiaje?

20 Mwanamke mwenye kiasi na anayemwogopa Mungu hajitukuzi kwa kujitakia makuu, au kushindana na mumewe. (Methali 16:18) Yeye hatafuti uradhi kwa kufuatia hasa kazi za kimwili bali yeye hutumia vipawa alivyopewa na Mungu ili kuwatumikia wengine—familia yake, Wakristo wenzake, majirani, na zaidi ya wote, Yehova. (Wagalatia 6:10; Tito 2:3-5) Fikiria mfano wa Malkia Esta katika Biblia. Ingawa alikuwa mrembo, alikuwa mwenye kiasi na mwenye kujitiisha. (Esta 2:13, 15) Alipoolewa, alimwonyesha mume wake, Mfalme Ahasuero, heshima kubwa tofauti na Vashti, mke wake wa kwanza. (Esta 1:10-12; 2:16, 17) Esta pia alikubaliana na maoni ya Mordekai, binamu yake mkubwa, kuhusu masuala yanayofaa—hata baada ya kuwa malkia. Lakini alikuwa mjasiri. Alifunua kwa ujasiri hila ya Hamani, mtu mwenye nguvu na ambaye alitaka kuwaangamiza Wayahudi. Yehova alimtumia Esta kwa njia kubwa ili kuwaokoa watu wake.—Esta 3:8-4:17; 7:1-10; 9:13.

21. Mwanamke Mkristo anawezaje kuendelea kuwa mwenye thamani zaidi kwa Yehova?

21 Bila shaka, zamani na hata leo, wanawake wanaomwogopa Yehova wamejitoa kikamili kwake na kwa ibada yake. Kwa hiyo, wanawake wanaomwogopa Mungu ni wenye thamani machoni pa Yehova. Dada Wakristo acheni Yehova awafinyange hatua kwa hatua kupitia roho yake ili mwendelee kuwa “chombo,” kinachopendeza zaidi “kilichotayarishwa kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 2:21; Waroma 12:2) Neno la Mungu linasema hivi kuhusu waabudu hao wenye thamani: “Mpeni baadhi ya matunda ya mikono yake, nazo kazi zake na zimsifu malangoni.” (Methali 31:31) Na iwe hivyo kwa kila mmoja wenu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ili kujua jinsi ya kutoa pongezi hizo, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2002, ukurasa wa 26-28.

^ fu. 16 Wimbo namba 212 katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Wanawake fulani Wakristo katika karne ya kwanza walithibitikaje kuwa wenye thamani machoni pa Yehova?

• Leo dada wengi wamefanyaje ili kuwa wenye thamani kwa Mungu?

• Ni katika njia zipi Yehova huwategemeza mama wasio na wenzi wa ndoa na dada wengine wasio na waume?

• Mwanamke anawezaje kuonyesha heshima ya kutoka moyoni kwa mpango wa ukichwa?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Mifano ya Kutafakari

Je, ungependa kutafakari juu ya mifano mingine zaidi ya wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia? Ikiwa ndivyo, tafadhali soma maandiko yaliyoonyeshwa chini. Unapotafakari juu ya watu mbalimbali wanaotajwa, jaribu kuona kanuni unazoweza kutumia kwa kadiri kubwa zaidi maishani mwako.—Waroma 15:4.

Sara: Mwanzo 12:1, 5; 13:18a; 21:9-12; 1 Petro 3:5, 6.

Wanawake Waisraeli wakarimu: Kutoka 35:5, 22, 25, 26; 36:3-7; Luka 21:1-4.

Debora: Waamuzi 4:1–5:31.

Ruthu: Ruthu 1:4, 5, 16, 17; 2:2, 3, 11-13; 4:15.

Mwanamke wa Shunemu: 2 Wafalme 4:8-37.

Mwanamke Mfoinike: Mathayo 15:22-28.

Martha na Maria: Marko 14:3-9; Luka 10:38-42; Yohana 11:17-29; 12:1-8.

Tabitha: Matendo 9:36-41.

Binti wanne wa Filipo: Matendo 21:9.

Fibi: Waroma 16:1, 2.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, wewe huwapongeza dada waseja ambao hutii sheria ya Mungu kwa ushikamanifu?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ni mambo gani hususa yanayoweza kutajwa katika sala kabla ya watoto kwenda shuleni?