Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanawake Walioufurahisha Moyo wa Yehova

Wanawake Walioufurahisha Moyo wa Yehova

Wanawake Walioufurahisha Moyo wa Yehova

“Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova.”—RUTHU 2:12.

1, 2. Tunaweza kunufaikaje kwa kutafakari mifano ya wanawake wanaotajwa katika Biblia ambao waliufurahisha moyo wa Yehova?

KUMWOGOPA Mungu kuliwachochea wanawake wawili wakatae kumtii Farao. Imani ilimchochea kahaba fulani kuhatarisha maisha yake ili awalinde wapelelezi wawili Waisraeli. Busara na unyenyekevu zilimsaidia mwanamke mmoja wakati wa matatizo kuokoa maisha ya watu wengi na kumzuia mtiwa-mafuta wa Yehova asiwe na hatia ya damu. Imani katika Yehova Mungu pamoja na roho ya ukaribishaji-wageni zilimchochea mama fulani aliyekuwa mjane kumpa nabii wa Mungu chakula alichokuwa amebakisha. Hiyo ni baadhi tu ya mifano mingi katika Biblia kuhusu wanawake walioufurahisha moyo wa Yehova.

2 Mtazamo wa Yehova kuelekea wanawake hao na baraka alizowapa huonyesha kwamba yeye hufurahishwa sana na sifa za kiroho ambazo ni muhimu zaidi kuliko jinsia ya mtu. Si rahisi watu kutanguliza hali yao ya kiroho kwa sababu ulimwengu wa leo unajishughulisha zaidi na mambo ya kimwili. Lakini inawezekana kufanya hivyo, kama inavyoonyesha na mamilioni ya wanawake wanaomwogopa Mungu ambao ni sehemu kubwa ya watu wa Mungu leo. Wanawake hao Wakristo huiga imani, busara, ukaribishaji-wageni, na sifa nyingine nzuri zilizoonyeshwa na wanawake wanaomwogopa Mungu ambao wanatajwa katika Biblia. Bila shaka, wanaume Wakristo pia wangependa kuiga sifa zilizoonyeshwa na wanawake hao wa kale ambao ni vielelezo vizuri. Ili tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo kwa ukamili zaidi, acheni tuchunguze kwa undani masimulizi ya Biblia kuhusu wanawake ambao wametajwa katika fungu la kwanza.—Waroma 15:4; Yakobo 4:8.

Wanawake Waliokataa Kumtii Farao

3, 4. (a) Kwa nini Shifra na Pua walikataa kumtii Farao alipowaagiza waue kila mtoto wa kiume Mwisraeli? (b) Yehova aliwabarikije wazalishaji wawili kwa sababu ya ujasiri na woga wao wa kimungu?

3 Katika kesi zilizofanywa huko Nuremberg, Ujerumani baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, wengi waliopatikana na hatia ya kuua watu wengi walijaribu kujitetea kwa kudai kwamba walifanya hivyo kwa kutii amri tu. Sasa walinganishe watu hao na wazalishaji wawili Waisraeli, Shifra na Pua, walioishi katika Misri ya kale wakati wa utawala wa Farao mmoja mkatili asiyetajwa jina. Akiogopa ongezeko la haraka la idadi ya Waebrania, Farao huyo aliwaamuru wazalishaji hao wahakikishe kwamba wamemwua kila mtoto wa kiume Mwebrania. Wanawake hao waliitikiaje amri hiyo ya kikatili? “Hawakufanya kama vile mfalme wa Misri alivyokuwa amewaambia, bali walikuwa wakiwahifadhi hai watoto wa kiume.” Kwa nini wanawake hao hawakumwogopa mwanadamu? Kwa sababu “walimwogopa Mungu wa kweli.”—Kutoka 1:15, 17; Mwanzo 9:6.

4 Naam, wazalishaji hao walimfanya Yehova kuwa kimbilio lao, naye akawa “ngao” yao na kuwalinda na hasira ya Farao. (2 Samweli 22:31; Kutoka 1:18-20) Lakini Yehova aliwabariki hata zaidi. Aliwabariki Shifra na Pua kuwa na familia zao wenyewe. Hata aliwaheshimu wanawake hao kwa kufanya majina na matendo yao yaandikwe katika Neno lake lililoongozwa kwa roho ili yasomwe na vizazi vya baadaye, lakini jina la Farao huyo halikumbukwi hata kidogo.—Kutoka 1:21; 1 Samweli 2:30b; Methali 10:7.

5. Leo wanawake wengi Wakristo huonyeshaje mtazamo kama wa Shifra na Pua, naye Yehova atawabarikije?

5 Je, leo kuna wanawake walio kama Shifra na Pua? Bila shaka! Kila mwaka, wanawake wengi kama Shifra na Pua huhubiri kwa ujasiri ujumbe wa Biblia unaookoa uhai katika nchi ambako “agizo la mfalme” linakataza kazi hiyo, na hivyo kuhatarisha uhuru wao au hata maisha yao. (Waebrania 11:23; Matendo 5:28, 29) Kwa kuchochewa na upendo kwa Mungu na jirani, wanawake hao wajasiri hawamruhusu yeyote awazuie kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, wanawake wengi Wakristo hukabili upinzani na mateso. (Marko 12:30, 31; 13:9-13) Kama vile Yehova alivyoona matendo ya Shifra na Pua, yeye anafahamu kabisa matendo ya wanawake hao wazuri na wajasiri, naye ataonyesha upendo wake kwao kwa kuhifadhi majina yao katika ‘kitabu chake cha uzima,’ ikiwa watavumilia kwa uaminifu mpaka mwisho.—Wafilipi 4:3; Mathayo 24:13.

Aliyekuwa Kahaba Aufurahisha Moyo wa Yehova

6, 7. (a) Ni habari gani ambazo Rahabu alijua kumhusu Yehova na watu wake, nazo zilimwathirije? (b) Rahabu anaheshimiwaje katika Neno la Mungu?

6 Katika mwaka wa 1473 K.W.K., kahaba mmoja aitwaye Rahabu aliishi katika jiji la Kanaani la Yeriko. Yaonekana kwamba Rahabu alikuwa mwanamke aliyejua habari nyingi kuhusu matukio ya wakati huo. Wakati wapelelezi wawili Waisraeli walipokimbilia nyumbani kwake, aliweza kuwasimulia mambo hususa kuhusu jinsi Waisraeli walivyotoka Misri kimuujiza, ingawa jambo hilo lilikuwa limetukia miaka 40 mapema! Pia alifahamu ushindi wa karibuni zaidi wa Waisraeli juu ya Wafalme Waamori, Sihoni na Ogu. Ona jinsi alivyoathiriwa na habari hizo. Aliwaambia hivi wapelelezi hao: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii, . . . kwa kuwa Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.” (Yoshua 2:1, 9-11) Naam, mambo ambayo Rahabu alijifunza kumhusu Yehova na matendo yake kwa niaba ya Waisraeli yalimgusa moyo na kumfanya amwamini.—Waroma 10:10.

7 Imani ya Rahabu ilimchochea kutenda. Aliwakaribisha wapelelezi Waisraeli “kwa njia ya amani,” naye alitii maagizo yao yenye kuokoa uhai wakati Waisraeli waliposhambulia Yeriko. (Waebrania 11:31; Yoshua 2:18-21) Hapana shaka kwamba matendo ya imani ya Rahabu yaliufurahisha moyo wa Yehova, kwa kuwa Yehova alimwongoza kwa roho mwanafunzi Mkristo Yakobo aandike jina la Rahabu pamoja na lile la Abrahamu rafiki ya Mungu, ili kuwa mfano wa kuigwa na Wakristo. Yakobo aliandika: “Vivyo hivyo, je, Rahabu yule kahaba hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kwa njia nyingine?”—Yakobo 2:25.

8. Yehova alimbarikije Rahabu kwa ajili ya imani na utii wake?

8 Yehova alimbariki Rahabu katika njia mbalimbali. Kwanza, aliokoa kimuujiza uhai wake pamoja na wa wale waliokimbilia nyumbani kwake, yaani, “nyumba ya baba yake na wote waliokuwa wake.” Kisha akawaruhusu watu hao waishi “katikati ya Israeli,” ambako walipaswa kutendewa kama wenyeji. (Yoshua 2:13; 6:22-25; Mambo ya Walawi 19:33, 34) Na si hayo tu. Yehova pia alimpa Rahabu pendeleo la kuwa nyanya wa Yesu Kristo. Huo ni wonyesho mkubwa sana wa fadhili zenye upendo kwa mwanamke Mkanaani ambaye wakati mmoja alikuwa mwabudu wa sanamu. *Zaburi 130:3, 4.

9. Mtazamo wa Yehova kuelekea Rahabu na wanawake fulani Wakristo wa karne ya kwanza unawezaje kuwatia moyo baadhi ya wanawake leo?

9 Kama Rahabu, wanawake fulani Wakristo, kuanzia karne ya kwanza mpaka leo, wameacha maisha yasiyo ya adili ili kumpendeza Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Bila shaka, baadhi yao walikulia katika mazingira yanayofanana na ya Wakanaani, ambapo ukosefu wa maadili ulikuwa umeenea sana na hata kuonwa kuwa jambo la kawaida. Hata hivyo, walibadili maisha yao kwa kuchochewa na imani inayotegemea ujuzi sahihi wa Maandiko. (Waroma 10:17) Hivyo, tunaweza pia kusema kuhusu wanawake hao kwamba “Mungu haoni aibu juu yao, kuitwa akiwa Mungu wao.” (Waebrania 11:16) Hiyo ni heshima iliyoje!

Abarikiwa kwa Busara Yake

10, 11. Ni hali gani zinazohusu Nabali na Daudi ambazo zilimchochea Abigaili kutenda?

10 Wanawake wengi waaminifu wa kale walionyesha busara kwa njia ya kipekee na hivyo wakawa wenye thamani sana kwa watu wa Yehova. Mmojawapo wa wanawake hao ni Abigaili, mke wa Nabali, Mwisraeli tajiri mwenye mashamba. Kwa sababu ya busara yake, Abigaili aliokoa maisha ya watu na kumzuia Daudi, ambaye angekuwa mfalme wa Israeli, asiwe na hatia ya damu. Tunaweza kusoma kumhusu Abigaili katika 1 Samweli sura ya 25.

11 Masimulizi hayo yanaanza kwa kumtaja Daudi na wafuasi wake ambao wamepiga kambi karibu na makundi ya Nabali, ambayo wanalinda mchana na usiku bila malipo kwa sababu ya fadhili yao kwa Nabali, Mwisraeli mwenzao. Vyakula vya Daudi na watu wake vinapoanza kupungua, anawatuma vijana kumi kwenda kwa Nabali wakamwombe chakula. Sasa Nabali ana nafasi ya kumshukuru na kumwonyesha Daudi heshima akiwa mtiwa-mafuta wa Yehova. Lakini Nabali hafanyi hivyo. Kwa hasira kali, Nabali anamtukana Daudi na kuwafukuza wanaume hao mikono mitupu. Daudi anaposikia hayo, anakusanya wanaume 400 wenye silaha na kuondoka kwenda kulipiza kisasi. Abigaili anapata kujua jinsi ambavyo mume wake ametenda kwa ukali naye anachukua hatua ya haraka na ya busara ya kumpelekea Daudi vyakula vingi ili kumtuliza. Kisha yeye mwenyewe anaenda kukutana na Daudi.—Mstari wa 2-20.

12, 13. (a) Abigaili alionyeshaje kuwa mwenye busara na pia mshikamanifu kwa Yehova na mtiwa-mafuta wake? (b) Abigaili alifanya nini aliporudi nyumbani, na ikawaje kwake?

12 Abigaili anapokutana na Daudi, anamsihi kwa unyenyekevu amhurumie, jambo linaloonyesha kwamba anamheshimu sana mtiwa-mafuta wa Yehova. Anasema, “Bila shaka Yehova atamfanyia bwana wangu nyumba inayodumu, kwa maana bwana wangu anapigana vita vya Yehova.” Kisha anaongeza kusema kwamba Yehova atamfanya Daudi kuwa kiongozi wa Israeli. (Mstari 28-30) Wakati huohuo, Abigaili anaonyesha ujasiri mwingi anapomwambia Daudi kwamba asipojizuia kulipiza kisasi atakuwa na hatia ya damu. (Mstari 26, 31) Sifa za Abigaili za unyenyekevu, heshima nyingi, na uwezo wa kufikiri vizuri zinafanya Daudi arudiwe na fahamu zake. Anasema: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.”—Mstari wa 32, 33.

13 Anaporudi nyumbani, kwa ujasiri Abigaili anataka kumweleza mume wake kuhusu zawadi aliyompa Daudi. Lakini anapompata, Nabali “amelewa kabisa.” Kwa hiyo, anangoja hadi Nabali anapotokwa na ulevi na kumwambia. Nabali anafanyaje? Anashtuka sana hivi kwamba anapatwa na aina fulani ya ugonjwa wa kupooza. Siku kumi baadaye, anakufa mkononi mwa Mungu. Daudi anaposikia kwamba Nabali amekufa, anamuuliza Abigaili kama atakubali kuwa mke wake. Bila shaka, Daudi anampenda na kumheshimu Abigaili sana naye anakubali kuolewa na Daudi.—Mstari wa 34-42.

Je, Unaweza Kuwa Kama Abigaili?

14. Ni sifa gani za Abigaili ambazo tungependa kuzisitawisha kwa kadiri kubwa zaidi?

14 Je, unaona sifa fulani za Abigaili ambazo wewe—uwe mwanamke au mwanamume—ungependa kusitawisha kwa kadiri kubwa zaidi? Labda ungependa kutenda kwa hekima na busara zaidi matatizo yanapotokea. Au huenda ungependa kuzungumza kwa utulivu na kwa njia inayofaa wakati hisia za wengine zinapopanda. Ikiwa ndivyo, basi sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Yeye anaahidi kuwapa hekima, utambuzi, na uwezo wa kufikiri wote ambao ‘wanaendelea kuomba kwa imani.’—Yakobo 1:5, 6; Methali 2:1-6, 10, 11.

15. Ni chini ya hali gani inakuwa muhimu hasa kwa wanawake Wakristo kuonyesha sifa kama zile zilizoonyeshwa na Abigaili?

15 Sifa hizo ni muhimu hasa kwa mwanamke aliye na mume asiyeamini ambaye hajali sana au hajali kabisa kanuni za Biblia. Labda anakunywa kupita kiasi. Tunatumaini kwamba wanaume hao watabadili mwenendo wao. Wengi wamefanya hivyo, mara nyingi kwa sababu ya kuona upole, heshima nyingi, na mwenendo safi kiadili wa wake zao.—1 Petro 3:1, 2, 4.

16. Hata hali ziweje nyumbani, dada Mkristo angeonyeshaje kwamba anathamini uhusiano wake na Yehova kuliko kitu kingine chochote?

16 Hata uwe unalazimika kuvumilia magumu ya aina gani nyumbani, kumbuka kwamba sikuzote Yehova yuko tayari kukusaidia. (1 Petro 3:12) Kwa hiyo, jitahidi kujiimarisha kiroho. Sali upate hekima na moyo mtulivu. Naam, mkaribie Yehova kupitia funzo la Biblia la ukawaida, sala, kutafakari, na kushirikiana na Wakristo wenzako. Upendo wa Abigaili kwa Mungu na mtazamo wake kuelekea mtumishi wake aliyetiwa mafuta hazikuathiriwa na maoni yasiyo ya kiroho ya mume wake. Alitenda kupatana na kanuni za uadilifu. Hata katika familia ambapo mume ni mtumishi wa Mungu mwenye mfano mzuri, mke Mkristo anatambua kwamba anahitaji kujitahidi kuimarisha na kudumisha hali yake mwenyewe ya kiroho. Ni kweli kwamba mume wake ana daraka la Kimaandiko kumtunza kiroho na kimwili, lakini ni lazima mke afanyie kazi ‘wokovu wake mwenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’—Wafilipi 2:12; 1 Timotheo 5:8.

Alipata “Thawabu ya Nabii”

17, 18. (a) Mjane wa Sarefathi alikabili jaribu gani la imani lisilo la kawaida? (b) Mjane huyo alifanyaje kuhusiana na ombi la Eliya, naye Yehova alimpa thawabu gani?

17 Jinsi Yehova alivyomtunza mjane maskini wakati wa nabii Eliya huonyesha kwamba anawathamini sana wale ambao hutegemeza ibada ya kweli kwa kujitoa wenyewe na mali zao. Kwa sababu ya ukame ulioendelea kwa muda mrefu wakati wa Eliya, watu wengi walikabiliwa na njaa, kutia ndani mjane fulani na mwanawe mchanga walioishi Sarefathi. Walipokuwa karibu kula chakula chao cha mwisho, mgeni alifika, ambaye alikuwa nabii Eliya. Aliomba afanyiwe jambo lisilokuwa la kawaida kabisa. Ingawa alijua hali mbaya ya mwanamke huyo, alimwomba amwokee “keki ndogo ya mviringo” akitumia mafuta na unga uliokuwa umebaki. Lakini akaongeza kusema: “Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli, amesema hivi, ‘Ule mtungi mkubwa wa unga hautamalizika, na ule mtungi mdogo wa mafuta hautapungua mpaka siku Yehova atakapoleta mvua juu ya uso wa nchi.’”—1 Wafalme 17:8-14.

18 Wewe ungetendaje kuhusiana na ombi hilo lisilo la kawaida? Yaonekana mjane wa Sarefathi alitambua kwamba Eliya alikuwa nabii wa Yehova, hivyo ‘akafanya kulingana na neno la Eliya.’ Yehova alitendaje kuhusiana na tendo lake la ukaribishaji-wageni? Aliandaa chakula kimuujiza kwa ajili ya mwanamke huyo, mwana wake, na Eliya wakati huo wa ukame. (1 Wafalme 17:15, 16) Naam, Yehova alimpa mjane wa Sarefathi “thawabu ya nabii,” hata ingawa hakuwa Mwisraeli. (Mathayo 10:41) Mwana wa Mungu pia alimsifu mjane huyo alipotaja mfano wake kwa watu wasio na imani wa mji wa nyumbani kwao, Nazareti.—Luka 4:24-26.

19. Leo wanawake wengi Wakristo huonyeshaje roho ya mjane wa Sarefathi, naye Yehova huhisije kuwahusu?

19 Leo, wanawake wengi Wakristo huonyesha roho ya mjane wa Sarefathi. Kwa mfano, kila juma, dada Wakristo wasio na ubinafsi—ambao wengi wao ni maskini na wana familia za kutunza—huwakaribisha waangalizi wasafirio na wake zao. Wengine huwakaribisha wahudumu wa wakati wote wa kwao wale chakula pamoja nao, husaidia wenye uhitaji, au kwa njia nyingine kujitoa wenyewe na mali zao kutegemeza kazi ya Ufalme. (Luka 21:4) Je, Yehova huona dhabihu hizo? Bila shaka! “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

20. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

20 Katika karne ya kwanza wanawake kadhaa waliomwogopa Mungu walikuwa na pendeleo la kumhudumia Yesu na mitume wake. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi wanawake hao walivyoufurahisha moyo wa Yehova, na tutachunguza mfano ambao umewekwa na wanawake wa siku hizi wanaomtumikia Yehova kwa moyo wote, hata katika hali ngumu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ukoo wa Yesu ulioandikwa na Mathayo hutaja majina ya wanawake wanne—Tamari, Rahabu, Ruthu, na Maria. Wote wanaheshimiwa sana katika Neno la Mungu.—Mathayo 1:3, 5, 16.

Kwa Kupitia

• Wanawake wafuatao waliufurahishaje moyo wa Yehova?

• Shifra na Pua

• Rahabu

• Abigaili

• Mjane wa Sarefathi

• Kutafakari juu ya mifano iliyowekwa na wanawake hao kunaweza kutusaidiaje kibinafsi? Toa mfano.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wanawake wengi waaminifu wamemtumikia Mungu japo “agizo la mfalme”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa nini Rahabu ni mfano mzuri wa mtu mwenye imani yenye matendo?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Unataka kuiga sifa gani zilizoonyeshwa na Abigaili?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Leo wanawake wengi Wakristo huonyesha roho ya mjane wa kale wa Sarefathi