Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Amenifundisha Tangu Ujana Wangu

Yehova Amenifundisha Tangu Ujana Wangu

Simulizi la Maisha

Yehova Amenifundisha Tangu Ujana Wangu

LIMESIMULIWA NA RICHARD ABRAHAMSON

“Ee Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu, na mpaka sasa ninaendelea kutangaza kazi zako za ajabu.” Acheni nieleze kwa nini maneno hayo ya Zaburi 71:17 yana maana ya kipekee kwangu.

MNAMO mwaka wa 1924 mama yangu Fannie Abrahamson, alitembelewa na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Nilikuwa na umri wa mwaka mmoja tu. Mara tu baada ya kufunzwa kweli za Biblia, Mama alikuwa akienda kuwaeleza majirani wake, naye pia alinifunza mimi, kaka yangu, na dada yangu. Hata kabla sijajua kusoma, alikuwa amenisaidia kukariri maandiko mengi yanayozungumzia baraka za Ufalme wa Mungu.

Katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1920, kikundi chetu cha Wanafunzi wa Biblia huko La Grande, katika jimbo la Oregon, Marekani, ambako nilizaliwa na kulelewa, kilikuwa na wanawake na watoto wachache. Ingawa tulikuwa mbali, tulitembelewa mara moja au mbili kwa mwaka na wahudumu wasafirio. Wahudumu hao walitoa hotuba zenye kutia moyo, wakahubiri nasi nyumba kwa nyumba, nao waliwajali watoto na kuwaonyesha fadhili. Shield Toutjian, Gene Orrell, na John Booth ni baadhi ya wahudumu hao wapendwa.

Katika mwaka wa 1931 hakuna yeyote kutoka katika kikundi chetu aliyeweza kuhudhuria kusanyiko huko Columbus, Ohio, ambako Wanafunzi wa Biblia walikubali rasmi kuitwa Mashahidi wa Yehova. Lakini makutaniko na vikundi vya mbali ambavyo havikuwakilishwa kwenye kusanyiko hilo vilikutana kwao mwezi wa Agosti mwaka huo ili kutangaza azimio lao la kukubali rasmi jina hilo. Kikundi chetu kidogo huko La Grande kilifanya hivyo. Kisha katika kampeni ya mwaka wa 1933 ya kugawanya kijitabu The Crisis, nilikariri kichwa fulani cha mazungumzo kutoka katika Biblia, na kwa mara ya kwanza, nikahubiri nyumba kwa nyumba nikiwa peke yangu.

Katika miaka ya 1930, upinzani dhidi ya kazi yetu ulikuwa unaongezeka. Ili kukabiliana nao, makutaniko yalipangwa katika vikundi-vikundi ambavyo vilifanya makusanyiko madogo na kushiriki katika kazi ya kuhubiri iliyoitwa kampeni za vikundi ambayo ilifanywa mara moja au mbili kila mwaka. Kwenye makusanyiko hayo, tulifundishwa njia za kuhubiri na tukaonyeshwa namna ya kushughulika kwa heshima na polisi waliotuingilia. Kwa kuwa mara nyingi Mashahidi walipelekwa mbele ya hakimu wa polisi au kwenye mahakama ya kawaida, tulikuwa tunakariri habari fulani katika kikaratasi cha maagizo kilichoitwa Utaratibu wa Mashtaka. Mafundisho hayo yalitusaidia kukabiliana na upinzani.

Ukuzi wa Mapema Katika Kweli ya Biblia

Niliendelea kupata ujuzi kuhusu kweli za Biblia na kuthamini tumaini linalotegemea Biblia la kuishi milele duniani chini ya Ufalme wa mbinguni wa Mungu. Wakati huo, ubatizo haukukaziwa kwa wale ambao hawakuwa na tumaini la kutawala mbinguni pamoja na Kristo. (Ufunuo 5:10; 14:1, 3) Hata hivyo, niliambiwa kwamba ikiwa nilikuwa nimeamua moyoni mwangu kufanya mapenzi ya Yehova, ingefaa nibatizwe. Nilibatizwa mnamo Agosti 1933.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, mwalimu wangu alifikiri kwamba nilikuwa nikifanya vema katika kusema mbele za watu, kwa hiyo akamhimiza Mama afanye mpango ili nipate mafunzo zaidi. Mama alifikiri kwamba hilo lingenisaidia kumtumikia Yehova vizuri zaidi. Kwa hiyo, alilipia mafunzo yangu kwa kumfulia mwalimu wangu nguo kwa mwaka mmoja. Mafunzo hayo yalinisaidia katika huduma yangu. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilipatwa na ugonjwa wa homa kali ya baridi-yabisi, ambayo ilifanya nikose shule kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Katika mwaka wa 1939, mhudumu wa wakati wote aliyeitwa Warren Henschel alikuja katika eneo letu. * Kiroho, ndugu huyo alikuwa kama ndugu yangu mkubwa, naye alikuwa akiandamana nami kwa muda wa saa nyingi katika kazi ya kuhubiri. Muda si muda alinisaidia kuanza utumishi wa upainia wakati wa likizo, ambao ulikuwa aina ya utumishi wa wakati wote wa muda mfupi. Wakati wa kiangazi cha mwaka huo, kikundi chetu kilifanywa kuwa kutaniko. Warren aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko, nami nikawekwa rasmi kuwa kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi. Warren alipoondoka kwenda kutumika Betheli, makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, mimi nikawa mtumishi wa kutaniko.

Kuanza Huduma ya Wakati Wote

Madaraka yaliyoongezeka kwa kutumikia nikiwa mtumishi wa kutaniko yaliimarisha zaidi tamaa yangu ya kuanza huduma ya kawaida ya wakati wote, ambayo nilianza nikiwa na umri wa miaka 17 baada ya kumaliza kidato cha tatu katika shule ya sekondari. Baba hakuwa Shahidi wa Yehova, lakini alitimiza mahitaji ya familia naye alikuwa mtu mwenye maadili ya juu. Alitaka niende chuoni, lakini akasema kwamba ikiwa sitamtegemea kwa chakula na makao, ningeweza kufanya nilivyotaka. Kwa hiyo, nikaanza upainia Septemba 1, 1940.

Nilipoondoka nyumbani, mama yangu aliniomba nisome Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Bila shaka, Yehova amenisaidia sana kwa kumtegemea sikuzote.

Baada ya muda mfupi nilijiunga na Joe na Margaret Hart waliokuwa wakitumikia kaskazini ya kati ya Jimbo la Washington. Katika eneo hilo kulikuwa na mashamba ya kufuga ng’ombe na kondoo, maeneo yaliyotengewa Wahindi wa Amerika, na pia miji na vijiji vingi vidogo-vidogo. Katika mwaka wa 1941, nilipewa mgawo wa kuwa mtumishi wa kutaniko katika kutaniko la Wenatchee, Washington.

Kwenye mojawapo ya makusanyiko yetu huko Walla Walla, Washington, nilitumikia kama mkaribishaji wa watu waliokuwa wakiingia katika uwanja wa kusanyiko. Nilimwona ndugu mmoja kijana akijitahidi bila kufanikiwa kutengeneza mfumo wa vikuza sauti. Kwa hiyo, nikamwambia tubadilishane migawo. Wakati mtumishi wa eneo, Albert Hoffman, aliporudi na kuona kwamba nilikuwa nimeacha mgawo wangu, alinieleza kwa tabasamu ya kirafiki umuhimu wa mtu kushikamana na mgawo wake mpaka atakapopewa mgawo mwingine. Sijasahau kamwe shauri hilo.

Mnamo Agosti mwaka wa 1941, Mashahidi wa Yehova walipanga kusanyiko kubwa huko St. Louis, Missouri. Joe na Margaret Hart walifunika gari lao lililokuwa wazi nyuma na kuweka viti. Sote tukiwa mapainia 9, tulisafiri kwa gari hilo umbali wa kilometa 2,400 mpaka St. Louis. Ilituchukua muda upatao majuma mawili kwenda na kurudi. Kwenye kusanyiko hilo, polisi walikadiria kwamba kulikuwa na kilele cha wahudhuriaji 115,000. Hata ingawa huenda hudhurio hilo halikufikia hesabu hiyo, bila shaka lilizidi idadi ya Mashahidi wapatao 65,000 waliokuwa nchini Marekani wakati huo. Kusanyiko hilo lilikuwa lenye kuchochea sana kiroho.

Utumishi Kwenye Betheli ya Brooklyn

Baada ya kurudi Wenatchee, nilipata barua iliyoniomba niende kutumika kwenye Betheli ya Brooklyn. Nilipofika huko Oktoba 27, 1941, nilipelekwa kwenye ofisi ya Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa idara ya uchapishaji. Alinieleza kwa fadhili jinsi maisha ya Betheli yalivyo na akakazia kwamba ili kufanikiwa kuishi huko ni muhimu kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Kisha nikapelekwa kwenye Idara ya Usafirishaji na kupewa kazi ya kufunga makatoni ya vichapo ili visafirishwe.

Januari 8, 1942, Joseph Rutherford, aliyesimamia kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote alikufa. Siku tano baadaye, waelekezi wa Sosaiti walimchagua Ndugu Knorr kuchukua mahali pake. Wakati W. E. Van Amburgh, aliyekuwa mwandishi na mweka-hazina wa Sosaiti kwa muda mrefu, alipoitangazia familia ya Betheli kifo hicho, alisema: “Ninaweza kukumbuka wakati C. T. Russell alipokufa [mwaka wa 1916] na mahali pake pakachukuliwa na J. F. Rutherford. Bwana aliendelea kuiongoza na kuifanikisha kazi Yake. Sasa, natarajia kabisa kwamba kazi itaendelea chini ya usimamizi wa Nathan H. Knorr, kwa sababu hii ni kazi ya Bwana wala si ya mwanadamu.”

Mnamo Februari 1942, ilitangazwa kwamba “Mafunzo ya Hali ya Juu ya Huduma ya Kitheokrasi” yangeanzishwa. Yalikusudiwa kuwazoeza wanabetheli kuboresha uwezo wao wa kufanya utafiti kuhusu habari za Biblia, kuzipanga ifaavyo, kisha kuzitoa kwa njia nzuri. Mafunzo niliyokuwa nimepata hapo awali kuhusu kusema mbele ya watu, yalinisaidia kufanya maendeleo haraka sana kuhusiana na programu hiyo.

Baada ya muda mfupi, nilipelekwa kwenye Idara ya Utumishi, inayosimamia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi nchini Marekani. Baadaye mwaka huo, iliamuliwa kuanzisha upya programu ya kuwatuma wahudumu kuyatembelea makutaniko ya Mashahidi. Baada ya muda, wahudumu hao wasafirio, walioitwa watumishi wa akina ndugu, walianza kuitwa waangalizi wa mzunguko. Mnamo mwaka wa 1942, mafunzo fulani yalianzishwa Betheli ili kuwazoeza akina ndugu kwa ajili ya huduma hiyo, nami nikapata pendeleo la kuwa kati ya wale waliopokea mafunzo hayo. Ninakumbuka hasa kwamba Ndugu Knorr, aliyekuwa mmoja wa walimu, alikazia jambo hili: “Usijaribu kuwapendeza wanadamu, kwa kuwa mwishowe hutampendeza yeyote. Mpendeze Yehova, nawe utawapendeza wale wote wanaompenda.”

Kazi ya kusafiri ilianzishwa mnamo Oktoba 1942. Baadhi yetu tuliokuwa Betheli tulifanya kazi hiyo katika miisho-juma fulani, tukitembelea makutaniko yaliyokuwa umbali wa kilometa 400 nje ya New York City. Tulichunguza ripoti za mahubiri za kutaniko na hudhurio la mikutano, tukafanya mikutano pamoja na wale waliokuwa na madaraka katika kutaniko, tukatoa hotuba moja au mbili, na kuhubiri pamoja na Mashahidi kutanikoni.

Katika mwaka wa 1944, nilikuwa miongoni mwa ndugu kutoka Idara ya Utumishi waliopewa mgawo wa kuzunguka kwa muda wa miezi sita katika majimbo ya Delaware, Maryland, Pennsylvania, na Virginia. Baadaye, niliyatembelea makutaniko huko Connecticut, Massachusetts, na Rhode Island, kwa miezi michache. Niliporudi Betheli nilifanya kazi isiyo ya wakati wote katika ofisi ya Ndugu Knorr na mwandishi wake Milton Henschel, ambako nilipata kujua jinsi kazi yetu inavyoendeshwa ulimwenguni pote. Pia nilifanya kazi isiyo ya wakati wote kwenye Ofisi ya Mweka-Hazina chini ya usimamizi wa W. E. Van Amburgh na msaidizi wake, Grant Suiter. Kisha katika mwaka wa 1946, nikawekwa kuwa msimamizi wa ofisi kadhaa huko Betheli.

Mabadiliko Makubwa Katika Maisha Yangu

Nilipokuwa nikitumikia makutaniko mwaka wa 1945, nilijuana na Julia Charnauskas huko Providence, Rhode Island. Kufikia katikati ya mwaka wa 1947 tulikuwa tunafikiria kufunga ndoa. Nilipenda sana utumishi wa Betheli, lakini wakati huohuo, haingewezekana kuleta mwenzi wa ndoa kutumikia huko. Kwa hiyo, mnamo Januari 1948, niliondoka Betheli, kisha nikafunga ndoa na Julia (Julie). Nilipata kazi isiyo ya wakati wote kwenye duka kubwa huko Providence, na tukaanza huduma ya upainia pamoja.

Mnamo Septemba 1949, niliombwa kufanya kazi ya mzunguko huko kaskazini-magharibi mwa Wisconsin. Lilikuwa badiliko kubwa sana kwangu na Julie kuhubiri hasa katika miji midogo na sehemu za mashambani ambako watu walifuga ng’ombe wa maziwa. Majira ya baridi kali yalikuwa marefu, na kwa majuma mengi kiwango cha baridi kilikuwa cha chini sana na kulikuwa na theluji nyingi. Hatukuwa na gari, lakini kila mara mtu fulani alitusafirisha hadi kwenye kutaniko jingine.

Muda mfupi baada ya kuanza kazi ya mzunguko, tulikuwa na kusanyiko la mzunguko. Ninakumbuka nikichunguza kwa makini kuona kwamba kila jambo lilikuwa likishughulikiwa vizuri, jambo ambalo lilifanya wengine wawe na wasiwasi kidogo. Kwa hiyo, mwangalizi wa wilaya, Nicholas Kovalak, akanieleza kwa fadhili kwamba ndugu wenyeji walizoea kufanya mambo kwa njia yao na kwamba sikupaswa kujaribu kuhangaikia kila jambo. Tangu wakati huo, shauri hilo limenisaidia kushughulikia migawo mingi.

Katika mwaka wa 1950, nilipata mgawo wa muda mfupi wa kusimamia idara ya mahali pa kulala kwa ajili ya wajumbe waliokuja kwenye kusanyiko letu la kwanza kati ya makusanyiko mengi makubwa yaliyofanywa katika Uwanja wa Yankee huko New York City. Kusanyiko hilo lilikuwa lenye kusisimua sana tangu mwanzo hadi mwisho, likiwa na wajumbe kutoka nchi 67 na kilele cha hudhurio la watu 123,707! Baada ya kusanyiko, mimi na Julie tuliendelea na kazi ya kusafiri ambayo tuliifurahia sana. Hata hivyo, tulihisi kwamba tulipaswa kuendelea kuwa na nia ya kutumika katika mgawo wowote wa wakati wote. Kwa hiyo, kila mwaka tulijaza fomu za maombi za utumishi wa Betheli na za umishonari. Katika mwaka wa 1952, tulifurahi kupata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 20 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, ambako tulipokea mazoezi ya kazi ya umishonari.

Kutumikia Katika Nchi za Kigeni

Tulipohitimu mnamo mwaka wa 1953, tulitumwa Uingereza, ambako nilitumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya kusini mwa nchi hiyo. Baada ya kufanya kazi hiyo ambayo mimi na Julie tuliifurahia sana kwa muda usiozidi mwaka mmoja, tulishangaa kupata mgawo wa kwenda Denmark. Ofisi ya tawi ya Denmark ilikuwa na uhitaji wa usimamizi mpya. Kwa kuwa nilikuwa karibu na nilikuwa nimezoezwa kufanya kazi hiyo huko Brooklyn, nilitumwa Denmark kusaidia. Tulisafiri kwa feri hadi Uholanzi, ambako tulipanda gari-moshi hadi Copenhagen, Denmark. Tulifika huko Agosti 9, 1954.

Mojawapo ya matatizo yaliyopaswa kushughulikiwa yalihusiana na ndugu wachache wenye madaraka ambao walikataa kutii mwongozo kutoka makao makuu ya Brooklyn. Pia, watafsiri watatu kati ya wanne waliokuwa wakitafsiri vichapo vyetu katika Kidenmark waliondoka Betheli na mwishowe wakaacha kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Lakini Yehova alijibu sala zetu. Mapainia wawili, Jørgen na Anna Larsen ambao walikuwa wakifanya kazi ya kutafsiri kwa muda mfupi, walijitoa kufanya kazi hiyo kwa wakati wote. Hivyo, magazeti yetu yaliendelea kutafsiriwa katika lugha ya Kidenmark bila kukosa hata toleo moja. Jørgen na Anna Larsen wangali Betheli ya Denmark, naye Jørgen ndiye mratibu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi.

Katika miaka hiyo ya mapema, tulitiwa moyo sana na ziara za ukawaida za Ndugu Knorr. Alikuwa akitembelea kila mmoja wetu, na kusimulia mambo yaliyoonwa ambayo yalitusaidia kufahamu jinsi ya kutatua matatizo. Katika ziara aliyofanya mwaka wa 1955, iliamuliwa tujenge ofisi mpya ya tawi yenye sehemu ya kuchapia ili tuweze kuchapisha magazeti ya Denmark. Uwanja ulipatikana kwenye kitongoji kilicho kaskazini mwa Copenhagen, na kufikia mwaka wa 1957, tulihamia jengo jipya. Harry Johnson, pamoja na mke wake Karin, ambao walikuwa tu ndio wamefika Denmark baada ya kuhitimu kutoka darasa la 26 la Gileadi, walisaidia kuweka mashine za uchapaji na kuhakikisha kwamba zinafanya kazi.

Tuliboresha mipango yetu ya kufanya makusanyiko makubwa nchini Denmark, na uzoefu niliopata nilipokuwa nikishughulika na mipango ya makusanyiko nchini Marekani ulinisaidia. Mnamo mwaka wa 1961, kusanyiko kubwa la kimataifa lililofanywa Copenhagen lilikuwa na wajumbe kutoka zaidi ya nchi 30. Kilele cha hudhurio kilikuwa 33,513. Katika mwaka wa 1969, tulikuwa wenyeji wa kusanyiko kubwa zaidi kuwahi kufanywa katika nchi za Skandinavia, lililokuwa na kilele cha wahudhuriaji 42,073!

Mnamo mwaka wa 1963, nilialikwa kuhudhuria darasa la 38 la Gileadi. Hayo yalikuwa mafundisho yaliyorekebishwa ambayo yalichukua muda wa miezi kumi nayo yalikusudiwa kuwazoeza hasa wafanyakazi wa ofisi ya tawi. Nilifurahi kujiunga tena na familia ya Betheli ya Brooklyn na kunufaika na uzoefu wa wale waliokuwa wamesimamia shughuli za makao makuu kwa miaka mingi.

Baada ya mafunzo hayo, nilirudi Denmark ili kuendelea na kazi zangu huko. Isitoshe, nilikuwa na pendeleo la kutumika nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia, na nilitembelea ofisi za tawi za Ulaya magharibi na kaskazini ili kuwatia moyo na kuwasaidia wafanyakazi watimize kazi zao. Hivi karibuni nimefanya kazi hiyo huko Afrika Magharibi na Karibea.

Mwishoni mwa miaka ya 1970, ndugu wa Denmark walianza kutafuta uwanja ambapo jengo kubwa zaidi lingejengwa kwa sababu ya kuongezeka kwa kazi ya utafsiri na uchapaji. Uwanja mzuri ulipatikana kilometa 60 hivi magharibi ya Copenhagen. Mimi pamoja na wengine tulipanga na kuchora ramani ya jengo hilo jipya, nami pamoja na Julie tulitazamia kuishi pamoja na familia ya Betheli kwenye makao hayo mapya mazuri. Lakini haikuwa hivyo.

Twarudi Brooklyn

Mnamo Novemba 1980, mimi na Julie tulialikwa kutumika kwenye Betheli ya Brooklyn, ambako tulifika mapema Januari 1981. Wakati huo tulikuwa na umri uliokaribia miaka 60, na haikuwa rahisi kurudi Marekani baada ya kutumia nusu ya maisha yetu pamoja na ndugu na dada zetu wapendwa wa nchi ya Denmark. Hata hivyo, hatukufikiria sana mahali tulipopendelea kuwa lakini tulijaribu kufikiria migawo yetu ya wakati huo na magumu yake.

Tuliwasili Brooklyn na kuzoea maisha ya huko. Julie alipewa kazi katika ofisi ya hesabu, na kazi yake ilikuwa kama ile aliyofanya nchini Denmark. Nilipewa kazi katika Idara ya Uandishi kusaidia kupanga ratiba ya kutolewa kwa vichapo vyetu. Mapema miaka ya 1980 njia yetu ya kufanya kazi ilibadilika huko Brooklyn kwa kuwa tuliacha kutumia taipureta na mashine nyingine za uchapaji na kuanza kutumia kompyuta na ofseti. Sikujua chochote kuhusu kompyuta lakini nilijua mambo machache kuhusu utaratibu wa kazi na kufanya kazi na watu.

Muda mfupi baadaye, kulikuwa na uhitaji wa kuimarisha utaratibu wa kufanya kazi katika Idara ya Sanaa tulipoanza kutumia michoro na picha za rangi katika uchapaji. Ingawa sikuwa na uzoefu wa usanii, ningeweza kusaidia kupanga kazi. Kwa hiyo, nilikuwa na pendeleo la kusimamia idara hiyo kwa muda wa miaka tisa.

Katika mwaka wa 1992, nilipewa mgawo wa kusaidia Halmashauri ya Utangazaji ya Baraza Linaloongoza na nikapelekwa katika Ofisi ya Mweka-Hazina. Hapa ninaendelea kushughulika na kazi mbalimbali za Mashahidi wa Yehova zinazohusiana na fedha.

Utumishi Wangu Tangu Ujanani

Tangu nilipokuwa kijana mdogo na wakati wa miaka 70 ya utumishi wa kujitoa, Yehova ameendelea kunifundisha kwa subira kupitia Neno lake, Biblia, na ndugu wenye kujali katika tengenezo lake zuri. Nimefurahia huduma ya wakati wote kwa miaka zaidi ya 63, na zaidi ya miaka 55 kati ya hiyo nimetumikia nikiwa pamoja na mke wangu mshikamanifu, Julie. Kwa kweli, ninahisi kwamba Yehova amenibariki sana.

Katika mwaka wa 1940, nilipoondoka nyumbani kuanza utumishi wa painia, baba yangu alidhihaki uamuzi wangu na kusema: “Mwanangu, ukiondoka nyumbani ukafanye kazi hiyo, usifikiri kwamba ukirudi kwangu kuomba msaada nitakusaidia.” Katika miaka iliyofuata sikurudi kumwomba msaada kamwe. Yehova amenitimizia mahitaji yangu kwa ukarimu, mara nyingi kupitia Wakristo wenzangu wenye kujali. Baadaye, baba yangu alianza kuheshimu kazi yetu na hata alifanya maendeleo katika kujifunza kweli ya Biblia kabla ya kufa mwaka wa 1972. Mama aliyekuwa na tumaini la kuishi mbinguni, aliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu hadi alipokufa mwaka wa 1985, akiwa na umri wa miaka 102.

Ingawa matatizo hutokea katika huduma ya wakati wote, mimi na Julie hatujawahi kamwe kufikiria kuacha mgawo wetu. Sikuzote Yehova ametutegemeza kushikamana na azimio letu. Hata wazazi wangu walipozeeka na kuhitaji msaada, dada yangu Victoria Marlin, alijitoa kusaidia na akawatunza kwa fadhili. Tunamshukuru sana kwa msaada wake wa upendo, ambao umetusaidia kuendelea katika huduma ya wakati wote.

Julie ameniunga mkono kwa ushikamanifu katika migawo yetu yote, akiiona kuwa sehemu ya wakfu wake kwa Yehova. Na ingawa nina umri wa miaka 80 na sina afya nzuri, ninahisi kwamba Yehova ametubariki sana. Mimi hutiwa moyo sana na mtunga-zaburi ambaye baada ya kusema kwamba Mungu alikuwa amemfunza tangu ujanani, alisihi, ‘Mpaka wakati wa uzee, Ee Mungu, usiniache, mpaka nitangaze habari za nguvu zako, kwa wale watakaokuja.’—Zaburi 71:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Warren alikuwa ndugu mkubwa wa Milton Henschel, aliyetumikia kwa miaka mingi akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na Mama mwaka wa 1940, nilipoanza upainia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na mapainia wenzangu Joe na Margaret Hart

[Picha katika ukurasa wa 23]

Siku ya arusi yetu, Januari 1948

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na wanafunzi wenzangu wa Gileadi mwaka wa 1953. Kuanzia kushoto hadi kulia: Don na Virginia Ward, Geertruida Stegenga, Julie, na mimi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Frederick W. Franz na Nathan H. Knorr huko Copenhagen, Denmark, mwaka wa 1961

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na Julie leo