Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatua Muhimu ya Kiroho!

Hatua Muhimu ya Kiroho!

Hatua Muhimu ya Kiroho!

Kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Katika Kiswahili

KATIKA Agosti 1, 2003, hatua muhimu ya kiroho ilifikiwa: Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika Kiswahili.

Kwa sasa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana pamoja na Biblia zingine ambazo zimetumiwa kwa muda mrefu na watu wanaomwogopa Mungu katika Afrika Mashariki na ya Kati. Hata hivyo, kwa nini bado kuna uhitaji wa kuwa na tafsiri nyingine ya Biblia? Ni nani aliye chanzo cha tafsiri hiyo? Unawezaje kuwa na hakika kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni yenye kuaminika?

Kwa Nini Kuna Tafsiri Nyingi Sana za Biblia?

Katika miaka ya hivi karibuni, tafsiri mpya nyingi sana za Biblia zimechapishwa. Tafsiri fulani mpya zimefanya Neno la Mungu lipatikane katika lugha kadhaa kwa mara ya kwanza kabisa. Hata hivyo, Biblia mpya pia zinatokezwa katika lugha ambazo tayari zina tafsiri nyingine za Biblia. Kwa nini? Kitabu kinachoitwa So Many Versions?, kilichoandikwa na Sakae Kubo na Walter Specht kinaeleza hivi: “Hakuna tafsiri yoyote ya Biblia ambayo inaweza kusemwa kwamba ndiyo ya mwisho kabisa. Lazima tafsiri ziende sambamba na ongezeko la utafiti wa Biblia na mabadiliko ya lugha.”

Katika karne ya 20, watu walielewa zaidi Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki—lugha ambazo zilitumiwa hapo kwanza kuiandika Biblia. Pia, hati za kale za Biblia ambazo ni sahihi zaidi kuliko zile zilizotumiwa na watafsiri wa Biblia wa miaka iliyopita, zimegunduliwa. Kwa hiyo, Neno la Mungu linaweza kutafsiriwa kwa usahihi zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote!

Kikitaja mashirika ya kibiashara, kichapo The Atlantic Monthly kinasema hivi: “Inashangaza kwamba uchapishaji wa Biblia ni biashara kubwa sana.” Na wakati mwingine tamaa ya kuchapisha kitabu kinachouzwa kwa wingi hufanya lile hangaiko la kutoa tafsiri sahihi lipuuzwe. Biblia fulani mpya hata hujasiria kung’oa mafungu ambayo wachapishaji wake wanayaona kuwa “hayasisimui” hata kidogo. Biblia nyingine hubadili maneno na mafungu ambayo huenda yakawaudhi wasomaji wa sasa. Kwa mfano, tafsiri hiyo hujaribu kuwavutia wale wanaotetea haki za wanawake kwa kumwita Mungu “Baba-Mama.”

Kulificha Jina la Mungu

Labda tabia inayoudhi zaidi ni ile inayohusu jina binafsi la Mungu—Yehova. (Wasomi fulani hulitafsiri jina hilo kuwa “Yahweh.”) Katika nakala za kale za Biblia, jina la Mungu liliandikwa kwa herufi nne za konsonanti ambazo zaweza kutoholewa kuwa YHWH au JHVH. Katika yale yanayoitwa maandiko ya Agano la Kale tu, jina hilo la pekee hupatikana karibu mara 7,000. (Kutoka 3:15; Zaburi 83:18) Basi ni wazi kwamba Muumba wetu alikusudia waabudu wake walijue na vilevile walitumie jina hilo!

Hata hivyo, karne nyingi zilizopita, hofu za kishirikina ziliwafanya Wayahudi waache kulitamka jina hilo la Mungu. Baadaye, maoni hayo ya kishirikina yakauathiri Ukristo pia. (Linganisha Matendo 20:29, 30; 1 Timotheo 4:1.) Hivyo likawa jambo la kawaida kwa watafsiri wa Biblia kutumia jina la cheo, “Bwana,” badala ya jina la Mungu. Leo, Biblia nyingi huliondoa kabisa jina la Mungu. Biblia fulani za kisasa hata hazitaji neno “jina” kwenye Yohana 17:6, ambapo Yesu alisema: “Nimelifunua jina lako.” Biblia Habari Njema hutafsiri mstari huo hivi: “Nimekufanya ujulikane.”

Kwa nini wanalichukia hivyo jina la Mungu? Fikiria habari zilizoandikwa katika kichapo Practical Papers for the Bible Translator. (Buku la 43, namba 4, 1992) Kichapo hicho huchapishwa na Muungano wa Vyama vya Biblia (UBS), shirika ambalo husimamia sehemu kubwa ya kazi ya kutafsiri Biblia duniani. Makala moja ilisema hivi: “Kwa kuwa bila shaka YHWH ni jina la mtu, jambo linalofaa zaidi lingekuwa kubadili matamshi ya neno hilo.” Lakini makala hiyo ikatoa tahadhari hii: “Hata hivyo, kuna mambo fulani ya kufikiriwa.”

Lakini je, mambo hayo ya kufikiriwa yana msingi kweli? Kulingana na kichapo hicho, wasomi fulani hudai hivi: “Tukiwatajia [watu wasio Wakristo] jina kama Yahweh, huenda likatokeza maana isiyofaa. . . , likionyesha kwamba ‘Yahweh’ ni Mungu wa kigeni, au ni Mungu mpya asiyejulikana, aliye tofauti na yule Mungu ambaye tayari wanamjua.” Hata hivyo, Biblia hufundisha na kusisitiza kwamba Yehova Mungu ni tofauti na miungu ambayo watu wasio Wakristo huabudu!—Isaya 43:10-12; 44:8, 9.

Wasomi fulani husema kwamba wanafuata tu mapokeo wakati wanapoliondoa jina la Mungu na badala yake kuweka “BWANA.” Lakini Yesu alishutumu kufuata mapokeo yanayomvunjia Mungu heshima. (Mathayo 15:6) Zaidi ya hayo, lile wazo la kuondoa jina na badala yake kuweka jina la cheo, halina msingi katika Maandiko. Yesu Kristo ana majina mengi ya cheo, kama vile “Neno la Mungu” na “Mfalme wa wafalme.” (Ufunuo 19:11-16) Je, jina la Yesu linapaswa kuondolewa na badala yake kuweka mojawapo ya majina hayo ya vyeo?

Makala nyingine katika kichapo hicho inasema hivi: “Kwa kawaida jina ‘Yehova’ linapaswa kuepukwa.” Wanatoa sababu gani? Wanasema kwamba, “Kwa ujumla, wasomi wanaamini kwamba matamshi ya kwanza huwakilishwa vizuri zaidi na jina ‘Yahweh.’” Hata hivyo, majina ya Biblia ambayo watu wengi wanayajua, kama vile Yeremia, Isaya, na Yesu pia yanatafsiriwa katika njia ambazo hazifanani na matamshi ya kwanza (Yir·meyahʹ, Yesha·yaʹhu, na Yehoh·shuʹa). Kwa kuwa tafsiri halali ya jina la Mungu ni Yehova—na watu wengi wanalijua jina hilo—wanaopinga lisitumiwe hawana msingi thabiti. Kwa kweli, yaonekana kule kukataa kulitumia jina la Mungu kunategemea maoni ya hisia na kibaguzi, wala si usomi.

Hata hivyo, suala linalohusika hapa si la usomi tu. Kwa mfano, mshauri wa shirika la Muungano wa Vyama vya Biblia (UBS) nchini India aliandika kuhusu matokeo ya kuliondoa jina la Mungu katika tafsiri ambamo lilikuwa zamani. Anakiri hivi: “Wahindu hawapendezwi na jina la cheo la Mungu; wanataka kulijua jina binafsi la Mungu, nao wasipolijua jina hilo hawawezi kuwa na uhusiano na yule mwenye jina hilo.” Kwa kweli, hivyo ndivyo ilivyo kwa wote wanaomtafuta Mungu. Kulijua jina la Mungu ni muhimu ili kufahamu kwamba yeye ni mtu ambaye tunaweza kumjua, wala si nguvu tu zisizo na utu. (Kutoka 34:6, 7) Kwa hiyo Biblia inatangaza hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Waroma 10:13) Waabudu wa Mungu lazima walitumie jina lake!

Tafsiri Inayomheshimu Mungu

Basi, hatua kubwa ilipigwa katika mwaka wa 1950 wakati ambapo chapa ya Kiingereza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilichapishwa kwa mara ya kwanza. Miaka kumi iliyofuata, yale maandiko ambayo kwa kawaida huitwa Agano la Kale, au Maandiko ya Kiebrania, yalichapishwa hatua kwa hatua. Mnamo mwaka wa 1961, Biblia nzima katika Kiingereza ilitolewa ikiwa buku moja. Jambo muhimu ni kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hulitumia jina Yehova kila mahali linapopatikana katika “Agano la Kale,” nalo linapatikana karibu mara 7,000. Jambo lenye kutokeza hata zaidi ni kule kurudishwa kwa jina la Mungu mara 237 katika “Agano Jipya,” au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Kulirudisha jina hilo humletea Mungu heshima na pia huleta uelewaji mpya. Kwa mfano, tafsiri nyingi hutafsiri andiko la Mathayo 22:44 hivi: “Bwana alimwambia Bwana wangu.” Lakini kwa kweli, ni nani anayesema na mwingine? Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inanukuu kwa usahihi andiko la Zaburi 110:1 inapoutafsiri mstari huo hivi: “Yehova alimwambia Bwana wangu.” Basi wasomaji wanaweza kuona tofauti muhimu iliyopo kati ya Yehova Mungu na Mwana wake.

Ni Nani Aliye Chanzo cha Tafsiri Hiyo?

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya huchapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society, ambalo ni shirika la kisheria linalowakilisha Mashahidi wa Yehova. Kwa zaidi ya miaka mia moja, Sosaiti hii imechapisha na kugawanya Biblia duniani kote. Kikundi cha Wakristo kinachoitwa Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mpya kiliikabidhi Sosaiti tafsiri hii hususa. Badala ya kujitafutia umashuhuri wa kibinafsi, washiriki wa halmashauri hiyo waliomba kwamba majina yao yasitajwe hata baada ya kifo chao.—Linganisha na 1 Wakorintho 10:31.

Hata hivyo, kwa nini tafsiri hii iliitwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya? Hilo lilionyesha uhakika thabiti kwamba wanadamu wako “mlangoni pa ulimwengu mpya” ulioahidiwa katika andiko la 2 Petro 3:13. Kama halmashauri hiyo yenyewe ilivyoandika, ni muhimu kwamba “wakati huu wa umalizio wa ulimwengu wa zamani” tafsiri za Biblia ziruhusu “kweli safi ya Neno la Mungu” iangaze.—Ona Utangulizi wa chapa ya 1950.

Tafsiri Sahihi

Jambo la kwanza lililotiliwa maanani ni usahihi. Watafsiri wa chapa ya Kiingereza walitafsiri moja kwa moja kutoka lugha za Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki, wakitumia hati bora zaidi zilizokuwapo. * Tahadhari ya pekee ilitumiwa pia ili kutafsiri maandishi ya kale kama yalivyo kwa kadiri iwezekanavyo—lakini katika lugha ambayo wasomaji wa siku hizi wanaweza kuielewa kwa urahisi.

Basi haishangazi kwamba wasomi fulani wameisifu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa usahihi wake. Profesa Benjamin Kedar, ambaye ni msomi wa Kiebrania nchini Israeli, alisema hivi mwaka wa 1989: “Katika utafiti wangu wa lugha kuhusiana na Biblia ya Kiebrania na tafsiri mbalimbali, mara nyingi mimi husoma chapa ya Kiingereza inayoitwa New World Translation. Kwa kufanya hivyo, maoni yangu huthibitishwa tena na tena kwamba tafsiri hii huonyesha juhudi za unyofu za kutuwezesha kuelewa kadiri iwezekanavyo maandishi ambayo ni sahihi kabisa.”

Kufanya Chapa Nyingine Zipatikane

Kwa kufaa basi, Watch Tower Society imefanya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ipatikane katika maeneo ambayo hayatumii Kiingereza. Hivi sasa inachapishwa, ikiwa nzima au ikiwa sehemu, katika lugha 44. Ili kurahisisha mradi huo, Sosaiti ilibuni mbinu ya kutafsiri Biblia ambayo hutumia utafiti wa maneno ya Biblia na utaalamu wa kompyuta. Sosaiti pia ilianzisha idara inayoitwa Huduma za Tafsiri, ambayo sasa iko Patterson, New York, ili kuwasaidia watafsiri. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova husimamia kwa ukaribu kazi ya kutafsiri Biblia kupitia Halmashauri ya Uandikaji. Lakini kazi hii hufanywaje hasa?

Kwanza, Wakristo waliojiweka wakfu huchaguliwa ili kufanyiza kikundi cha kutafsiri. Imeonekana kwamba watafsiri wanapofanya kazi pamoja badala ya kufanya kazi wakiwa mtu mmoja-mmoja, wao hutokeza tafsiri ambayo ni bora na yenye kusawazika zaidi. (Linganisha na Methali 11:14.) Kwa ujumla, kila mshiriki wa kikundi hicho tayari huwa na uzoefu wa kutafsiri vichapo vya Sosaiti. Kisha kikundi hicho hupewa mazoezi kamili kuhusu kanuni za msingi za kutafsiri Biblia na kutumia programu za pekee za kompyuta.

Kikundi cha kutafsiri huagizwa kitafsiri Biblia ambayo ni (1) sahihi, (2) yenye upatano, (3) ambayo maneno yake hutafsiriwa kama yalivyo kabisa kulingana na lugha, na bado (4) iwe yenye kueleweka kwa urahisi na watu wa kawaida. Mambo hayo hutimizwaje? Hebu ifikirie Biblia hii mpya ambayo imetolewa. Kikundi cha watafsiri kilianza kwa kuteua maneno muafaka ya Kiswahili kwa ajili ya maneno yote muhimu ya Biblia yanayotumiwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza. Kompyuta iliratibiwa kuonyesha maneno ya Biblia yanayofanana na pia maneno yenye maana sawa. Pia ilionyesha maneno ya awali ya Kigiriki au Kiebrania ambayo yalitokeza maneno ya Kiingereza ili mtafsiri aweze kuchunguza jinsi maneno hayo ya Kigiriki au Kiebrania yalivyotafsiriwa mahali penginepo katika tafsiri ya Kiingereza. Hayo yote yalisaidia sana katika uteuzi wa maneno muafaka ya Kiswahili. Halafu kikundi cha watafsiri walipokubaliana juu ya maneno hayo, wakaanza kuitafsiri Biblia, wakitumia kompyuta ili kuona maneno ya Kiswahili walipokuwa wakitafsiri kila mstari.

Hata hivyo, kutafsiri huhusisha mambo mengi zaidi kuliko tu kubadili maneno kutoka lugha moja hadi nyingine. Ilikuwa lazima kazi nyingi ifanywe ili kuhakikisha maneno ya Kiswahili yaliyoteuliwa yalitoa mawazo sahihi ya Kimaandiko katika kila muktadha. Pia watafsiri walihakikisha kwamba sarufi na mtiririko wa maneno ni mzuri na wenye kueleweka. Basi, kazi ngumu iliyofanyiwa mradi huo wa kuitafsiri Biblia inaonekana wazi. Chapa ya Kiswahili ya Tafsiri ya Ulimwengu  Mpya hulitafsiri Neno la Mungu kwa njia ambayo ni rahisi kusoma, wazi, yenye kueleweka, na inayoshikamana kabisa na maandishi ya kale.

Tunakutia moyo uichunguze mwenyewe kwa makini Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Unaweza kuipata kutoka kwa wachapaji wa gazeti hili au kutoka kwa kutaniko la kwenu la Mashahidi wa Yehova. Unaweza kuisoma kila siku ukiwa na uhakika kwamba imetafsiri kwa usahihi maneno ya Mungu katika lugha yako mwenyewe. Bila shaka, muda si muda utakubali kwamba kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kiswahili kwa kweli ni hatua muhimu ya kiroho!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Tafsiri The New Testament in the Original Greek, ya Westcott na Hort, ilitumiwa hasa kutafsiri maandishi ya Kigiriki. Tafsiri Biblia Hebraica ya R. Kittel ilitumiwa hasa kutafsiri Maandiko ya Kiebrania.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Baadhi ya Sehemu Muhimu za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya

Ni Wazi na Inasomeka kwa Urahisi

Mistari Imekusanywa Katika Mafungu: Badala ya kufanya kila mstari kuwa fungu linalotenganishwa, mistari inakusanywa katika mafungu. Hilo linamsaidia msomaji kufuata jinsi mawazo ya waandikaji wa Biblia yanavyofuatana.

Maneno ya Mwanzoni mwa Ukurasa: Yakiwa yameonyeshwa juu karibu kwenye kurasa zote, maneno hayo yanasaidia kupata haraka mahali ambapo masimulizi ya Biblia hupatikana.

Marejeo ya Pambizoni: Kila ukurasa una marejeo ambayo yanakuelekeza kwenye maandiko ya Biblia yanayolingana.

Fahirisi: Nyuma ya kitabu kuna sehemu yenye kichwa “Fahirisi ya Baadhi ya Maneno ya Biblia.” Kwa kawaida, maneno yaliyochaguliwa na mahali yanapopatikana katika Biblia yanaorodheshwa pamoja na maelezo mafupi yanayoonyesha muktadha.

Nyongeza: Mfuatano wa makala fupi-fupi kuhusu mafundisho ya msingi ya Biblia na habari nyingine.