Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hubiri Ili Kufanya Wanafunzi

Hubiri Ili Kufanya Wanafunzi

Hubiri Ili Kufanya Wanafunzi

“Prisila na Akila walipomsikia [Apolo], wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” —Matendo 18:26.

1. Ingawa Apolo alikuwa “amewaka roho,” alihitaji nini?

PRISILA na Akila, wenzi wa ndoa Wakristo wa karne ya kwanza, walimsikia Apolo akitoa hotuba kwenye sinagogi moja katika jiji la Efeso. Apolo alikuwa amenasa fikira za wasikilizaji wake kwa ufasaha na uwezo wake wa kushawishi. Alikuwa “amewaka roho,” naye alikuwa ‘akifundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu.’ Hata hivyo, ilikuwa wazi kwamba Apolo ‘alifahamu ubatizo wa Yohana tu.’ Yale ambayo Apolo alihubiri kumhusu Kristo yalikuwa ya kweli lakini hayakutosha. Tatizo lilikuwa kwamba hakuwa na ujuzi wa kutosha kumhusu Kristo. Apolo alihitaji kuongeza ujuzi wake kuhusu daraka la Yesu Kristo katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova.—Matendo 18:24-26.

2. Prisila na Akila walikabili jambo gani gumu?

2 Bila kukawia, Prisila na Akila walijitoa kumsaidia Apolo aweze kushika “mambo yote” ambayo Kristo aliamuru. (Mathayo 28:19, 20) Masimulizi hayo yanasema kwamba ‘walimchukua Apolo na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’ Hata hivyo, kuna mambo fulani kumhusu Apolo ambayo yangewafanya Wakristo fulani wasite kumfundisha. Ni mambo gani hayo? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jitihada za Prisila na Akila za kuzungumzia Maandiko pamoja na Apolo? Kuchunguza masimulizi hayo ya zamani kunaweza kutusaidiaje kuelekeza juhudi zetu katika kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

Kazia Fikira Juu ya Mahitaji ya Watu

3. Kwa nini malezi ya Apolo hayakuwazuia Prisila na Akila wasimfundishe?

3 Akiwa Myahudi wa asili, yaelekea kwamba Apolo alilelewa katika jiji la Aleksandria. Wakati huo Aleksandria ulikuwa mji mkuu wa Misri na kituo cha elimu ya juu, kilichokuwa mashuhuri kwa sababu ya maktaba yake kubwa. Mji huo ulikuwa na wakaaji wengi Wayahudi, kutia ndani wasomi. Hivyo, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania inayojulikana kuwa Septuagint ilitafsiriwa huko. Si ajabu kwamba Apolo alikuwa “mwenye ujuzi mwingi sana wa Maandiko”! Akila na Prisila walikuwa watengenezaji wa mahema. Je, ufasaha wa Apolo uliwaogopesha? La. Kwa upendo walimwona kama mtu tu, wakafikiria mahitaji yake, na jinsi ambavyo wangeweza kumsaidia.

4. Apolo alipata wapi msaada aliohitaji na kwa njia gani?

4 Hata ingawa Apolo alikuwa msemaji mwenye ufasaha sana alihitaji kufundishwa. Msaada aliohitaji haungepatikana kwenye chuo kikuu chochote bali ungepatikana miongoni mwa washiriki wenzake katika kutaniko la Kikristo. Apolo angenufaika na habari ambazo zingetokana na uelewaji sahihi zaidi wa mpango wa Mungu wa wokovu. Prisila na Akila ‘walimchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’

5. Hali ya kiroho ya Prisila na Akila ilikuwaje?

5 Prisila na Akila walikuwa wenye nguvu kiroho na wenye imani thabiti. Yaelekea ‘sikuzote walikuwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye alitaka kutoka kwao sababu ya tumaini lao,’ hata kama mtu huyo alikuwa tajiri, maskini, msomi, au mtumwa. (1 Petro 3:15) Akila na mke wake waliweza ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Ni wazi kwamba walikuwa wanafunzi wenye bidii wa Maandiko. Apolo alichochewa sana na mafundisho yaliyotegemea ‘neno la Mungu lililo hai na lenye nguvu,’ ambalo hugusa moyo.—Waebrania 4:12.

6. Tunajuaje kwamba Apolo alithamini msaada aliopata?

6 Apolo alithamini kielelezo cha walimu wake naye akawa mwenye ustadi zaidi katika kufanya wanafunzi. Alitumia ujuzi wake kikamili katika kazi ya kutangaza habari njema, hasa kwa Wayahudi. Apolo alisaidia kwa njia ya pekee kuwashawishi Wayahudi wamwamini Kristo. ‘Kwa kuwa alikuwa hodari katika Maandiko,’ aliweza kuwathibitishia kwamba manabii wote wa zamani walitazamia kuja kwa Kristo. (Matendo 18:24, Union Version) Masimulizi hayo yanaongeza kusema kwamba baadaye Apolo alienda Akaya, ambako ‘aliwasaidia sana wale waliokuwa wameamini kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu; kwa maana kwa juhudi nyingi alithibitisha kikamili hadharani kuwa Wayahudi ni wenye makosa, huku akionyesha kwa Maandiko kwamba Yesu alikuwa ndiye Kristo.’—Matendo 18:27, 28.

Jifunze Kutokana na Kielelezo cha Walimu Wengine

7. Akila na Prisila walipataje kuwa walimu stadi?

7 Akila na Prisila walipataje kuwa walimu stadi wa Neno la Mungu? Mbali na bidii yao katika funzo la kibinafsi na kuhudhuria mikutano, bila shaka, kushirikiana kwa ukaribu na mtume Paulo kuliwasaidia sana. Paulo alikaa nyumbani kwa Prisila na Akila huko Korintho kwa miezi 18. Walifanya kazi pamoja ya kutengeneza na kurekebisha mahema. (Matendo 18:2, 3) Wazia jinsi mazungumzo yao kuhusu Maandiko yalivyokuwa yenye kina! Bila shaka, walinufaika sana kiroho kwa kushirikiana na Paulo. Andiko la Methali 13:20 linasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” Mashirika mazuri yaliwasaidia kuwa na mazoea mazuri ya kiroho.—1 Wakorintho 15:33.

8. Prisila na Akila walijifunza nini kwa kumtazama Paulo akihubiri?

8 Wakati Prisila na Akila walipomtazama Paulo akitangaza Ufalme, walitambua kwamba alikuwa mwalimu bora. Masimulizi katika Matendo yanasema kwamba Paulo “alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi [huko Korintho] kila sabato na alikuwa akiwashawishi Wayahudi na Wagiriki.” Baadaye, Sila na Timotheo walipojiunga naye, Paulo ‘alianza kushughulika sana na lile neno, akiwatolea Wayahudi ushahidi ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Kristo.’ Prisila na Akila waliona kwamba Paulo alihamia nyumba iliyokuwa karibu na sinagogi ambapo watu waliitikia vizuri zaidi alipoona kwamba washiriki wa sinagogi hawakupendezwa sana na ujumbe wake. Huko Paulo aliweza kumsaidia Krispo “ofisa-msimamizi wa sinagogi,” kuwa mwanafunzi. Yaelekea Prisila na Akila walitambua kwamba kumfanya mtu huyo mmoja kuwa mwanafunzi kulikuwa na matokeo makubwa sana katika eneo hilo. Masimulizi hayo yanasema: “Krispo . . . akawa mwamini katika Bwana, na ndivyo na watu wote wa nyumba yake. Na wengi kati ya Wakorintho waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.”—Matendo 18:4-8.

9. Prisila na Akila walifanyaje baada ya kutazama kielelezo cha Paulo?

9 Prisila na Akila na watangazaji wengine wa Ufalme waliiga kielelezo cha Paulo katika kuhubiri. Mtume huyo aliwahimiza hivi Wakristo wengine: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Kwa kuiga kielelezo cha Paulo, Prisila na Akila walimsaidia Apolo kuelewa mafundisho ya Kikristo kwa usahihi zaidi. Naye Apolo akawasaidia wengine. Bila shaka, Prisila na Akila walisaidia kufanya wanafunzi huko Roma, Korintho, na Efeso.—Matendo 18:1, 2, 18, 19; Waroma 16:3-5.

10. Umejifunza mambo gani katika Matendo sura ya 18 yatakayokusaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi?

10 Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza Matendo sura ya 18? Kama vile yaelekea Akila na Prisila walijifunza kutoka kwa Paulo, tunaweza kuboresha uwezo wetu wa kufanya wanafunzi kwa kuiga kielelezo cha walimu wazuri wa Neno la Mungu. Tunaweza kushirikiana na wale ambao ‘hushughulika sana na lile neno’ na ambao ‘huwatolea wengine ushahidi kamili.’ (Matendo 18:5, Kingdom Interlinear Translation) Tunaweza kuchunguza jinsi wanavyoifikia mioyo ya watu kwa kufundisha kwa ustadi na kwa ushawishi. Ustadi huo unaweza kutusaidia kufanya wanafunzi. Tunapojifunza Biblia na mtu fulani, tunaweza kumwomba awaalike washiriki wengine wa familia yake au majirani wajiunge naye. Au tunaweza kumwomba atueleze ikiwa kuna wengine ambao tunaweza kujifunza Biblia pamoja nao.—Matendo 18:6-8.

Tafuta Nafasi za Kufanya Wanafunzi

11. Wanafunzi wapya wanaweza kupatikana wapi?

11 Paulo na Wakristo wenzake walijitahidi kufanya wanafunzi kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba, sokoni, na waliposafiri—naam, kila mahali. Ukiwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii unayetaka kufanya wanafunzi, je, unaweza kupanua utumishi wako wa shambani? Je, unaweza kutumia ifaavyo nafasi za kutafuta watu wanaostahili na kuwahubiria? Ni kwa kutumia njia gani watangazaji wa habari njema wenzetu wamepata wanafunzi? Kwanza na tuchunguze kuhubiri kwa njia ya simu.

12-14. Ili kuonyesha manufaa ya mahubiri ya simu, simulia jambo ulilojionea au mojawapo ya mambo yaliyotajwa kwenye mafungu haya.

12 Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba huko Brazili, Mkristo tutakayemwita Maria alimpa trakti mwanamke mmoja kijana aliyekuwa anaondoka katika jengo fulani. Maria alitumia kichwa cha trakti hiyo kama utangulizi, na kumwuliza, “Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu Biblia?” Mwanamke huyo akamjibu: “Ningependa. Lakini tatizo ni kwamba mimi ni mwalimu, na hutumia wakati wangu wote kufundisha.” Maria alimweleza kwamba wangeweza kuzungumzia habari za Biblia kupitia simu. Mwanamke huyo alimpa Maria namba yake ya simu, kisha jioni hiyohiyo akaanza kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? * kupitia simu.

13 Alipokuwa akihubiri kupitia simu, dada mmoja ambaye ni mhudumu wa wakati wote huko Ethiopia alishangaa alipozungumza na mwanamume mmoja na kusikia kelele fulani. Mwanamume huyo alimwomba ampigie simu baadaye. Dada huyo alipompigia simu, mwanamume huyo aliomba msamaha na kusema kwamba wakati simu hiyo ilipopigwa mara ya kwanza, yeye na mke wake walikuwa wakigombana vikali. Aliposikia hivyo, dada huyo alitumia nafasi hiyo kueleza kwamba Biblia ina mwongozo wa hekima wa kutatua matatizo ya familia. Alimwambia kwamba familia nyingi zimesaidiwa na kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Siku chache baada ya kumpelekea kitabu hicho, dada huyo alimpigia simu tena mwanamume huyo. Alisema: “Kitabu hiki kimeokoa ndoa yangu!” Mwanamume huyo alifanya mkutano na familia yake na kuieleza mambo mazuri aliyokuwa amesoma katika kitabu hicho. Baada ya muda mfupi, funzo la Biblia la nyumbani lilianzishwa, na mtu huyo akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida.

14 Mtangazaji mmoja wa Ufalme huko Denmark ambaye alianzisha funzo la Biblia kwa kuhubiri kupitia simu anasema: “Mwangalizi wa utumishi alinitia moyo nishiriki katika mahubiri ya kutumia simu. Mwanzoni nilisita nikisema: ‘Sipendelei mahubiri hayo.’ Hata hivyo, siku moja nilipiga moyo konde na nikampigia simu mwenye-nyumba wa kwanza. Sonja alijibu simu hiyo, na baada ya mazungumzo mafupi akakubali vichapo vinavyozungumzia Biblia. Jioni moja tulizungumza kuhusu uumbaji, na mwanamke huyo akataka kusoma kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation. * Nilimwambia kwamba ingekuwa vema kama tungekutana uso kwa uso na kuzungumzia habari hiyo. Alikubali. Nilipofika, Sonja alikuwa tayari kujifunza na tangu wakati huo tumekuwa tukijifunza kila juma.” Dada yetu Mkristo anamalizia: “Nilikuwa nimesali kwa miaka mingi ili nipate funzo la Biblia, lakini sikutazamia kupata funzo kupitia mahubiri ya simu.”

15, 16. Unaweza kusimulia mambo gani yaliyoonwa ili kuonyesha manufaa ya kuwa macho kutumia njia mbalimbali za kuanzisha mafunzo ya Biblia?

15 Wengi wanapata mafanikio kwa sababu ya kutumia madokezo ya kuhubiria watu mahali popote wanapopatikana. Mwanamke mmoja Mkristo huko Marekani alisimamisha gari lake karibu na gari la biashara kwenye sehemu ya kuegesha magari. Mwanamke aliyekuwa ndani ya gari hilo alipomwona, dada huyo alimweleza kuhusu kazi yetu ya kufundisha watu Biblia. Mwanamke huyo alisikiliza, akatoka nje ya gari, na kukaribia gari la dada huyo. Kisha akasema: “Nimefurahi sana kwamba umeegesha gari lako ili kuzungumza nami. Kwa muda mrefu sijapokea vichapo vyenu vinavyozungumzia Biblia. Isitoshe, ningependa kujifunza Biblia tena. Je, utajifunza pamoja nami?” Kwa hiyo, dada yetu alitafuta nafasi inayofaa ya kuhubiri habari njema.

16 Dada mmoja huko Marekani anasimulia jinsi alivyofanya alipotembelea hospitali moja ya kibinafsi: Alizungumza na mkurugenzi aliyesimamia kazi fulani katika hospitali hiyo na kumwambia kwamba angependa kujitolea kusaidia kutimiza mahitaji ya kiroho ya watu walioishi huko. Dada yetu aliongeza kusema kwamba angependa kujifunza Biblia kila juma bila malipo pamoja na wote waliotaka kuhudhuria funzo hilo. Mkurugenzi huyo alimpa ruhusa ya kutembelea vyumba vya wakaaji mbalimbali. Baada ya muda mfupi, alikuwa akiongoza funzo la Biblia mara tatu kwa juma pamoja na wakaaji 26, na mmoja wao anahudhuria mikutano yetu kwa ukawaida.

17. Ni njia gani ambayo mara nyingi inakuwa na matokeo katika kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

17 Watangazaji fulani wa Ufalme hupata matokeo mazuri kwa kuanzisha funzo la Biblia moja kwa moja. Asubuhi moja, kutaniko lenye wahubiri 105 walifanya jitihada ya pekee ili kumtolea kila mwenye nyumba waliyekutana naye nafasi ya kujifunza Biblia. Wahubiri 86 walishiriki katika kazi ya kuhubiri, na baada ya kuhubiri kwa muda wa saa mbili, walianzisha mafunzo mapya ya Biblia yapatayo 15.

Endelea Kuwatafuta Wanaostahili

18, 19. Tunapaswa kukumbuka agizo gani muhimu la Yesu, na tunapaswa kuazimia kufanya nini ili kulitimiza?

18 Ukiwa mtangazaji wa Ufalme, huenda ukataka kujaribu kutumia madokezo yaliyotajwa katika makala hii. Bila shaka, lingekuwa jambo la hekima kuzingatia desturi za kwenu unapofikiria njia za kuhubiri. Zaidi ya yote, na tukumbuke agizo la Yesu la kutafuta wanaostahili na kuwasaidia wawe wanafunzi.—Mathayo 10:11; 28:19.

19 Ili kutimiza kusudi hilo, na ‘tulitumie sawasawa neno la kweli.’ Tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia ushawishi unaotegemea kabisa Maandiko. Hilo litatusaidia kufikia mioyo ya wenye kusikiliza na kuwachochea kutenda. Tunapomtegemea Yehova katika sala, tunaweza kushiriki katika kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. Kazi hiyo inathawabisha sana. Kwa hiyo, acheni ‘tufanye yote tuwezayo ili tujitoe kwa Mungu tukiwa watu waliokubaliwa,’ sikuzote tukimheshimu Yehova tukiwa watangazaji wa Ufalme wenye bidii, ambao huhubiri wakiwa na kusudi la kufanya wanafunzi.—2 Timotheo 2:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Apolo alihitaji kufafanuliwa njia ya Mungu kwa ukamili zaidi?

• Prisila na Akila walijifunza kutoka kwa mtume Paulo katika njia gani mbalimbali?

• Umejifunza nini kuhusu kazi ya kufanya wanafunzi katika Matendo sura ya 18?

• Unawezaje kutafuta nafasi za kufanya wanafunzi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Prisila na Akila ‘walimfafanulia Apolo kwa usahihi zaidi njia ya Mungu’

[Picha katika ukurasa wa 20]

Apolo alikuwa stadi katika kufanya wanafunzi

[Picha katika ukurasa wa 21]

Paulo alihubiri popote alipoenda

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tafuta nafasi za kuhubiri