Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso?

Je, Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso?

Je, Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso?

WATU wachache huamini kwamba dunia itakuwa paradiso. Wengi hufikiri kwamba dunia haitaendelea kuwapo kamwe. Kulingana na kitabu The Sacred Earth, cha Brian Leigh Molyneaux, dunia hii ilitokana na ‘mlipuko mkubwa uliotokea ulimwenguni’ mamilioni ya miaka iliyopita. Wengi wanaamini kwamba ikiwa mwanadamu mwenyewe hataiharibu dunia, huenda mwishowe dunia na ulimwengu wote “vitateketea kabisa kwa moto.”

Mtunga-mashairi Mwingereza wa karne ya 17, John Milton, hakuwa na maoni hayo mabaya. Katika shairi lake maarufu Paradise Lost, aliandika kwamba Mungu aliumba dunia iwe makao ya paradiso kwa ajili ya familia ya kibinadamu. Paradiso hiyo ya kwanza ilipotea. Hata hivyo, Milton aliamini kwamba ingerudishwa—kwamba siku moja mkombozi aitwaye Yesu Kristo “angewathawabisha waaminifu wake, na kuwakaribisha waishi maisha ya raha mustarehe . . . Mbinguni au Duniani.” Milton alisema hivi kwa uhakika: “Wakati huo Dunia itakuwa Paradiso.”

Je, Paradiso Itakuwa Mbinguni au Duniani?

Watu wengi wa dini wana maoni kama ya Milton kwamba mwishowe watapata thawabu ya aina fulani kwa sababu ya kuteseka sana hapa duniani. Lakini watafurahia thawabu hiyo wapi? Je, wataifurahia “Mbinguni au Duniani”? Wengine hata hawaoni kama wanaweza kuifurahia duniani. Wanasema kwamba watu watafurahia “maisha ya raha mustarehe” baada tu ya kuondoka duniani na kwenda kuishi katika makao ya roho mbinguni.

Kitabu Heaven—A History, kilichoandikwa na C. McDannell na B. Lang kinasema kwamba Irenaeus, mwanatheolojia wa karne ya pili, aliamini kwamba maisha katika paradiso iliyorudishwa “hayangekuwa katika makao fulani ya mbali ya kimbingu, bali yangekuwa duniani.” Kitabu hicho kinasema kwamba, ingawa viongozi wa kidini kama vile John Calvin na Martin Luther walitumaini kwenda mbinguni, wao waliamini pia kwamba “Mungu angeifanya dunia kuwa mpya.” Wafuasi wa dini nyingine wamekuwa na imani kama hiyo. Pia McDannell na Lang wanasema kwamba baadhi ya Wayahudi waliamini kwamba katika wakati wa Mungu unaofaa, magumu yote yanayowapata wanadamu “yataondolewa kisha maisha duniani yawe yenye kuridhisha.” Waajemi wa kale waliamini kwamba “hali ya kwanza ya dunia itarudishwa na watu wataishi tena kwa amani,” chasema kichapo The Encyclopaedia of Middle Eastern Mythology and Religion.

Ni nini kilichotukia kuhusiana na tumaini la kuwa na paradiso duniani? Je, maisha yetu duniani ni ya muda tu? Kama mwanafalsafa Myahudi wa karne ya kwanza Philo alivyoamini, je, maisha hayo ni “kipindi kifupi tu, ambacho mara nyingi hukumbwa na misiba” tunapokuwa katika safari ya kwenda katika makao ya roho? Au je, Mungu alikuwa na kusudi fulani tofauti alipoiumba dunia na kuwaweka wanadamu humo katika hali za kiparadiso? Je, wanadamu wanaweza kupata uradhi wa kweli wa kiroho na maisha ya raha mustarehe hapa duniani? Kwa nini usichunguze yale ambayo Biblia husema kuhusu jambo hilo? Kama vile mamilioni ya watu wanavyoamini, huenda ukafikia mkataa kwamba kuwa na tumaini la kuishi katika dunia paradiso iliyorudishwa ni jambo ambalo kwa kweli linapatana na akili.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Mtunga-mashairi, John Milton, aliamini kwamba Paradiso ingerudishwa

[Picha katika ukurasa wa 2 zimeandaliwa na]

COVER: Earth: U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Earth: U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA; John Milton: Leslie’s