Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kabla na Baadaye—Kanuni za Biblia Zilimfanya Abadilike Sana

Kabla na Baadaye—Kanuni za Biblia Zilimfanya Abadilike Sana

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Kabla na Baadaye—Kanuni za Biblia Zilimfanya Abadilike Sana

ALIPOKUWA kijana, Adrian alikuwa mwenye uchungu na hasira kali. Tabia yake ya kukasirika haraka ilifanya awe mwenye kulipuka kwa hasira kali. Alikuwa anakunywa, anavuta sigara, na kuishi maisha yasiyo maadilifu. Adrian alijulikana kuwa mhuni na alikuwa na chanjo mwilini iliyoonyesha imani yake ya kutofuata sheria. Anasema hivi kuhusu wakati huo: “Nilinyolewa nywele kama mhuni na kuipaka gundi iliyoifanya isimame. Wakati mwingine niliipaka rangi nyekundu au nyingineyo.” Adrian alitoboa pia pua yake.

Adrian alihamia nyumba iliyokuwa imechakaa ambamo aliishi na vijana wengine waasi. Humo walikunywa pombe na kutumia dawa za kulevya. “Nilijidunga sindano ya mchanganyiko mbalimbali wa dawa za kulevya na dawa zozote ambazo ningeweza kupata,” anasema Adrian. “Nilipokosa dawa za kulevya au gundi, nilitoa petroli katika magari ya watu na kuinusa ili nilewe.” Adrian alikuwa mwenye kutisha na mwenye jeuri sana kwa sababu aliishi maisha ya uhalifu ya mitaani. Kwa ujumla watu hawakutaka kujishughulisha naye. Wakati huohuo, kwa sababu ya sifa yake mbaya Adrian hakuwa na marafiki wazuri.

Hatua kwa hatua, Adrian alitambua kwamba “marafiki” wake walishirikiana naye ili kujinufaisha tu. Isitoshe, aliona kwamba “hasira na jeuri yote haikuwa imetimiza kitu.” Akiwa bila kusudi na mwenye kuvunjika moyo, Adrian aliwaacha marafiki wake. Alipopata nakala ya Mnara wa Mlinzi mahali fulani pa ujenzi, alivutiwa na ujumbe unaotegemea Biblia naye akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Adrian alikubali kwa shauku mwaliko huu: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Kwa hiyo, baada ya muda mfupi Adrian aliona kwamba anahitaji kuanza kutumia kanuni zinazopatikana katika Maandiko Matakatifu.

Adrian alipozidi kupata ujuzi wa Biblia, dhamiri yake ilianza kufanya kazi vizuri na maisha yake yakabadilika. Alisaidiwa kudhibiti hasira yake na kusitawisha sifa ya kujizuia. Kwa sababu ya nguvu za Neno la Mungu, utu wa Adrian ulibadilika kabisa.—Waebrania 4:12.

Hata hivyo, Biblia ingewezaje kuwa na uvutano mkubwa kadiri hiyo? Kujua Maandiko hutusaidia “kuvaa utu mpya.” (Waefeso 4:24) Naam, utu wetu hubadilika tunapoishi kupatana na ujuzi sahihi unaopatikana katika Biblia. Lakini ujuzi huo hubadili watu jinsi gani?

Kwanza, Biblia hutaja tabia fulani zisizofaa tunazohitaji kuacha. (Methali 6:16-19) Pili, Maandiko hutuhimiza tuonyeshe sifa zinazofaa ambazo hutokana na roho takatifu ya Mungu. Hizo zinatia ndani “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Wagalatia 5:22, 23.

Kuyaelewa matakwa ya Mungu kwa undani kulimsaidia Adrian ajichunguze na kutambua sifa alizohitaji kusitawisha na tabia alizopaswa kuacha. (Yakobo 1:22-25) Lakini huo ulikuwa mwanzo tu. Zaidi ya ujuzi, Adrian alihitaji kuchochewa na kitu fulani ili afanye mabadiliko.

Adrian alijifunza kwamba utu mpya wenye kupendeza hufanyizwa “kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.” (Wakolosai 3:10) Baadaye alitambua kwamba utu wa Mkristo unapaswa kufanana na utu wa Mungu. (Waefeso 5:1) Kupitia funzo la Biblia, Adrian alijifunza jinsi Yehova anavyoshughulika na wanadamu na kutambua sifa nzuri za Mungu kama vile upendo, fadhili, wema, rehema, na uadilifu. Ujuzi huo ulimchochea Adrian kumpenda Yehova na kujitahidi kuwa mtu anayekubaliwa naye.—Mathayo 22:37.

Mwishowe, Adrian aliweza kuizuia hasira yake kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Sasa yeye na mke wake wanajitahidi sana kuwasaidia wengine wabadili maisha yao kupitia ujuzi wa Biblia. “Tofauti na wengi wa marafiki wangu wa zamani ambao sasa wamekufa, mimi niko hai na ninafurahia maisha pamoja na familia yangu,” asema Adrian. Maisha yake yanathibitisha kwamba Biblia ina nguvu za kuboresha maisha.

[Blabu katika ukurasa wa 25]

“Hasira na jeuri yote haikuwa imetimiza kitu”

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

Kanuni za Biblia Zinazofanya Kazi

Zifuatazo ni baadhi ya kanuni za Biblia ambazo zimewasaidia watu wengi wenye hasira na jeuri kuwa wenye kufanya amani:

“Iweni wenye kufanya amani na watu wote. Msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu.” (Waroma 12:18, 19) Acheni Mungu aamue atalipiza kisasi kwa nani na wakati gani. Anaweza kufanya hivyo kwa kuwa anajua mambo yote, na adhabu yoyote anayotoa itaonyesha hukumu yake kamilifu.

“Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Waefeso 4:26, 27) Mtu anaweza kuwa na sababu nzuri ya kukasirika pindi fulani. Akikasirika, hapaswi kubaki “katika hali ya kuchokozeka.” Kwa nini? Kwa sababu kufanya hivyo kunaweza kumchochea afanye jambo fulani ovu, na hivyo ‘kumpa Ibilisi nafasi,’ jambo linaloweza kufanya tukose kibali cha Yehova Mungu.

“Acha hasira na uache ghadhabu; Usijionyeshe umewaka hasira ili tu kufanya uovu.” (Zaburi 37:8) Hisia zisizozuiwa humfanya mtu atende bila kujizuia. Mtu anaposhindwa kuzuia hasira, anaweza kusema au kufanya mambo yatakayowaumiza wengine.