Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’

‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’

‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’

“Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.”—2 TIMOTHEO 2:15.

1, 2. (a) Kwa nini wafanyakazi huhitaji vifaa? (b) Wakristo wanashiriki kazi gani, nao huonyeshaje kwamba wanatafuta kwanza Ufalme?

WAFANYAKAZI wanahitaji vifaa ili viwasaidie kufanya kazi yao. Lakini haitoshi tu kuwa na kifaa chochote. Mfanyakazi anahitaji kifaa kinachofaa, na anapaswa kukitumia kwa njia inayofaa. Kwa mfano, ikiwa unajenga kibanda na unataka kuunganisha mbao mbili, hungehitaji tu nyundo na misumari. Ungehitaji kujua jinsi ya kupigilia msumari kwenye mbao bila kuupinda. Ni jambo gumu na hata lenye kukatisha tamaa kujaribu kuupigilia msumari kwenye mbao ikiwa hujui jinsi ya kutumia nyundo. Lakini vifaa vinapotumiwa sawasawa vinatusaidia kutimiza kazi kwa njia yenye kuridhisha.

2 Tukiwa Wakristo tuna kazi muhimu sana ya kufanya. Yesu Kristo aliwahimiza wafuasi wake ‘watafute kwanza ufalme.’ (Mathayo 6:33) Tunawezaje kufanya hivyo? Njia moja ni kuwa wenye bidii katika kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Njia nyingine ni kutegemea kabisa Neno la Mungu katika huduma yetu. Nayo njia ya tatu ni kuwa na mwenendo mzuri. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 8:25; 1 Petro 2:12) Ili tuwe na matokeo na kufurahia kazi hiyo ya Kikristo, tunahitaji vifaa vinavyofaa na kujua jinsi ya kuvitumia sawasawa. Kuhusiana na kazi hiyo, mtume Paulo aliweka kielelezo bora akiwa mfanyakazi Mkristo, naye aliwatia moyo waamini wenzake wamwige. (1 Wakorintho 11:1; 15:10) Hivyo basi, tunaweza kujifunza nini kutoka kwa mfanyakazi mwenzetu, Paulo?

Paulo, Mtangazaji wa Ufalme Mwenye Bidii

3. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mtume Paulo alikuwa mfanyakazi wa Ufalme mwenye bidii?

3 Paulo alikuwa mfanyakazi wa aina gani? Bila shaka, Paulo alikuwa mwenye bidii naye alijikakamua kabisa kueneza habari njema katika eneo kubwa la Mediterania. Akieleza sababu iliyofanya awe na shauku katika kazi ya kutangaza Ufalme, mtume huyo asiyechoka alisema hivi: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!” (1 Wakorintho 9:16) Je, Paulo alitaka tu kuokoa uhai wake? La. Yeye hakuwa mwenye ubinafsi. Badala yake, alitaka wengine pia wanufaike na habari njema. Aliandika hivi: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.”—1 Wakorintho 9:23.

4. Wafanyakazi Wakristo huthamini zaidi kifaa gani?

4 Mtume Paulo alikuwa mfanyakazi mwenye kiasi ambaye alitambua kwamba hangeweza kutegemea ustadi wake tu. Kama vile seremala huhitaji nyundo, Paulo alihitaji kifaa kinachofaa ili kukazia kweli ya Mungu katika mioyo ya wasikilizaji wake. Alitumia kifaa gani hasa? Alitumia Neno la Mungu, Maandiko Matakatifu. Vivyo hivyo, Biblia nzima ndicho kifaa kikuu tunachotumia kutusaidia kufanya wanafunzi.

5. Ili tuwe wahudumu wenye matokeo, tunahitaji kufanya nini zaidi ya kunukuu tu maandiko?

5 Paulo alijua kwamba kutumia sawasawa Neno la Mungu kulihusisha mengi zaidi ya kulinukuu tu. Alitumia “ushawishi.” (Matendo 28:23) Jinsi gani? Paulo alitumia kwa mafanikio Neno la Mungu lililoandikwa ili kuwasadikisha wengi wakubali kweli ya Ufalme. Alijadiliana nao. Kwa miezi mitatu, Paulo ‘alitoa hotuba na kutumia ushawishi kuhusu ufalme wa Mungu’ katika sinagogi moja huko Efeso. Baadhi ya watu walisikiliza ingawa ‘wengine waliendelea kujifanya wenyewe wagumu na kutoamini.’ Kwa sababu ya huduma ya Paulo huko Efeso ‘neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi.’—Matendo 19:8, 9, 20.

6, 7. Paulo aliitukuzaje huduma yake, nasi tunawezaje kufanya hivyo?

6 Paulo alikuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii naye ‘aliitukuza huduma yake.’ (Waroma 11:13) Jinsi gani? Hakutaka kujitukuza wala hakuona aibu kujulikana hadharani kuwa mmoja wa wafanyakazi wenzi wa Mungu. Badala yake, aliiona huduma yake kuwa pendeleo lenye kuheshimika sana. Paulo alitumia Neno la Mungu kwa ustadi na kwa matokeo. Utendaji wake wenye matokeo uliwatia wengine moyo na kuwachochea watimize huduma yao kikamili zaidi. Katika njia hiyo pia, huduma yake ilitukuzwa.

7 Kama Paulo, tunaweza kutukuza kazi yetu tukiwa wahudumu kwa kutumia Neno la Mungu mara nyingi na kwa matokeo. Katika sehemu zote za huduma yetu, lengo letu linapaswa kuwa kuzungumzia jambo fulani katika Maandiko pamoja na watu wengi iwezekanavyo. Tunawezaje kufanya hivyo kwa ushawishi? Fikiria njia tatu muhimu (1) Elekeza fikira za wengine kwenye Neno la Mungu katika njia inayofanya liheshimiwe. (2) Eleza kwa busara yale ambayo Biblia husema kisha uonyeshe jinsi yanavyotumika. (3) Tumia Maandiko kueleza mambo katika njia yenye kusadikisha.

8. Leo tuna vifaa gani vya kuhubiri Ufalme, nawe umevitumiaje?

8 Leo watangazaji wa Ufalme wana vifaa ambavyo Paulo hakuwa navyo wakati wa huduma yake. Vifaa hivyo vinatia ndani, vitabu, magazeti, broshua, vikaratasi vya ukaribishaji, trakti, kaseti, na video. Katika karne iliyopita, kadi za kutoa ushahidi, santuri, magari yenye vikuza-sauti, na matangazo ya redio yalitumiwa. Bila shaka, kifaa chetu bora zaidi ni Biblia, nasi tunapaswa kutumia kifaa hicho muhimu kwa njia nzuri na inayofaa.

Lazima Huduma Yetu Itegemee Neno la Mungu

9, 10. Tunaweza kujifunza nini kutokana na shauri la Paulo kwa Timotheo kuhusiana na kulitumia Neno la Mungu?

9 Tunawezaje kutumia Neno la Mungu kwa matokeo? Kwa kufuata maneno haya ya Paulo kwa mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.” (2 Timotheo 2:15) ‘Kulitumia sawasawa neno la kweli’ kunahusisha nini?

10 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kutumia sawasawa’ kihalisi linamaanisha “kukata kwa kunyooka” au “kupasua njia iliyonyooka.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno hilo limetumiwa tu katika himizo la Paulo kwa Timotheo. Neno hilohilo linaweza kutumiwa kufafanua jinsi ya kukata mtaro ulionyooka kutoka upande mmoja wa shamba hadi mwingine. Bila shaka, mkulima mwenye uzoefu angeona aibu kama angekata mtaro uliojipinda. Ili Timotheo awe “mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu,” alikumbushwa kwamba hangepaswa kukengeuka kutoka kwenye mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu. Timotheo hakupaswa kuruhusu maoni yake ya kibinafsi yaathiri mafundisho yake. Mahubiri na mafundisho yake yalipaswa kutegemea kabisa Maandiko. (2 Timotheo 4:2-4) Katika njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu wangesaidiwa kuona mambo jinsi Yehova anavyoyaona, badala ya kufuata falsafa za kilimwengu. (Wakolosai 2:4, 8) Ndivyo ilivyo leo.

Lazima Tuwe na Mwenendo Mzuri

11, 12. Mwenendo wetu unahusianaje na kulitumia sawasawa Neno la Mungu?

11 Tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kulitumia sawasawa Neno la Mungu kwa kutangaza kweli zake. Lazima mwenendo wetu upatane na Neno hilo. “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu,” kwa hiyo hatupaswi kuwa wafanyakazi wanafiki. (1 Wakorintho 3:9) Neno la Mungu linasema: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi? Wewe, unayechukizwa na sanamu, je, wewe huiba katika mahekalu?” (Waroma 2:21, 22) Kwa hiyo, tukiwa wafanyakazi wa Mungu leo, njia moja ambayo tunaweza kulitumia Neno la Mungu sawasawa ni kwa kufuata himizo hili: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

12 Tunaweza kutarajia matokeo gani tunapolitumia sawasawa Neno la Mungu? Fikiria uvutano wa Neno la Mungu lililoandikwa juu ya maisha ya watu wenye mioyo minyoofu.

Neno la Mungu Lina Nguvu za Kubadili Watu

13. Mtu anaweza kufanya mabadiliko gani anapotumia Neno la Mungu?

13 Watu wanapokubali kwamba Neno la Mungu linategemeka, ujumbe wake unakuwa na uvutano wenye nguvu ambao huwasaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani mwao. Paulo alikuwa ameona neno la Mungu likitenda kazi na alikuwa ameshuhudia matokeo yake mazuri juu ya wale ambao waligeuka na kuwa Wakristo katika Thesalonike la kale. Kwa hiyo, aliwaambia: “Sisi tunamshukuru Mungu pia bila kuacha, kwa sababu mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini.” (1 Wathesalonike 2:13) Wakristo hao na pia wafuasi wote wa kweli wa Kristo, wanajua kwamba akili ndogo ya mwanadamu haiwezi kulinganishwa na hekima ya juu ya Mungu. (Isaya 55:9) Wathesalonike ‘walilipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu,’ wakawa vielelezo kwa waamini wengine.—1 Wathesalonike 1:5-7.

14, 15. Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu kadiri gani, na kwa nini?

14 Neno la Mungu lina nguvu kama Yehova, aliye Chanzo chake. Linatoka kwa “Mungu aliye hai,” ambaye kwa neno lake “mbingu zilifanywa,” na sikuzote neno hilo ‘hufanikiwa katika yale ambayo limetumwa.’ (Waebrania 3:12; Zaburi 33:6; Isaya 55:11) Msomi mmoja wa Biblia alisema: “Mungu hajitengi na Neno lake. Halikani kana kwamba halihusiani naye. . . . Kwa hiyo, sikuzote li hai, na kamwe halikosi kuwa na matokeo linapotamkwa; kwa kuwa linatuunganisha na Mungu aliye hai.”

15 Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu kadiri gani? Una nguvu nyingi sana. Kwa kufaa, Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12.

16. Neno la Mungu linawezaje kumbadili mtu kikamili?

16 Ujumbe wa Neno la Mungu lililoandikwa ni ‘wenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili.’ Kwa hiyo, una nguvu nyingi sana zinazopenya zaidi kuliko kifaa chochote cha mwanadamu. Neno la Mungu huchoma sehemu za ndani kabisa za mtu nalo linaweza kumbadili kindani, kuwa na uvutano kuhusu jinsi anavyofikiri na mambo anayopenda, na kumfanya awe mfanyakazi anayemwogopa Mungu na mwenye kukubalika. Neno hilo lina nguvu kama nini!

17. Eleza jinsi nguvu za Neno la Mungu zinavyobadili watu.

17 Neno la Mungu hufunua jinsi mtu alivyo kindani kinyume na anavyofikiri alivyo au jinsi anavyotaka wengine wamwone. (1 Samweli 16:7) Wakati mwingine, hata mtu mwovu anaweza kuficha jinsi alivyo kindani kwa kujifanya kuwa mwenye fadhili au mwenye kumcha Mungu. Waovu hutenda kwa unafiki wakiwa na nia mbaya. Watu wenye kiburi hujifanya kuwa wanyenyekevu huku wakitamani kusifiwa na watu. Hata hivyo, kwa kufunua waziwazi yaliyo moyoni, Neno la Mungu linaweza kumchochea kwa nguvu mtu mnyenyekevu avue utu wa kale na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Waefeso 4:22-24) Mafundisho ya Neno la Mungu yanaweza pia kumbadili mtu mwenye haya akawa Shahidi wa Yehova mwenye ujasiri na mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii.—Yeremia 1:6-9.

18, 19. Ukitumia habari iliyo kwenye mafungu haya au jambo ulilojionea katika utumishi wa shambani, eleza jinsi kweli ya Biblia inavyoweza kubadili mtazamo wa mtu.

18 Nguvu za Neno la Mungu za kubadili watu zina matokeo mazuri juu ya watu kila mahali. Kwa mfano, watangazaji wa Ufalme kutoka Phnom Penh, Kambodia, walihubiri mkoa wa Kompong Cham mara mbili kwa mwezi. Baada ya kusikia makasisi wengine wakiongea vibaya kuhusu Mashahidi wa Yehova, kasisi mmoja mwanamke ambaye ni mwenyeji, alipanga kukutana na Mashahidi hao wakati ambapo wangetembelea tena mkoa huo. Aliwarushia maswali mengi kuhusu kusherehekea sikukuu naye alisikiliza kwa makini walipojadiliana naye wakitumia Maandiko. Kisha akasema: “Sasa ninajua yale ambayo makasisi wenzangu walisema kuwahusu si ya kweli! Walidai kwamba hamtumii Biblia, lakini ninyi mmeitumia asubuhi yote!”

19 Mwanamke huyo aliendelea kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na Mashahidi na hakuruhusu vitisho vya kuachishwa ukasisi vimzuie. Alimweleza rafiki yake kuhusu mazungumzo hayo ya Biblia, naye pia akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Rafiki huyo alifurahia sana mambo aliyokuwa akijifunza hivi kwamba kwenye mojawapo ya ibada za kanisa analohudhuria, alichochewa kusema, “Njooni, mjifunze Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova!” Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo aliyekuwa kasisi, na pia wengineo walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

20. Kisa cha mwanamke fulani anayeishi nchini Ghana kinaonyeshaje nguvu za Neno la Mungu?

20 Kisa cha Paulina, mwanamke anayeishi nchini Ghana, kinaonyesha pia jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu. Mtangazaji mmoja wa Ufalme wa wakati wote alijifunza Biblia pamoja naye akitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. * Paulina alikuwa katika ndoa ya wake wengi naye aliona uhitaji wa kufanya mabadiliko, lakini mume wake na watu wake wote wa ukoo wakampinga vikali. Babu yake, ambaye ni jaji wa mahakama kuu na mzee wa kanisa, alijaribu kumzuia kwa kutumia vibaya andiko la Mathayo 19:4-6. Jaji huyo alizungumza kwa mamlaka, lakini Paulina akatambua mara moja kwamba hivyo ndivyo Shetani alivyopotosha Maandiko alipomjaribu Yesu Kristo. (Mathayo 4:5-7) Alikumbuka jinsi Yesu alivyozungumza waziwazi kuhusu ndoa, aliposema kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa mwanamume na mwanamke, si mwanamume na wanawake, na kwamba hao wawili, wala na si watatu wangekuwa mwili mmoja. Alishikilia uamuzi wake na mwishowe, kulingana na desturi za kwao, akapewa talaka kutokana na ndoa hiyo ya wake wengi. Muda mfupi baadaye, alikuwa mtangazaji wa Ufalme aliyebatizwa mwenye furaha.

Endelea Kulitumia Sawasawa Neno la Mungu

21, 22. (a) Tunataka kuazimia kufanya nini tukiwa watangazaji wa Ufalme? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

21 Kwa kweli, Neno la Mungu lililoandikwa ni kifaa chenye nguvu tunachoweza kutumia kuwasaidia wengine wafanye mabadiliko maishani mwao ili wamkaribie Yehova. (Yakobo 4:8) Kama vile wafanyakazi stadi hutumia vifaa ili kupata matokeo mazuri, na tuazimie kujitahidi kutumia kwa ustadi Neno la Mungu, Biblia, katika kazi yetu tuliyopewa na Mungu tukiwa watangazaji wa Ufalme.

22 Tunawezaje kutumia Maandiko kwa njia yenye matokeo zaidi katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi? Njia moja ni kusitawisha uwezo mbalimbali tukiwa walimu wenye kusadikisha. Tafadhali kazia fikira makala inayofuata, kwa kuwa inadokeza njia mbalimbali za kufundisha na kuwasaidia wengine waukubali ujumbe wa Ufalme.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Watangazaji wa Ufalme wana vifaa gani?

• Ni katika njia gani Paulo alikuwa kielelezo akiwa mfanyakazi wa Ufalme?

• Ni nini kinachohusika katika kulitumia sawasawa Neno la Mungu?

• Neno la Yehova lililoandikwa lina nguvu kadiri gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Baadhi ya vifaa ambavyo Wakristo hutumia katika kazi ya kutangaza Ufalme