Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunatarajia Ulimwengu Usio na Uhalifu

Tunatarajia Ulimwengu Usio na Uhalifu

Tunatarajia Ulimwengu Usio na Uhalifu

WAZIA, ikiwa unaweza, ulimwengu usio na wahalifu! Hakungekuwa na uhitaji wa polisi, magereza, au mifumo ya mahakama yenye gharama kubwa na yenye kutatanisha. Ungekuwa ulimwengu ambapo kila mtu angeheshimu uhai na mali ya wengine. Je, mambo hayo yanasikika kuwa ndoto tu? Unaweza kufikiri hivyo, lakini hivyo ndivyo Biblia inavyoahidi kwamba kutakuwa na mabadiliko mazuri sana. Kwa nini usichunguze yale ambayo Maandiko hutabiri kuhusu uhalifu na maovu mengine duniani?

Katika kitabu cha Zaburi tunasoma: “Usijionyeshe umewaka hasira kwa sababu ya watenda-maovu. Usiwaonee wivu wale wanaofanya mambo yasiyo ya uadilifu. Kwa maana watakauka haraka kama majani, nao watafifia kama majani mapya ya kijani kibichi. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:1, 2, 11) Kwa kweli, hakuna mtu anayeweza kumzuia Mungu asitimize ahadi hiyo na ahadi zake nyingine zenye kutia moyo.

Mungu ataleta baraka hizo kupitia Ufalme wake. Katika Sala ya Bwana, Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake wasali Ufalme huo uje, na mapenzi ya Mungu yafanywe “duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Hivi karibuni, chini ya Ufalme huo, hakuna mtu duniani ambaye atafanya uhalifu kwa sababu ya umaskini, uonevu, au ubinafsi. Badala yake, Neno la Mungu linasema: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Naam, sikuzote Yehova Mungu atawaandalia kwa wingi vitu vizuri watu wote watakaoishi duniani. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba wanadamu watachochewa na upendo kwa Mungu na jirani, na uhalifu hautakuwapo tena ulimwenguni.