Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso

Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso

Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso

TANGU zamani, watu wengi wameamini kwamba mwishowe wataondoka duniani na kwenda mbinguni. Wengine wamehisi kwamba Muumba wetu hakukusudia kamwe dunia iwe makao yetu ya kudumu. Nao wale wanaojinyima raha za mwili kwa sababu ya imani, wana maoni yanayopita mipaka. Wengi wao wanaamini kwamba dunia na vitu vyote vilivyomo ni viovu, na humzuia mtu asikamilike kiroho na kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu.

Watu wenye maoni yaliyotajwa hapo juu, ama hawakujua yale Mungu alisema kuhusu paradiso duniani au waliamua kuyapuuza. Kwa kweli, leo wengi hawataki kuchunguza yale ambayo Mungu aliwaongoza watu kwa roho yake waandike kuhusu paradiso katika Neno lake Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Lakini ni jambo la hekima kuamini Neno la Mungu badala ya maoni ya wanadamu. (Waroma 3:4) Bila shaka, ni muhimu kufanya hivyo kwa kuwa Biblia hutuonya kwamba kiumbe mwenye nguvu lakini asiyeonekana amewapofusha wanadamu kiroho na sasa ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’—Ufunuo 12:9; 2 Wakorintho 4:4.

Kwa Nini Kuna Maoni Yenye Kutatanisha?

Maoni yanayopingana kuhusu nafsi yamefanya watu watatanike kuhusu kusudi la Mungu kuelekea dunia. Wengi wanaamini kwamba tuna nafsi isiyoweza kufa, yaani, kitu fulani kilicho tofauti na mwili wa binadamu ambacho huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Wengine huamini kwamba nafsi ilikuweko kabla ya mwili wa binadamu kuumbwa. Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba Plato, mwanafalsafa Mgiriki, aliamini kwamba nafsi “imefungwa ndani ya mwili ili kuadhibiwa kwa dhambi ilizofanya ilipokuwa mbinguni.” Vivyo hivyo, Origen, mwanatheolojia wa karne ya tatu alisema kwamba “nafsi zilifanya dhambi [mbinguni] kabla ya kuungana na mwili” na hivyo “zikafungwa [ndani ya mwili duniani] ili kuadhibiwa kwa ajili ya dhambi zao.” Na wengi wanaamini kwamba dunia ni mahali pa kufanyiwa majaribio tu mtu anapokuwa safarini kwenda mbinguni.

Pia kuna maoni mbalimbali kuhusu jambo linaloipata nafsi mtu anapokufa. Kulingana na kitabu History of Western Philosophy, Wamisri walikuwa na maoni ya kwamba “nafsi za wafu zilishuka kwenda kuzimuni.” Baadaye wanafalsafa walidai kwamba nafsi za wafu hazikushuka katika giza la kuzimu bali zilipanda kwenye makao ya roho ya hali ya juu. Inasemekana kwamba Socrates, mwanafalsafa Mgiriki, aliamini kwamba mtu anapokufa nafsi “huhamia mahali pasipoonekana . . . na kuishi huko milele pamoja na miungu.”

Biblia Husema Nini?

Biblia ambayo ni Neno la Mungu lililoandikwa kwa roho yake, haisemi kamwe kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa. Jisomee andiko la Mwanzo 2:7. Linasema: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” Andiko hilo ni wazi kabisa. Mungu alipomuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, Hakuweka kitu fulani kisicho na mwili ndani yake. Hakufanya hivyo kwa kuwa Biblia inasema kwamba ‘mtu alipata kuwa nafsi hai.’ Mwanadamu huyo hakuwa na nafsi ndani yake bali yeye mwenyewe alikuwa nafsi.

Alipoumba dunia na wanadamu, Yehova hakukusudia mwanadamu afe. Kusudi la Mungu lilikuwa kwamba wanadamu waishi milele duniani katika hali za Kiparadiso. Adamu alikufa kwa sababu tu hakutii sheria ya Mungu. (Mwanzo 2:8, 15-17; 3:1-6; Isaya 45:18) Mtu wa kwanza alipokufa, je, alienda katika makao fulani ya roho? La! Adamu, ambaye alikuwa nafsi, alirudi katika mavumbi yasiyo na uhai ambayo kutoka kwayo aliumbwa.—Mwanzo 3:17-19.

Sote tumerithi dhambi na kifo kutoka kwa babu yetu Adamu. (Waroma 5:12) Kifo hicho kinamaanisha kuacha kuishi, kama vile Adamu. (Zaburi 146:3, 4) Kwa kweli, katika vitabu vyake 66, Biblia haihusianishi kamwe maneno “-sioweza kufa” au “-a milele” na neno “nafsi.” Badala yake, Maandiko yanasema wazi kwamba nafsi, ambayo ni mtu mwenyewe, inaweza kufa.—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4.

Je, kwa Kawaida Vitu vya Kimwili Ni Viovu?

Namna gani maoni ya kwamba vitu vya kimwili, kutia ndani dunia, ni viovu? Maoni hayo yalishikiliwa na wafuasi wa dini iliyoanzishwa huko Uajemi katika karne ya tatu W.K. na mtu aliyeitwa Mani. Kichapo The New Encyclopædia Britannica kinasema: ‘Dini hiyo ilianzishwa kwa sababu ya mateso ambayo kwa kawaida humpata mwanadamu.’ Mani aliamini kwamba kuwa mwanadamu ni “jambo lisilo la kawaida, lisilovumilika, na ovu kabisa.” Pia aliamini kwamba nafsi ingeepuka tu “mateso” hayo kwa kuacha mwili na dunia, na kwenda kuishi maisha ya kiroho katika makao ya roho.

Tofauti na maoni hayo, Biblia hutuambia kuwa Mungu aliona kwamba “kila kitu alichokuwa amefanya” alipoumba dunia na wanadamu, kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Wakati huo, hapakuwa kizuizi kati ya wanadamu na Mungu. Adamu na Hawa walifurahia uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, kama vile mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo alivyofurahia uhusiano wa karibu sana pamoja na Baba yake wa mbinguni.—Mathayo 3:17.

Kama wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, hawangefanya dhambi, wangekuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu milele katika dunia paradiso. Walianza maisha katika Paradiso, kwa kuwa Maandiko yanatuambia: “Yehova Mungu a[li]panda bustani katika Edeni, kuelekea mashariki, na hapo akamweka mtu ambaye alikuwa amemfanya.” (Mwanzo 2:8) Hawa aliumbwa katika bustani hiyo ya kiparadiso. Kama Adamu na Hawa hawangefanya dhambi, wao pamoja na wazao wao wakamilifu wangefanya kazi pamoja kwa furaha hadi dunia yote iwe paradiso. (Mwanzo 2:21; 3:23, 24) Wanadamu wangeishi milele katika Paradiso hiyo ya kidunia.

Kwa Nini Wengine Huenda Mbinguni?

Huenda ukasema, ‘lakini Biblia inasema kwamba watu wataenda mbinguni, sivyo?’ Ndiyo. Baada ya Adamu kufanya dhambi, Yehova alikusudia kuanzisha Ufalme wa kimbingu ambao baadhi ya wazao wa Adamu ‘wangetawala wakiwa wafalme juu ya dunia’ pamoja na Yesu Kristo. (Ufunuo 5:10; Waroma 8:17) Wangefufuliwa na kupewa uhai usioweza kufa mbinguni. Hesabu yao kamili ni watu 144,000, na wa kwanza kati yao walikuwa wanafunzi waaminifu wa Yesu katika karne ya kwanza.—Luka 12:32; 1 Wakorintho 15:42-44; Ufunuo 14:1-5.

Hata hivyo, mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu waaminifu waondoke duniani na kwenda mbinguni. Hata Yesu alipokuwa duniani, alisema: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu.” (Yohana 3:13) Kupitia “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo, Mungu aliandaa fidia ili kuwezesha wale wanaoonyesha imani katika dhabihu ya Yesu wapate uzima wa milele. (Waroma 5:8) Lakini mamilioni ya wanadamu hao wataishi wapi milele?

Kusudi la Mungu la Awali Litatimizwa

Ingawa Mungu alikusudia kuchukua baadhi ya wanadamu wakatawale pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wa kimbingu, hilo halimaanishi kwamba watu wote wazuri wanaenda mbinguni. Yehova aliumba dunia ili iwe makao ya kiparadiso ya wanadamu. Hivi karibuni, Mungu atatimiza kusudi hilo la awali.—Mathayo 6:9, 10.

Chini ya utawala wa Yesu Kristo na watawala wenzake wa kimbingu, kutakuwa na amani na furaha duniani pote. (Zaburi 37:9-11) Wale walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa na kufurahia afya kamilifu. (Matendo 24:15) Kwa kuwa waaminifu kwa Mungu, wanadamu watiifu watapewa kile ambacho wazazi wetu wa kwanza walipoteza, yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani wakiwa wanadamu wakamilifu.—Ufunuo 21:3, 4.

Yehova Mungu hakosi kamwe kutimiza yale anayokusudia kufanya. Alisema hivi kupitia nabii wake Isaya: “Kama vile mvua inayonyesha hushuka, na theluji, kutoka mbinguni nayo hairudi mahali pale, mpaka kwa kweli iwe imeinywesha dunia na kuifanya izae na kuchipuka, na mbegu kweli iwe imepewa mpandaji na mkate kupewa anayekula, ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:10, 11.

Kitabu cha Biblia cha Isaya kinaonyesha kimbele jinsi maisha yatakavyokuwa katika dunia Paradiso. Hakuna mkaaji wa Paradiso atakayesema “Mimi ni mgonjwa.” (Isaya 33:24) Wanyama hawatawadhuru wanadamu. (Isaya 11:6-9) Watu watajenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake nao watapanda mazao na kula mpaka kuridhika. (Isaya 65:21-25) Isitoshe, Mungu “atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.

Hivi karibuni, wanadamu watiifu wataishi chini ya hali hizo bora sana. ‘Watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’ (Waroma 8:21) Itafurahisha kama nini kuishi milele katika dunia Paradiso iliyoahidiwa! (Luka 23:43) Unaweza kuishi katika Paradiso hiyo ikiwa unatenda sasa kupatana na ujuzi sahihi wa Maandiko na unaonyesha imani katika Yehova Mungu na Yesu Kristo. Na unaweza kuwa na uhakika kwamba ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kutakuwa na dunia paradiso.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Adamu na Hawa walikusudiwa kuishi milele katika dunia paradiso

[Picha katika ukurasa wa 7]

Katika dunia Paradiso . . .

watajenga nyumba

watapanda mizabibu

watabarikiwa na Yehova

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA