Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme

Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme

Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme

“Agripa akamwambia Paulo: ‘Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.’”—MATENDO 26:28.

1, 2. Kwa nini mtume Paulo alisimama mbele ya Gavana Festo na Mfalme Agripa wa Pili?

KATIKA mwaka wa 58 W.K., Mfalme Herode Agripa wa Pili na dada yake Bernike walimtembelea Gavana Mroma, Porkio Festo, huko Kaisaria. Walikuwa wamealikwa na Gavana huyo, nao ‘wakaingia kwa fahari nyingi katika chumba cha baraza pamoja na viongozi wa kijeshi na vilevile wanaume waheshimiwa katika jiji.’ Ndipo Festo akaamuru mtume Mkristo Paulo aletwe mbele zao. Kwa nini mfuasi huyo wa Yesu Kristo alisimama mbele ya kiti cha hukumu cha Gavana Festo?—Matendo 25:13-23.

2 Mambo ambayo Festo aliwaeleza wageni wake yanajibu swali hilo. Alisema: “Mfalme Agripa na ninyi wanaume wote mliopo pamoja nasi, ninyi mnaona mtu huyu ambaye kuhusu yeye umati wote wa Wayahudi ukiwa pamoja umepeleka ombi kwangu katika Yerusalemu na hapa pia, ukipaaza sauti kwamba hapaswi kuishi tena kamwe. Lakini mimi nikaona hakuwa amefanya jambo lolote linalostahili kifo. Kwa hiyo mwanamume huyu mwenyewe alipokata rufani kwa Mheshimiwa, niliamua kumpeleka. Lakini kuhusu yeye sina jambo hakika la kumwandikia Bwana wangu. Kwa hiyo nikamleta mbele yenu, na hasa mbele yako wewe, Mfalme Agripa, ili, baada ya kumhoji kihukumu, nipate jambo fulani la kuandika. Kwa maana linaonekana kuwa jambo lisilo la akili kwangu kumpeleka mfungwa bila kuonyesha mashtaka juu yake.”—Matendo 25:24-27.

3. Kwa nini viongozi wa kidini walimshtaki Paulo?

3 Maneno ya Festo yanaonyesha kwamba Paulo alikuwa ameshtakiwa kwa uwongo kwamba alikuwa mchochezi, kosa ambalo lilistahili hukumu ya kifo. (Matendo 25:11) Lakini Paulo hakuwa na hatia. Mashtaka hayo yalitokana na wivu wa viongozi wa kidini wa Yerusalemu. Walipinga kazi ya Paulo ya kutangaza Ufalme nao walichukizwa sana kuona kwamba aliwasaidia wengine wawe wafuasi wa Yesu Kristo. Chini ya ulinzi mkali, Paulo alisafirishwa kutoka Yerusalemu hadi jiji la bandarini la Kaisaria, ambako alikata rufani kwa Kaisari. Kutoka hapo angepelekwa Roma.

4. Mfalme Agripa alisema maneno gani yenye kushangaza?

4 Wazia Paulo akiwa katika jumba la gavana mbele ya watu ambao walitia ndani mtawala wa eneo muhimu la Miliki ya Roma. Mfalme Agripa anamgeukia Paulo na kusema: “Unaruhusiwa kujitetea.” Paulo anapozungumza, jambo la kustaajabisha linatukia. Mfalme anaanza kuguswa moyo na mambo ambayo Paulo anasema. Naam, Mfalme Agripa anasema: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.”—Matendo 26:1-28.

5. Kwa nini maneno ya Paulo kwa Agripa yalikuwa yenye matokeo sana?

5 Hebu wazia! Kwa sababu Paulo alijitetea kwa njia ya ustadi, mtawala huyo aliguswa moyo na nguvu zenye kupenya za Neno la Mungu. (Waebrania 4:12) Kwa nini njia ya Paulo ya kujitetea ilikuwa yenye matokeo sana? Nasi tunaweza kujifunza jambo gani kutoka kwa Paulo ambalo linaweza kutusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi? Tunapochanganua njia yake ya kujitetea, mambo mawili makuu yanadhihirika: (1) Paulo alikuwa mwenye ushawishi katika mazungumzo yake. (2) Alitumia ujuzi wake wa Neno la Mungu kwa ustadi, kama vile msanii hutumia kifaa fulani kwa njia yenye matokeo.

Tumia Ustadi wa Kushawishi

6, 7. (a) Neno “ushawishi” linamaanisha nini kama linavyotumiwa katika Biblia? (b) Ushawishi ni muhimu kadiri gani katika kuwasaidia wengine wakubali mafundisho ya Biblia?

6 Katika kitabu cha Matendo, maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa ushawishi yametumiwa mara nyingi kumhusu Paulo. Kutumia ushawishi kunahusianaje na kazi yetu ya kufanya wanafunzi?

7 Katika lugha ya awali ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno “shawishi” linamaanisha “kusadikisha” au kumfanya mtu “abadili maoni yake kwa kujadiliana naye au kwa kuchunguza pamoja naye kanuni za maadili,” chasema kichapo Expository Dictionary of New Testament Words cha Vine. Tunaelewa zaidi maana ya neno hilo tunapochunguza maana ya msingi. Maana hiyo ya msingi inatoa wazo la kumtumaini mtu. Kwa hiyo ukimshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, umemsadikisha akutumaini, na hivyo aamini kwamba fundisho hilo ni la kweli. Bila shaka, haitoshi tu kumweleza mtu yale ambayo Biblia husema ili aiamini na kutenda kupatana nayo. Lazima msikilizaji wako asadiki kwamba yale unayosema ni ya kweli, hata kama yeye ni mtoto, jirani, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako, au mtu wa ukoo.—2 Timotheo 3:14, 15.

8. Ni nini kinachohusika katika kumsadikisha mtu ukweli fulani wa Biblia?

8 Unawezaje kumsadikisha mtu kwamba yale unayosema kutoka katika Neno la Mungu ni kweli? Paulo alijitahidi kubadili maoni ya watu aliozungumza nao kwa kujadiliana nao kupatana na akili, kutoa hoja zinazofaa, na kuwasihi kwa bidii. * Kwa hiyo, badala tu ya kusema kwamba jambo fulani ni kweli, unahitaji kutoa uthibitisho wenye kuridhisha kuunga mkono maneno yako. Unawezaje kufanya hivyo? Hakikisha kwamba maneno yako yanategemea kabisa Neno la Mungu wala si maoni yako mwenyewe. Pia, toa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono maneno yako ya kutoka moyoni yanayotegemea Biblia. (Methali 16:23) Kwa mfano, ukisema kwamba wanadamu watiifu watafurahia maisha katika dunia paradiso, tumia Maandiko kama vile Luka 23:43 au Isaya 65:21-25 kuunga mkono maneno hayo. Unawezaje kutoa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono hoja yako ya Kimaandiko? Unaweza kutumia mifano inayotegemea mambo ambayo yamempata msikilizaji wako. Unaweza kumkumbusha mambo fulani madogo anayofurahia bila malipo yoyote, kama vile machweo ya jua yenye kupendeza, harufu nzuri ya ua, ladha nzuri ya tunda, au furaha unayopata kwa kumtazama ndege akilisha makinda yake. Msaidie aone kwamba mambo hayo yenye kufurahisha yanathibitisha kwamba Muumba wetu anataka tufurahie maisha duniani.—Mhubiri 3:11, 12.

9. Tunawezaje kuonyesha busara tunapohubiri?

9 Unapojaribu kumshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, jihadhari shauku yako isifanye uonekane kama unashikilia maoni yako tu, na hivyo kutofikia akili na moyo wa msikilizaji wako. Kitabu Shule ya Huduma kinatoa tahadhari hii: ‘Kwa kawaida ukifichua kwa dharau fundisho fulani la uwongo ambalo mtu anapenda sana, mtu huyo hatakubali kweli hata umsomee Maandiko mangapi. Kwa mfano, ukishutumu tu sherehe zinazopendwa kwamba ni za kipagani, huenda watu wasibadili maoni yao kuzihusu. Kwa kawaida unaweza kufanikiwa kwa kujadiliana nao.’ Kwa nini ujitahidi sana kuwa mwenye busara? Kitabu hicho kinasema: ‘Kujadiliana hufanya watu wachangie mazungumzo, huwasaidia kufikiria mambo hayo baadaye, na kuwafanya waweze kusikiliza wakati ujao. Kusababu kunaweza kushawishi sana.’—Wakolosai 4:6.

Ushawishi Unaochochea Moyo

10. Paulo alianzishaje mazungumzo yake ya kujitetea mbele ya Agripa?

10 Sasa na tuchunguze kwa makini maneno ambayo Paulo alitumia kujitetea katika Matendo sura ya 26. Ona jinsi alivyoanza mazungumzo yake. Katika utangulizi wake, Paulo alitafuta sababu nzuri ya kumpongeza Agripa, hata ingawa mfalme huyo alikuwa na uhusiano wenye aibu pamoja na dada yake Bernike. Paulo alisema: “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi, Mfalme Agripa, ninajihesabu mwenyewe kuwa mwenye furaha kwamba ninajitetea mbele yako leo, hasa kwa kuwa wewe una ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo ninakuomba unisikie kwa subira.”—Matendo 26:2, 3.

11. Maneno ya Paulo kwa Agripa yalionyeshaje heshima, nayo yalikuwa na manufaa gani?

11 Je, umeona kwamba Paulo alitambua cheo cha juu cha Agripa kwa kumwita Mfalme, jina lake la cheo? Kwa kufanya hivyo na pia kwa kuchagua maneno yake kwa hekima, Paulo alimwonyesha Agripa heshima. (1 Petro 2:17) Mtume huyo alikiri kwamba Agripa alijua desturi na sheria za raia zake Wayahudi ambazo zilikuwa ngumu kueleweka, na kusema kwamba alikuwa mwenye furaha kwa kuwa aliweza kujitetea mbele ya mtawala kama huyo mwenye ujuzi. Paulo, aliyekuwa Mkristo, hakutenda kana kwamba alikuwa mtu bora kuliko Agripa ambaye hakuwa Mkristo. (Wafilipi 2:3) Badala yake, Paulo alimwomba mfalme huyo amsikilize kwa subira. Hivyo, Paulo akatokeza hali ambayo yaelekea ingemfanya Agripa, na pia wasikilizaji wengine, wakubali mambo aliyotaka kusema. Alikuwa anaweka msingi wa kutegemeza hoja zake kwa kuzungumzia mambo ambayo wote walikubaliana.

12. Tunawezaje kuchochea mioyo ya wasikilizaji wetu tunapofanya kazi ya kutangaza Ufalme?

12 Acheni tuchochee mioyo ya wasikilizaji wetu tangu mwanzo hadi mwisho wa mazungumzo yetu kuhusu ujumbe wa Ufalme kama vile Paulo alivyofanya mbele ya Agripa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuonyesha tunamheshimu kikweli mtu tunayemhubiria na kwamba tunapendezwa kikweli na malezi na maoni yake.—1 Wakorintho 9:20-23.

Tumia Neno la Mungu kwa Ustadi

13. Unawezaje kuwachochea wasikilizaji wako kama Paulo?

13 Paulo alitamani kuwachochea wasikilizaji wake watende kupatana na habari njema. (1 Wathesalonike 1:5-7) Ili kutimiza hilo, aliuchochea moyo wao wa mfano ambao ni chanzo cha msukumo wa kutenda. Tunapochunguza zaidi namna Paulo alivyojitetea mbele ya Agripa, ona jinsi Paulo ‘alivyotumia neno la Mungu sawasawa’ kwa kurejelea mambo yaliyosemwa na Musa na manabii.—2 Timotheo 2:15.

14. Eleza jinsi Paulo alivyotumia ushawishi alipokuwa mbele ya Agripa.

14 Paulo alijua kwamba Agripa alikuwa Myahudi kwa jina tu. Alitaja ujuzi wa Agripa kuhusu Dini ya Kiyahudi na kusema kwamba mahubiri yake yalihusu hasa ‘kutosema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia’ kuhusu kifo na ufufuo wa Masihi. (Matendo 26:22, 23) Akizungumza na Agripa moja kwa moja, Paulo aliuliza: “Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii?” Agripa alitatanika. Kama angesema kwamba hakuwaamini manabii, sifa yake akiwa mwamini Myahudi ingeharibika. Na kama angekubaliana na hoja ya Paulo, angekuwa anakiri hadharani kwamba anakubaliana na maoni ya mtume huyo na hivyo kuitwa Mkristo, jambo ambalo lilikuwa hatari. Paulo alijibu swali lake mwenyewe kwa hekima, akisema: “Ninajua unawaamini.” Moyo wa Agripa ulimchochea kujibuje? Alijibu: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Matendo 26:27, 28) Ingawa Agripa hakupata kuwa Mkristo, ni wazi kwamba Paulo alimgusa moyo kwa kadiri fulani kwa ujumbe wake.—Waebrania 4:12.

15. Paulo aliwezaje kuanzisha kutaniko huko Thesalonike?

15 Je, umeona kwamba mazungumzo ya Paulo kuhusu habari njema yalihusisha kutangaza ujumbe na kushawishi? Kwa kuwa Paulo alitumia njia hiyo ‘alipolitumia neno la Mungu sawasawa,’ baadhi ya watu waliomsikiliza waliacha kuwa wasikilizaji tu na wakawa waamini. Hivyo ndivyo ilivyotukia huko Thesalonike ambako Paulo alitafuta katika sinagogi Wayahudi na watu wa mataifa waliomwogopa Mungu. Andiko la Matendo 17:2-4 linasema: “Kulingana na desturi ya Paulo akaingia ndani walimokuwa, na kwa sabato tatu akajadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu . . . Ikawa kwamba baadhi yao wakawa waamini.” Paulo alikuwa mwenye kushawishi. Alitoa hoja, akaeleza, na kuthibitisha kupitia Maandiko kwamba Yesu ndiye Masihi aliyekuwa ameahidiwa kwa muda mrefu. Ikawaje? Kutaniko la waamini lilianzishwa.

16. Unawezaje kupata furaha kubwa zaidi katika kuhubiri juu ya Ufalme?

16 Je, unaweza kuwa mwenye ustadi zaidi katika kushawishi unapofafanua Neno la Mungu? Ikiwa ndivyo, utapata uradhi na furaha zaidi katika kazi yako ya kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Wahubiri wa habari njema wamepata uradhi na furaha zaidi kwa kufuata madokezo ya kuitumia Biblia zaidi katika kazi ya kuhubiri.

17. Ili kuonyesha manufaa ya kutumia Biblia katika huduma, simulia jambo ulilojionea au uonyeshe umuhimu wa kufanya hivyo kama inavyoonyeshwa katika fungu hili.

17 Kwa mfano, mwangalizi mmoja asafiriye wa Mashahidi wa Yehova aliandika hivi: “Sasa ndugu na dada wengi hubeba Biblia mkononi wanapohubiri nyumba kwa nyumba. Kufanya hivyo kumewasaidia wahubiri kuwasomea andiko fulani baadhi ya watu wengi wanaokutana nao. Kumemsaidia mwenye nyumba na pia mhubiri kuihusianisha huduma yetu na Biblia, wala si magazeti na vitabu tu.” Bila shaka, kubeba Biblia mkononi tunapohubiri kunategemea mambo kadhaa, kutia ndani desturi za eneo tunalohubiri. Hata hivyo, tunahitaji kutamani kuwa na sifa ya kutumia Neno la Mungu kwa ustadi ili kushawishi wengine wakubali ujumbe wa Ufalme.

Uwe na Maoni ya Mungu Kuhusu Huduma

18, 19. (a) Mungu huionaje huduma yetu, na kwa nini tusitawishe maoni kama yake? (b) Ni nini kitakachotusaidia tufanikiwe kufanya ziara za kurudia? (Ona sanduku lenye kichwa “Jinsi ya Kufanikiwa Kufanya Ziara za Kurudia,” kwenye ukurasa wa 16.)

18 Njia nyingine ya kufikia mioyo ya wasikilizaji wetu inahusisha kuiona huduma jinsi Mungu anavyoiona na kuwa wenye subira. Mapenzi ya Mungu ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Je, sisi tuna tamaa kama hiyo? Yehova pia ni mwenye subira, na subira yake huwapatia wengi nafasi ya kufikia toba. (2 Petro 3:9) Kwa hiyo, tunapopata mtu anayetaka kusikiliza ujumbe wa Ufalme, huenda ikawa lazima kumrudia tena na tena ili kukuza upendezi huo. Inachukua muda na subira kungojea mbegu za kweli zikue. (1 Wakorintho 3:6) Sanduku lililo katika makala hii lenye kichwa, “Jinsi ya Kufanikiwa Kufanya Ziara za Kurudia” lina madokezo ya kukuza upendezi huo. Kumbuka kwamba maisha ya watu—matatizo na hali zao—hubadilika daima. Huenda ukahitaji kuwatembelea mara nyingi ili kuwapata nyumbani, lakini jitihada hizo zinafaa. Tunataka kuwapa nafasi ya kusikia ujumbe wa Mungu wa wokovu. Kwa hiyo, mwombe Yehova Mungu akupatie hekima ya kusitawisha ustadi wa ushawishi katika kazi yako ya kuwasaidia wengine waukubali ujumbe wa Ufalme.

19 Wafanyakazi Wakristo wanaweza kufanya jambo gani jingine wanapompata mtu anayetaka kusikia mengi zaidi kuhusu ujumbe wa Ufalme? Tutapata madokezo katika makala yetu inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa habari zaidi kuhusu ushawishi, ona somo la 48 na 49 katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini njia ya Paulo ya kujitetea mbele ya Mfalme Agripa ilikuwa yenye matokeo?

• Ujumbe wetu unawezaje kuuchochea moyo?

• Ni nini kitakachotusaidia kutumia Neno la Mungu kwa matokeo na kuufikia moyo?

• Tunawezaje kuiona huduma jinsi Mungu anavyoiona?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

Jinsi ya Kufanikiwa Kufanya Ziara za Kurudia

• Onyesha kwamba unapendezwa na watu kikweli.

• Chagua habari ya kuzungumzia yenye kuvutia katika Biblia.

• Weka msingi wa jambo mtakalozungumzia katika kila ziara inayofuata.

• Endelea kumfikiria mtu huyo baada ya kuondoka.

• Rudi haraka, labda baada ya siku moja au mbili, ili kufuatia upendezi.

• Kumbuka kwamba lengo lako ni kuanzisha funzo la Biblia la nyumbani.

• Sali ili Yehova akuze upendezi.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Paulo alitumia ushawishi alipokuwa mbele ya Gavana Festo na Mfalme Agripa