Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wakati wa kuzingirwa na kuharibiwa kwa Yerusalemu, Ezekieli alikuwa “bubu” katika njia gani?

Kwa msingi, katika njia ya kwamba hakuwa na la kuongezea kwenye ujumbe wa kinabii wa Yehova ambao tayari alikuwa ametangaza.

Nabii Ezekieli alianza utumishi wake akiwa mlinzi mwaminifu kwa wahamishwa Waisraeli kule Babiloni katika “mwaka wa tano wa uhamisho wa mfalme Yehoyakini,” yaani, katika mwaka wa 613 K.W.K. (Ezekieli 1:2, 3) Katika siku ya kumi, mwezi wa kumi, mwaka wa 609 K.W.K., alijulishwa kupitia roho ya Mungu kuhusu wakati ambapo Wababiloni wangeanza kuzingira Yerusalemu. (Ezekieli 24:1, 2) Matokeo ya kuzingirwa huko yangekuwa nini? Je, Yerusalemu na wakaaji wake wasio na imani wangeokoka? Akiwa mlinzi, Ezekieli alikuwa tayari ametangaza ujumbe hakika wa uharibifu kutoka kwa Yehova, na hapakuwa na uhitaji kwa Ezekieli kuongezea lolote, kana kwamba kuufanya ujumbe huo uwe wenye kusadikisha zaidi. Ezekieli alikuwa bubu kwa habari ya jambo lolote zaidi kuhusu kuzingirwa kwa Yerusalemu.—Ezekieli 24:25-27.

Miezi sita hivi baada ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., mtu fulani aliyekimbia alimletea Ezekieli huko Babiloni habari za kuharibiwa kwa jiji takatifu. Jioni iliyotangulia kufika kwa mtu huyo, Yehova ‘alikifungua kinywa cha Ezekieli naye hakuwa bubu tena.’ (Ezekieli 33:22) Huo ndio uliokuwa mwisho wa ububu wa Ezekieli.

Je, Ezekieli alikuwa bubu kihalisi wakati huo? Bila shaka sivyo, kwa sababu hata baada ya “ububu” huo, alitoa unabii ulioelekezwa hasa kwenye nchi jirani ambazo zilishangilia kuanguka kwa Yerusalemu. (Ezekieli, sura za 25-32) Mapema katika kazi ya Ezekieli akiwa nabii na mlinzi, Yehova alikuwa amemwambia: “Nitaufanya ulimi wako ushikamane na kaakaa la kinywa chako, nawe hakika utakuwa bubu, na kwao wewe hutakuwa mtu mwenye kutoa karipio, kwa sababu wao ni nyumba yenye kuasi. Nami ninaposema nawe, nitakifungua kinywa chako.” (Ezekieli 3:26, 27) Wakati ambapo Yehova hakuwa na ujumbe wowote kwa ajili ya Israeli, Ezekieli alipaswa kuwa bubu kuhusiana na taifa hilo. Ezekieli alipaswa kusema yale ambayo Yehova alimtaka aseme wakati ambapo Yehova alimtaka aseme. Ezekieli alikuwa bubu kuhusiana na kusema maneno yenye umuhimu wa kinabii kwa Waisraeli.

Jamii ya mlinzi ya siku hizi, yaani, Wakristo watiwa-mafuta, wamekuwa wakionya kuhusu kuharibiwa kwa Jumuiya ya Wakristo, inayofananishwa na Yerusalemu la zamani. Wakati “dhiki kuu” itakapoanza na kuharibu “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini za uwongo, jamii ya watiwa-mafuta ya Ezekieli hawatahitaji kusema lolote zaidi kuhusu kuangamizwa kwa Jumuiya ya Wakristo, ambayo ni sehemu kuu ya milki hiyo.—Mathayo 24:21; Ufunuo 17:1, 2, 5.

Naam, siku itafika ambapo mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao watakuwa bubu, bila lolote zaidi la kuwajulisha Jumuiya ya Wakristo. Itakuwa wakati ambapo “zile pembe kumi” na “yule mnyama-mwitu” watamharibu Babiloni Mkubwa na kumwacha uchi. (Ufunuo 17:16) Lakini hilo halimaanishi kwamba Wakristo watakuwa bubu kihalisi. Kama vile wanavyofanya sasa, wao watamsifu Yehova na kumtaja kila siku na “katika vizazi vyote vitakavyokuja.”—Zaburi 45:17; 145:2.