Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”

“Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”

“Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”

“Acheni amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu . . . Na mjionyeshe kuwa wenye shukrani.”—WAKOLOSAI 3:15.

1. Tunaona tofauti gani kati ya kutaniko la Kikristo na ulimwengu ulio chini ya utawala wa Shetani?

KATIKA makutaniko 94,600 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, kuna roho ya shukrani. Kila mkutano huanza na kumalizika kwa sala inayotia ndani maneno ya shukrani kwa Yehova. Mara nyingi sisi husikia maneno “asante,” “karibu,” au mengine yanayofanana na hayo yakitoka vinywani mwa vijana na wazee na vilevile Mashahidi wapya na wa zamani wanapoungana katika ibada na ushirika wenye furaha. (Zaburi 133:1) Ni tofauti kama nini na ubinafsi ambao umeenea kati ya wengi ‘wasiomjua Yehova na wale wasiotii habari njema’! (2 Wathesalonike 1:8) Tunaishi katika ulimwengu usio na shukrani. Si ajabu tunapokumbuka kwamba mungu wa ulimwengu huu ni Shetani Ibilisi, mchochezi mkuu wa ubinafsi, ambaye roho yake ya kiburi na uasi imeenea katika jamii ya wanadamu!—Yohana 8:44; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19.

2. Tunapaswa kutii onyo gani, na ni maswali gani tutakayochunguza?

2 Kwa kuwa tumezungukwa na ulimwengu wa Shetani, tunahitaji kuwa waangalifu ili tusiathiriwe na mitazamo yake. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo wa Efeso hivi: “Wakati fulani mlitembea . . . kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha katikati yao kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayopendwa na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu sawa na wale wengine.” (Waefeso 2:2, 3) Hivyo pia ndivyo wengi walivyo leo. Basi, tunaweza kudumishaje roho ya shukrani? Yehova hutoa msaada gani? Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tuna shukrani kwelikweli?

Sababu za Kuwa Wenye Shukrani

3. Tuna sababu gani ya kumshukuru Yehova?

3 Tunapaswa kutoa shukrani zetu kwa Yehova Mungu, Muumba na Mpaji-Uhai wetu, hasa tunapofikiria zawadi nyingi ambazo ametupa. (Yakobo 1:17) Tunamshukuru Yehova kila siku kwa kuwa tuko hai. (Zaburi 36:9) Kila mahali, tunaona ushuhuda mwingi wa kazi za Yehova, kama vile jua, mwezi, na nyota. Dunia yetu yenye madini mengi yanayotegemeza uhai, anga lenye mchanganyiko mzuri wa hewa muhimu, na mizunguko tata ya asili, yote hayo yanaonyesha deni letu kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. “Wewe mwenyewe umefanya mambo mengi, Ee Yehova Mungu wangu,” akaimba Mfalme Daudi, “naam, kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea; hakuna wa kulinganishwa nawe. Ikiwa ningetaka kueleza na kusema juu yake, zimekuwa nyingi sana kuliko vile ninavyoweza kusimulia.”—Zaburi 40:5.

4. Kwa nini tunapaswa kumshukuru Yehova kwa ajili ya ushirika wenye furaha tulio nao katika makutaniko yetu?

4 Ingawa hawako katika paradiso halisi, watumishi wa Yehova leo wanathamini kuishi katika paradiso ya kiroho. Katika Majumba yetu ya Ufalme na makusanyikoni, tunaona matunda ya roho ya Mungu yakifanya kazi kati ya waamini wenzetu. Wanapowahubiria watu ambao hawajui sana mambo ya dini, Mashahidi fulani hurejezea yale ambayo Paulo alizungumzia katika barua yake kwa Wagalatia. Kwanza, wao hukazia uangalifu kwenye “matendo ya mwili” na kuwauliza wasikilizaji yale ambayo wameona. (Wagalatia 5:19-23) Wengi hukubali haraka kwamba mambo hayo yameenea sana katika jamii ya wanadamu leo. Wanapoonyeshwa ufafanuzi wa matunda ya roho ya Mungu na kualikwa kwenye Jumba la Ufalme kujionea wenyewe matunda hayo, wengi hukiri haraka hivi: “Kwa kweli Mungu yupo katikati yenu.” (1 Wakorintho 14:25) Hilo halitokei katika Jumba moja tu la Ufalme. Hata uende wapi, unapokutana na yeyote kati ya Mashahidi wa Yehova wapatao milioni sita, utaona roho ileile ya furaha na shangwe. Kwa kweli, ushirika huo wenye kujenga ni sababu nzuri ya kumshukuru Yehova, yule anayewapa roho yake inayowezesha yote hayo.—Sefania 3:9; Waefeso 3:20, 21.

5, 6. Tunawezaje kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya fidia, ambayo ni zawadi kuu zaidi kutoka kwa Mungu?

5 Zawadi kuu zaidi, tuzo kamilifu zaidi ambayo Yehova ametoa, ni Mwana wake, Yesu, ambaye dhabihu ya fidia ilitolewa kupitia yeye. “Ikiwa Mungu alitupenda hivi,” akaandika mtume Yohana, “basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:11) Ndiyo, tunaonyesha shukrani zetu kwa ajili ya fidia kwa kuonyesha upendo na shukrani zetu kwa Yehova na pia kwa kuishi maisha yetu kwa njia inayoonyesha kwamba tunawapenda wengine.—Mathayo 22:37-39.

6 Tunaweza kujifunza mambo mengi zaidi kuhusu kuonyesha shukrani kwa kufikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na taifa la kale la Israeli. Kwa kutumia Sheria aliyotoa kupitia Musa, Yehova aliwafundisha watu wake mambo mengi. Kupitia “picha ya ujuzi na ya ile kweli katika Sheria,” tunaweza kujifunza mengi yanayoweza kutusaidia kufuata shauri hili la Paulo: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.”—Waroma 2:20; Wakolosai 3:15.

Mambo Matatu Tunayoweza Kujifunza Kutokana na Sheria ya Musa

7. Mpango wa kutoa sehemu ya kumi uliwawezeshaje Waisraeli kuonyesha shukrani zao kwa Yehova?

7 Katika Sheria ya Musa, Yehova alionyesha njia tatu ambazo Waisraeli wangeweza kuonyesha uthamini wa kweli kwa ajili ya wema wake. Kwanza, kupitia sehemu ya kumi. Sehemu ya kumi ya mazao ya nchi, pamoja na “sehemu ya kumi ya mifugo na ya kundi,” ingekuwa “kitu kitakatifu kwa Yehova.” (Mambo ya Walawi 27:30-32) Waisraeli walipotii, Yehova aliwabariki sana. “‘Leteni ghalani sehemu zote za kumi, ili kuwe na chakula nyumbani mwangu; nanyi, tafadhali, mnijaribu kwa njia hii,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’”—Malaki 3:10.

8. Kulikuwa na tofauti gani kati ya matoleo ya hiari na sehemu ya kumi?

8 Pili, zaidi ya kutoa sehemu ya kumi, Yehova alipanga Waisraeli watoe michango ya hiari. Alimwagiza Musa awaambie Waisraeli hivi: “Mtakapoingia katika nchi ambamo nitawapeleka ninyi, itatukia kwamba mtakapokula mkate wowote wa nchi hiyo, mtamtolea Yehova mchango.” Baadhi ya mazao ya kwanza ya ‘unga wenye chenga-chenga ukiwa keki za mviringo’ yangetolewa yakiwa “mchango kwa Yehova” katika vizazi vyao vyote. Ona kwamba hakukuwa na kiwango hususa kilichotakiwa cha mazao hayo ya kwanza. (Hesabu 15:18-21) Lakini, Waisraeli walipoonyesha shukrani zao kwa kutoa michango, walihakikishiwa baraka kutoka kwa Yehova. Mpango kama huo unaonekana kuhusiana na hekalu la maono ya Ezekieli. Tunasoma hivi: “Ya kwanza kati ya matunda ya kwanza yaliyoiva ya kila kitu na kila mchango wa kila kitu kutoka katika michango yenu yote—yatakuwa ni ya makuhani; na matunda ya kwanza ya unga wenu wenye chenga-chenga mtawapa makuhani, ili kufanya baraka ikae juu ya nyumba yako.”—Ezekieli 44:30.

9. Yehova alifundisha nini kupitia mpango wa kuacha masalio?

9 Tatu, Yehova alifanya mpango wa kuokota masalio. “Mnapovuna mavuno ya nchi yenu,” Mungu akaagiza, “msivune kabisa ukingo wa shamba lenu, nayo masalio ya mavuno yenu msiyaokote. Pia, usikusanye masalio ya shamba lako la mizabibu, wala usiokote zabibu zilizotawanyika za shamba lako la mizabibu. Ziache kwa ajili ya mwenye kuteseka na mkaaji mgeni. Mimi ni Yehova Mungu wenu.” (Mambo ya Walawi 19:9, 10) Kwa mara nyingine tena, hakuna kiwango hususa kilichotakiwa. Kila Mwisraeli angejiamulia kiwango ambacho angewaachia wenye uhitaji. Mfalme Sulemani mwenye hekima alieleza hivi kwa kufaa: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Methali 19:17) Kwa hiyo Yehova aliwafundisha watu wake kuwa na huruma na kuwafikiria watu wenye uhitaji.

10. Matokeo yalikuwa nini Waisraeli walipokosa kuonyesha shukrani?

10 Yehova aliwabariki Waisraeli walipotii kwa kutoa sehemu ya kumi, wakatoa michango ya hiari, na kuwaandalia maskini. Lakini Waisraeli walipokosa kuonyesha shukrani, walipoteza kibali cha Yehova. Hilo lilitokeza madhara na baadaye wakapelekwa uhamishoni. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21) Basi, tunajifunza nini?

Jinsi Tunavyoonyesha Shukrani

11. Ni njia gani kuu tunayoweza kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova?

11 Njia kuu tunayoweza kumsifu Yehova na kuonyesha shukrani zetu huhusisha ‘kutoa.’ Ni kweli kwamba, tukiwa Wakristo, hatuko chini ya Sheria ya Musa, hatuwajibiki kutoa dhabihu za wanyama au mazao. (Wakolosai 2:14) Hata hivyo, mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo Waebrania: “Tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Kwa kutumia uwezo wetu na mali zetu kumtolea Yehova dhabihu ya sifa, iwe ni katika huduma ya hadharani au katika “makundi yaliyokutanika” ya Wakristo wenzetu, tunaweza kuonyesha shukrani zetu za kutoka moyoni kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova Mungu. (Zaburi 26:12) Tunapofanya hivyo, tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambazo Waisraeli walipaswa kuonyesha shukrani zao kwa Yehova?

12. Kuhusu daraka letu la Kikristo, tunaweza kujifunza nini kutokana na mpango wa kutoa sehemu ya kumi?

12 Kwanza kabisa, kama tulivyotangulia kuona, mpango wa kutoa sehemu ya kumi haukuwa wa hiari; kila Mwisraeli alikuwa na wajibu wa kuitoa. Tukiwa Wakristo, tuna daraka la kushiriki katika huduma na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Utendaji huo si wa hiari. Katika unabii wake kuhusu wakati wa mwisho, Yesu alisema hivi waziwazi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kuhusu mikutano ya Kikristo, mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Sisi huonyesha shukrani zetu kwa Yehova tunapokubali kwa shangwe daraka letu la kuhubiri na kufundisha, hali kadhalika kushirikiana na ndugu zetu kwa ukawaida katika mikutano ya kutaniko, tukiyaona mambo hayo kuwa pendeleo na heshima.

13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mpango wa kutoa michango ya hiari na masalio?

13 Pia, tunaweza kufaidika kwa kuchunguza ile mipango mingine miwili ambayo Waisraeli wangeweza kuonyesha shukrani zao—michango ya hiari na masalio. Tofauti na kutoa sehemu ya kumi, jambo ambalo lilikuwa takwa lenye wajibu uliotajwa waziwazi, michango ya hiari na mpango wa masalio haikuhitaji kiwango hususa kilichowekwa. Badala yake, mtumishi wa Yehova angeweza kuonyesha kiwango cha uthamini aliokuwa nao moyoni ambao ulimchochea kutenda. Vivyo hivyo, ingawa tunajua kwamba kushiriki katika huduma na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni wajibu wa msingi wa kila mtumishi wa Yehova, je, tunashiriki kwa moyo wote na kwa roho ya kupenda? Je, tunaona mambo hayo kuwa nafasi ya kuonyesha uthamini wetu kutoka moyoni kwa ajili ya mambo yote ambayo Yehova ametufanyia? Je, tunashiriki kwa kadiri kubwa katika utendaji huo, kwa kiwango ambacho hali zetu zinaturuhusu? Au tunayaona yote hayo kuwa wajibu tu ambao tunapaswa kutimiza? Hayo, bila shaka, ni maswali ambayo lazima sisi binafsi tuyajibu. Mtume Paulo alisema hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 6:4.

14. Yehova anatazamia tufanye nini katika utumishi wake?

14 Yehova Mungu anajua vizuri hali zetu. Anajua uwezo wetu. Anathamini dhabihu zinazotolewa na watumishi wake kwa hiari, ziwe kubwa au ndogo. Hatazamii sisi sote tutoe kiwango kilekile, wala hatuwezi kufanya hivyo. Alipokuwa akizungumzia kutoa vitu vya kimwili, mtume Paulo aliwaambia Wakristo Wakorintho hivi: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” (2 Wakorintho 8:12) Kanuni hiyo inatumika pia katika utumishi wetu kwa Mungu. Jambo ambalo hufanya utumishi wetu ukubalike kwa Yehova si kiwango tunachotimiza, bali jinsi tunavyoutimiza—kwa shangwe na kwa moyo wote.—Zaburi 100:1-5; Wakolosai 3:23.

Sitawisha na Udumishe Roho ya Upainia

15, 16. (a) Kuna uhusiano gani kati ya huduma ya upainia na kuonyesha shukrani? (b) Wale ambao hawawezi kuwa mapainia wanawezaje kuonyesha roho ya upainia?

15 Njia yenye kuthawabisha ya kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova ni kuingia katika huduma ya wakati wote. Wakichochewa na upendo kwa Yehova na shukrani kwa ajili ya fadhili zake zisizostahiliwa, watumishi wengi waliojiweka wakfu wamefanya mabadiliko makubwa maishani mwao ili wapate wakati zaidi wa kumtumikia Yehova. Wengine wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida, wakitumia wastani wa saa 70 kila mwezi wakihubiri habari njema na kuwafundisha watu kweli. Wengine ambao labda wanazuiwa na hali mbalimbali, mara kwa mara hupanga kutumia saa 50 kwa mwezi wakihubiri wakiwa mapainia wasaidizi.

16 Lakini namna gani watumishi wa Yehova walio wengi ambao hawawezi kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida au wasaidizi? Wanaweza kuonyesha shukrani zao kwa kusitawisha na kudumisha roho ya upainia. Jinsi gani? Kwa kuwatia moyo wale wanaoweza kufanya upainia, kwa kuwachochea watoto wao wawe na tamaa ya kufanya utumishi wa wakati wote, na kwa kuhubiri kwa bidii kulingana na hali zao. Kile tunachotoa katika huduma yetu hutegemea kiwango cha uthamini tulio nao moyoni kwa ajili ya mambo ambayo Yehova ametufanyia, anatufanyia, na ambayo bado atatufanyia.

Kuonyesha Shukrani kwa ‘Vitu Vyetu Vyenye Thamani’

17, 18. (a) Tunawezaje kuonyesha shukrani kwa ‘vitu vyetu vyenye thamani’? (b) Yesu aliuonaje mchango wa mjane, na kwa nini?

17 “Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani,” lasema andiko la Methali 3:9, “na kwa matunda ya kwanza ya mazao yako yote.” Watumishi wa Yehova hawatakiwi kutoa sehemu ya kumi leo. Badala yake, Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Korintho: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kutoa michango ya hiari ili kutegemeza kazi ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote pia huonyesha shukrani zetu. Uthamini wa kutoka moyoni hutuchochea kufanya hivyo kwa ukawaida, labda hata kuweka kando kitu fulani kila juma, kama walivyofanya Wakristo wa kwanza.—1 Wakorintho 16:1, 2.

18 Shukrani zetu kwa Yehova hazionyeshwi na kiwango tunachotoa. Badala yake, zinaonyeshwa na roho tuliyo nayo tunapotoa. Yesu aliona hilo alipokuwa akiwatazama watu wakitumbukiza zawadi zao katika masanduku ya hazina hekaluni. Yesu alipomwona mjane mwenye uhitaji akitumbukiza ndani “sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana,” alisema hivi: “Ninawaambia ninyi kwa kweli, Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, ametumbukiza ndani zaidi kuliko hao wote. Kwa maana wote hawa walitumbukiza zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani riziki yote aliyokuwa nayo.”—Luka 21:1-4.

19. Kwa nini ni vizuri kuchunguza upya jinsi tunavyoonyesha shukrani zetu?

19 Pitio hili la jinsi tunavyoweza kuonyesha shukrani na lituchochee kuchunguza upya jinsi tunavyoonyesha shukrani zetu. Je, tunaweza kuongeza dhabihu zetu za sifa kwa Yehova na kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote kwa michango yetu? Kwa kadiri tunavyofanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu mkarimu na mwenye upendo, Yehova, atafurahi kwa kuwa tunajionyesha kuwa wenye shukrani.

Je, Unakumbuka?

• Tuna sababu gani za kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova?

• Tunajifunza mambo gani kutokana na kutoa sehemu ya kumi, michango ya hiari, na masalio?

• Tunawezaje kusitawisha roho ya upainia?

• Tunawezaje kutumia ‘vitu vyetu vyenye thamani’ kumshukuru Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

“Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu”

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ni mambo gani matatu yanayoonyeshwa hapa tunayoweza kujifunza kutokana na Sheria?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ni dhabihu gani tunazoweza kutoa?