Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nitamlipa Yehova Nini?”

“Nitamlipa Yehova Nini?”

Simulizi la Maisha

“Nitamlipa Yehova Nini?”

LIMESIMULIWA NA MARIA KERASINIS

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, niliwavunja moyo sana wazazi wangu, nikatengwa na familia yangu na kudhihakiwa kijijini. Nilisihiwa, nikahimizwa, na hata kutishwa ili nivunje uaminifu wangu kwa Mungu—lakini wapi! Nilikuwa na uhakika kwamba ningepata faida za kiroho ikiwa ningeendelea kushikamana na kweli za Biblia. Ninapokumbuka miaka 50 ambayo nimemtumikia Yehova, nakubaliana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?”—Zaburi 116:12.

NILIZALIWA mwaka wa 1930, katika kijiji cha Aggelokastro, kilicho umbali wa kilometa 20 kutoka bandari ya Cenchreae, upande wa mashariki wa Rasi ya Korintho, ambapo kutaniko la Wakristo wa kweli lilianzishwa katika karne ya kwanza.—Matendo 18:18; Waroma 16:1.

Familia yetu iliishi kwa amani. Baba alikuwa mkuu wa kijiji naye aliheshimiwa sana. Nilikuwa mtoto wa tatu kati ya watoto watano. Wazazi wangu walitulea kuwa wafuasi waaminifu wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Nilihudhuria Misa kila Jumapili. Nilikuwa nikitubu mbele ya sanamu, nikiwasha mishumaa katika makanisa ya vijijini, na kufunga kila wakati. Mara nyingi nilitaka kuwa mtawa. Baada ya muda, nikawa wa kwanza katika familia yetu kuwavunja moyo wazazi wangu.

Kusisimuliwa na Kweli za Biblia

Nilipokuwa na umri wa miaka 18 hivi, nilipata kujua kwamba Katina, mmoja wa shemeji zangu, aliyekuwa akiishi katika kijiji jirani, alikuwa akisoma vichapo vya Mashahidi wa Yehova, naye alikuwa ameacha kwenda kanisani. Jambo hilo lilinihangaisha sana, kwa hiyo nikaamua kumsaidia arudie njia niliyoiona kuwa sawa. Basi, alipokuja kututembelea, nilipanga twende kutembea, nikikusudia tupitie nyumbani kwa kasisi. Kasisi huyo alianzisha mazungumzo kwa kuwadhihaki Mashahidi wa Yehova, akiwaita wazushi ambao wamempotosha Katina. Mazungumzo hayo yaliendelea kwa muda wa siku tatu. Katina alipinga madai yote hayo kwa kutumia hoja za Biblia alizokuwa ametayarisha vizuri. Mwishowe, kasisi huyo akamwambia kwamba kwa kuwa yeye ni msichana mrembo, mwenye akili, anapaswa kufurahia ujana wake na kupendezwa na Mungu atakapokuwa mzee.

Sikuwaambia wazazi wangu chochote kuhusiana na mazungumzo hayo, lakini Jumapili iliyofuata, sikwenda kanisani. Mchana, kasisi akaja moja kwa moja katika duka letu. Nikajitetea kwa kumwambia kwamba nilipaswa kukaa dukani ili nimsaidie Baba.

“Je, kweli hiyo ndiyo sababu, au yule msichana alikuchochea?” kasisi huyo akaniuliza.

“Imani ya watu hao ni bora kuliko yetu,” nikamwambia moja kwa moja.

Kasisi akamgeukia baba yangu, na kumwambia: “Bwana Economos, mfukuze Katina mara moja; ameanzisha moto nyumbani kwako.”

Familia Yangu Yanigeuka

Hayo yalitokea mwishoni mwa miaka ya 1940 wakati ambapo kulikuwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Ugiriki. Akiogopa kwamba huenda askari wa msituni wangeninyakua, Baba alipanga niondoke kijijini niende nyumbani kwa dada yangu katika kijiji alikoishi Katina. Kwa miezi miwili niliyokaa huko, nilisaidiwa kuelewa mambo ambayo Biblia inasema kuhusu masuala mbalimbali. Nilivunjika moyo kuona kwamba mafundisho mengi ya Kanisa Othodoksi hayakupatana na Maandiko. Nilipata kujua kwamba Mungu hakubali matumizi ya sanamu katika ibada, kwamba desturi nyingi za kidini—kama vile kuabudu msalaba—hazikutokana na Ukristo, na kwamba ili mtu ampendeze Mungu, anapaswa kumwabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23; Kutoka 20:4, 5) Pia, nilijifunza kwamba Biblia hutoa tumaini zuri la uzima wa milele hapa duniani! Kweli hizo za Biblia zilikuwa baadhi ya faida za kwanza nilizopata mimi binafsi kutoka kwa Yehova.

Wakati huohuo, dada yangu na mume wake walitambua kwamba sikufanya ishara ya msalaba kabla ya kula, wala sikusali mbele ya sanamu za kanisa. Usiku mmoja wote wawili walinipiga. Siku iliyofuata, niliamua kuondoka nyumbani kwao, nami nikaenda nyumbani kwa shangazi yangu. Shemeji yangu akamjulisha baba yangu. Punde si punde, Baba akaja akilia na kujaribu kunifanya nibadili nia yangu. Shemeji yangu alipiga magoti mbele yangu, akiniomba msamaha, nami nikamsamehe. Ili kumaliza jambo hilo, waliniomba nirudi kanisani, lakini nikashikilia msimamo wangu.

Niliporudi kijijini kwa Baba, mikazo iliendelea. Sikuwa na njia ya kuwasiliana na Katina, wala sikuwa na kichapo cha kusoma, hata Biblia. Nilifurahi sana wakati ambapo mmoja wa binamu zangu alijaribu kunisaidia. Alipoenda Korintho, alikutana na Shahidi naye akaja na kitabu “Let God Be True” pamoja na nakala ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, vichapo nilivyoanza kuvisoma kisiri.

Maisha Yabadilika Ghafula

Upinzani mkali uliendelea kwa miaka mitatu. Sikuwasiliana na Mashahidi wowote, wala sikuweza kupokea kichapo chochote. Hata hivyo, bila kujua, maisha yangu yalikuwa karibu kubadilika sana.

Baba aliniambia kwamba niende kwa mjomba wangu huko Thesalonike. Kabla ya kuondoka kwenda Thesalonike, nilienda katika duka la fundi wa nguo huko Korintho anishonee koti. Nilishangaa nilipomkuta Katina akifanya kazi huko! Tulifurahi sana kuonana baada ya muda mrefu hivyo. Sote wawili tulipokuwa tukiondoka dukani, tulikutana na kijana mzuri sana aliyekuwa akirudi nyumbani kutoka kazini, akiendesha baiskeli. Alikuwa akiitwa Charalambos. Baada ya kujuana, tuliamua kwamba tutaoana. Wakati huo pia, Januari 9, 1952, ndipo nilipoonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa.

Charalambos alikuwa amebatizwa. Yeye pia alipata upinzani kutoka kwa familia yake. Charalambos alikuwa na bidii sana. Alikuwa msaidizi wa msimamizi wa kutaniko naye alikuwa akiongoza mafunzo mengi ya Biblia. Punde baadaye, ndugu zake wakaikubali kweli, na leo washiriki wengi wa familia zao pia wanamtumikia Yehova.

Baba yangu alimpenda sana Charalambos, kwa hiyo akakubali tufunge ndoa, lakini Mama hakukubali kwa urahisi. Licha ya yote hayo, Charalambos nami tukafunga ndoa Machi 29, 1952. Kaka yangu na mmoja wa binamu zangu tu ndio waliohudhuria harusi yetu. Sikujua wakati huo kwamba Charalambos angekuwa baraka kwelikweli—zawadi bora kutoka kwa Yehova! Nikiwa mwandamani wake, nilitumia maisha yangu katika utumishi wa Yehova.

Kuwaimarisha Ndugu Zetu

Mwaka wa 1953, mimi na Charalambos tuliamua kuhamia Athene. Kwa kuwa tulitaka kutimiza mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri, Charalambos aliacha kazi aliyokuwa akifanya katika biashara ya familia na kupata kazi ya muda. Tulitumia vipindi vya alasiri pamoja katika huduma ya Kikristo na tukaongoza mafunzo mengi ya Biblia.

Kwa sababu huduma yetu ilikuwa imewekewa vizuizi na serikali, tulihitaji kutumia busara. Kwa mfano, tuliamua kuweka nakala ya gazeti la Mnara wa Mlinzi katika dirisha la kioski, au kibanda, katikati ya Athene, ambapo mume wangu alikuwa akifanya kazi ya muda. Polisi mwenye cheo alituambia kwamba gazeti hilo limepigwa marufuku. Hata hivyo, aliomba kuchukua nakala moja, akaulize kwenye ofisi ya usalama. Walipomhakikishia kwamba gazeti hilo lilikuwa halali, alirudi kutujulisha. Mara tu ndugu wengine waliokuwa na vioski waliposikia, wao pia wakaanza kuweka nakala za Mnara wa Mlinzi katika madirisha ya vioski vyao. Mtu mmoja alichukua Mnara wa Mlinzi kutoka katika kioski chetu, akawa Shahidi, naye sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko.

Pia tulifurahi kumwona ndugu yangu mdogo akijifunza kweli. Alikuja Athene kusomea katika chuo cha ubaharia, nasi tukaenda pamoja naye kusanyikoni. Makusanyiko yetu yalikuwa yakifanywa kisiri, misituni. Alipendezwa na mambo aliyosikia, lakini punde baadaye akaanza kusafiri. Katika moja ya safari zake, alifika katika bandari moja huko Argentina. Alipokuwa huko, mishonari mmoja alipanda meli hiyo ili kuhubiri, naye ndugu yangu akamwomba magazeti yetu. Tulifurahi sana tulipopokea barua yake akisema: “Nimepata kweli. Niandikishieni magazeti hayo.” Leo, yeye na familia yake wanamtumikia Yehova kwa uaminifu.

Katika mwaka wa 1958, mume wangu aliombwa atumikie akiwa mwangalizi anayesafiri. Kwa kuwa kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku na hali zilikuwa ngumu sana, waangalizi wanaosafiri hawakutumikia pamoja na wake zao. Mwezi wa Oktoba 1959, tuliwaomba ndugu wanaohusika kwenye ofisi ya tawi ikiwa ingewezekana niandamane naye. Wakakubali. Tulipaswa kutembelea na kuimarisha makutaniko ya Ugiriki kaskazini na kati.

Safari hizo hazikuwa rahisi. Kulikuwa na barabara chache sana za lami. Kwa kuwa hatukuwa na gari, kwa kawaida tulipanda magari ya umma au magari ya mizigo yaliyokuwa yamebeba kuku na bidhaa nyingine. Tulivaa viatu vya mpira ili kutembea katika njia zenye matope. Kwa kuwa katika kila kijiji kulikuwa na jeshi la mgambo, tulilazimika kuingia vijijini usiku ili kuepuka kuhojiwa.

Akina ndugu walithamini sana ziara hizo. Ingawa wengi wao walifanya kazi nyingi katika mashamba yao, walijitahidi sana kuhudhuria mikutano iliyokuwa ikifanywa usiku sana katika nyumba mbalimbali. Pia, ndugu hao walikuwa wakarimu sana nao walitupa vitu vilivyo bora, ingawa walikuwa na vichache sana. Nyakati nyingine tulilala na familia nzima katika chumba kimoja. Imani, uvumilivu, na bidii ya akina ndugu ilikuwa faida nyingine kubwa kwetu.

Kupanua Utumishi Wetu

Mwezi wa Februari 1961, tulipokuwa tukitembelea ofisi ya tawi ya Athene, tuliulizwa kama tungependa kutumikia huko Betheli. Tulijibu kwa maneno ya Isaya: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isaya 6:8) Miezi miwili baadaye, tulipokea barua iliyotuambia twende Betheli haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, mnamo Mei 27, 1961, tulianza kutumikia Betheli.

Tulifurahia sana mgawo wetu mpya, tukastarehe upesi. Mume wangu alifanya kazi katika idara za Utumishi na Maandikisho, na baadaye akatumikia kwa muda katika Halmashauri ya Tawi. Nilikuwa na migawo mbalimbali. Kulikuwa na washiriki 18 wa familia hiyo wakati huo, lakini kwa karibu miaka mitano, kulikuwa na watu 40 hivi kwa sababu shule ya wazee ilikuwa ikifanywa Betheli. Asubuhi, niliosha vyombo, nikamsaidia mpishi, nikatandika vitanda 12, na kupanga meza kwa ajili ya chakula cha mchana. Alasiri, nilipiga nguo pasi na kuosha vyoo na vyumba. Mara moja kwa juma nilifanya kazi katika dobi. Kulikuwa na kazi nyingi, lakini nilifurahi kusaidia.

Tulijishughulisha sana katika migawo yetu ya Betheli hali kadhalika katika utumishi wa shambani. Mara nyingi hata tuliongoza mafunzo saba ya Biblia. Mwishoni mwa majuma, niliandamana na Charalambos alipokuwa akitoa hotuba katika makutaniko mbalimbali. Tulikuwa pamoja nyakati zote.

Tulijifunza Biblia pamoja na wenzi wa ndoa waliokuwa wakishirikiana na Kanisa Othodoksi la Kigiriki na ambao pia walikuwa rafiki za kasisi aliyekuwa akiongoza shirika la kanisa la kukabiliana na wazushi. Katika nyumba yao, chumba kimoja kilikuwa kimejaa sanamu, ambapo uvumba ulikuwa ukifukizwa mfululizo na nyimbo za Byzantium zilichezwa mchana kutwa. Kwa muda fulani, tuliwatembelea siku za Alhamisi ili kujifunza Biblia pamoja nao, naye rafiki yao kasisi alikuwa akiwatembelea kila Ijumaa. Siku moja, walituomba tusikose kwenda nyumbani kwao kwa sababu walitaka kutuonyesha kitu fulani. Kitu cha kwanza walichotuonyesha ni kile chumba. Walikuwa wameondolea mbali sanamu zote na kukirekebisha. Wenzi hao walifanya maendeleo zaidi na kubatizwa. Kwa ujumla, tumefurahi kuona watu 50 hivi tuliojifunza Biblia pamoja nao wakijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Faida ya pekee niliyopata ni kushirikiana na akina ndugu watiwa-mafuta. Ziara za washiriki wa Baraza Linaloongoza, kama vile Ndugu Knorr, Franz, na Henschel, zilikuwa zenye kutia moyo sana. Baada ya miaka zaidi ya 40, bado ninahisi kwamba kutumikia Betheli ni pendeleo na heshima kubwa.

Kukabiliana na Ugonjwa na Kifo

Katika mwaka wa 1982 mume wangu alianza kuwa na dalili za ugonjwa wa Alzheimer. Kufikia mwaka wa 1990 afya yake ilikuwa imezorota, na mwishowe akahitaji kutunzwa daima. Miaka minane ya mwisho ya maisha yake, hatukuweza kutoka Betheli hata kidogo. Ndugu wengi wapendwa katika familia ya Betheli, na pia waangalizi, walifanya mipango ya kutusaidia. Hata hivyo, licha ya usaidizi wao wenye fadhili, nililazimika kutumia saa nyingi mchana na usiku nikimtunza. Mambo yalikuwa magumu sana nyakati nyingine, na mara nyingi sikulala usiku.

Julai 1998 mume wangu mpendwa akafa. Ijapokuwa ninamkosa sana, ninafarijiwa kwa kujua kwamba yuko mikononi mwa Yehova, na ninajua kwamba Yehova atamkumbuka pamoja na mamilioni ya watu wengine katika ufufuo.—Yohana 5:28, 29.

Kuthamini Faida Nilizopata Kutoka kwa Yehova

Ingawa mume wangu alikufa, sina upweke. Bado nina pendeleo la kutumikia Betheli, nami ninafurahia upendo na utunzaji wa familia nzima ya Betheli. Familia yangu kubwa zaidi inatia ndani ndugu na dada zangu wa kiroho kutoka Ugiriki nzima. Ingawa sasa nina umri wa zaidi ya miaka 70, bado ninaweza kufanya kazi siku nzima jikoni na mezani.

Mwaka wa 1999 ndoto yangu ilitimia nilipotembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko New York. Siwezi kueleza jinsi nilivyohisi. Ilikuwa pindi yenye kujenga na isiyoweza kusahaulika.

Ninapokumbuka, kwa kweli naamini kwamba niliyatumia maisha yangu kwa njia bora. Kazi bora ambayo mtu yeyote anaweza kuwa nayo ni kumtumikia Yehova kwa wakati wote. Naweza kusema kwa uhakika kwamba sijawahi kukosa chochote. Yehova alinitunza mimi na mume wangu kwa upendo kiroho na kimwili. Kutokana na mambo ambayo nimejionea maishani, ninaelewa sababu iliyomfanya mtunga-zaburi aulize: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?”—Zaburi 116:12.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mimi na Charalambos tulikuwa pamoja sikuzote

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mume wangu akiwa ofisini mwake katika ofisi ya tawi

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ninauona utumishi wa Betheli kuwa pendeleo kubwa