Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Pata Furaha Tele Katika Yehova’

‘Pata Furaha Tele Katika Yehova’

‘Pata Furaha Tele Katika Yehova’

“Upate furaha tele katika Yehova, naye atakupa maombi ya moyo wako.”—ZABURI 37:4.

1, 2. Chanzo cha furaha ya kweli ni nani, na Mfalme Daudi alionyeshaje jambo hilo?

“WENYE furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, . . . wenye furaha ni wale walio na rehema, . . . wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” Taarifa hizo pamoja na mafafanuzi mengine sita ya wenye furaha, ni utangulizi wenye kuvutia wa yale Mahubiri ya Mlimani ya Yesu yanayojulikana sana, yaliyoandikwa na Mathayo, mwandishi wa Injili. (Mathayo 5:3-11) Maneno ya Yesu yanatuhakikishia kwamba tunaweza kupata furaha.

2 Wimbo mtakatifu ulioandikwa na Mfalme Daudi wa Israeli ya kale unaonyesha kwamba Yehova ndiye Chanzo cha furaha ya kweli. “Upate furaha tele katika Yehova,” akasema Daudi, “naye atakupa maombi ya moyo wako.” (Zaburi 37:4) Lakini kumjua Yehova na utu wake kunawezaje kutokeza “furaha tele”? Kuchunguza mambo ambayo amefanya na atakayofanya ili kutimiza kusudi lake kunawezaje kukupa tarajio la kupokea “maombi ya moyo wako”? Majibu yanaweza kupatikana kwa kuchunguza kwa uangalifu Zaburi 37, mstari wa 1 hadi 11.

“Usiwaonee Wivu”

3, 4. Kama andiko la Zaburi 37:1 linavyoonyesha, Daudi anatoa shauri gani, na kwa nini inafaa kulifuata leo?

3 Tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” nao uovu umeenea sana. Tumeona maneno ya mtume Paulo yakitimia: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:1, 13) Ni rahisi kama nini kuathiriwa na yale yanayoonekana kuwa mafanikio na ufanisi wa watu waovu! Yote hayo yanaweza kutukengeusha, na kutufanya tupoteze mtazamo wetu wa kiroho. Ona jinsi maneno ya kwanza ya Zaburi 37 yanavyotuonyesha hatari iliyopo: “Usijionyeshe umewaka hasira kwa sababu ya watenda-maovu. Usiwaonee wivu wale wanaofanya mambo yasiyo ya uadilifu.”

4 Kila siku vyombo vya habari ulimwenguni huwa na habari nyingi za matendo ya udhalimu. Wafanyabiashara ambao si waaminifu wanaendelea na shughuli zao kwa uhuru. Wahalifu huwashambulia wasio na uwezo. Wauaji hujificha wasipatikane au hata hawaadhibiwi. Mifano yote hiyo ya upotovu wa haki inaweza kutufanya tukasirike na kukosa kuwa na amani ya akili. Yanayoonekana kuwa mafanikio ya watenda-maovu huenda hata yakafanya tuwe na wivu. Lakini je, kukasirika kwetu kutaboresha hali hiyo? Je, kuonea wivu yale yanayoonekana kuwa mafanikio ya watu waovu kunabadili matokeo yao? Sivyo hata kidogo! Na kwa kweli hakuna haja ya ‘kuwaka hasira.’ Kwa nini?

5. Kwa nini watenda-maovu wanalinganishwa na majani?

5 Mtunga-zaburi anajibu hivi: “Kwa maana watakauka haraka kama majani, nao watafifia kama majani mapya ya kijani kibichi.” (Zaburi 37:2) Huenda majani mapya ya kijani kibichi yakaonekana kuwa yenye kupendeza, lakini hukauka na kufa haraka. Ndivyo ilivyo na watenda-maovu. Ule unaoonekana kuwa ufanisi wao si wa kudumu. Wanapokufa, mapato yao yasiyo ya haki hutoweka. Mwishowe, kila mtu hupata haki yake. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” akaandika Paulo. (Waroma 6:23) Watenda-maovu na wote ambao si waadilifu mwishowe watapokea “mshahara” wao. Hayo ni maisha ya ubatili kama nini!—Zaburi 37:35, 36; 49:16, 17.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na andiko la Zaburi 37:1, 2?

6 Basi, je, tuuruhusu ufanisi unaopitilia mbali wa watenda-maovu utuhangaishe? Hili ndilo tunalojifunza katika mistari ya kwanza miwili ya Zaburi 37: Usiruhusu kamwe mafanikio yao yakukengeushe kutoka katika njia ambayo umechagua ya kumtumikia Yehova. Badala yake, endelea kukaza fikira zako katika baraka na miradi ya kiroho.—Methali 23:17.

“Mtegemee Yehova na Ufanye Mema”

7. Kwa nini tunapaswa kumtegemea Yehova?

7 Mtunga-zaburi anatuhimiza ‘tumtegemee Yehova na kufanya mema.’ (Zaburi 37:3a) Tunapolemewa na mahangaiko au hata shaka, tunapaswa kuwa na uhakika imara katika Yehova. Yeye ndiye hutoa ulinzi kamili wa kiroho. “Yeyote anayekaa mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi,” akaandika Musa, “atajipatia makao katika kivuli cha Mweza-Yote.” (Zaburi 91:1) Tunapohangaishwa na ongezeko la uvunjaji wa sheria katika mfumo huu wa mambo, tunahitaji kumtegemea Yehova hata zaidi. Tunapoteguka mguu, tunafurahi tunapotegemezwa na rafiki. Vivyo hivyo, tunapojitahidi kutembea kwa uaminifu, tunahitaji utegemezo wa Yehova.—Isaya 50:10.

8. Kushiriki katika huduma ya Kikristo kunaweza kutusaidiaje kuepuka kuhangaishwa kupita kiasi na ufanisi wa watu waovu?

8 Njia moja ya kuepuka kuhangaishwa na ufanisi wa watu waovu ni kujishughulisha na kazi ya kuwatafuta na kuwasaidia watu walio mfano wa kondoo wapate ujuzi sahihi kuhusu makusudi ya Yehova. Kwa sababu ya ongezeko la uovu, tunahitaji kujishughulisha kikamili katika kuwasaidia wengine. “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine,” akaandika mtume Paulo, “kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” ‘Wema’ mkuu tunaoweza kutenda ni kuwajulisha wengine ile habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, kazi yetu ya kuhubiri hadharani ni “dhabihu ya sifa.”—Waebrania 13:15, 16; Wagalatia 6:10.

9. Daudi alimaanisha nini aliposema, “ukae duniani”?

9 “Ukae duniani,” Daudi aendelea, “na utende kwa uaminifu.” (Zaburi 37:3b) Katika siku za Daudi, ‘dunia’ ilikuwa eneo ambalo Yehova alikuwa amewapa Israeli, ile Nchi ya Ahadi. Wakati wa utawala wa Sulemani mipaka yake ilianzia Dani upande wa kaskazini hadi Beer-sheba upande wa kusini. Hayo ndiyo yaliyokuwa makao ya Israeli. (1 Wafalme 4:25) Leo, popote tunapokaa duniani, tunatarajia wakati ambao dunia nzima itakuwa paradiso katika ulimwengu mpya wa uadilifu. Kwa sasa, tunakaa katika usalama wa kiroho.—Isaya 65:13, 14.

10. ‘Tukitenda kwa uaminifu’ tunapata matokeo gani?

10 ‘Tukitenda kwa uaminifu,’ tutapata matokeo gani? Methali iliyoongozwa na roho ya Mungu hutukumbusha hivi: “Mtu mwenye matendo ya uaminifu atapata baraka nyingi.” (Methali 28:20) Kuvumilia kwetu kwa uaminifu katika kuhubiri habari njema popote tunapokaa, na kwa yeyote tunayeweza, kwa kweli hutuletea baraka kutoka kwa Yehova. Kwa mfano, Frank na mke wake, Rose, walianza mgawo wa upainia miaka 40 iliyopita katika mji fulani huko kaskazini mwa Scotland. Watu wachache waliokuwa wanapendezwa na kweli huko walikuwa wamekengeuka. Mapainia hao wawili hawakuvunjika moyo, bali walianza kuhubiri na kufanya wanafunzi. Sasa, kuna kutaniko kubwa katika mji huo. Kwa kweli Yehova amebariki uaminifu wa wenzi hao. “Baraka kuu zaidi,” Frank anaeleza kwa unyenyekevu, “ni kwamba bado tuko katika kweli na Yehova anaendelea kututumia.” Ndiyo, ‘tunapotenda kwa uaminifu,’ tunapata baraka nyingi.

‘Pata Furaha Tele Katika Yehova’

11, 12. (a) Tunawezaje ‘kupata furaha tele katika Yehova’? (b) Unaweza kujiwekea mradi gani kuhusu funzo la kibinafsi, na unaweza kupata matokeo gani?

11 Ili kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova na kuendelea kumtegemea, lazima ‘tupate furaha tele katika Yehova.’ (Zaburi 37:4a) Tunafanyaje hivyo? Badala ya kujishughulisha na hali zetu wenyewe, hata ziwe ngumu kadiri gani, tunamfanya Yehova kuwa hangaiko letu. Njia moja ya kufanya hivyo ni kutenga wakati wa kulisoma Neno lake. (Zaburi 1:1, 2) Je, usomaji wako wa Biblia hukuletea furaha? Utapata furaha ikiwa unasoma ukiwa na kusudi la kujifunza mengi kumhusu Yehova. Kwa nini usitue kidogo baada ya kusoma mafungu fulani kisha ujiulize, ‘Fungu hili limenifundisha nini kumhusu Yehova?’ Huenda utaona inafaa kuwa na kitabu au karatasi karibu wakati unaposoma Biblia. Kila mara unapotua ili kutafakari maana ya yale ambayo unasoma, andika maneno yatakayokukumbusha moja ya sifa za Yehova zinazovutia. Katika zaburi nyingine, Daudi aliimba: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mkombozi wangu.” (Zaburi 19:14) Uangalifu tunaoukazia Neno la Mungu ‘humpendeza’ Yehova na kutufurahisha sisi.

12 Tunaweza kupataje furaha kutokana na kujifunza na kutafakari? Tunaweza kuweka mradi wa kujifunza mambo mengi tuwezavyo kumhusu Yehova na njia zake. Vichapo kama Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi na Mkaribie Yehova * hutupa habari nyingi tunazoweza kutafakari kwa uthamini. Kisha Daudi awahakikishia waadilifu kwamba Yehova ‘atawapa maombi ya mioyo yao.’ (Zaburi 37:4b) Uhakika huo ndio uliomchochea mtume Yohana kuandika maneno haya: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia. Zaidi ya hayo, tukijua kwamba yeye hutusikia kwa habari ya jambo lolote tunaloomba, tunajua tutapata mambo yaliyoombwa kwa kuwa tumeyaomba kwake.”—1 Yohana 5:14, 15.

13. Miaka ya hivi karibuni, kazi ya kuhubiri Ufalme imepanukaje katika nchi nyingi?

13 Tukiwa washika-utimilifu, furaha yetu kubwa zaidi ni kuona enzi kuu ya Yehova ikitetewa. (Methali 27:11) Je, mioyo yetu haijai shangwe tunaposikia kuhusu kazi kubwa ya kuhubiri ambayo ndugu zetu wanafanya katika nchi ambazo hapo zamani zilikuwa chini ya utawala wa kimabavu au kidikteta? Tunatarajia kwa hamu kuona uhuru zaidi ambao huenda ukatokea kabla ya mwisho wa mfumo huu. Watumishi wengi wa Yehova katika nchi za magharibi wanashiriki kwa bidii kuwahubiria wanafunzi, wakimbizi, na wengineo ambao wanakaa kwa muda katika nchi hizo na wana uhuru wa ibada. Tunatumaini kwamba watu hao wanaporudi nyumbani, wataendelea kuacha nuru ya kweli iangaze katika lile linaloonekana kuwa giza lisiloweza kupenywa.—Mathayo 5:14-16.

“Mkabidhi Yehova Njia Yako”

14. Kuna uthibitisho gani kwamba tunaweza kumtegemea Yehova?

14 Inafariji kama nini kujua kwamba mahangaiko yetu na ile inayoonekana kuwa mizigo yenye kulemea inaweza kuondolewa! Jinsi gani? “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea,” asema Daudi na kuongezea, “naye mwenyewe atatenda.” (Zaburi 37:5) Katika makutaniko yetu, tuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba tunaweza kumtegemea Yehova. (Zaburi 55:22) Wale walio katika utumishi wa wakati wote, wawe mapainia, waangalizi wasafirio, mishonari, au Wanabetheli, wote wanaweza kushuhudia kwamba Yehova hatakosa kuwatunza watu wake. Kwa nini usiongee na wale unaowajua na kuwauliza jinsi ambavyo Yehova amewasaidia? Bila shaka utasikia mambo mengi yanayoonyesha kwamba hata wakati wa magumu, mkono wa Yehova haushindwi kamwe. Sikuzote yeye huandaa mahitaji ya maisha.—Zaburi 37:25; Mathayo 6:25-34.

15. Uadilifu wa watu wa Mungu huangazaje?

15 Tunapomtumaini na kumtegemea Yehova kabisa, tunaweza kuona utimizo wa maneno ya mtunga-zaburi: “Naye atauleta uadilifu wako kama nuru, na haki yako kama katikati ya mchana.” (Zaburi 37:6) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi watu husema uwongo kutuhusu. Lakini Yehova hufumbua macho ya watu wanyoofu ili kuwasaidia kutambua kwamba huduma yetu ya hadharani huchochewa na upendo wetu kwa Yehova na kwa jirani. Na wakati huohuo, mwenendo wetu mnyoofu, ingawa husemwa vibaya na wengi, huonekana waziwazi. Yehova hututegemeza tunapokabili upinzani na mateso ya aina yoyote. Kwa hiyo, uadilifu wa watu wa Mungu huangaza kama jua katikati ya mchana.—1 Petro 2:12.

“Kaa Kimya . . . na Kumngojea kwa Kutamani”

16, 17. Kupatana na Zaburi 37:7, huu ni wakati wa kufanya nini, na kwa nini?

16 Kisha mtunga-zaburi anasema: “Kaa kimya mbele za Yehova na kumngojea kwa kutamani. Usijionyeshe umewaka hasira kwa sababu ya mtu yeyote anayeifanikisha njia yake, kwa sababu ya mtu anayetimiza mawazo yake.” (Zaburi 37:7) Hapa Daudi anakazia uhitaji wa kungojea kwa subira Yehova atende. Ingawa mwisho wa mfumo huu wa mambo bado haujaja, hiyo si sababu ya kulalamika. Je, hatujaona kwamba rehema na subira za Yehova ni kuu kuliko tulivyofikiri mwanzoni? Je, sisi pia tunaweza kuonyesha kwamba tunangoja kwa subira huku tunapojishughulisha na kazi ya kuhubiri habari njema kabla ya ule mwisho kuja? (Marko 13:10) Huu si wakati wa kutenda haraka-haraka, kwa njia inayoweza kutunyang’anya shangwe yetu na usalama wetu wa kiroho. Huu ndio wakati wa kuupinga hata zaidi uvutano wenye kufisidi wa ulimwengu wa Shetani. Na huu ndio wakati wa kudumisha usafi wa kiadili na kutohatarisha kamwe msimamo wetu mwadilifu mbele za Yehova. Na tuendelee kuondolea mbali mawazo yasiyo ya adili na kuepuka kuwa na uhusiano usiofaa pamoja na watu wa jinsia tofauti, au hata watu wa jinsia moja.—Wakolosai 3:5.

17 “Acha hasira na uache ghadhabu,” Daudi anatushauri. “Usijionyeshe umewaka hasira ili tu kufanya uovu. Kwa maana watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.” (Zaburi 37:8, 9) Ndiyo, tunaweza kutarajia kwa uhakika wakati—ambao sasa umekaribia sana—wakati ambapo Yehova atafutilia mbali kutoka duniani ufisadi wote na wale wanaousababisha.

“Bado Muda Kidogo Tu”

18, 19. Unapata kitia-moyo gani kutokana na andiko la Zaburi 37:10?

18 “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo.” (Zaburi 37:10) Maneno hayo yanatutia moyo kama nini tunapokaribia mwisho wa mfumo huu na mwisho wa matokeo mabaya ya kutomtegemea Yehova! Serikali au mamlaka zozote ambazo zimetokezwa na wanadamu zimeshindwa kabisa. Na sasa tunakaribia wakati wa kurudishwa kwa utawala wa Mungu, Ufalme wa Yehova mikononi mwa Yesu Kristo. Utasimamia kikamili mambo yote ya ulimwengu na kuwaondoa wapinzani wote wa Ufalme wa Mungu.—Danieli 2:44.

19 Katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu, hata utafute namna gani, hutaweza kumwona “mtu mwovu.” Mtu yeyote atakayemwasi Yehova ataondolewa haraka. Mtu anayeshambulia enzi yake kuu au anayekataa mamlaka ya Mungu hatakuwako. Jirani zako wote watakuwa na nia ileile ya kutaka kumpendeza Yehova kama wewe. Hilo litafanya kuwe na usalama kama nini—hakuna vifuli, vizuizi, chochote ambacho kitaondoa tumaini na furaha kamili!—Isaya 65:20; Mika 4:4; 2 Petro 3:13.

20, 21. (a) “Wapole” wanaotajwa katika Zaburi 37:11 ni nani, nao wanapata wapi “wingi wa amani”? (b) Tutapata baraka gani tukimwiga Daudi Mkuu?

20 Ndipo “wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:11a) Ndiyo, “wapole” ni wale wanaomngojea Yehova kwa unyenyekevu ili aondoe dhuluma zote zinazowapata. “Watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:11b) Hata sasa tunapata wingi wa amani katika paradiso ya kiroho inayohusianishwa na kutaniko la kweli la Kikristo.

21 Ingawa bado dhiki zetu hazijaondolewa, tunategemezana na kuwafariji wale ambao wameshuka moyo. Kwa sababu hiyo, watu wa Yehova wameridhika moyoni. Ndugu waliowekwa rasmi kuwa wachungaji huhangaikia mahitaji yetu ya kiroho—na hata wakati mwingine ya kimwili—na kutuwezesha kuvumilia dhiki kwa ajili ya uadilifu. (1 Wathesalonike 2:7, 11; 1 Petro 5:2, 3) Amani hiyo ni yenye thamani kama nini! Pia tuna tumaini la kuishi milele katika Paradiso yenye amani inayokaribia kufika. Basi, na tumwige yule Daudi Mkuu, Yesu Kristo, ambaye bidii yake kwa ajili ya Yehova ilimchochea amtumikie kwa uaminifu mpaka mwisho. (1 Petro 2:21) Kwa kufanya hivyo, tutaendelea kuwa na furaha tukimsifu yule ambaye tunapata furaha tele katika yeye, Mungu wetu, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kujibu?

• Umejifunza nini kutokana na Zaburi 37:1, 2?

• Unawezaje ‘kupata furaha tele katika Yehova’?

• Kuna uthibitisho gani unaoonyesha kwamba tunaweza kumtegemea Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wakristo ‘hawawaonei wivu wale wanaofanya mambo yasiyo ya uadilifu’

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Mtegemee Yehova na ufanye mema”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Pata furaha tele katika Yehova kwa kujifunza mambo mengi uwezavyo kumhusu

[Picha katika ukurasa wa 12]

“Wapole wataimiliki dunia”