Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tayari kwa Ajili Ya Kila Kazi Njema”

“Tayari kwa Ajili Ya Kila Kazi Njema”

“Tayari kwa Ajili Ya Kila Kazi Njema”

“ENDELEA kuwakumbusha wajitiishe na kuzitii serikali na mamlaka zikiwa watawala, wawe tayari kwa ajili ya kila kazi njema.” (Tito 3:1) Mtume Paulo alimaanisha kazi gani njema alipowaandikia waamini wenzake maneno hayo? Msomi wa Biblia E. F. Scott alitaja kazi moja njema, na kusema: “Mbali na kutii mamlaka, Wakristo wanapaswa kuwa tayari kwa ajili ya kila kazi njema. . . . Inapokuwa lazima, Wakristo wanapaswa kuwa kati ya watu wa kwanza kabisa kuonyesha roho ya kusaidia jamii. Mara kwa mara kutakuwa na moto, magonjwa, misiba mbalimbali, wakati ambapo raia wema wote watataka kuwasaidia jirani zao.”

Wakristo hushiriki kufanya kazi fulani za kusaidia jamii maadamu kazi hizo hazipingani na sheria za Mungu. (Matendo 5:29) Kwa mfano, kwa agizo la idara ya zimamoto, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyoko Ebina, nchini Japan, hufanya kila mwaka zoezi la jinsi ya kutenda moto ukitokea. Kwenye pindi hizo, Wanabetheli wote hukusanyika pamoja ili kusikiliza maagizo yanayotolewa na mwakilishi wa idara ya zimamoto.

Mbali na hayo, kwa zaidi ya miaka kumi, ofisi hiyo ya tawi imeshirikiana na mamlaka za mitaa katika maonyesho yanayodhaminiwa ili kuwafahamisha watu kuhusu uzuiaji wa moto. Kwenye maonyesho hayo, makampuni na mashirika kutoka jijini huonyesha jinsi wanavyopambana na moto na jinsi ya kuuzuia. Mara nyingi ofisi hiyo ya tawi imesifiwa na kupewa zawadi kwa ajili ya ustadi na kujitolea kwa washiriki wake. Katika mwaka wa 2001, walipewa tuzo la kwanza katika maonyesho hayo. Wako tayari kufanya kazi njema inayoweza kuokoa maisha ya watu moto ukitokea.

Utumishi Wenye Thamani

Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanapendezwa na kazi njema iliyo muhimu zaidi, ambayo pia inaokoa maisha ya watu. Wao huwatembelea jirani zao mara kwa mara ili kuwahubiria habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Mashahidi huwatia moyo watu wajifunze na kutumia kanuni za Biblia katika maisha yao ili kuboresha maisha yao sasa na kuwa na tumaini la uzima wa milele katika ulimwengu utakaokuwa na amani na usalama wa kweli.

Huenda wengine wasione thamani ya utumishi unaotolewa na Mashahidi wa Yehova, na hivyo kuwaona kuwa wenye kusumbua watu. Hata hivyo, Hakimu Jean Crepeau wa Mahakama Kuu ya Quebec nchini Kanada alikuwa na maoni tofauti. Mashahidi wa Yehova wa huko walikuwa wamepinga sheria ndogo ya jiji la Blainville, Quebec, ambayo iliwataka wawe na leseni ya kuwatembelea watu nyumba kwa nyumba. Katika uamuzi wa mahakama, Hakimu Crepeau alisema: “Kutembelewa na Mashahidi wa Yehova ni sehemu ya utumishi wa jamii wa Kikristo . . . vichapo ambavyo Mashahidi huwapa watu wanaopendezwa vina habari nzito, inayoshughulika na mambo kama vile dini, Biblia, dawa za kulevya, ulevi, elimu ya vijana, matatizo katika ndoa na talaka.” Uamuzi huo uliendelea kusema: “Mahakama inafanya uamuzi kwamba kuwalinganisha Mashahidi wa Yehova na wachuuzi ni matusi, kuwashushia heshima, kuwadhuru, na kuwadhihaki.”

Mashahidi wa Yehova huchangia hali njema ya jamii ambamo wanaishi kwa kuwasaidia watu kutatua matatizo katika maisha yao ya kila siku na kuwapa tumaini la wakati ujao. Biblia huwawezesha kufanya kazi hiyo. “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Je, ungependa kujua jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyokuwa “tayari kwa ajili ya kila kazi njema”? Tunakukaribisha ukubali wakusaidie ujifunze zaidi kuhusu Biblia na hivyo uweze kushiriki katika utumishi huo muhimu wa jamii ambao wao hufanya katika eneo lenu na ulimwenguni pote.

[Picha katika ukurasa wa 30, 31]

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushirikiana na mamlaka za kilimwengu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mashahidi wanajulikana kwa sababu ya kuwasaidia jirani zao