Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi

Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi

Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi

“Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—MATHAYO 24:42.

1, 2. Ni nini kinachoonyesha kwamba tunaishi katika umalizio wa mfumo huu wa mambo?

“KARNE ya ishirini iliathiriwa sana na vita,” anasema mwandishi Bill Emmott. Ingawa anakiri kwamba kumekuwa na vita na jeuri katika historia yote ya mwanadamu, Emmott anaendelea kusema: “Karne ya ishirini imekuwa tofauti na karne nyingine kwa kuwa imekuwa na vita vingi zaidi. Ilikuwa karne ambayo vita vilivyohusisha ulimwengu mzima vilipiganwa kwa mara ya kwanza . . . Isitoshe, katika karne hiyohiyo, vita vingine vilivyohusisha ulimwengu mzima vilipiganwa pia.”

2 Yesu Kristo alitabiri kwamba kungekuwa na vita ambavyo ‘taifa lingepigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.’ Hata hivyo, vita hivyo ni sehemu moja tu ya ile ‘ishara ya kuwapo kwa Kristo na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Katika unabii huu muhimu, Yesu pia alitaja njaa kali, tauni, na matetemeko ya nchi. (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:6, 7, 10, 11) Katika njia nyingi, maafa hayo yameongezeka na kuwa mabaya zaidi. Uovu wa mwanadamu umeongezeka, kama inavyoonyeshwa na mtazamo wake kuelekea Mungu na wanadamu wenzake. Pia maadili yanazidi kuzorota na uhalifu na jeuri vimeongezeka. Watu wamekuwa wenye kupenda fedha kuliko kumpenda Mungu, wakijishughulisha sana na anasa. Mambo hayo yote yanathibitisha kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari.”—2 Timotheo 3:1-5.

3. “Ishara za nyakati” zinapaswa kuwa na matokeo gani juu yetu?

3 Unaonaje mwelekeo wa wanadamu ambao unazidi kuwa mbaya? Wengi hawajali, na hata wamekuwa wagumu kuhusiana na matukio ya sasa yenye kuhuzunisha. Watu mashuhuri na wasomi wa ulimwengu hawatambui maana ya “ishara za nyakati”; wala viongozi wa kidini hawatoi mwongozo unaofaa kuhusiana na jambo hilo. (Mathayo 16:1-3) Lakini Yesu aliwashauri hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mathayo 24:42) Katika andiko hilo Yesu anatutia moyo tuwe wenye kulinda na pia ‘tuendelee kukesha.’ Ili kuendelea kukesha, ni lazima tudumu tukiwa macho. Kufanya hivyo kunahusisha mengi zaidi ya kutambua kwamba tunaishi katika siku za mwisho, na kwamba hali ni ngumu. Ni lazima tusadiki kabisa kwamba “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Tukiwa na usadikisho huo, tutaweza kuwa wenye kulinda na kutambua uharaka wa nyakati. Kwa hiyo, tunapaswa kutafakari swali hili: ‘Ni nini kitakachotusaidia kuimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho uko karibu?’

4, 5. (a) Ni nini kitakachoimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho wa mfumo huu mwovu uko karibu, na kwa nini? (b) Taja ufanani mmoja uliopo kati ya siku za Noa na kuwapo kwa Mwana wa binadamu?

4 Fikiria jinsi hali zilivyokuwa kabla tu ya tukio la kipekee katika historia ya mwanadamu, yaani, ile Gharika kuu ya siku za Noa. Watu walikuwa wabaya sana hivi kwamba Yehova ‘aliumia moyoni mwake.’ Alisema: “Nitawafutilia mbali kutoka usoni pa nchi wanadamu ambao nimeumba.” (Mwanzo 6:6, 7) Naye akafanya vivyo hivyo. Yesu alilinganisha siku hizo na wakati wetu na kusema: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37.

5 Ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba Yehova anahisi kuhusu ulimwengu wa sasa kama alivyohisi kuhusu ulimwengu wa kabla ya Gharika. Kwa kuwa aliangamiza ulimwengu usiomwogopa wa siku za Noa, bila shaka ataharibu ulimwengu mwovu wa sasa. Tukielewa vizuri ufanani uliopo kati ya siku hizo na siku zetu tutaimarisha usadikisho wetu kwamba mwisho wa ulimwengu wa sasa uko karibu. Hivyo basi, ni mambo gani yanayofanana? Kuna angalau mambo matano. Kwanza, onyo kuhusu kuja kwa uharibifu linatolewa waziwazi.

Walionywa Kuhusu “Mambo Ambayo Yalikuwa Bado Hayajaonekana”

6. Yehova aliamua kufanya nini katika siku za Noa?

6 Katika siku za Noa, Yehova alisema hivi: “Roho yangu haitavumiliana sikuzote na mwanadamu kwa kuwa yeye pia ni mwili. Kwa hiyo siku zake zitakuwa miaka 120.” (Mwanzo 6:3) Kutolewa kwa amri hiyo ya Mungu katika mwaka wa 2490 K.W.K. kulionyesha kwamba mwisho wa ulimwengu huo usiomwogopa Mungu ulikuwa umeanza. Wazia kilichomaanishwa na amri hiyo kwa watu walioishi siku hizo! Ni miaka 120 tu iliyokuwa imebaki kabla ya Yehova kuleta “gharika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu za uhai ndani yao.”—Mwanzo 6:17.

7. (a) Noa aliitikiaje onyo kuhusu Gharika? (b) Tunapaswa kuitikiaje maonyo kuhusu mwisho wa mfumo huu?

7 Noa alipokea onyo kuhusu kuja kwa uharibifu huo miaka mingi mapema, naye alitumia kwa hekima muda huo kujitayarisha kwa ajili ya kuokoka. “Baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana,” asema mtume Paulo, “[Noa] alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Namna gani sisi? Miaka 90 hivi imepita tangu siku za mwisho za mfumo huu wa mambo zianze mwaka wa 1914. Hakika tunaishi katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Tunapaswa kuitikiaje maonyo ambayo tumepewa? Biblia inasema: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Sasa ndio wakati wa kufanya mapenzi ya Yehova huku tukitambua uharaka wa nyakati.

8, 9. Ni maonyo gani ambayo Yehova ametoa leo, nayo yanatangazwaje?

8 Katika nyakati zetu, wanafunzi wanyoofu wa Biblia wamejifunza katika Maandiko yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu kwamba mfumo huu utaharibiwa. Je, tunaamini hayo? Ona yale Yesu Kristo aliyosema waziwazi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Yesu alisema pia kwamba angekuja akiwa Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu naye angetenganisha watu kama vile mchungaji hutenganisha kondoo na mbuzi. Wale ambao wangepatikana hawastahili ‘wangekatiliwa mbali milele, lakini waadilifu wangeingia katika uzima wa milele.’—Mathayo 25:31-33, 46.

9 Yehova ameendelea kufanya watu wake watambue maonyo hayo kwa njia ya vikumbusho vya wakati unaofaa kupitia chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Isitoshe, kila taifa, kabila, lugha, na watu wanahimizwa ‘wamwogope Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.’ (Ufunuo 14:6, 7) Sehemu muhimu ya ujumbe wa Ufalme ambao unahubiriwa duniani pote na Mashahidi wa Yehova ni onyo kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa utawala wa kibinadamu. (Danieli 2:44) Onyo hilo linapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Mungu Mweza Yote hutimiza ahadi zake sikuzote. (Isaya 55:10, 11) Alifanya hivyo katika siku za Noa, na atafanya vivyo hivyo leo.—2 Petro 3:3-7.

Upotovu wa Kingono Waenea Sana

10. Upotovu wa kingono ulikuwa umeenea kadiri gani siku za Noa?

10 Wakati wetu unafanana na siku za Noa katika njia nyingine. Yehova alikuwa amemwamuru mwanamume na mwanamke wa kwanza ‘waijaze dunia’ na wanadamu, wakitumia kwa heshima uwezo wa kingono waliopewa na Mungu ndani ya mpango wa ndoa. (Mwanzo 1:28) Katika siku za Noa, malaika wasiotii waliwachafua wanadamu kwa ngono zisizo za asili. Walishuka duniani, wakajivika miili ya kibinadamu, wakafanya ngono na wanawake warembo, na kuzaa watoto ambao walikuwa nusu-binadamu, nusu-mashetani, yaani Wanefili. (Mwanzo 6:2, 4) Dhambi ya malaika hao wenye tamaa ya ngono inafananishwa na upotovu wa Sodoma na Gomora. (Yuda 6, 7) Hivyo, upotovu wa kingono ukaenea sana siku hizo.

11. Ni hali gani za kiadili ambazo zinafanya wakati wetu ufanane na siku za Noa?

11 Namna gani hali ya kiadili leo? Watu wengi katika siku hizi za mwisho wanajishughulisha sana na mambo ya ngono. Kuhusu watu hao, Paulo anaeleza waziwazi kwamba ‘wameishiwa na ufahamu wote wa maadili’; wengi wamejitoa wenyewe “ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.” (Waefeso 4:19) Ponografia, ngono kabla ya ndoa, kutendea watoto vibaya kingono, na ngono za watu wa jinsia moja ni mambo ambayo yameneea sana. Tayari wengine ‘wanapokea ndani yao wenyewe malipo kamili’ kwa kupata magonjwa yanayoambukizwa kupitia ngono, kuvunjika kwa familia, na matatizo mengine ya kijamii.—Waroma 1:26, 27.

12. Kwa nini tunapaswa kusitawisha chuki kwa mambo mabaya?

12 Katika siku za Noa, Yehova alileta Gharika kuu na kukomesha ulimwengu huo uliokuwa na kichaa cha ngono. Hatupaswi kamwe kusahau kwamba kwa kweli siku hizi ni kama siku za Noa. “Dhiki kuu” inayokuja itaondoa duniani ‘waasherati, wazinzi, wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, na wanaume wanaolala na wanaume.’ (Mathayo 24:21; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Ni jambo la haraka kama nini kusitawisha chuki kwa mambo mabaya na kuepuka kabisa hali zinazoweza kutuingiza katika uasherati!—Zaburi 97:10; 1 Wakorintho 6:18.

Dunia ‘Yajaa Jeuri’

13. Kwa nini dunia “ilijaa jeuri” katika siku za Noa?

13 Inapotaja hali nyingine inayofanana na ya siku za Noa, Biblia inasema: “Dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ikajaa jeuri.” (Mwanzo 6:11) Kwa kweli, jeuri haikuwa jambo jipya. Kaini, mwana wa Adamu alimuua ndugu yake aliyekuwa mwadilifu. (Mwanzo 4:8) Akionyesha roho ya jeuri ya siku hizo, Lameki alitunga shairi akijigamba kuhusu jinsi alivyomuua mwanamume mmoja kijana, kwa dai la kujitetea. (Mwanzo 4:23, 24) Kilichokuwa tofauti katika siku za Noa ni kiwango cha jeuri. Wakati wana wa Mungu wa kimalaika wasiotii walipooa wanawake duniani na kuzaa Wanefili, jeuri iliongezeka kwa kiwango kisicho na kifani. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inaonyesha kwamba neno la awali la Kiebrania linalorejelea majitu hao linamaanisha ‘Waangushaji’, yaani, “watu wenye kuwaangusha wengine.” (Mwanzo 6:4) Kwa sababu hiyo, dunia ‘ilijaa jeuri.’ (Mwanzo 6:13) Wazia matatizo ambayo lazima Noa alikabiliana nayo kulea watoto katika mazingira hayo! Hata hivyo, Noa alionekana kuwa ‘mwadilifu mbele za Yehova kati ya kizazi hicho.’—Mwanzo 7:1.

14. Leo ulimwengu ‘umejaa jeuri’ kwa kadiri gani?

14 Kumekuwa na jeuri katika historia yote ya mwanadamu. Lakini kama ilivyokuwa katika siku za Noa, wakati wetu pia umekuwa na jeuri isiyo na kifani. Mara nyingi tunasikia juu ya jeuri ya nyumbani, vitendo vya ugaidi, kampeni za maangamizi ya watu wengi, au mauaji ya watu wengi yanayofanywa na majambazi bila kusudi hususa. Isitoshe, kuna umwagikaji wa damu unaosababishwa na vita. Dunia imejaa jeuri tena. Kwa nini? Ni nini ambacho kimesababisha ongezeko hilo? Jibu linaonyesha hali nyingine inayofanana na ya siku za Noa.

15. (a) Ni nini kimefanya jeuri iongezeke siku hizi za mwisho? (b) Tunaweza kutazamia nini kwa uhakika?

15 Ufalme wa Kimasihi wa Mungu ulipoanzishwa mbinguni mwaka wa 1914, Mfalme aliyetawazwa, Yesu Kristo, alichukua hatua muhimu sana. Shetani Ibilisi na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:9-12) Kabla ya Gharika, malaika wasiotii waliacha kwa hiari makao yao mbinguni; lakini nyakati za sasa wamefukuzwa kwa nguvu. Isitoshe, sasa hawawezi kujivika miili ya kibinadamu duniani ili kufurahia anasa haramu za kimwili. Kwa hiyo, wakiwa wamekata tamaa, wenye hasira, na wenye kuogopa hukumu inayokuja, wao huchochea wanadamu na matengenezo mbalimbali kutenda uhalifu na jeuri ya kinyama na ya kiwango kikubwa hata zaidi kuliko ile ya siku za Noa. Yehova aliufutilia mbali ulimwengu wa kabla ya Gharika baada ya malaika wasiotii na wazao wao kujaza uovu duniani. Uwe na hakika kwamba atafanya vivyo hivyo katika siku zetu! (Zaburi 37:10) Hata hivyo, leo wale wanaolinda wanajua kwamba ukombozi wao uko karibu.

Ujumbe Unahubiriwa

16, 17. Ni ufanani gani wa nne uliopo kati ya siku za Noa na siku zetu?

16 Jambo la nne linaloonyesha ufanani kati ya siku zetu na za kabla ya Gharika linaonekana katika kazi ambayo Noa aliagizwa kufanya. Noa alijenga safina kubwa. Pia alikuwa “mhubiri.” (2 Petro 2:5) Alihubiri ujumbe gani? Yaonekana katika mahubiri yake Noa aliwasihi watu watubu na kuwaonya kuhusu uharibifu uliokuwa unakuja. Yesu alisema kwamba watu wa siku za Noa “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.

17 Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova wanapofanya kwa bidii kazi yao ya kuhubiri, ujumbe wa Ufalme wa Mungu unahubiriwa duniani pote. Karibu kila mahali duniani watu wanaweza kusikia na kusoma ujumbe wa Ufalme katika lugha yao wenyewe. Nakala zaidi ya 25,000,000 za Mnara wa Mlinzi, unaotangaza Ufalme wa Yehova, huchapishwa katika lugha zaidi ya 140. Kwa kweli, habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” Bila shaka, mwisho utakuja Mungu atakaporidhika kwamba kazi hiyo imekamilika.—Mathayo 24:14.

18. Itikio la wengi kwa kazi yetu ya kuhubiri linafananaje na la watu wengi katika siku za Noa?

18 Kwa kufikiria hali ya kutopendezwa kabisa na mambo ya kiroho na ukosefu wa maadili kabla ya Gharika, tunaweza kuelewa ni kwa nini familia ya Noa ilichekelewa, ikatukanwa, na kudhihakiwa na majirani wasioamini. Hata hivyo, mwisho ulikuja. Vivyo hivyo, “wadhihaki na dhihaka zao” wamekuwa wengi siku hizi za mwisho. “Lakini siku ya Yehova itakuja kama mwizi,” Biblia inasema. (2 Petro 3:3, 4, 10) Na bila shaka itakuja wakati uliowekwa. Haitachelewa. (Habakuki 2:3) Ni jambo la hekima kama nini kuwa wenye kulinda!

Wachache Tu Ndio Wanaookoka

19, 20. Tunaweza kuona ufanani gani kati ya Gharika na uharibifu wa mfumo huu wa mambo?

19 Ufanani kati ya siku za Noa na siku zetu hauhusu tu uovu wa watu na kuharibiwa kwao. Kama vile kulivyokuwa na watu waliookoka Gharika, pia kutakuwa na watu watakaookoka mwisho wa mfumo huu wa mambo. Watu waliookoka Gharika walikuwa wanyenyekevu na maisha yao yalikuwa tofauti na ya watu wengine kwa ujumla. Walitii onyo la Mungu na wakajitenga na ulimwengu mwovu wa wakati huo. Biblia inasema, ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova.’ Naye “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.” (Mwanzo 6:8, 9) Kati ya wanadamu wote, familia moja, “watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Naye Yehova Mungu aliwaamuru hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.”—Mwanzo 9:1.

20 Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba ‘umati mkubwa utatoka katika ile dhiki kuu.’ (Ufunuo 7:9, 14) Umati mkubwa utakuwa na watu wangapi? Yesu mwenyewe alisema: “Lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Kwa kulinganishwa na mabilioni ya watu wanaoishi duniani sasa, waokokaji wa dhiki kuu inayokuja watakuwa wachache. Lakini huenda wakawa na pendeleo kama lile la waokokaji wa Gharika. Huenda waokokaji hao wakaruhusiwa kuzaa watoto kwa muda fulani ambao watakuwa sehemu ya jamii mpya ya kidunia.—Isaya 65:23.

“Endeleeni Kukesha”

21, 22. (a) Umenufaikaje kwa kuchunguza masimulizi kuhusu Gharika? (b) Andiko la mwaka wa 2004 ni gani, na kwa nini tunapaswa kutii shauri la andiko hilo?

21 Ingawa Gharika inaonekana kana kwamba haihusiani na wakati wetu, kwa wazi inatoa onyo tusilopaswa kupuuza. (Waroma 15:4) Mambo yanayofanana kati ya siku za Noa na siku zetu yanapaswa kufanya tutambue umuhimu wa matukio ya sasa na kufanya tuwe macho kuhusu kuja kwa Yesu kama mwizi ili kutekeleza hukumu juu ya waovu.

22 Leo, Yesu Kristo anaongoza kazi kubwa sana ya ujenzi wa kiroho. Waabudu wa kweli wanaokolewa na kupata usalama katika paradiso ya kiroho iliyo kama safina. (2 Wakorintho 12:3, 4) Ili kuhifadhiwa wakati wa dhiki hiyo kuu, ni lazima tubaki katika paradiso hiyo. Nje ya paradiso hiyo ya kiroho kuna ulimwengu wa Shetani ambao uko tayari kummeza yeyote anayesinzia kiroho. Kwa hiyo, ni muhimu kwamba ‘tuendelee kukesha’ na kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova.—Mathayo 24:42, 44.

Je, Unakumbuka?

• Yesu alitoa shauri gani kuhusu kuja kwake?

• Yesu analinganisha kuwapo kwake na kipindi gani?

• Nyakati zetu zinafananaje na siku za Noa?

• Kutafakari ufanani uliopo kati ya siku za Noa na siku zetu kunapaswa kuwa na matokeo gani juu ya kutambua kwetu uharaka wa nyakati?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 18]

Andiko la mwaka wa 2004 litakuwa: “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari.”—Mathayo 24:42, 44.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Noa alitii onyo la Mungu. Je, sisi tunaitikia vivyo hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 16, 17 ]

“Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa”