Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujifunza Kutoka kwa Familia ya Kibinadamu ya Yesu

Kujifunza Kutoka kwa Familia ya Kibinadamu ya Yesu

Kujifunza Kutoka kwa Familia ya Kibinadamu ya Yesu

UNAJUA nini kuhusu watu wa familia ya karibu ya Yesu, ambao aliishi nao duniani kwa miaka ya kwanza 30 hadi alipobatizwa? Vitabu vya Injili hutuambia nini? Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza familia yake? Majibu ya maswali hayo yanaweza kukunufaisha.

Je, Yesu alizaliwa katika familia tajiri? Yosefu, baba yake mlezi, alikuwa seremala. Kazi hiyo ilihitaji nguvu nyingi, na mara nyingi ilihusisha kukata miti ili kupata mbao. Wazazi wa kibinadamu wa Yesu walipoenda Yerusalemu siku 40 hivi baada ya kuzaliwa kwake, walitoa dhabihu kama Sheria ilivyoamuru. Je, walitoa kondoo-dume pamoja na njiwa-tetere au hua kama Sheria ilivyoamuru? La. Inaonekana kwamba hawangeweza kupata dhabihu hizo. Hata hivyo, Sheria ilikuwa na mpango kwa ajili ya maskini. Kulingana na mpango huo, Yosefu na Maria walitoa “njiwa-tetere wawili au hua wachanga wawili.” Kwa kuwa walitoa wanyama wasio ghali, hilo linaonyesha kwamba familia hiyo ilikuwa maskini.—Luka 2:22-24; Mambo ya Walawi 12:6, 8.

Unaweza kuona kwamba Yesu Kristo, Mtawala wa wakati ujao wa wanadamu, alizaliwa katika familia ya hali ya chini, ambayo ilihitaji kujitahidi sana ili kupata riziki. Alipokuwa mtu mzima, Yesu alikuwa seremala kama baba yake mlezi. (Mathayo 13:55; Marko 6:3) “Ingawa [Yesu] alikuwa tajiri” alipokuwa kiumbe wa roho mwenye nguvu mbinguni, Biblia inasema kwamba “alikuja kuwa maskini” kwa ajili yetu. Alijishusha akawa binadamu na akakulia katika familia ya kawaida. (2 Wakorintho 8:9; Wafilipi 2:5-9; Waebrania 2:9) Yesu hakuzaliwa katika familia tajiri, na huenda jambo hilo lilifanya wengi wajihisi huru kumkaribia. Cheo chake hakikufanya wamwogope. Walimthamini kwa sababu ya mafundisho yake, sifa zake zenye kuvutia, na miujiza yake. (Mathayo 7:28, 29; 9:19-33; 11:28, 29) Tunaweza kuona hekima ya Yehova Mungu kwa kuruhusu Yesu azaliwe katika familia ya kawaida.

Sasa na tuchunguze watu wa familia ya Yesu na kuona mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwao.

Yosefu Alikuwa Mtu Mwadilifu

Yosefu alipotambua kwamba mchumba wake alikuwa na mimba “kabla ya wao kuungana pamoja,” bila shaka, ilikuwa vigumu sana kwake kuchagua kati ya upendo wake kwa Maria na chuki yake kwa tendo ambalo lingedhaniwa kuwa uasherati. Aliona hali hiyo yote kuwa inaingilia haki yake ya kuwa mume wa Maria. Siku hizo, mwanamke aliyechumbiwa alionwa kana kwamba ameolewa. Baada ya kufikiria jambo hilo kwa uzito, Yosefu aliamua kumtaliki Maria kisiri ili Maria asipigwe mawe kama mzinzi.—Mathayo 1:18; Kumbukumbu la Torati 22:23, 24.

Ndipo malaika akamtokea Yosefu katika ndoto na kusema: “Usiogope kumchukua Maria mke wako na kwenda naye nyumbani, kwa maana mimba iliyo ndani yake imetokana na roho takatifu. Yeye atazaa mwana, nawe lazima umwite jina lake Yesu, kwa maana ataokoa watu wake kutoka katika dhambi zao.” Baada ya kupokea mwongozo huo wa Mungu, Yosefu alitii, akamchukua Maria na kwenda naye nyumbani kwake.—Mathayo 1:20-24.

Kwa kuamua hivyo, mtu huyo mwadilifu na mwaminifu alihusika katika kutimizwa kwa maneno haya ambayo Yehova alisema kupitia nabii Isaya: “Tazama! Mwanamwali kwa kweli atapata mimba, naye atazaa mwana, naye hakika atamwita jina lake Imanueli.” (Isaya 7:14) Bila shaka, Yosefu alikuwa mtu wa kiroho ambaye alithamini pendeleo la kuwa baba mlezi wa Masihi, ingawa mwana huyo wa kwanza wa Maria hakuwa mtoto wake.

Yosefu hakufanya ngono na Maria mpaka alipomzaa mwana wake. (Mathayo 1:25) Haikuwa rahisi kwa Yosefu na Maria ambao walikuwa wameoana karibuni kutokuwa na uhusiano wa kingono, lakini yaonekana hawakutaka hali yoyote yenye kutatanisha itokee kuhusu Baba ya mtoto huyo. Hicho ni kielelezo kizuri kama nini cha kujizuia! Yosefu alitanguliza mambo ya kiroho badala ya tamaa zake za asili.

Katika pindi nne mbalimbali, Yosefu alipokea mwongozo wa kimalaika kuhusu kumlea mwana huyo akiwa baba mlezi. Mitatu kati ya miongozo hiyo ilihusu mahali pa kumlelea mvulana huyo. Ilikuwa muhimu kutii mara moja ili kuokoa uhai wa mtoto huyo. Katika pindi zote hizo, Yosefu alichukua hatua mara moja, na kwanza akampeleka mtoto huyo mchanga Misri, kisha akamrudisha Israeli. Utii wa Yosefu ulimlinda Yesu asiuawe wakati Herode alipoagiza watoto wa kiume wauawe. Pia, utii huo ulifanya unabii mbalimbali kuhusu Masihi utimizwe.—Mathayo 2:13-23.

Yosefu alimfunza Yesu kazi ambayo ingeweza kumsaidia kujitegemeza. Kwa hiyo, Yesu hakuitwa tu “mwana wa yule seremala” bali pia “yule seremala.” (Mathayo 13:55; Marko 6:3) Mtume Paulo aliandika kwamba Yesu ‘alijaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe.’ Kwa kawaida jambo hilo lingetia ndani kufanya kazi kwa bidii ili kuitegemeza familia.—Waebrania 4:15.

Mwishowe, katika masimulizi ya mwisho kumhusu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunaona uthibitisho kwamba Yosefu alijitoa kwa ajili ya ibada ya kweli. Yosefu aliipeleka familia yake Yerusalemu kwa ajili ya Pasaka. Wanaume tu ndio waliotakiwa kuhudhuria, lakini ilikuwa desturi ya Yosefu kwenda Yerusalemu pamoja na familia yake “mwaka baada ya mwaka.” Alijidhabihu sana, kwa kuwa iliwabidi kutembea kilometa 100 hivi kutoka Nazareti hadi Yerusalemu. Hata hivyo, katika pindi inayotajwa katika Maandiko, Yesu aliachwa na kikundi cha watu aliokuwa akisafiri nao. Alipatikana hekaluni akiwasikiliza na kuwauliza maswali walimu wa Sheria. Ingawa Yesu alikuwa na umri wa miaka 12 tu, alikuwa na hekima na ujuzi mwingi wa Neno la Mungu. Kutokana na tukio hilo, tunaona kwamba ni lazima wazazi wa Yesu wawe walimfundisha vizuri na kumlea kuwa mvulana wa kiroho. (Luka 2:41-50) Yaonekana Yosefu alikufa muda fulani baada ya hapo kwa kuwa hatajwi tena katika Maandiko.

Naam, Yosefu alikuwa mtu mwadilifu aliyeitunza familia yake vizuri kiroho na kimwili. Je, unamwiga Yosefu kwa kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwako unapotambua mapenzi ya Mungu kwetu leo? (1 Timotheo 2:4, 5) Je, unatii yale ambayo Mungu anasema katika Neno lake, na hivyo kuonyesha ujitiisho kama wa Yosefu? Je, unawafundisha watoto wako ili waweze kuzungumza na wengine mambo ya kiroho yanayofaa?

Maria Alikuwa Mtumishi wa Mungu Asiye na Ubinafsi

Maria, mama ya Yesu alikuwa mtumishi mzuri sana wa Mungu. Malaika Gabrieli alipotangaza kwamba angezaa, yeye alishangaa. Maria alikuwa bikira kwa kuwa ‘hakuwa amelala na mwanamume.’ Alipotambua kwamba angezaa kwa nguvu ya roho takatifu, alikubali ujumbe huo kwa unyenyekevu na kusema: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:30-38) Alithamini sana pendeleo hilo la kiroho hivi kwamba alikuwa tayari kukabili magumu yoyote ambayo yangetokana na uamuzi wake.

Kwa kweli, kukubali mgawo huo kulibadili maisha yake yote akiwa mwanamke. Alipoenda Yerusalemu ili akatakaswe, mzee mmoja mwenye kumheshimu Mungu aliyeitwa Simeoni alimwambia hivi: “Upanga mrefu utaichoma nafsi yako.” (Luka 2:25-35) Yaonekana, alikuwa anazungumzia jinsi ambavyo Maria angehisi kumwona Yesu akikataliwa na wengi na mwishowe kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso.

Yesu alipoendelea kukua, Maria aliyaweka akilini mambo yaliyotukia katika maisha ya Yesu, “akikata kauli moyoni mwake.” (Luka 2:19, 51) Kama Yosefu, Maria alikuwa mtu wa kiroho naye aliyahifadhi moyoni matukio na matamko yaliyotimiza unabii. Bila shaka, mambo ambayo malaika Gabrieli alimwambia yalibaki akilini mwake: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Naam, alichukua kwa uzito pendeleo la kuwa mama wa kibinadamu wa Masihi.

Hali ya kiroho ya Maria ilidhihirika tena wakati alipokutana na Elisabeti, mtu wa ukoo wake ambaye pia alikuwa amechukua mimba kimuujiza. Alipomwona, Maria alimtukuza Yehova na kuonyesha jinsi alivyolipenda Neno la Mungu. Aligusia sala ya Hana inayopatikana katika 1 Samweli sura ya 2 na kutaja pia mambo fulani katika vitabu vingine vya Maandiko ya Kiebrania. Ujuzi huo wa Maandiko ulionyesha kwamba alikuwa na sifa za kustahili kuwa mama mwenye kujitoa aliyemwogopa Mungu. Angeshirikiana na Yosefu kumlea mwana wake kiroho.—Mwanzo 30:13; 1 Samweli 2:1-10; Malaki 3:12; Luka 1:46-55.

Maria aliamini kabisa kwamba mwana wake alikuwa Masihi, na imani yake haikufifia hata baada ya Yesu kufa. Muda mfupi baada ya Yesu kufufuliwa, Maria alikuwa kati ya wanafunzi waaminifu waliokutanika pamoja na mitume ili kusali. (Matendo 1:13, 14) Alidumisha uaminifu wake hata ingawa alipatwa na maumivu makali kumwona mwana wake mpendwa akifa kwenye mti wa mateso.

Unaweza kunufaikaje kwa kujifunza juu ya maisha ya Maria? Je, unakubali pendeleo la kumtumikia Mungu bila kujali ni mambo mangapi utakayodhabihu? Je, unafikiria uzito wa pendeleo hilo leo? Je, unayaweka akilini mambo yaliyotabiriwa na Yesu na kuyalinganisha na yale yanayotukia sasa, ‘ukikata kauli moyoni mwako’? (Mathayo sura ya 24 na 25; Marko sura ya 13; Luka sura ya 21) Je, unamwiga Maria kwa kuwa na ujuzi wa Neno la Mungu na kulitumia mara nyingi katika mazungumzo yako? Je, utadumisha imani yako katika Yesu japo maumivu makali ya akili ambayo huenda yakakupata kwa sababu ya kuwa mfuasi wake?

Ndugu za Yesu Walibadilika

Inaonekana kwamba ndugu za Yesu walianza kumwamini baada ya kifo chake. Yaonekana hiyo ndiyo sababu hawakuwepo alipokufa kwenye mti wa mateso, hivyo ikambidi amkabidhi mama yake kwa mtume Yohana. Watu wa ukoo wa Yesu hawakumheshimu, hata pindi moja walisema kwamba “amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Kwa kuwa Yesu alikuwa na watu wa familia wasioamini, leo wale ambao watu wao wa familia si waamini wanaweza kuwa na hakika kwamba Yesu anaelewa jinsi wanavyohisi wanapodhihakiwa na watu wa ukoo kwa ajili ya imani yao.

Hata hivyo, inaonekana baada ya ufufuo wa Yesu, ndugu zake walianza kumwamini. Walikuwa kati ya kikundi cha watu waliokusanyika Yerusalemu kabla ya Pentekoste ya 33 W.K. na kusali kwa bidii pamoja na mitume. (Matendo 1:14) Ni wazi kwamba ufufuo wa ndugu yao wa kambo uliwachochea kubadili moyo na kuwa wanafunzi wake. Hatupaswi kamwe kukata tumaini kuhusu watu wa ukoo wasiokubali imani yetu.

Kulingana na Maandiko, Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu ambaye Yesu alimtokea kibinafsi, alitimiza daraka kubwa katika kutaniko la Kikristo. Aliwaandikia Wakristo wenzake barua kwa mwongozo wa roho ya Mungu, akiwashauri wadumishe imani yao. (Matendo 15:6-29; 1 Wakorintho 15:7; Wagalatia 1:18, 19; 2:9; Yakobo 1:1) Yuda, ndugu mwingine wa kambo wa Yesu, aliandika barua kwa mwongozo wa roho ili kuwatia moyo waamini wenzake wafanye pigano kali kwa ajili ya imani. (Yuda 1) Ni muhimu kuona kwamba Yakobo na Yuda hawakujaribu kuwasadikisha Wakristo wenzao kwa kuonyesha katika barua zao kwamba walikuwa na mamlaka kwa sababu ya uhusiano wao wa kiukoo na Yesu. Tunajifunza somo lililoje kutoka kwao kuhusu sifa ya kiasi!

Kwa hiyo, tunajifunza nini kutoka kwa familia ya Yesu? Bila shaka, tunajifunza mambo yanayohusu ujitoaji ambayo yanaweza kuonyeshwa katika njia kama hizi: (1) Jitiishe kwa uaminifu kwa mapenzi ya Mungu na kukabiliana na majaribu yanayotokana na kufanya hivyo. (2) Tanguliza mambo ya kiroho hata kama kufanya hivyo kunamaanisha kudhabihu mambo fulani. (3) Walee watoto wako kupatana na Maandiko. (4) Usikate tumaini kuhusu watu wa familia wasiokubali imani yako. (5) Usijigambe kuhusu uhusiano wowote ambao huenda ukawa nao pamoja na ndugu wenye madaraka katika kutaniko la Kikristo. Naam, kujifunza juu ya familia ya Yesu ya kibinadamu hufanya tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye na kuthamini zaidi kwamba Yehova alichagua familia ya kawaida kumlea Yesu alipokuwa mtoto.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Yosefu alimchukua Maria kuwa mke wake na akahusika katika kutimizwa kwa unabii mbalimbali kumhusu Masihi

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yosefu na Maria waliwafunza watoto wao mambo ya kiroho na umuhimu wa kufanya kazi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ingawa ndugu za Yesu walilelewa katika familia ya kiroho, walimwamini baada ya kifo chake

[Picha katika ukurasa wa 8]

Yakobo na Yuda, ndugu za kambo wa Yesu waliwatia moyo Wakristo wenzao