Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova

Uwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova

Uwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova

“Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—MATHAYO 24:44.

1. Kwa nini tuifikirie siku ya Yehova?

ITAKUWA siku ya pigano na ghadhabu, ya taabu na maumivu makali, ya giza na ukiwa. Hapana shaka kwamba ‘siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha’ itakuja juu ya mfumo huu mwovu wa mambo, kama vile Gharika ilivyowaangamiza waovu katika siku za Noa. Haitakosa kuja. Hata hivyo, “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.” (Yoeli 2:30-32; Amosi 5:18-20) Mungu ataharibu maadui wake na kuwaokoa watu wake. Kwa kutambua uharaka wa nyakati, nabii Sefania anasema: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) Hata hivyo, hukumu hiyo ya Mungu itatekelezwa wakati gani?

2, 3. Kwa nini ni muhimu tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

2 Yesu alisema: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:36) Kwa kuwa hatujui wakati barabara, ni muhimu tutii maneno ya andiko la mwaka wa 2004: “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari.”—Mathayo 24:42, 44.

3 Akionyesha jinsi wale walio tayari watakavyokusanywa haraka mahali penye usalama huku wengine wakiachwa, Yesu alisema: “Watu wawili watakuwa shambani: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa; wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe la kusagia: mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.” (Mathayo 24:40, 41) Hali yetu binafsi itakuwaje wakati huo muhimu? Je, tutakuwa tayari, au siku hiyo itatupata ghafula? Mengi yanategemea hatua tunazochukua sasa. Ili tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova tunahitaji kuepuka mtazamo fulani ambao umeenea sana leo, tukatae kujiingiza katika hali fulani ya kiroho, na kuepuka mitindo fulani ya maisha.

Epuka Mtazamo wa Kutojali

4. Watu wa siku za Noa walikuwa na mtazamo gani?

4 Fikiria siku za Noa. Biblia inasema: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Safina ingekuwa kitu kisicho cha kawaida na chenye kuonekana waziwazi. Isitoshe, Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Watu wa siku za Noa hawakubadili mwenendo wao hata walipohubiriwa na kuona safina ikijengwa. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa.” Watu ambao Noa alihubiria walijishughulisha sana na mambo ya kibinafsi na anasa hivi kwamba “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.

5. Wakaaji wa Sodoma katika siku za Loti walikuwa na maoni gani?

5 Hali ilikuwa vivyo hivyo katika siku za Loti. Maandiko yanatuambia: “Walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, walikuwa wakijenga. Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote.” (Luka 17:28, 29) Baada ya malaika kumwonya Loti kuhusu uharibifu uliokuwa unakaribia, Loti alizungumza na wakwe zake kuhusu yale ambayo yangetokea. Lakini, machoni pao “alionekana kama mtu aliyekuwa anafanya mzaha.”—Mwanzo 19:14.

6. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani?

6 Kama ilivyokuwa katika siku za Noa na Loti “ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu” kutakavyokuwa, akasema Yesu. (Mathayo 24:39; Luka 17:30) Kwa kweli, watu wengi leo wana mtazamo wa kutojali. Ni lazima tujihadhari tusiathiriwe na mtazamo kama huo. Hakuna ubaya kufurahia chakula na kinywaji kizuri kwa kiasi. Vivyo hivyo, ndoa ni mpango wa Mungu. Hata hivyo, ikiwa mambo hayo yamekuwa muhimu zaidi maishani mwetu na hivyo kutufanya tupuuze mambo ya kiroho, je, kweli tuko tayari kwa ajili ya siku ya Yehova yenye kuogopesha?

7. Ni swali gani muhimu tunalopaswa kujiuliza kabla ya kuchukua hatua fulani, na kwa nini?

7 “Wakati uliobaki umepungua,” akasema mtume Paulo. “Tangu sasa wale walio na wake na wawe kana kwamba hawana.” (1 Wakorintho 7:29-31) Ni wakati mchache tu unaobaki ili tumalize kazi tuliyopewa na Mungu ya kuhubiri juu ya Ufalme. (Mathayo 24:14) Paulo anawashauri hata watu waliofunga ndoa wasijishughulishe sana na wenzi wao na hivyo kutotanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao. Bila shaka, mtazamo wa kiakili ambao Paulo alipendekeza ni kinyume na ule wa kutojali. Yesu alisema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” (Mathayo 6:33) Unapofanya uamuzi wowote au kabla ya kuchukua hatua fulani, unapaswa kujiuliza swali hili, ‘Jambo hili litanizuia nisitangulize Ufalme maishani mwangu katika njia gani?’

8. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahangaikia sana mambo ya kawaida maishani?

8 Namna gani tukitambua kwamba tayari tunahangaikia sana mambo ya kawaida maishani, hivi kwamba hatupati nafasi kwa ajili ya mambo ya kiroho? Je, kuna tofauti kati ya mtindo wetu wa maisha na ule wa majirani ambao hawana ujuzi sahihi wa Maandiko na si watangazaji wa Ufalme? Ikiwa hakuna tofauti yoyote, basi tunahitaji kusali kuhusu jambo hilo. Yehova anaweza kutusaidia kuwa na mtazamo unaofaa wa akili. (Waroma 15:5; Wafilipi 3:15) Anaweza kutusaidia kutanguliza mambo yanayohusu Ufalme, kufanya yaliyo sawa, na kutimiza wajibu wetu kwake.—Waroma 12:2; 2 Wakorintho 13:7.

Epuka Kusinzia Kiroho

9. Kulingana na andiko la Ufunuo 16:14-16, kwa nini ni muhimu kuepuka kusinzia kiroho?

9 Ule unabii unaotaja ‘vita ya siku kuu ya Mungu Mweza-Yote’ inayokuja kwenye Har-Magedoni, unaonya kwamba huenda wengine wasiendelee kukesha. “Tazama! Ninakuja kama mwizi,” Bwana Yesu Kristo anasema. “Mwenye furaha ni yule anayekaa macho na kutunza mavazi yake ya nje, ili asipate kutembea akiwa uchi na watu waitazame aibu yake.” (Ufunuo 16:14-16) Mavazi ya nje yanayotajwa hapa yanamaanisha mambo yanayotutambulisha kuwa Mashahidi wa Kikristo wa Yehova. Hayo yanatia ndani kazi yetu tukiwa watangazaji wa Ufalme na pia mwenendo wetu wa Kikristo. Tukijikuta katika hali ya kutotenda, huenda tukavuliwa mavazi yetu yanayotutambulisha kuwa Wakristo. Hilo ni jambo lenye aibu na hatari. Lazima tuepuke kusinzia na kuchoka kiroho. Tunawezaje kuepuka mwelekeo huo?

10. Kwa nini kusoma Biblia kila siku hutusaidia tubaki macho kiroho?

10 Biblia hukazia mara kwa mara uhitaji wa kuendelea kukesha na kutunza akili zetu. Kwa mfano, masimulizi ya Injili hutukumbusha hivi: “Endeleeni kukesha” (Mathayo 24:42; 25:13; Marko 13:35, 37); “iweni tayari” (Mathayo 24:44); “endeleeni kutazama, endeleeni kukesha,” (Marko 13:33); “endeleeni kuwa tayari” (Luka 12:40). Baada ya kusema kwamba siku ya Yehova itakuja bila kutazamiwa juu ya ulimwengu huu, mtume Paulo anawahimiza waamini wenzake hivi: “Basi, na tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali na tukae macho na kutunza akili zetu.” (1 Wathesalonike 5:6) Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Yesu Kristo aliyetukuzwa anakazia jinsi atakavyokuja kwa ghafula, anaposema: “Mimi ninakuja upesi.” (Ufunuo 3:11; 22:7, 12, 20) Manabii wengi Waebrania walieleza na kuonya pia kuhusu siku kuu ya Yehova ya hukumu. (Isaya 2:12, 17; Yeremia 30:7; Yoeli 2:11; Sefania 3:8) Kusoma Neno la Mungu, Biblia, kila siku na kutafakari mambo tunayosoma kutatusaidia sana kubaki macho kiroho.

11. Kwa nini funzo la Biblia la kibinafsi ni muhimu ili kuendelea kulinda kiroho?

11 Kwa kweli, kujifunza Maandiko kibinafsi kwa bidii tukitumia vichapo vinavyozungumzia Biblia ambavyo huandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kutatuchochea kuendelea kulinda. (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, funzo la kibinafsi hunufaisha tu linapofanywa kwa kuendelea na kwa ukawaida. (Waebrania 5:14–6:3) Tunapaswa kula chakula kigumu cha kiroho kwa ukawaida. Huenda leo ikawa vigumu kupata wakati wa kujifunza. (Waefeso 5:15, 16) Hata hivyo, kusoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia wakati tu tuna nafasi hakutoshi. Funzo la kibinafsi la ukawaida ni muhimu ili tubaki wenye “afya katika imani” na kuendelea kukesha.—Tito 1:13.

12. Mikutano ya Kikristo na makusanyiko hutusaidiaje kupambana ili tusisinzie kiroho?

12 Mikutano ya Kikristo na makusanyiko hutusaidia pia kupambana ili tusisinzie kiroho. Jinsi gani? Kupitia maagizo tunayopokea. Kwenye mikutano hiyo tunakumbushwa kwa ukawaida kuhusu kukaribia kwa siku ya Yehova. Mikutano ya Kikristo ya kila juma hutupa pia nafasi za “kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” Kuchochewa huko hutusaidia tuendelee kuwa macho kiroho. Kwa hiyo, haishangazi kwamba tunaamriwa kukutana kwa ukawaida ‘kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’—Waebrania 10:24, 25.

13. Huduma ya Kikristo hutusaidiaje kuendelea kukesha kiroho?

13 Tunasaidiwa pia kuwa macho tunaposhiriki kwa moyo wote katika huduma ya Kikristo. Njia bora zaidi ya kutambua ishara za nyakati na maana yake ni kuzungumza na wengine kuhusu habari hiyo. Na tunapoona wale tunaojifunza Biblia pamoja nao wakifanya maendeleo na kuanza kutenda kulingana na yale wanayojifunza, kutambua kwetu uharaka wa nyakati kunaongezeka. “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji,” akasema mtume Petro, “tunzeni akili zenu kikamili.” (1 Petro 1:13) Njia bora ya kuepuka uchovu wa kiroho ni ‘sikuzote kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58.

Epuka Mitindo ya Maisha Yenye Kudhuru Kiroho

14. Kama inavyoelezwa katika Luka 21:34-36, Yesu anatoa onyo gani kuhusu mitindo fulani ya maisha?

14 Katika unabii wake muhimu kuhusu ishara ya kuwapo kwake, Yesu alitoa onyo lingine. Alisema: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Yesu alieleza kwa usahihi mitindo ya maisha ambayo watu kwa ujumla wangefuatia: kula kupita kiasi, ulevi, na maisha yanayoleta mahangaiko.

15. Kwa nini tunapaswa kuepuka kula na kunywa kupita kiasi?

15 Kula kupita kiasi na kunywa sana hakupatani na kanuni za Biblia na kwapaswa kuepukwa. Biblia inasema: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi.” (Methali 23:20) Hata hivyo, si lazima mtu ale au anywe kupita kiasi ili kuhatarisha hali yake ya kiroho. Kula na kunywa kunaweza kufanya mtu asinzie na awe mvivu hata kabla ya kuwa mlafi na mlevi. “Mvivu anajionyesha kutamani,” inasema methali ya Biblia, “lakini nafsi yake haina chochote.” (Methali 13:4) Mtu kama huyo anaweza kutaka kufanya mapenzi ya Mungu, lakini hawezi kutimiza tamaa yake kwa sababu ya uzembe.

16. Tunawezaje kuepuka kulemewa na mahangaiko kuhusu familia zetu?

16 Yesu alionya kuhusu mahangaiko gani ya maisha? Hayo yanatia ndani mahangaiko ya kibinafsi, kuiandalia familia mahitaji yake, na kadhalika. Si jambo la hekima kuacha mambo hayo yatulemee. Yesu aliuliza: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” Aliwashauri hivi wasikilizaji wake: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” Kutanguliza mambo yanayohusu Ufalme maishani mwetu na kuwa na hakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu kutatuepusha na mahangaiko na kutusaidia kuendelea kukesha.—Mathayo 6:25-34.

17. Kufuatia vitu vya kimwili kunawezaje kuleta mahangaiko?

17 Mahangaiko yanaweza pia kusababishwa na kufuatia vitu vya kimwili. Kwa mfano, watu fulani hufanya maisha yao yawe magumu kwa kununua vitu wasivyoweza kugharimia. Wengine wameshawishiwa na mipango inayokusudiwa kufanya mtu atajirike haraka na pia vitega-uchumi ambavyo ni hatari. Nao wengine, hunaswa katika mtego wa kufuatia elimu ili wafanikiwe kifedha. Ni kweli kwamba, kiwango fulani cha elimu kinaweza kumsaidia mtu kupata kazi. Hata hivyo, ukweli ni kwamba wengine wamepatwa na madhara ya kiroho kwa kutumia wakati mwingi wakifuatia elimu ya juu. Ni hatari sana kujikuta katika hali hiyo siku ya Yehova inapokaribia. Biblia inatoa onyo hili: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.”—1 Timotheo 6:9.

18. Tunapaswa kusitawisha uwezo gani ili tusishawishiwe kufuatia vitu vya kimwili?

18 Jambo muhimu linaloweza kutuzuia tusishawishiwe kufuatia vitu vya kimwili ni kusitawisha uwezo wa kupambanua yaliyo sawa na yaliyo makosa tunapofanya maamuzi. Tunasitawisha uwezo huo kwa kula kwa ukawaida ‘chakula kigumu cha kiroho cha watu wakomavu,’ na kwa ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu kwa kuzitumia.’ (Waebrania 5:13, 14) Kuhakikisha “mambo yaliyo ya maana zaidi” tunapopanga mambo ya kutangulizwa kutatulinda pia tusifanye maamuzi mabaya.—Wafilipi 1:10.

19. Tunapaswa kufanya nini tunapotambua kwamba hatuna wakati wa kutosha kufuatia mambo ya kiroho?

19 Maisha ya kufuatia vitu vya kimwili yanaweza kutupofusha na kufanya tusiwe na wakati wa kutosha au tukose kabisa wakati wa kufuatia mambo ya kiroho. Tunawezaje kujichunguza na kuepuka kunaswa na maisha kama hayo? Tunahitaji kufikiria kwa sala ni kwa njia gani na kadiri gani tunaweza kufanya maisha yetu yawe rahisi. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Usingizi wa mtumishi ni mtamu, bila kujali kama anakula kidogo au kingi; lakini wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.” (Mhubiri 5:12) Je, tunatumia nguvu na wakati mwingi kutunza vitu vya kimwili visivyo vya lazima? Kadiri tunavyokuwa na vitu vingi, ndivyo tunavyotumia pesa nyingi kuvitunza, kuvilipia bima, na kuvilinda. Je, tunaweza kunufaika kwa kufanya maisha yetu yawe rahisi kwa kuondoa vitu fulani?

Hakikisha Kwamba Uko Tayari

20, 21. (a) Mtume Petro anatoa uhakikisho gani kuhusu siku ya Yehova? (b) Ni matendo na vitendo gani tunavyopaswa kuendelea kufanya huku tukiwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

20 Ulimwengu wa siku za Noa ulifikia mwisho wake, nao mfumo huu wa mambo pia utafikia mwisho. Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi, ambayo katika hiyo mbingu zitapitilia mbali kwa kelele ya kuvuma, lakini vitu vyake vya msingi vikiwa moto sana vitayeyushwa, na dunia na kazi zilizo ndani yake zitafunuliwa.” Mbingu za mfano, yaani serikali mbovu, na dunia ya mfano, yaani wanadamu waliotengwa na Mungu, havitaokoka hasira kali ya Mungu inayowaka. Akionyesha jinsi tunavyoweza kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo, Petro anasema: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!”—2 Petro 3:10-12.

21 Baadhi ya matendo na vitendo vya ujitoaji kimungu ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kushiriki katika kuhubiri habari njema. Na tufanye mambo hayo kwa kujitoa kwa Mungu kwa moyo wote huku tukisubiri siku kuu ya Yehova. Acheni ‘tufanye yote tuwezayo ili mwishowe Mungu atupate tukiwa bila doa na bila dosari na tukiwa katika amani.’—2 Petro 3:14.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

• Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahangaikia sana mambo ya kawaida maishani?

• Ni nini kitakachotusaidia tuepuke kusinzia kiroho?

• Ni mitindo gani ya maisha yenye kudhuru tunayopaswa kuepuka, na jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Watu wa siku za Noa hawakujali hukumu iliyokuwa inakaribia. Je, wewe unajali?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unaweza kufanya maisha yako yawe rahisi ili upate wakati zaidi wa kufuatia mambo ya kiroho?