Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Kutoka Katika Kitabu cha Mwanzo—I

Mambo Makuu Kutoka Katika Kitabu cha Mwanzo—I

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Kutoka Katika Kitabu cha Mwanzo—I

NENO “mwanzo” linamaanisha “chimbuko” au “asili.” Hilo ni jina linalofaa kitabu ambacho husimulia jinsi ulimwengu mzima ulivyotokea, jinsi dunia ilivyotayarishwa iwe makao ya wanadamu, na jinsi wanadamu walivyopata kuishi duniani. Musa aliandika kitabu hiki katika nyika ya Sinai, na yaelekea alikimaliza mwaka wa 1513 K.W.K.

Kitabu cha Mwanzo kinatueleza kuhusu ulimwengu uliotangulia Gharika, kuhusu kilichotukia baada ya Gharika, na jinsi Yehova Mungu alivyoshughulika na Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu. Makala hii itazungumzia mambo makuu katika kitabu cha Mwanzo 1:1–11:9, hasa kufikia wakati ambapo Yehova alianza kushughulika na mzee wa ukoo Abrahamu.

ULIMWENGU ULIOTANGULIA GHARIKA

(Mwanzo 1:1-7:24)

Maneno ya utangulizi ya kitabu cha Mwanzo, “hapo mwanzo,” yanarejelea mabilioni ya miaka iliyopita. Matukio ya zile “siku” sita za uumbaji, yaani, kipindi cha nyakati za kazi ya pekee ya uumbaji, yanaelezwa kupatana na jinsi ambavyo mtazamaji mwanadamu angaliyaelewa kama angalikuwa duniani. Kufikia mwisho wa siku ya sita, Mungu alimwumba mwanadamu. Ingawa Paradiso inapotea baada ya muda mfupi kwa sababu ya kutotii kwa mwanadamu, Yehova anatoa tumaini. Unabii wa kwanza wa Biblia unamtaja “uzao” ambaye ataondoa madhara ya dhambi na kumponda Shetani kichwa.

Katika miaka 1,600 inayofuata, Shetani anafaulu kukengeusha wanadamu wote watoke kwa Mungu, isipokuwa watu wachache waaminifu kama vile Abeli, Enoko, na Noa. Kwa mfano, Kaini anamuua Abeli ndugu yake mwadilifu. ‘Watu wanaanza kuliitia jina la Yehova,’ yaelekea katika njia isiyofaa. Akionyesha roho ya jeuri ya siku hizo, Lameki anatunga shairi kuhusu jinsi alivyomuua kijana mmoja kwa dai la kujitetea. Hali zinazidi kuwa mbaya wakati wana wa kimalaika wa Mungu wasiotii wanapooa wanawake na kuzaa majitu wenye jeuri wanaoitwa Wanefili. Lakini, Noa mwaminifu anajenga safina, na kuwaonya wengine kwa ujasiri kuhusu Gharika inayokaribia, naye na familia yake wanaokoka maafa yanayoletwa na Gharika hiyo.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:16—Mungu angewezaje kutokeza nuru katika siku ya kwanza kama hakuwa amefanya mianga hadi siku ya nne? Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘fanya’ katika mstari wa 16 si sawa na neno ‘umba’ linalotumiwa katika Mwanzo 21, sura ya 1, mstari wa 1, 21, na 27. “Mbingu” ambazo zilitia ndani mianga ziliumbwa muda mrefu kabla ya “siku ya kwanza” kuanza. Lakini nuru ya mianga hiyo haikuwa imefika kwenye uso wa dunia. Katika siku ya kwanza, “kukawa na nuru” kwa sababu nuru ilipenya mawingu mazito na kuonekana duniani. Hivyo, dunia iliyokuwa inazunguka ikaanza kuwa na vipindi vya mchana na usiku. (Mwanzo 1:1-3, 5) Bado vyanzo vya nuru hiyo havikuonekana kutoka duniani. Hata hivyo, katika kipindi cha nne cha uumbaji, badiliko muhimu lilitokea. Sasa, jua, mwezi, na nyota zilifanywa ‘ziangaze dunia.’ (Mwanzo 1:17) ‘Mungu alizifanya’ katika maana ya kwamba sasa zingeweza kuonekana kutoka duniani.

3:8—Je, Yehova Mungu alizungumza na Adamu moja kwa moja? Biblia inaonyesha kwamba mara nyingi Mungu alitumia malaika alipozungumza na wanadamu. (Mwanzo 16:7-11; 18:1-3, 22-26; 19:1; Waamuzi 2:1-4; 6:11-16, 22; 13:15-22) Msemaji mkuu wa Mungu alikuwa Mwana wake mzaliwa wa pekee, aliyeitwa “Neno.” (Yohana 1:1) Inaelekea Mungu alizungumza na Adamu na Hawa kupitia huyo “Neno.”—Mwanzo 1:26-28; 2:16; 3:8-13.

3:17—Udongo ulilaaniwa katika njia gani, na kwa muda gani? Laana iliyotamkwa juu ya udongo ilimaanisha kwamba ingekuwa vigumu sana kuulima. Wazao wa Adamu waliathiriwa sana na matokeo ya kulaaniwa kwa udongo ambao ulitokeza mibaruti kiasi kwamba Lameki, baba ya Noa, alitaja “maumivu ya mikono yetu yanayoletwa na udongo ambao Yehova amelaani.” (Mwanzo 5:29) Baada ya Gharika, Yehova alimbariki Noa na wanawe na kuwaeleza kusudi Lake kwamba waijaze dunia. (Mwanzo 9:1) Yaonekana laana ya Mungu juu ya udongo iliondolewa.—Mwanzo 13:10.

4:15—Yehova aliwekaje “ishara kwa ajili ya Kaini”? Biblia haisemi kwamba Kaini mwenyewe alitiwa alama au ishara kwa njia fulani. Yaonekana ishara hiyo ilihusisha amri nzito iliyojulikana na kufuatwa na wengine na ambayo ilikusudiwa kumlinda asiuawe kwa kulipiza kisasi.

4:17—Kaini alitoa mke wapi? Adamu ‘alizaa wana na mabinti.’ (Mwanzo 5:4) Kwa hiyo, Kaini alimchukua mmoja wa dada zake au pengine mmoja wa wapwa zake wa kike kuwa mke wake. Baadaye, Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli haikuruhusu ndoa kati ya ndugu na dada wa kimwili.—Mambo ya Walawi 18:9.

5:24—Mungu ‘alimchukua Enoko’ katika njia gani? Yaonekana Enoko alikabili hatari ya kuuawa, lakini Mungu hakuruhusu ateseke mikononi mwa adui zake. Mtume Paulo aliandika: “Enoko alihamishwa ili asione kifo.” (Waebrania 11:5) Hiyo haimaanishi kwamba Mungu alimchukua akampeleka mbinguni, ambako aliendelea kuishi. Yesu ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza kwenda mbinguni. (Yohana 3:13; Waebrania 6:19, 20) Huenda ‘kuhamishwa kwa Enoko ili asione kifo’ kulimaanisha kwamba Mungu alimtia katika hali ya njozi ya kinabii kisha akakomesha uhai wake akiwa katika hali hiyo. Chini ya hali hizo, Enoko hakuteseka, wala ‘kuona kifo’ mikononi mwa adui zake.

6:6—Ni katika maana gani inaweza kusemwa kwamba Yehova ‘alijuta’ kwamba alimwumba mwanadamu? Hapa neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘alijuta’ linamaanisha kubadili mtazamo au nia. Kwa kuwa Yehova ni mkamilifu yeye hakukosea katika kumwumba mwanadamu. Hata hivyo, alibadili maoni yake kuhusiana na kizazi kiovu kilichoishi kabla ya Gharika. Mungu alibadili mtazamo wake wa kuwa Muumba wa wanadamu na badala yake akawa mwangamizi wao kwa sababu alichukizwa na uovu wao. Kwa kuwa Mungu aliwahifadhi wanadamu fulani, jambo hilo linaonyesha kwamba alijuta tu kuhusiana na waovu.—2 Petro 2:5, 9.

7:2—Ni nini kilichotumiwa kutofautisha wanyama safi na wasio safi? Yaonekana njia ya kutofautisha wanyama safi na wasio safi ilitegemea dhabihu zilizotolewa katika ibada, bali si kama mnyama huyo alifaa kuliwa au la. Mwanadamu hakuwa akila nyama kabla ya Gharika. Maneno “safi” na “-sio safi” yalianza kutumiwa kuhusu chakula katika Sheria ya Musa tu, nayo yaliacha kutumiwa sheria hiyo ilipokoma. (Matendo 10:9-16; Waefeso 2:15) Yaonekana, Noa alijua ni mnyama yupi aliyefaa kutolewa dhabihu katika ibada ya Yehova. Mara tu alipotoka katika safina, Noa ‘alimjengea Yehova madhabahu na kuchukua baadhi ya wanyama wote walio safi na baadhi ya viumbe wote wanaoruka ambao ni safi, akatoa matoleo ya kuteketezwa juu ya ile madhabahu.’—Mwanzo 8:20.

7:11—Maji yaliyosababisha Gharika duniani pote yalitoka wapi? Katika kipindi cha pili, au “siku” ya pili ya uumbaji, wakati “anga” la dunia lilipofanywa, kulikuwa maji “yaliyo chini ya anga” na maji “yaliyo juu ya anga.” (Mwanzo 1:6, 7) Maji yaliyokuwa “chini” ni yale ambayo tayari yalikuwa duniani. Maji yaliyokuwa “juu” ni unyevunyevu mwingi uliokuwa angani juu ya dunia, ambao ulifanyiza “kilindi kikubwa cha maji.” Maji hayo yote yalimwagika juu ya dunia katika siku za Noa.

Mambo Tunayojifunza:

1:26.Kwa kuwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu, wanaweza kuonyesha sifa zake. Kwa kweli tunapaswa kujitahidi kusitawisha sifa kama vile upendo, rehema, fadhili, wema, na subira, kwa kumwiga Yule aliyetufanya.

2:22-24.Ndoa ni mpango wa Mungu. Kifungo cha ndoa ni kitakatifu na ni cha kudumu, naye mume ndiye kichwa cha familia.

3:1-5, 16-23.Ili tupate furaha tunapaswa kutambua enzi kuu ya Yehova maishani mwetu.

3:18, 19; 5:5; 6:7; 7:23.Neno la Yehova hutimia sikuzote.

4:3-7.Yehova alipendezwa na dhabihu ya Abeli kwa sababu alikuwa mtu mwadilifu na mwenye imani. (Waebrania 11:4) Kwa upande mwingine, matendo ya Kaini yalionyesha kwamba hakuwa na imani. Kazi zake zilikuwa mbovu na zilionyesha wivu, chuki, na uuaji. (1 Yohana 3:12) Isitoshe, yaelekea hakuifikiria kwa uzito dhabihu yake naye aliitoa kidesturi tu. Tunapaswa kumtolea Yehova dhabihu zetu za sifa kwa moyo wote na kuwa na mtazamo na mwenendo unaofaa.

6:22.Ingawa ilichukua miaka mingi kujenga safina, Noa alifanya sawasawa na vile Mungu alivyomwamuru. Kwa hiyo, Noa na familia yake walihifadhiwa wakati wa Gharika. Yehova huzungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa naye hutoa mwongozo kupitia tengenezo lake. Tutanufaika tukisikiliza na kutii.

7:21-24.Yehova haharibu waadilifu pamoja na waovu.

WANADAMU WAINGIA KATIKA KIPINDI KIPYA

(Mwanzo 8:1–11:9)

Wanadamu wanaingia katika kipindi kipya baada ya ulimwengu uliotangulia Gharika kutoweka. Wanadamu wanaruhusiwa kula nyama, lakini wanaamuriwa wajiepushe na damu. Yehova anaruhusu adhabu ya kifo kwa wauaji naye anaanzisha agano la upinde wa mvua, akiahidi kwamba hataleta kamwe Gharika nyingine. Wana watatu wa Noa wanakuwa mababu wa jamii yote ya kibinadamu, lakini kitukuu wake Nimrodi anakuwa “mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.” Badala ya kusambaa na kuijaza dunia, watu wanaamua kujenga mnara na jiji linaloitwa Babeli ili kujifanyia jina maarufu. Makusudi yao yanazuiwa pale Yehova anapoivuruga lugha yao na kuwatawanya duniani kote.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

8:11—Ikiwa miti iliharibiwa na Gharika, yule njiwa alitoa wapi jani la mzeituni? Mambo mawili yanawezekana. Kwa kuwa mzeituni ni mti unaoweza kustahimili hali ngumu, huenda ikawa haukukauka ingawa ulifunikwa na maji kwa miezi kadhaa wakati wa Gharika. Maji ya gharika yalipopungua, mzeituni huo ungetokea tena kwenye udongo mkavu na kuchipua majani. Huenda pia jani la mzeituni ambalo Noa aliletewa na njiwa lilitolewa kwenye mti mchanga ambao ulichipuka baada ya maji ya gharika kupungua.

9:20-25—Kwa nini Noa alimlaani Kanaani? Inaelekea kwamba Kanaani alikuwa na hatia ya tendo fulani potovu alilomfanyia babu yake Noa. Ingawa Hamu, baba ya Kanaani, alishuhudia tendo hilo, yeye hakumzuia bali yaonekana alieneza habari hizo. Hata hivyo, Shemu na Yafethi, wana wengine wawili wa Noa, walimfunika baba yao. Kwa sababu hiyo walibarikiwa lakini Kanaani akalaaniwa, naye Hamu akateseka kwa sababu ya aibu iliyoupata uzao wake.

10:25—Dunia ilikuwa ‘imegawanyika’ jinsi gani siku za Pelegi? Pelegi aliishi kutoka mwaka wa 2269 hadi 2030 K.W.K. “Katika siku zake” Yehova alisababisha mgawanyiko mkubwa kwa kuvuruga lugha ya wajenzi wa Babeli na kuwatawanya duniani pote. (Mwanzo 11:9) Hivyo, “dunia [au, wakaaji wa dunia] ilikuwa imegawanyika” katika siku za Pelegi.

Mambo Tunayojifunza:

9:1; 11:9.Hakuna mpango au jitihada ya mwanadamu inayoweza kuzuia kusudi la Yehova.

10:1-32.Sura ya 5 na 10 ambazo zina taarifa mbili za ukoo wa kabla na baada ya Gharika zinaunganisha jamii yote ya wanadamu na mwanadamu wa kwanza, Adamu, kupitia wana watatu wa Noa. Waashuru, Wakaldayo, Waebrania, Wasiria, na makabila fulani ya Arabia, ni wazao wa Shemu. Waethiopia, Wamisri, Wakaanani, na makabila fulani ya Afrika na Arabia ni wazao wa Hamu. Wahindi na Wazungu ni wazao wa Yafethi. Wanadamu wote ni wa ukoo mmoja, na wote huzaliwa wakiwa na usawa machoni pa Mungu. (Matendo 17:26) Kujua jambo hilo kunapaswa kuathiri jinsi tunavyowaona na kuwatendea wengine.

Neno la Mungu Linaweza Kuwa na Nguvu

Sehemu ya kwanza ya kitabu cha Mwanzo ndiyo tu ina masimulizi sahihi kuhusu historia ya mapema ya mwanadamu. Sehemu hiyo inatusaidia kufahamu kusudi la Mungu la kuwaweka wanadamu duniani. Inatia moyo kama nini kuona kwamba hakuna jitihada za binadamu, kama zile za Nimrodi, zinazoweza kuzuia kusudi hilo lisitimizwe!

Kuchunguza mambo yanayotajwa chini ya sehemu, “Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa,” kutakusaidia uelewe baadhi ya sehemu ngumu za Kimaandiko unaposoma Biblia kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Maelezo yaliyo chini ya kichwa kidogo “Mambo Tunayojifunza” yatakuonyesha jinsi unavyoweza kunufaika kutokana na usomaji wa Biblia wa kila juma. Inapofaa, maelezo hayo yanaweza pia kutumiwa kwa ajili ya mahitaji ya kwenu kwenye Mkutano wa Utumishi. Kwa kweli, Neno la Yehova liko hai na linaweza kuwa na nguvu katika maisha yetu.—Waebrania 4:12.