Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwisho wa Vita

Mwisho wa Vita

Mwisho wa Vita

‘Tuna umri wa miaka 12 tu. Hatuwezi kubadili hali ya siasa na vita, lakini tunataka kuishi! Tunasubiri amani. Je, itakuja wakati wetu?’—Watoto wa darasa la tano

‘Tunataka kwenda shuleni na kuwatembelea marafiki na familia zetu bila kuogopa kutekwa nyara. Ninatumaini serikali itasikiliza. Tunataka maisha bora. Tunataka amani.’—Alhaji, mwenye umri wa miaka 14

MANENO hayo yenye kugusa moyo yanaonyesha tumaini la kutoka moyoni la vijana ambao wameteseka kwa miaka mingi kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe. Wangependa tu kuishi maisha ya kawaida. Lakini si rahisi kugeuza matumaini kuwa mambo halisi. Je, tutapata kuishi katika ulimwengu usio na vita?

Katika miaka ya hivi karibuni, mataifa yamejitahidi kukomesha vita fulani vya wenyewe kwa wenyewe kwa kushinikiza pande zinazozozana kutia sahihi mapatano ya amani. Nchi fulani zimetuma majeshi ya kudumisha amani ili kuhakikisha kwamba mapatano hayo yamefuatwa. Lakini ni nchi chache ambazo zina pesa na tamaa ya kusimamia mambo katika nchi za mbali ambako chuki kali na kutoaminiana kati ya vikundi vinavyopigana hufanya iwe vigumu sana kudumisha mapatano. Mara nyingi, mapigano huzuka tena majuma au miezi michache tu baada ya kutia sahihi mapatano ya kusimamisha vita. Kama taasisi ya SIPRI inavyosema, “ni vigumu kupata amani iwapo wapiganaji wana nia na uwezo wa kuendelea kupigana.”

Wakati huohuo, vita hivyo ambavyo si rahisi kukomeshwa vimekumba sehemu nyingi sana za dunia nazo huwakumbusha Wakristo unabii fulani wa Biblia. Kitabu cha Ufunuo hutaja kipindi kigumu katika historia ambapo mpanda-farasi wa mfano ‘angeondoa amani duniani.’ (Ufunuo 6:4) Vita hivyo ambavyo vilitabiriwa kwamba vingeendelea bila kukoma ni sehemu ya ishara yenye mambo mengi inayoonyesha kwamba sasa tunaishi katika kipindi kinachoitwa na Biblia “siku za mwisho.” * (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, Neno la Mungu hutuhakikishia kwamba siku hizi za mwisho zinatangulia kipindi cha amani.

Biblia inasema katika Zaburi 46:9 kwamba ili kupata amani ya kweli, ni lazima vita vikome katika dunia nzima wala si katika eneo moja tu. Isitoshe, zaburi hiyohiyo inataja kihususa kuharibiwa kwa silaha zilizotumiwa sana katika nyakati za Biblia, yaani, upinde na mkuki. Vilevile, silaha ambazo zimeongezeka leo zinapaswa kuharibiwa iwapo wanadamu wataishi kwa amani.

Hivyo basi, vita huchochewa na chuki na pupa bali si risasi na silaha. Pupa ni kisababishi kikuu cha vita, na mara nyingi chuki husababisha jeuri. Watu wanahitaji kubadili njia yao ya kufikiri ili kung’oa hisia hizo zenye kuleta madhara. Wanahitaji kuelimishwa ili waishi kwa amani. Hivyo, nabii wa kale Isaya anasema kwamba vita vitakoma wakati ambapo wanadamu ‘hawatajifunza vita tena.’—Isaya 2:4.

Hata hivyo, leo tunaishi katika ulimwengu unaowafundisha watu wazima na watoto, watukuze vita badala ya kuthamini amani. Inasikitisha kwamba hata watoto wanazoezwa kuua.

Walijifunza Kuua

Alipokuwa na umri wa miaka 14, Alhaji aliachishwa utumishi wa jeshi. Alikuwa na umri wa miaka kumi alipotekwa na jeshi la waasi lililomzoeza kupigana kwa kutumia bunduki aina ya AK-47. Baada ya kulazimishwa kuwa askari, alishambulia maeneo kadhaa ili kupora chakula na kuteketeza nyumba kwa moto. Pia aliua na kukata watu viungo vya mwili. Leo, Alhaji huona ni vigumu sana kusahau vita na kuishi maisha ya kiraia. Abraham, mtoto mwingine ambaye alikuwa askari, pia alijifunza kuua na hakutaka kurudisha silaha yake. Alisema: “Wakiniambia niende zangu bila bunduki yangu, sijui nitafanya nini wala nitakula nini.”

Zaidi ya watoto 300,000, wavulana kwa wasichana, ambao ni askari, bado wanapigana na kufa katika vita visivyokoma vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoikumba dunia yetu. Kiongozi mmoja wa waasi alisema hivi: “Wao hutii amri; hawajali kurudi kwa wake zao familia zao; nao hawaogopi.” Hata hivyo, watoto hao wanahitaji na wanastahili kuishi maisha bora.

Katika nchi zilizositawi, huenda watu wakakosa kuelewa hali mbaya ya watoto ambao ni askari. Hata hivyo, watoto wengi wa nchi zilizositawi wanajifunza kupigana vita katika nyumba zao. Jinsi gani?

Kwa mfano, fikiria José anayeishi kusini-mashariki mwa Hispania. Alikuwa kijana aliyefurahia judo na karate. Alipenda sana upanga mrefu wa kijapani ambao baba yake alimnunulia kama zawadi ya Krismasi. Naye alipenda pia michezo ya video, hasa ile yenye jeuri. Mnamo Aprili 1, 2000 aliiga kihalisi jeuri ya mwigizaji aliyependa. Katika mauaji makubwa ya kijeuri, aliua baba yake, mama yake, na dada yake kwa ule upanga ambao baba yake alimnunulia. “Nilitaka kuwa peke yangu ulimwenguni; sikutaka wazazi wangu wanitafute,” akawaeleza polisi.

Mwandishi na ofisa wa jeshi Dave Grossman, alieleza hivi kuhusu vitumbuizo vyenye jeuri: “Tunafikia kiwango cha kutokuwa na hisia zozote ambapo kuumiza na kutesa watu kumekuwa namna ya kujiburudisha: tunapata furaha kuona mambo hayo badala ya kuyachukia. Tunajifunza kuua, na tunajifunza kufurahia jambo hilo.”

Alhaji na José walijifunza kuua. Hawakukusudia kuwa wauaji, lakini kwa kuzoezwa kwa njia moja au nyingine, kufikiri kwao kulipotoshwa. Mazoezi hayo, yawe kwa watoto au kwa watu wazima, hufanya watu waanze kujihusisha na jeuri na vita.

Kujifunza Amani Badala ya Vita

Amani ya kudumu haiwezi kupatikana maadamu watu wanajifunza kuua. Zaidi ya miaka 2,700 iliyopita, nabii Isaya aliandika: “Laiti ungesikiliza amri [za Mungu]! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Watu wanapopata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kujifunza kupenda sheria Yake, wanachukia jeuri na vita. Hata sasa wazazi wanaweza kuhakikisha kwamba michezo ya watoto wao haichochei jeuri. Watu wazima pia wanaweza kujifunza kushinda chuki na pupa. Mashahidi wa Yehova wametambua tena na tena kwamba Neno la Mungu lina uwezo wa kubadili nyutu za watu.—Waebrania 4:12.

Fikiria kisa cha Hortêncio. Wakati alipokuwa kijana alilazimishwa kujiunga na jeshi. Mazoezi ya kijeshi yalikusudiwa “kuchochea ndani yetu tamaa ya kuua watu wengine na kutokuwa na woga wowote wa kuua,” anaeleza. Alipigana vita fulani vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo viliendelea kwa muda mrefu huko Afrika. “Vita hivyo viliathiri utu wangu,” anakiri. “Hata leo bado ninakumbuka mambo yote niliyofanya. Ninasikitika sana kuhusu mambo niliyolazimishwa kufanya.”

Hortêncio aliguswa moyo sana wakati askari mwenzake alipozungumza naye kuhusu Biblia. Alivutiwa na ahadi ya Mungu katika Zaburi 46:9 kwamba atakomesha aina zote za vita. Kadiri alivyojifunza Biblia, ndivyo alivyotamani kuacha kupigana. Baada ya muda mfupi yeye na rafiki zake walifukuzwa jeshini, nao wakajiweka wakfu kwa Yehova Mungu. “Kweli ya Biblia ilinisaidia kupenda adui yangu,” Hortêncio anaeleza. “Niliona kwamba nilikuwa nikimtenda Yehova dhambi kwa kupigana vitani, kwa kuwa anasema hatupaswi kuua jirani zetu. Ili kuonyesha upendo huo, ilinibidi kubadili maoni yangu na kutowaona watu kuwa adui zangu.”

Hali hizo halisi za maisha zinaonyesha kwamba kwa kweli elimu ya Biblia huchangia amani. Hilo halishangazi. Nabii Isaya alisema kwamba kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya elimu ya Mungu na amani. Alitabiri hivi: “Wana wako wote watakuwa watu waliofundishwa na Yehova, na amani ya wana wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Nabii huyohuyo aliona kimbele wakati ambapo watu wa mataifa yote wangemiminika kwenye ibada safi ya Yehova Mungu ili kujifunza njia zake. Matokeo yangekuwaje? ‘Wangefua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halingeinua upanga juu ya taifa, wala hawangejifunza vita tena.’—Isaya 2:2-4.

Kupatana na unabii huo, Mashahidi wa Yehova wanashiriki katika kazi ya duniani pote ya kuelimisha watu. Kazi hiyo imewasaidia mamilioni ya watu kushinda chuki ambayo husababisha vita vya wanadamu.

Amani ya Ulimwengu Ni Hakika

Zaidi ya kutoa elimu, Mungu amesimamisha serikali au “ufalme,” ambao una uwezo wa kuleta amani duniani pote. Inafaa kuona kwamba Biblia humtaja Yesu Kristo, Mtawala aliyechaguliwa na Mungu, kuwa “Mkuu wa Amani.” Pia inatuhakikishia kwamba “hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.”—Isaya 9:6, 7.

Tuna uhakika gani kwamba utawala wa Kristo utaondoa kila aina ya vita? Nabii Isaya anaongeza kusema: “Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.” (Isaya 9:7) Mungu ana tamaa na uwezo wa kudumisha amani. Yesu ana uhakika kabisa kuhusu ahadi hiyo. Ndiyo sababu aliwafundisha wafuasi wake wasali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yafanywe duniani. (Mathayo 6:9, 10) Mwishowe ombi hilo la unyoofu litakapojibiwa, dunia haitaharibiwa tena na vita.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kuchunguza uthibitisho kwamba tunaishi katika siku za mwisho, ona sura ya 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Elimu ya Biblia huchangia amani ya kweli