Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimebarikiwa Sana kwa Kudumisha Roho ya Umishonari

Nimebarikiwa Sana kwa Kudumisha Roho ya Umishonari

Simulizi la Maisha

Nimebarikiwa Sana kwa Kudumisha Roho ya Umishonari

LIMESIMULIWA NA TOM COOKE

Mlio wa bunduki ulikatiza kwa ghafula utulivu wa alasiri. Risasi zilipita kwa kasi katikati ya miti shambani mwetu. Ni nini kilichokuwa kikiendelea? Baada ya muda mfupi tulipata habari kwamba mapinduzi yametokea na kwamba sasa Uganda ilitawaliwa na Jemadari Idi Amin. Ulikuwa mwaka wa 1971.

KWA nini mimi na mke wangu Ann, tulihama nchi ya Uingereza yenye amani ya kadiri fulani na kwenda katika eneo hilo la Afrika lenye msukosuko na hatari? Nadhani kwa kiasi fulani mimi ni mtu jasiri kiasili, lakini nilichochewa hasa na kielelezo cha wazazi wangu waliokuwa wenye bidii katika kazi ya Ufalme.

Ninakumbuka siku fulani yenye joto mnamo Agosti 1946 wakati wazazi walipotembelewa na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza. Walisimama mlangoni na kuzungumza na wageni hao wawili kwa muda ulioonekana kuwa mrefu sana. Wageni hao, Fraser Bradbury na Mamie Shreve walirudi mara nyingi, na miezi iliyofuata, maisha ya familia yetu yakabadilika sana.

Kielelezo cha Ujasiri cha Wazazi Wangu

Wazazi wangu walishiriki katika kazi nyingi za kijamii. Kwa mfano, muda mfupi kabla ya kuanza kujifunza Biblia, tulikuwa tumepamba nyumba yetu kwa picha za Winston Churchill. Wakati wa uchaguzi wa kitaifa uliofanywa baada ya vita, halmashauri ya chama cha kisiasa cha Conservative ilifanyia mikutano yake nyumbani kwetu. Familia yetu pia ilijuana na watu mashuhuri katika dini na katika jamii. Ingawa wakati huo nilikuwa na umri wa miaka tisa tu, niliona jinsi watu wetu wa ukoo walivyoshtuka walipojua kwamba tulikuwa tunabadili dini kuwa Mashahidi wa Yehova.

Kielelezo cha Mashahidi tulioshirikiana nao, ambao walikuwa wajasiri na wenye kujitoa kwa nafsi yote, kiliwachochea wazazi wangu kuanza kazi ya kuhubiri. Muda si muda, baba yangu alianza kutoa hotuba hadharani akitumia kikuza-sauti kwenye eneo lenye maduka mengi la Spondon, kijijini kwetu. Sisi watoto tulisimama mahali ambapo tungeweza kuonekana huku tumeinua magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa kweli, nilipokutana na wanafunzi wenzangu, nilitamani ardhi ipasuke na kunimeza.

Kielelezo cha wazazi wangu kilimchochea dada yangu mkubwa Daphne, aanze upainia. Mnamo 1955, alihudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower kisha akapewa mgawo wa umishonari Japani. * Hata hivyo, dada yangu mdogo, Zoe, aliacha kumtumikia Yehova.

Wakati huohuo, nilimaliza shule ambako nilisomea uchoraji na usanii wa maandishi. Siku hizo, wanafunzi wenzangu walizungumza sana kuhusu kulazimishwa kujiunga na jeshi la kujenga taifa. Waliona kama ni mzaha nilipowaambia kwamba singeweza kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Suala hilo liliniwezesha kuwa na mazungumzo mengi sana ya Biblia pamoja na baadhi ya wanafunzi hao. Muda mfupi baadaye, nilifungwa gerezani kwa miezi 12 kwa kukataa utumishi wa jeshi. Baadaye, nilimwoa mmoja wa wanafunzi katika chuo hicho cha sanaa ambaye alionyesha kupendezwa na ujumbe wa Biblia. Lakini nitampa Ann nafasi ya kueleza jinsi alivyojifunza kweli.

Jinsi Ann Alivyopata Kweli

“Familia yetu haikupendezwa na mambo ya kidini, na sikuwa nimebatizwa katika dini yoyote. Lakini nilipendezwa na masuala ya kidini na nilijiunga na rafiki zangu kwenda kwenye kanisa lolote lile. Nilianza kupendezwa na Biblia nilipomsikiliza Tom na Shahidi mwingine wakizungumza kwa shauku na wanafunzi wengine chuoni. Nilishtuka sana Tom na huyo Shahidi mwingine walipofungwa gerezani kwa kukataa utumishi wa jeshi.

“Niliendelea kuwasiliana na Tom alipokuwa gerezani, na upendezi wangu wa Biblia ukaongezeka. Nilipoenda London kupata elimu zaidi, nilikubali kujifunza Biblia na Muriel Albrecht. Muriel alikuwa ametumikia akiwa mishonari huko Estonia, naye pamoja na mama yake walinitia moyo sana. Baada ya majuma machache, nilianza kuhudhuria mikutano na kutoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! nikiwa nimesimama nje ya kituo cha gari-moshi cha Victoria.

“Nilihudhuria mikutano katika Kutaniko la Southwark, kusini mwa London. Kutaniko hilo lilikuwa na akina ndugu na dada wa kiroho wa mataifa mbalimbali, na wengi wao walikuwa maskini. Ingawa nilikuwa mgeni, walinitendea kama mmoja wao. Upendo nilioona katika kutaniko hilo ulinisadikisha kwamba yale niliyokuwa nikijifunza ni kweli, nami nikabatizwa mwaka wa 1960.”

Miradi Ileile Lakini Hali Tofauti

Baadaye, mwaka wa 1960 mimi na Ann tulioana, na tulikuwa na mradi wa kuwa mishonari. Lakini hali zetu zilibadilika tulipojua kwamba tungepata mtoto. Baada ya binti yetu Sara kuzaliwa, mimi na Ann bado tulikuwa na tamaa ya kutumikia katika nchi yenye uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme. Nilituma maombi ya kazi katika nchi kadhaa, na hatimaye katika Mei 1966, nikapata barua ya kuonyesha kwamba nimeajiriwa katika Wizara ya Elimu huko Uganda. Lakini wakati huo, Ann alikuwa na mimba ya mtoto wetu wa pili. Wengine hawakuona kama ni jambo la hekima kwetu hata kuwazia jambo hilo. Tulishauriana na daktari wetu ambaye alisema: “Ikiwa mnaenda, lazima msafiri kabla mimba ya mke wako haijafikisha miezi saba.” Hivyo, tukaondoka mara moja kwenda Uganda. Basi, wazazi wetu hawakumwona binti yetu wa pili Rachel hadi alipokuwa na umri wa miaka miwili. Kwa kuwa sasa sisi tuna wajukuu, tunaelewa vizuri kabisa roho ya kujitoa ya wazazi wetu wapendwa.

Tulipofika Uganda mwaka wa 1966 tulisisimuka sana na wakati huohuo tukawa na woga. Tuliposhuka tu kwenye ndege, tulivutiwa sana na rangi mbalimbali zilizokuwa nyangavu sana. Kwanza tuliishi karibu na mji mdogo wa Iganga ulio kilometa 50 kutoka Jinja, mji ambao uko kwenye chanzo cha Mto Nile. Washiriki wa kikundi kilichokuwa Jinja ndio Mashahidi walioishi karibu zaidi nasi. Kikundi hicho kilisimamiwa na mishonari Gilbert na Joan Walters, na Stephen na Barbara Hardy. Nilituma maombi ya kuhamishwa nikafanye kazi Jinja ili niweze kukisaidia vizuri zaidi kikundi hicho. Tulihamia Jinja muda mfupi baada ya Rachel kuzaliwa. Huko tulifurahia kutumikia pamoja na kikundi kidogo cha Mashahidi waaminifu, ambacho kilikua na hatimaye kikawa kutaniko la pili nchini Uganda.

Kutumikia Tukiwa Familia Katika Nchi ya Kigeni

Mimi na Ann tunahisi kwamba tulichagua mazingira mazuri ya kulelea watoto wetu. Tulifurahia kufanya kazi pamoja na mishonari wa nchi mbalimbali na kusaidia kutaniko changa likue. Tulifurahia ushirika wa ndugu na dada zetu wa Uganda, ambao mara nyingi walitutembelea nyumbani. Stanley na Esinala Makumba walitutia moyo sana.

Wageni wetu hawakuwa akina ndugu tu, kwa kuwa tulizungukwa na wanyama wa aina mbalimbali. Viboko walikuwa wakitoka katika Mto Nile usiku na kukaribia sana nyumba yetu. Ninakumbuka vizuri wakati tulipompata chatu mwenye urefu wa meta sita kwenye shamba letu. Wakati mwingine tulienda kuwaona wanyama kwenye mbuga za wanyama ambako simba na wanyama wengine wa mwituni walitembea-tembea bila vizuizi.

Katika huduma, wenyeji ambao hawakuwa wameona kigari cha kumbebea mtoto walituona kuwa watu wasio wa kawaida. Tulipohubiri nyumba kwa nyumba, watoto wengi wadogo walikuwa wakitufuata. Watu walitutazama kwa heshima na kumgusa mtoto mzungu. Tulifurahia kutoa ushahidi kwa sababu watu walikuwa wenye adabu sana. Tulifikiri kwamba kila mtu angekubali kweli kwa kuwa ilikuwa rahisi sana kuanzisha mafunzo ya Biblia. Lakini ilikuwa vigumu kwa wengi kuacha mapokeo yasiyo ya Kimaandiko. Hata hivyo, wengi walikubali kufuata viwango vya juu vya maadili ya Biblia, na washiriki wa kutaniko wakaongezeka. Kusanyiko letu la kwanza tulilofanya mjini Jinja mwaka wa 1968, lilikuwa hatua muhimu. Bado mimi hufurahi ninapokumbuka ubatizo wa baadhi ya watu tuliojifunza nao Biblia ambao ulifanyiwa Mto Nile. Lakini muda mfupi baadaye amani yetu ingevurugwa.

Marufuku Ilijaribu Imani na Busara Yetu

Jemadari Idi Amin alitwaa mamlaka katika mwaka wa 1971. Kulikuwa na mvurugo mkubwa mjini Jinja, na tulipokuwa tukinywa chai katika bustani yetu ndipo hali iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii ilipotukia. Katika miaka miwili iliyofuata, Wahindi wengi walifukuzwa. Wageni wengi waliamua kuondoka, jambo lililoathiri sana shule na hospitali. Ndipo kukatokea tangazo kali kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku. Kwa sababu ya kujali usalama wetu, Wizara ya Elimu ilituhamisha hadi kwenye jiji kuu, Kampala. Kuhama huko, kulitunufaisha kwa njia mbili. Hatukujulikana sana huko Kampala na hivyo tungeweza kutembea kwa uhuru zaidi. Pia kulikuwa na kazi nyingi katika kutaniko na katika huduma ya shambani.

Hali ya Brian na Marion Wallace pamoja na watoto wao wawili ilifanana na yetu, nao pia waliamua kuendelea kuishi Uganda. Tulifurahia sana ushirika wao tulipokuwa tukitumikia pamoja katika Kutaniko la Kampala wakati huo mgumu. Tulitiwa moyo sana na mambo tuliyokuwa tumesoma kuhusu ndugu zetu waliokuwa wakitumikia chini ya marufuku katika nchi nyingine. Tulikutana katika vikundi vidogo-vidogo, na mara moja kwa mwezi, tulifanya mikutano mikubwa zaidi kwenye Bustani ya Mimea huko Entebbe, ambako tulijifanya tunafurahia karamu. Binti zetu walifurahia sana mpango huo.

Tulihitaji kujihadhari sana kuhusu njia tulizotumia kuhubiri. Wazungu wangeonekana kwa urahisi kama wangetembelea nyumba za Waganda. Kwa hiyo, tulihubiri kwenye maduka, nyumba za orofa, na vyuo vikuu. Njia moja niliyotumia madukani ni kuuliza bidhaa fulani ambayo nilijua haipatikani tena, kama vile sukari au mchele. Kama mwenye duka angesikitika kuhusu hali nchini, ningemhubiria ujumbe wa Ufalme. Njia hiyo ilikuwa na matokeo sana. Mara kwa mara, niliondoka dukani nikiwa nimepata rudio na pia kiasi kidogo cha bidhaa iliyokuwa vigumu kupatikana.

Wakati huohuo, jeuri ilikuwa ikizuka kila mahali. Kwa sababu ya kuzorota kwa uhusiano kati ya Uganda na Uingereza, serikali ilikataa kuongeza muda wa kibali changu cha kufanya kazi. Hivyo, mwaka wa 1974, tulihuzunika kuwaaga ndugu zetu baada ya kuishi Uganda kwa miaka minane. Lakini, tulidumisha roho ya umishonari.

Twahamia New Guinea

Mnamo Januari 1975, tulienda Papua New Guinea nafasi ya kazi ilipojitokeza huko. Hivyo tukaanza miaka minane ya utumishi wenye furaha katika eneo hili la Pasifiki. Maisha yetu pamoja na akina ndugu na katika huduma yalikuwa yenye manufaa na yenye kuridhisha.

Familia yetu inakumbuka muda tuliokaa Papua New Guinea kuwa kipindi cha drama za Biblia. Kila mwaka, tulihusika katika kutayarisha drama za kusanyiko la wilaya, nasi tulifurahia wee! Tulifurahia ushirika wa familia nyingi za kiroho, ambazo zilikuwa na uvutano mzuri juu ya binti zetu. Binti yetu mkubwa, Sara, aliolewa na painia wa pekee, Ray Smith, na wote wawili walitumikia wakiwa mapainia wa pekee karibu na mpaka wa Irian Jaya (sasa ni Papua, mkoa wa Indonesia). Waliishi kijijini katika nyumba ya nyasi, naye Sara husema kwamba alipata mazoezi mazuri sana kwenye mgawo huo.

Kuzoea Hali Zenye Kubadilika

Wakati huo wazazi wangu walihitaji utunzaji zaidi. Badala ya sisi kurudi Uingereza, wazazi wangu walikubali kuja kuishi nasi, na sote tukahamia Australia mwaka wa 1983. Pia walikaa kwa muda fulani pamoja na dada yangu Daphne, ambaye bado alikuwa akiishi Japani. Wazazi wangu walipokufa, mimi na Ann tuliamua kuanza upainia wa kawaida, na utumishi huo ulifanya nipate pendeleo lililoniogopesha sana.

Baada tu ya kuanza upainia tuliombwa tufanye kazi ya kuzunguka. Tangu utotoni, niliona ziara ya mwangalizi wa mzunguko kuwa tukio la kipekee. Sasa nilikuwa mwangalizi wa mzunguko. Mgawo huo ndio uliokuwa mgumu zaidi kati ya migawo tuliyokuwa tumefurahia kufikia wakati huo, lakini mara nyingi Yehova alitusaidia katika njia ambazo hatukuwa tumeshuhudia hapo awali.

Wakati wa ziara ya mwangalizi wa eneo la dunia Ndugu Theodore Jaracz nchini Australia mwaka wa 1990, tulimuuliza kama alifikiri tulikuwa wazee sana tusiweze kuwa watumishi wa wakati wote katika nchi nyingine. Alisema: “Namna gani Visiwa vya Solomon?” Hivyo, mimi na Ann tulipokuwa na umri wa miaka 50 na kitu, tulisafiri kwenda katika mgawo wetu rasmi wa kwanza wa umishonari.

Kutumikia Katika “Visiwa Vyenye Furaha”

Visiwa vya Solomon vinajulikana kuwa Visiwa Vyenye Furaha, na tumefurahia sana utumishi wetu huko katika miaka 10 iliyopita. Mimi na Ann tulipata kujua fadhili nyororo za ndugu na dada wa Visiwa vya Solomon nilipotumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya. Tuliguswa mioyo na ukarimu tulioonyeshwa. Wote walinionyesha fadhili nilipojitahidi kueleza mambo kwa njia niliyofikiri kuwa inaeleweka katika lugha ya Pijini ya Visiwa vya Solomon. Hiyo ni mojawapo ya lugha zenye maneno machache zaidi duniani.

Punde tu baada ya kufika katika Visiwa vya Solomon, wapinzani walijaribu kutuzuia tusitumie Jumba letu la Kusanyiko. Kanisa la Anglikana liliwashtaki Mashahidi wa Yehova, likidai kwamba sehemu fulani ya Jumba jipya la Kusanyiko huko Honiara ilikuwa katika ardhi yao. Serikali ilikubali dai lao, hivyo tukakata rufani dhidi ya uamuzi huo kwenye Mahakama Kuu. Matokeo ya rufani hiyo yangeamua kama tungebomoa Jumba letu la Kusanyiko linalotoshea watu 1,200.

Kesi hiyo ilisikilizwa mahakamani kwa juma moja. Wakili wa kanisa hilo aliongea kwa kiburi alipokuwa akitoa hoja zake dhidi yetu. Kisha Ndugu Warren Cathcart kutoka New Zealand, ambaye alikuwa wakili wetu akatoa hoja zake kwa njia yenye kusadikisha na kuthibitisha kwamba hoja za washtaki wetu hazikuwa na msingi. Kufikia Ijumaa, habari kuhusu kesi hiyo yenye kuvutia zilikuwa zimeenea sana, nayo mahakama ilijaa wakuu wa dini na serikali, na ndugu zetu Wakristo. Ninakumbuka kosa kwenye taarifa rasmi kuhusu ratiba ya Mahakama. Ilisema: “Kesi Kati ya Serikali ya Visiwa vya Solomon na Kanisa la Melanesia dhidi ya Yehova.” Tulishinda kesi hiyo.

Hata hivyo, utulivu wa kadiri katika Visiwa hivyo Vyenye Furaha haukudumu. Mimi na Ann tulijikuta tena katikati ya msukosuko na jeuri iliyosababishwa na mapinduzi ya kijeshi. Chuki ya kikabila ilisababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe. Serikali ilipinduliwa Juni 5, 2000, na mji mkuu ukakaliwa na wapiganaji wenye silaha. Kwa majuma kadhaa, Jumba letu la Kusanyiko lilitumiwa kama kituo cha watu wasio na makao. Wenye mamlaka walishangaa kuona kwamba ndugu zetu Wakristo wa makundi mawili yaliyokuwa yanakizozana, walikuwa wakiishi pamoja kama familia moja yenye amani ndani ya Jumba la Kusanyiko. Huo ulikuwa ushahidi ulioje!

Hata wapiganaji waliheshimu msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova. Hilo lilituwezesha kumshawishi mmoja wa makamanda kuruhusu vichapo na vifaa vingine visafirishwe kwa lori na kupelekewa kikundi kidogo cha akina ndugu katika eneo lililosimamiwa na jeshi la wapinzani. Tulipozipata familia ambazo zilikuwa zimetenganishwa nasi kwa miezi kadhaa, sote tulilengwa-lengwa na machozi.

Twashukuru kwa Mambo Mengi

Tunapofikiria maisha yetu katika utumishi wa Yehova, tunashukuru kwa mambo mengi sana. Tukiwa wazazi, tumefurahi kuwaona binti zetu wawili na waume zao, Ray na John, wakiendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Wametutegemeza sana katika mgawo wetu wa umishonari.

Kwa miaka 12 iliyopita, mimi na Ann tumekuwa na pendeleo la kutumika katika ofisi ya tawi ya Visiwa vya Solomon, na wakati huo tumeona idadi ya watangazaji wa Ufalme katika visiwa hivyo ikiongezeka maradufu na kuzidi 1,800. Hivi karibuni, nimepata pendeleo lingine la kuhudhuria Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi huko Patterson, New York. Kwa kweli, tumefurahia maisha yenye kuridhisha na yenye baraka nyingi kwa kudumisha roho ya umishonari.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona makala “Hatukusita-sita” katika gazeti Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 1977, la Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Siku ya arusi yetu, 1960

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tukiwa Uganda, Stanley na Esinala Makumba waliitia moyo sana familia yetu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Sara akielekea kwenye nyumba ya jirani

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kuchora picha kulinisaidia kuwafundisha wakaaji wa Visiwa vya Solomon

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kukutana na kutaniko la mbali katika Visiwa vya Solomon

[Picha katika ukurasa wa 26]

Familia yetu leo