Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sauti Yao Ilifika Katika Dunia Yote”

“Sauti Yao Ilifika Katika Dunia Yote”

“Sauti Yao Ilifika Katika Dunia Yote”

‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.’—MATHAYO 28:19.

1, 2. (a) Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi gani? (b) Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza waliweza kutimiza kazi nyingi hivyo?

MUDA mfupi kabla ya Yesu kupanda mbinguni, aliwapa wanafunzi wake kazi fulani. Aliwaambia hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.’ (Mathayo 28:19) Hiyo ilikuwa kazi kubwa kwelikweli!

2 Hebu wazia! Siku ya Pentekoste 33 W.K., wanafunzi 120 hivi walimwagiwa roho takatifu nao wakaanza kutimiza kazi hiyo kwa kuwaeleza wengine kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa ambaye kupitia kwake wokovu ungepatikana. (Matendo 2:1-36) Kikundi hicho kidogo kingewezaje kuwafikia “watu wa mataifa yote”? Jambo hilo halingewezekana kwa wanadamu, lakini “kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” (Mathayo 19:26) Wakristo wa mapema walisaidiwa na roho takatifu ya Yehova, nao walitambua uharaka wa nyakati. (Zekaria 4:6; 2 Timotheo 4:2) Hivyo, baada ya miaka michache tu, mtume Paulo angeweza kusema kwamba habari njema ilikuwa ikihubiriwa “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

3. Ni nini kilichofunika “ngano” ambayo ni Wakristo safi?

3 Katika miaka iliyo mingi ya karne ya kwanza, ibada ya kweli iliendelea kuenea. Hata hivyo, Yesu alikuwa ametabiri kwamba wakati ungefika ambapo Shetani angepanda “magugu” nayo “ngano” ambayo ni Wakristo wa kweli ingefunikwa kwa karne nyingi hadi wakati wa mavuno. Unabii huo ulitimia baada ya mitume kufa.—Mathayo 13:24-39.

Ongezeko la Haraka Leo

4, 5. Kuanzia mwaka wa 1919 Wakristo watiwa-mafuta walianza kufanya kazi gani, na kwa nini hiyo ilikuwa kazi kubwa sana?

4 Mnamo mwaka wa 1919 wakati ulifika wa kutenganisha magugu na ngano ambayo ni Wakristo safi. Wakristo watiwa-mafuta walijua kwamba bado walihitaji kufanya ile kazi kubwa waliyokabidhiwa na Yesu. Waliamini kabisa kwamba walikuwa wakiishi katika “siku za mwisho” nao walijua unabii huu wa Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:14) Naam, walijua kwamba kulikuwa na kazi nyingi ya kufanya.

5 Hata hivyo, Wakristo hao watiwa-mafuta walikuwa na kazi kubwa sana sawa na wanafunzi katika mwaka wa 33 W.K. Idadi yao ilikuwa elfu chache tu katika nchi chache. Wangewezaje kuhubiri habari njema “katika dunia yote inayokaliwa”? Kumbuka kwamba idadi ya watu duniani ilikuwa imeongezeka kutoka milioni 300 hivi Makaisari walipokuwa wakitawala, hadi bilioni 2 hivi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Idadi hiyo ingeendelea kuongezeka haraka katika karne yote ya 20.

6. Kufikia miaka ya 1930 Wakristo watiwa-mafuta walikuwa wamehubiri habari njema kwa kadiri gani?

6 Lakini kama vile ndugu zao wa karne ya kwanza, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walianza kazi waliyokabidhiwa huku wakiwa na imani kamili katika Yehova, na roho yake ilikuwa pamoja nao. Katikati ya miaka ya 1930 waeneza-injili wapatao 56,000 walikuwa wametangaza kweli ya Biblia katika nchi 115. Tayari kazi nyingi ilikuwa imefanywa, lakini bado kulikuwa na kazi nyingi zaidi.

7. (a) Ni kazi gani nyingine kubwa sana ambayo Wakristo watiwa-mafuta walikabili? (b) Kwa msaada wa “kondoo wengine,” kazi ya kukusanya imefanywa kwa kiwango gani kufikia sasa?

7 Kisha, walipopata ufahamu zaidi kuhusu ule “umati mkubwa” unaotajwa katika Ufunuo 7:9 wakatambua kwamba walikabili kazi nyingine kubwa sana. Pia ufahamu huo ulifanya Wakristo hao wenye bidii watambue kwamba wangepata msaada. Umati usio na hesabu wa “kondoo wengine,” yaani, waamini wenye tumaini la kuishi duniani, ulipaswa kukusanywa “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Yohana 10:16) Waamini hao ‘wangemtolea Yehova utumishi mtakatifu mchana na usiku.’ (Ufunuo 7:15) Hiyo inamaanisha kwamba wangesaidia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Isaya 61:5) Mwishowe, Wakristo watiwa-mafuta walifurahi kuona idadi ya waeneza-injili ikiongezeka kwa makumi ya maelfu, kisha kwa mamilioni. Katika mwaka wa 2003, kilele kipya cha 6,429,351 walishiriki katika kazi ya kuhubiri. Idadi kubwa ya wahubiri hao ni wa umati mkubwa. * Wakristo watiwa-mafuta wanathamini msaada huo, nao kondoo wengine wanafurahia pendeleo la kutegemeza ndugu zao watiwa-mafuta.—Mathayo 25:34-40.

8. Mashahidi wa Yehova waliitikiaje walipokabili mikazo mikubwa iliyotokea wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu?

8 Jamii ya ngano ilipodhihirika tena Shetani aliishambulia vikali. (Ufunuo 12:17) Alitendaje umati mkubwa ulipoanza kutokea? Kwa jeuri kali! Hatuna shaka kwamba yeye ndiye aliyechochea shambulio dhidi ya ibada ya kweli katika Vita vya Pili vya Ulimwengu. Katika pande zote mbili zilizokuwa zikipigana, Wakristo walikabili mkazo mkubwa. Ndugu na dada wengi wapendwa walipatwa na majaribu makali sana, na hata wengine wakafa kwa sababu ya imani yao. Hata hivyo, walionyesha wanakubaliana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Katika umoja na Mungu nitalisifu neno lake. Nimeliweka tegemeo langu kwa Mungu; sitaogopa. Mwenye mwili wa nyama anaweza kunitenda nini?” (Zaburi 56:4; Mathayo 10:28) Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine waliimarishwa na roho ya Yehova kusimama imara pamoja. (2 Wakorintho 4:7) Kwa sababu hiyo ‘neno la Mungu liliendelea kukua.’ (Matendo 6:7) Vita vilipoanza mwaka wa 1939, kulikuwa na Wakristo waaminifu 72,475 walioshiriki katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, ripoti isiyo kamili ya mwaka wa 1945, mwaka ambao vita hivyo viliisha, ilionyesha kwamba Mashahidi 156,299 walikuwa wakieneza habari njema. Shetani alishindwa kwelikweli!

9. Ni shule gani mpya zilizotangazwa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu?

9 Bila shaka, machafuko ya Vita vya Pili vya Ulimwengu hayakufanya watumishi wa Yehova watilie shaka kwamba kazi ya kuhubiri ingetimizwa. Hata katika mwaka wa 1943 vita vilipokuwa vimepamba moto kabisa, shule mbili mpya zilitangazwa. Shule moja ambayo sasa inaitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ilikusudiwa kufanywa katika makutaniko yote ili kuzoeza kila Shahidi kuhubiri na kufanya wanafunzi. Ile nyingine, Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, ilikusudiwa kuwazoeza mishonari ambao wangeendeleza kazi ya kuhubiri katika nchi za kigeni. Naam, vita vilipomalizika, Wakristo wa kweli walikuwa tayari kwa ajili ya utendaji ulioongezeka.

10. Bidii ya watu wa Yehova ilionekanaje wazi katika mwaka wa 2003?

10 Shule hizo zimetimiza kazi nzuri kama nini! Wote ambao wamezoezwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, vijana kwa wazee, wazazi kwa watoto na hata walemavu wameshiriki na wanaendelea kushiriki katika kutimiza kazi kubwa waliyokabidhiwa na Yesu. (Zaburi 148:12, 13; Yoeli 2:28, 29) Katika mwaka wa 2003, wastani wa watu 825,185 kila mwezi walionyesha kwamba wanatambua uharaka wa nyakati kwa kushiriki katika utumishi wa upainia kwa muda au kwa wakati wote. Katika mwaka huohuo, Mashahidi wa Yehova walitumia muda wa saa 1,234,796,477 kuwaelezea wengine habari njema za Ufalme. Hakika Yehova anafurahia bidii ya watu wake!

Katika Nchi za Kigeni

11, 12. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba mishonari wametimiza mambo mengi mazuri?

11 Kwa miaka mingi, wahitimu wa shule ya Gileadi wametimiza mambo mengi mazuri nao wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamefanya vivyo hivyo katika miaka ya hivi karibuni. Kwa mfano, nchini Brazili kulikuwa na wahubiri chini ya 400 wakati mishonari wa kwanza walipofika huko mwaka wa 1945. Mishonari hao na wengine waliokuja baadaye walifanya kazi kwa bidii pamoja na ndugu zao wa Brazili wenye juhudi, naye Yehova amebariki sana jitihada zao. Wale wanaokumbuka siku hizo za mapema wanafurahi kama nini wanapoona kwamba Brazili iliripoti kilele kipya cha wahubiri 607,362 mwaka wa 2003!

12 Fikiria nchi ya Japani. Kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, nchi hiyo ilikuwa na wahubiri wa Ufalme wapatao mia moja. Wakati wa vita, mateso makali yalipunguza idadi ya wahubiri, na vita vilipokwisha, ni Mashahidi wachache tu waliokuwa hai kiroho na kimwili. (Methali 14:32) Bila shaka, mnamo 1949, wachache hao waliodumisha utimilifu wao kabisa walifurahi kuwapokea mishonari 13 wa kwanza waliozoezwa Gileadi. Muda si muda, mishonari hao walianza kuvutiwa na shauku na ukarimu wa ndugu zao Wajapani na kuwapenda. Zaidi ya miaka 50 baadaye, Japani iliripoti kilele cha wahubiri 217,508 katika mwaka wa 2003! Kwa kweli, Yehova amewabariki sana watu wake katika nchi hiyo. Kuna ripoti kama hizo kutoka nchi nyingine nyingi. Wale wanaoweza kuhubiri katika nchi za kigeni wamesaidia sana kuenezwa kwa habari njema, hivi kwamba katika mwaka wa 2003 habari hiyo ilisikiwa katika nchi, visiwa, na maeneo 235 ulimwenguni. Naam, umati mkubwa unatoka katika “mataifa yote.”

‘Kutoka Makabila Yote, Vikundi vya Watu, na Lugha’

13, 14. Yehova alionyeshaje umuhimu wa kuhubiri habari njema katika ‘lugha zote’?

13 Muujiza wa kwanza kuripotiwa baada ya wanafunzi kutiwa mafuta na roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K. ulikuwa kuzungumza katika lugha za waliokusanyika. Huenda wote waliowasikiliza wanafunzi hao walizungumza lugha ya kimataifa, labda Kigiriki. Kwa kuwa walikuwa “watu wenye kumheshimu Mungu,” yaelekea pia walielewa ibada iliyofanywa katika lugha ya Kiebrania hekaluni. Lakini walivutiwa sana waliposikia habari njema katika lugha yao ya asili.—Matendo 2:5, 7-12.

14 Leo, pia kazi ya kuhubiri inafanywa katika lugha nyingi. Ilitabiriwa kwamba umati mkubwa haungetoka tu katika mataifa bali pia katika “makabila na vikundi vya watu na lugha.” Kupatana na hilo, Yehova alitabiri hivi kupitia Zekaria: “Watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Ingawa Mashahidi wa Yehova hawana zawadi ya kusema katika lugha mbalimbali, wanajua umuhimu wa kufundisha katika lugha za watu.

15, 16. Mishonari na wahubiri wengine wamekubali jinsi gani kufanya kazi ngumu ya kuhubiri katika lugha za wenyeji?

15 Ni kweli kwamba leo kuna lugha chache zinazotumiwa na watu wengi, kama vile Kiingereza, Kifaransa, na Kihispania. Lakini wale ambao wameondoka nyumbani kwao wakatumikie katika nchi nyingine hujitahidi kujifunza lugha za wenyeji ili iwe rahisi kwa wale ‘wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele,’ kupata habari njema. (Matendo 13:48) Hilo linaweza kuwa jambo gumu. Akina ndugu katika taifa la Tuvalu huko Pasifiki Kusini walipohitaji vichapo katika lugha yao, mmoja wa mishonari alikubali kufanya kazi ngumu ya kutafsiri. Kwa kuwa hakukuwa na kamusi yoyote, alianza kuandika orodha ya maneno ya Kituvalu. Baada ya muda, kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani * kilichapishwa katika Kituvalu. Mishonari walipofika Kurasao hakukuwa na kichapo chochote cha Biblia wala kamusi katika lugha ya wenyeji ya Papiamento. Pia wengi hawakupatana kuhusu jinsi lugha hiyo inavyopaswa kuandikwa. Hata hivyo, miaka miwili baada ya mishonari wa kwanza kuwasili, trakti ya kwanza inayozungumzia Biblia ilichapishwa katika lugha hiyo. Leo, Papiamento ni mojawapo ya lugha 113 ambazo gazeti Mnara wa Mlinzi huchapishwa sambamba na la Kiingereza.

16 Huko Namibia mishonari wa kwanza hawakupata Shahidi yeyote mwenyeji ambaye angewasaidia kutafsiri. Isitoshe, lugha moja ya wenyeji, Nama, haikuwa na maneno ambayo hutumiwa mara nyingi kama vile “-kamilifu.” Mishonari mmoja anaripoti: “Nilitumia hasa walimu wa shule waliokuwa wakijifunza Biblia ili wanisaidie kutafsiri. Kwa kuwa walikuwa na ujuzi kidogo kuhusu kweli, ilinibidi kuketi nao ili kuhakikisha kwamba kila sentensi ilikuwa sahihi.” Hata hivyo, mwishowe trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya ilitafsiriwa katika lugha nne za wenyeji. Leo, gazeti Mnara wa Mlinzi linachapishwa kwa ukawaida katika lugha ya Kwanyama na Ndonga.

17, 18. Mashahidi wanakabili kazi gani ngumu nchini Mexico na nchi nyingine?

17 Kihispania ndiyo lugha kuu ya Mexico. Hata hivyo, kabla ya Wahispania kufika, wenyeji walizungumza lugha nyingi na baadhi ya lugha hizo bado zinatumika. Hivyo, vichapo vya Mashahidi wa Yehova huko Mexico sasa huchapishwa katika lugha saba za wenyeji na pia katika Lugha ya Ishara ya Mexico. Huduma ya Ufalme katika lugha ya Maya ndicho kilichokuwa kichapo cha kwanza kuchapishwa kila mwezi katika lugha ya Wahindi wenyeji wa Amerika. Kwa kweli, kati ya watangazaji wa Ufalme 572,530 nchini Mexico kuna maelfu ya watu wa kabila la Maya, Azteki, na wengineo.

18 Hivi karibuni, watu wengi sana wamekimbilia nchi za kigeni wakiwa wakimbizi, au wakahama kwa sababu za kiuchumi. Kwa sababu hiyo, kwa mara ya kwanza nchi nyingi sasa zina maeneo yenye watu wengi wanaosema lugha za kigeni. Mashahidi wa Yehova wamekubali kufanya kazi hiyo ngumu. Kwa mfano, zaidi ya Kiitaliano kuna makutaniko na vikundi vinavyotumia lugha 22 nchini Italia. Ili kuwasaidia ndugu wawahubirie watu wanaosema lugha nyingine, hivi karibuni kulikuwa na madarasa ya kufundisha lugha 16 kutia ndani Lugha ya Ishara ya Kiitaliano. Katika nchi nyingine nyingi, Mashahidi wa Yehova wanafanya jitihada hiyohiyo kuwafikia wahamiaji wengi. Naam, kwa msaada wa Yehova, umati mkubwa unaendelea kutoka katika vikundi vya watu wa lugha nyingi sana.

“Katika Dunia Yote”

19, 20. Ni maneno gani ya Paulo yanayotimizwa katika njia kubwa leo? Eleza.

19 Katika karne ya kwanza, mtume Paulo aliandika hivi: “Je, walikosa kusikia? Kwani, kwa kweli, ‘sauti yao ilifika katika dunia yote, na maneno yao mpaka miisho ya dunia inayokaliwa.’” (Waroma 10:18) Maneno hayo yalikuwa kweli katika karne ya kwanza na ni ya kweli hata zaidi leo. Mamilioni ya watu, labda wengi zaidi kuliko wakati wowote wa zamani, wanasema hivi: “Nitambariki Yehova nyakati zote; daima sifa yake itakuwa katika kinywa changu.”—Zaburi 34:1.

20 Zaidi ya hayo, kazi hiyo inasonga mbele. Idadi ya watangazaji wa Ufalme inazidi kuongezeka. Wakati mwingi zaidi unatumiwa katika kazi ya kuhubiri. Mamilioni ya ziara za kurudia na mamia ya maelfu ya mafunzo ya Biblia yanaongozwa. Na wapya wanaopendezwa wanazidi kuongezeka. Mwaka jana, kilele kipya cha watu 16,097,622 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Bila shaka, bado kuna kazi nyingi ya kufanya. Na tuendelee kuiga utimilifu imara wa ndugu zetu ambao wamevumilia mateso makali. Na tuonyeshe bidii kama ya ndugu zetu wote ambao tangu mwaka wa 1919 wamejitoa katika utumishi wa Yehova. Wote na wakubaliane na kiitikio hiki cha mtunga-zaburi: “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah. Msifuni Yah!”—Zaburi 150:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona ripoti ya kila mwaka kwenye ukurasa wa 18 hadi 21 katika gazeti hili.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Katika mwaka wa 1919 akina ndugu walianza kufanya kazi gani, na kwa nini hiyo ilikuwa kazi kubwa sana?

• Ni nani waliokusanywa ili kusaidia kazi ya kuhubiri?

• Mishonari na wahubiri wengine wanaotumikia katika nchi za kigeni wametimiza mambo gani mengi?

• Unaweza kutaja uthibitisho gani kuonyesha kwamba Yehova anabariki kazi ya watu wake leo?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 18-21]

2003 RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Machafuko ya Vita vya Pili vya Ulimwengu hayakufanya Wakristo watilie shaka kwamba kazi ya kuhubiri ingetimizwa

[Hisani]

Explosion: U.S. Navy photo; others: U.S. Coast Guard photo

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Umati mkubwa ungetoka katika makabila na lugha zote