Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wote na Wautangaze Utukufu wa Yehova

Wote na Wautangaze Utukufu wa Yehova

Wote na Wautangaze Utukufu wa Yehova

“Mhesabieni Yehova utukufu na nguvu. Mhesabieni Yehova utukufu wa jina lake.”—ZABURI 96:7, 8.

1, 2. Yehova anahesabiwa utukufu kutoka chanzo gani, na ni nani wanaohimizwa washiriki kufanya hivyo?

DAUDI, mwana wa Yese, alikulia karibu na Bethlehemu akiwa mvulana mchungaji. Bila shaka, mara nyingi alitazama anga kubwa lenye nyota nyingi katika usiku mtulivu, alipokuwa akichunga kondoo za baba yake katika malisho ya kondoo ya mbali! Ni wazi kwamba alikumbuka mambo hayo aliyoona alipoongozwa na roho takatifu ya Mungu kutunga na kuimba maneno haya yenye kupendeza ya Zaburi ya 19: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake. Kamba yake ya kupimia imefika duniani pote, na maneno yake yamefika kwenye miisho ya nchi yenye kuzaa.”—Zaburi 19:1, 4.

2 Mbingu zenye kutia woga ambazo Yehova aliumba hutangaza utukufu wake siku baada ya siku, usiku baada ya usiku, bila usemi, maneno, wala sauti. Uumbaji haukomi kamwe kuutangaza utukufu wa Mungu, na hilo hutunyenyekeza tutafakari ushuhuda huo wa kimya-kimya ambao huonekana “duniani pote” na wakaaji wote wa dunia. Hata hivyo, ushahidi ambao uumbaji unatoa kimya-kimya hautoshi. Wanadamu waaminifu wanahimizwa washirikiane na uumbaji kutoa ushahidi kwa kutumia sauti zao. Mtunga-zaburi asiyetajwa jina aliwaambia waabudu waaminifu maneno haya yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu: “Mhesabieni Yehova utukufu na nguvu. Mhesabieni Yehova utukufu wa jina lake.” (Zaburi 96:7, 8) Wale ambao wana uhusiano wa karibu na Yehova wanafurahia kutenda kulingana na himizo hilo. Hivyo basi, ni nini kinachohusika katika kumhesabia Mungu utukufu?

3. Kwa nini wanadamu humhesabia Mungu utukufu?

3 Kumhesabia Mungu utukufu kunahusisha mengi zaidi kuliko maneno matupu tu. Waisraeli katika siku za Isaya walimtukuza Mungu kwa midomo tu, lakini wengi hawakuwa wanyoofu. Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Watu hawa wamekaribia na vinywa vyao, nao wamenitukuza kwa midomo yao mitupu, nao wameupeleka moyo wao mbali nami.” (Isaya 29:13) Sifa yoyote iliyotolewa na watu hao haikuwa na maana. Ili sifa iwe na maana, ni lazima itoke katika moyo uliojaa upendo kwa Yehova na unaotambua kwa unyoofu utukufu wake wa kipekee. Yehova pekee ndiye Muumba. Yeye ndiye Mweza-Yote, Mwenye Haki, na mwenye upendo usio na kifani. Yeye ndiye chanzo cha wokovu wetu na mwenye haki ya kutawala ambaye kila kiumbe mbinguni na duniani kinapaswa kujitiisha kwake. (Ufunuo 4:11; 19:1) Ikiwa tunaamini mambo hayo kikweli, na tumtukuze kwa moyo wetu wote.

4. Yesu alitoa maagizo gani kuhusu jinsi ya kumtukuza Mungu, na tunawezaje kuyatimiza?

4 Yesu Kristo alitueleza jinsi ya kumtukuza Mungu. Alisema hivi: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi na kujionyesha kuwa wanafunzi wangu.” (Yohana 15:8) Tunazaa matunda mengi jinsi gani? Kwanza, kwa kuhubiri kwa nafsi yote “habari njema ya ufalme” na hivyo kujiunga na vitu vyote vilivyoumbwa ‘kutangaza’ kuhusu ‘sifa za Mungu ambazo hazionekani.’ (Mathayo 24:14; Waroma 1:20) Isitoshe, kwa njia hiyo sote tunashiriki—kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja—kufanya wanafunzi wapya ambao wanaongezea sauti zao katika kumwimbia Yehova Mungu sifa. Pili, tunasitawisha matunda ambayo roho takatifu inatokeza ndani yetu na kujitahidi kuiga sifa bora za Yehova Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 5:1; Wakolosai 3:10) Kwa kuiga sifa hizo, sisi humtukuza Mungu kwa mwenendo wetu wa kila siku.

“Katika Dunia Yote”

5. Eleza jinsi Paulo alivyokazia daraka la Wakristo la kumtukuza Mungu kwa kuwaeleza wengine imani yao.

5 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alikazia daraka la Wakristo la kumtukuza Mungu kwa kuwaeleza wengine imani yao. Ujumbe mkuu katika kitabu cha Waroma ni kwamba wale tu wanaoonyesha imani katika Yesu Kristo ndio wanaoweza kuokolewa. Katika sura ya 10 ya barua yake, Paulo alionyesha kwamba Wayahudi wa asili wa siku zake bado walikuwa wakijaribu kuwa na msimamo wa uadilifu kwa kufuata Sheria ya Musa, ingawa “Kristo [alikuwa] mwisho wa Sheria.” Kwa hiyo, Paulo anasema: “Ukitangaza waziwazi lile ‘neno lililo katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kuonyesha imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa.” Tangu wakati huo na kuendelea, “[hakujawa] na tofauti kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa maana kuna Bwana yuleyule juu ya wote, aliye tajiri kwa wale wote wanaomwitia. Kwa maana ‘kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.’”—Waroma 10:4, 9-13.

6. Paulo alitumiaje andiko la Zaburi 19:4?

6 Kisha kwa kupatana na akili Paulo anauliza hivi: “Watawezaje kumwitia yeye ambaye hawajamwamini? Nao watamwaminije yeye ambaye hawajamsikia? Nao watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?” (Waroma 10:14) Paulo anasema hivi kuhusu Waisraeli: “Si wote waliotii habari njema.” Kwa nini Waisraeli hawakutii? Kwa sababu walikosa imani wala si kwa sababu walikosa nafasi ya kufanya hivyo. Paulo anaonyesha jambo hilo kwa kunukuu andiko la Zaburi 19:4 na kuonyesha kwamba linahusiana na kazi ya Kikristo ya kuhubiri wala si ule ushahidi wa kimya-kimya unaotolewa na uumbaji. Anasema hivi: “Kwani, kwa kweli, ‘sauti yao ilifika katika dunia yote, na maneno yao mpaka miisho ya dunia inayokaliwa.’” (Waroma 10:16, 18) Naam, kama vile uumbaji usio na uhai unavyomtukuza Yehova, Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kila mahali habari njema za wokovu na hivyo kumtukuza Mungu “duniani pote.” Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo pia alieleza jinsi habari njema zilivyokuwa zimehubiriwa kwa mapana na marefu. Alisema kwamba habari njema zilikuwa zimehubiriwa “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

Mashahidi Wenye Bidii

7. Kulingana na Yesu, Wakristo wana daraka gani?

7 Yaelekea Paulo aliandika barua yake kwa Wakolosai miaka 27 hivi baada ya kifo cha Yesu Kristo. Kazi ya kuhubiri ingeweza kueneaje hadi Kolosai katika muda mfupi hivyo? Ilienea hivyo kwa sababu Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa wenye bidii na Yehova alibariki bidii yao. Yesu alikuwa ametabiri kwamba wafuasi wake wangekuwa wahubiri wenye bidii aliposema hivi: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10) Zaidi ya kutoa unabii huo, Yesu alitoa amri hii katika mistari ya mwisho ya Injili ya Mathayo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Muda mfupi baada ya Yesu kupanda mbinguni, wafuasi wake waliweza kutimiza maneno hayo.

8, 9. Kulingana na Matendo, Wakristo waliitikiaje amri za Yesu?

8 Baada ya kumwagwa kwa roho takatifu, siku ya Pentekoste 33 W.K., jambo la kwanza ambalo wafuasi washikamanifu wa Yesu walifanya ni kutoka na kuhubiri, wakiueleza umati uliokuwa Yerusalemu “juu ya mambo makuu ya Mungu.” Kazi yao ya kuhubiri ilikuwa na matokeo sana, na “nafsi karibu elfu tatu” zikabatizwa. Wanafunzi waliendelea kumtukuza Mungu hadharani na kwa bidii, hivyo wakapata matokeo mazuri.—Matendo 2:4, 11, 41, 46, 47.

9 Muda si muda, viongozi wa kidini walitambua utendaji wa Wakristo hao. Kwa kukasirishwa na jinsi Petro na Yohana walivyozungumza waziwazi, viongozi hao waliwaamuru mitume hao waache kuhubiri. Nao wakajibu hivi: “Hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” Baada ya kutishwa na kuachiliwa, Petro na Yohana walirudi kwa ndugu zao, na wote wakaungana kusali kwa Yehova. Walimwomba Yehova hivi kwa ujasiri: ‘Wawezeshe watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote.’—Matendo 4:13, 20, 29.

10. Ni upinzani gani ulioanza kujitokeza, nao Wakristo wa kweli walitendaje?

10 Mambo yaliyotukia baadaye yalithibitisha kwamba sala hiyo ilipatana na mapenzi ya Yehova. Mitume walikamatwa, kisha wakafunguliwa kimuujiza na malaika. Malaika huyo aliwaambia: “Nendeni, na, mkiisha kusimama katika hekalu, semeni na watu maneno yote juu ya maisha haya.” (Matendo 5:18-20) Yehova aliendelea kuwabariki mitume kwa sababu walitii. Kwa hiyo, “kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Matendo 5:42) Ni wazi kwamba upinzani mkali haukuweza kabisa kuwazuia wafuasi wa Yesu wasimhesabie Mungu utukufu hadharani.

11. Wakristo wa mapema walikuwa na mtazamo gani kuhusu kazi ya kuhubiri?

11 Muda mfupi baadaye, Stefano alikamatwa na kupigwa mawe hadi akafa. Alipouawa mateso makali yalitokea huko Yerusalemu, na wanafunzi wote isipokuwa mitume walilazimika kutawanyika kutoka Yerusalemu. Je, walivunjwa moyo na mateso? Hata kidogo. Tunasoma hivi: “Wale waliokuwa wametawanywa wakapita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:1, 4) Bidii ya kutangaza utukufu wa Mungu ilionekana tena na tena. Katika Matendo sura ya 9 tunasoma kwamba Farisayo Sauli wa Tarso, alipokuwa akisafiri kuelekea Damasko ili akaanzishe mateso dhidi ya wanafunzi wa Yesu, alimwona Yesu katika maono na akapigwa na upofu. Anania alimponya Sauli upofu wake kimuujiza huko Damasko. Ni jambo gani ambalo Sauli, ambaye baadaye aliitwa mtume Paulo, alifanya kwanza? Sura hiyo inasema: ‘Alianza mara moja kumhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba Huyu ndiye Mwana wa Mungu.’—Matendo 9:20.

Kila Mtu Alishiriki Katika Kazi ya Kuhubiri

12, 13. (a) Kulingana na wanahistoria, kutaniko la Kikristo la mapema lilijulikana kwa jambo gani? (b) Kitabu cha Matendo na maneno ya Paulo yanakubalianaje na taarifa za wanahistoria?

12 Inajulikana sana kwamba kila mtu katika kutaniko la Kikristo la mapema alishiriki katika kazi ya kuhubiri. Philip Schaff anaandika hivi kuhusu Wakristo wa siku hizo: ‘Kila kutaniko lilizingatia kazi ya kuhubiri, na kila Mkristo alihubiri.’ (Historia ya Kanisa la Kikristo, cha Kiingereza) W. S. Williams anasema hivi: ‘Kwa ujumla tunaweza kusema kwamba Wakristo wote wa Kanisa la mapema, hasa wale waliokuwa na zawadi za roho za kuponya, walihubiri injili.’ (Huduma Tukufu ya Watu wa Kawaida, cha Kiingereza) Tena anasisitiza hivi: “Yesu Kristo hakusema kwamba kazi ya kuhubiri ni pendeleo la watu fulani wenye cheo.” Hata Celsus, adui wa kale wa Ukristo, aliandika hivi: “Wafumaji wa sufu, washona-viatu, watengeneza-ngozi, watu wa kawaida wasio na elimu yoyote, walikuwa wahubiri wa injili wenye bidii.”

13 Usahihi wa taarifa hizo unaonyeshwa na habari za historia katika kitabu cha Matendo. Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., baada ya wanafunzi wote kumwagiwa roho takatifu, wanaume kwa wanawake walitangaza hadharani mambo matukufu ya Mungu. Baada ya mateso yaliyosababishwa na kuuawa kwa Stefano, Wakristo wote waliokuwa wametawanyika katika maeneo mbalimbali walieneza habari njema kwa mapana na marefu. Miaka 28 hivi baadaye, Paulo alikuwa akiwaandikia Wakristo wote Waebrania, wala si jamii ndogo tu ya makasisi, aliposema: “Kupitia yeye sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Akieleza jinsi alivyoiona kazi ya kuhubiri Paulo alisema: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!” (1 Wakorintho 9:16) Ni wazi kwamba Wakristo wote waaminifu wa karne ya kwanza walihisi hivyo.

14. Kuna uhusiano gani kati ya imani na kuhubiri?

14 Kwa kweli, Mkristo wa kweli anapaswa kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwa sababu inahusiana sana na imani. Paulo alisema: “Kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Waroma 10:10) Je, ni kikundi kidogo tu katika kutaniko, kama vile jamii ya makasisi, ambacho huonyesha imani na hivyo kuwa na daraka la kuhubiri? La, hasha! Wakristo wote wa kweli husitawisha imani yenye nguvu katika Bwana Yesu Kristo nao huchochewa kutangaza hadharani imani hiyo kwa wengine. Wasipofanya hivyo, imani yao imekufa. (Yakobo 2:26) Kwa sababu Wakristo wote washikamanifu wa karne ya kwanza katika Wakati wetu wa Kawaida walionyesha imani yao kwa njia hiyo, walililetea sifa kuu jina la Yehova.

15, 16. Toa mifano ili kuonyesha kwamba kazi ya kuhubiri iliendelea kujapokuwa matatizo?

15 Katika karne ya kwanza, Yehova aliwabariki watu wake kwa ukuzi japo matatizo ndani na nje ya kutaniko. Kwa mfano, Matendo sura ya 6 inataja hali fulani ya kutoelewana kati ya wageuzwa-imani waliozungumza Kiebrania na wale waliozungumza Kigiriki. Tatizo hilo lilitatuliwa na mitume. Hivyo, tunasoma: “Neno la Mungu likaendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani ukaanza kuitii imani.”—Matendo 6:7.

16 Baadaye, kulitokea mvutano wa kisiasa kati ya Mfalme Herode Agripa wa Yudea na watu wa Tiro na Sidoni. Wakaaji wa majiji hayo walimwomba afanye amani nao kwa kumsifusifu, na hivyo akatoa hotuba ya watu wote. Watu waliokusanyika walianza kupaaza sauti: “Ni sauti ya mungu, wala si ya mwanadamu!” Papo hapo malaika wa Yehova akampiga Herode Agripa, naye akafa kwa sababu hakumpa Mungu utukufu.” (Matendo 12:20-23) Lilikuwa jambo lenye kushtua kama nini kwa wale waliowatumaini watawala wa kibinadamu! (Zaburi 146:3, 4) Hata hivyo, Wakristo waliendelea kumtukuza Yehova. Hivyo, “neno la Yehova likaendelea kukua na kuenea” japo hali hiyo ya kisiasa yenye msukosuko.—Matendo 12:24.

Wakati Huo na Sasa

17. Katika karne ya kwanza, idadi yenye kuongezeka ilijiunga na kazi gani?

17 Naam, kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote katika karne ya kwanza lilifanyizwa na wasifaji wa Yehova Mungu wenye bidii. Wakristo wote washikamanifu walieneza habari njema. Baadhi yao walipata watu wenye kupendezwa na, kama Yesu alivyosema, wakawafundisha kutii mambo yote aliyowaamuru. (Mathayo 28:19, 20) Kwa sababu hiyo kutaniko likakua, na watu wengi zaidi wakajiunga na Mfalme Daudi wa kale kumhesabia Yehova sifa. Wote walikubaliana na maneno haya yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu: “Ninakusifu, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote, nami nitalitukuza jina lako mpaka wakati usio na kipimo, kwa maana fadhili zako zenye upendo ni kuu kunielekea mimi.”—Zaburi 86:12, 13.

18. (a) Kuna tofauti gani kati ya kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza na dini za leo zinazojiita za Kikristo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

18 Kwa kuzingatia mambo hayo, maneno ya profesa wa theolojia Allison A. Trites yanaamsha fikira. Akilinganisha dini za leo zinazojiita za Kikristo, alisema: “Makanisa leo hukua kibiolojia (wakati watoto wa familia fulani ambayo huenda kanisani wanapodai kuwa na imani) au kwa kuhama (wakati mshiriki mpya anapohama kutoka kanisa lingine). Hata hivyo, katika kitabu cha matendo, ukuzi ulitokana na kugeuza watu imani, kwa kuwa kutaniko lilikuwa linaanza tu kazi yake.” Je, hilo linamaanisha kwamba Ukristo wa kweli haukui jinsi Yesu alivyosema ungepaswa kukua? La, hasha! Wakristo wa kweli leo ni wenye bidii katika kumhesabia Mungu sifa hadharani kama walivyofanya Wakristo wa karne ya kwanza. Tutaona jambo hilo katika makala inayofuata.

Je, Unaweza Kueleza?

• Sisi humtukuza Mungu katika njia gani?

• Paulo alitumiaje andiko la Zaburi 19:4?

• Kuna uhusiano gani kati ya imani na kuhubiri?

• Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilijulikana kwa jambo gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8, 9 zimeandaliwa na]

Mbingu zinashuhudia daima utukufu wa Yehova

[Hisani]

Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kazi ya kuhubiri na sala zinahusiana sana