Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ahadi Unazoweza Kutumaini

Ahadi Unazoweza Kutumaini

Ahadi Unazoweza Kutumaini

MIKA nabii wa Mungu alijua kwamba mara nyingi ahadi hazitegemeki. Katika siku zake, hata wenzi wa karibu zaidi hawangeweza kutumainiwa kutimiza ahadi zao sikuzote. Kwa hiyo, Mika alionya: “Msimwamini mwenzi. Msimtegemee rafiki msiri. Linda milango ya kinywa chako kutokana na yeye anayelala kifuani pako.”—Mika 7:5.

Je, Mika aliruhusu hali hiyo ya kusikitisha ifanye atilie shaka ahadi zote? La! Alitumaini kabisa ahadi za Mungu wake Yehova. Mika aliandika hivi: “Lakini mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7.

Kwa nini Mika alikuwa na uhakika huo? Kwa sababu alijua kwamba Yehova hutimiza ahadi zake sikuzote. Kila neno ambalo Mungu alikuwa amewaapia mababu za Mika lilitimia kabisa. (Mika 7:20) Uaminifu wa Yehova wakati uliopita ulifanya Mika aamini kwamba Yeye angetimiza ahadi Zake za wakati ujao.

“Halikukosa Kutimia Hata Neno Moja”

Kwa mfano, Mika alijua kwamba Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri. (Mika 7:15) Yoshua ambaye alishuhudia ukombozi huo, aliwatia moyo Waisraeli wenzake watumaini ahadi zote za Mungu. Kwa msingi gani? Yoshua aliwakumbusha, “Nanyi mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote, kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.”—Yoshua 23:14.

Waisraeli walijua vizuri kwamba Yehova alikuwa amewafanyia mambo mazuri. Alitimiza ahadi yake kwa babu yao Abrahamu mwenye kumwogopa Mungu kwamba uzao wake ungekuwa mwingi kama nyota na ungemiliki nchi ya Kanaani. Yehova pia alimwambia Abrahamu kwamba wazao wake wangeteswa kwa miaka 400 lakini wangerudi Kanaani “katika kizazi cha nne.” Na yote hayo yakatimia.—Mwanzo 15:5-16; Kutoka 3:6-8.

Waisraeli walikaribishwa vizuri huko Misri katika siku za Yosefu, mwana wa Yakobo. Baadaye, Wamisri waliwalazimisha kwa ukatili kufanya kazi ngumu, lakini kupatana na ahadi ya Mungu, wazao hao wa Abrahamu walikombolewa kutoka utumwani Misri baada ya kipindi cha vizazi vinne. *

Katika miaka 40 iliyofuata, Waisraeli waliona uthibitisho zaidi kwamba Yehova hutimiza ahadi zake sikuzote. Waamaleki walipowashambulia Waisraeli bila kuchokozwa, Mungu aliwapigania na kuwalinda watu wake. Alitosheleza mahitaji yao yote ya kimwili wakati wa safari yao ya miaka 40 nyikani na mwishowe akawaingiza katika Nchi ya Ahadi. Yoshua alipochanganua jinsi Yehova alivyoshughulika na wazao wa Abrahamu, angeweza kusema hivi kwa uhakika: “Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa ameipa nyumba ya Israeli; mambo yote yalitimia.”—Yoshua 21:45.

Sitawisha Imani Katika Ahadi za Mungu

Unawezaje kusitawisha imani katika ahadi za Yehova, kama Mika na Yoshua? Unawezaje kusitawisha tumaini katika wengine? Kwa kujua mambo mengi iwezekanavyo kuwahusu. Kwa mfano, unaweza kujua jinsi walivyo wenye kutegemeka kwa kuona kwamba wao hujaribu kutimiza ahadi zao zote kwa uaminifu. Unapozidi kuwajua watu hao, unaanza kuwatumaini hatua kwa hatua. Unaweza kufanya vivyo hivyo unapositawisha imani katika ahadi za Mungu.

Njia moja ya kusitawisha imani katika ahadi hizo ni kutafakari juu ya uumbaji na sheria zinazouongoza. Wanasayansi wanaziamini sheria hizo, kama zile ambazo hufanya chembe moja ya binadamu igawanyike na kuongezeka na hivyo kutokeza chembe nyingi sana zinazofanyiza mwili wako. Bila shaka, sheria zinazoongoza tabia ya vitu na nishati katika ulimwengu wote zilianzishwa na Mtunga-Sheria anayetegemeka kabisa. Hakika, unaweza kutumaini ahadi zake, kama vile unavyoweza kutumaini sheria zinazoongoza uumbaji wake.—Zaburi 139:14-16; Isaya 40:26; Waebrania 3:4.

Kupitia nabii Isaya, aliyeishi wakati mmoja na Mika, Yehova alitumia mfano wa majira ambayo hutokea kwa ukawaida na pia mzunguko wa maji wenye kushangaza ili kuonyesha jinsi neno lake linavyotegemeka. Kila mwaka mvua ilinyesha. Ililowesha udongo na kuwawezesha watu kupanda mbegu zao na kuvuna. Yehova alisema hivi kuhusiana na hilo: “Kama vile mvua inayonyesha hushuka, na theluji, kutoka mbinguni nayo hairudi mahali pale, mpaka kwa kweli iwe imeinywesha dunia na kuifanya izae na kuchipuka, na mbegu kweli iwe imepewa mpandaji na mkate kupewa anayekula, ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:10, 11.

Ahadi Hakika Kuhusu Paradiso

Unaweza kusitawisha tumaini katika Muumba kwa kuchunguza uumbaji, lakini kuna jambo lingine unalohitaji kufanya ikiwa unataka kujifunza kuhusu ahadi ambazo ni sehemu ya ‘neno linalotoka katika kinywa chake.’ Ili kujifunza kuhusu ahadi hizo na kuzitumaini, unahitaji kuchunguza Maandiko yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu kuhusu kusudi lake kwa dunia na namna anavyoshughulika na wanadamu.—2 Timotheo 3:14-17.

Nabii Mika alizitumaini ahadi za Yehova. Leo, tofauti na wakati wa Mika, unaweza kupata habari nyingi zaidi zilizoongozwa na roho ya Mungu. Unaposoma Biblia na kuitafakari, wewe pia unaweza kusitawisha imani kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Ahadi hizo zinahusu wanadamu wote wala si wazao wa Abrahamu tu. Yehova alimwahidi hivi mzee huyo wa ukoo mwenye kumwogopa: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Sehemu ya kwanza ya “uzao” wa Abrahamu ni Masihi, Yesu Kristo.—Wagalatia 3:16.

Kupitia Yesu Kristo, Yehova atahakikisha kwamba wanadamu watiifu wanabarikiwa. Mungu ameahidi kufanya nini leo? Andiko la Mika 4:1, 2 linajibu kwa maneno haya ya kinabii: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na vikundi vya watu vitamiminika huko. Na mataifa mengi hakika yatakwenda na kusema: ‘Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova na kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.’”

Wale wanaojifunza kuhusu njia za Yehova ‘hufua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu.’ Wao huacha tabia zozote za kivita. Hivi karibuni, dunia itajawa na watu wanyoofu, na hakuna mtu atakayewatetemesha kwa woga. (Mika 4:3, 4) Naam, Neno la Mungu linaahidi kwamba chini ya utawala wa Ufalme mikononi mwa Yesu Kristo, Yehova atawaondoa wakandamizaji wote duniani.—Isaya 11:6-9; Danieli 2:44; Ufunuo 11:18.

Hata wale ambao wameteseka na kufa kwa sababu ya uasi wa mwanadamu dhidi ya Mungu watafufuliwa wakiwa na taraja la kuishi milele duniani. (Yohana 5:28, 29) Shetani na roho wake waovu ambao ndio huchochea uovu, hawatakuwepo, nayo matokeo ya dhambi ya Adamu yataondolewa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. (Mathayo 20:28; Waroma 3:23, 24; 5:12; 6:23; Ufunuo 20:1-3) Na itakuwaje kwa wanadamu watiifu? Watapewa uzima wa milele nao watakuwa na afya kamilifu katika dunia paradiso!—Zaburi 37:10, 11; Luka 23:43; Ufunuo 21:3-5.

Hizo ni ahadi nzuri kama nini! Lakini je, unaweza kuziamini? Ndiyo. Hizo si ahadi za wanadamu ambao huenda wakawa na nia nzuri lakini wasiwe na uwezo wa kuzitimiza. Hizo ni ahadi za Mungu Mweza-Yote, asiyeweza kusema uwongo na ambaye “hakawii kuhusiana na ahadi yake.” (2 Petro 3:9; Waebrania 6:13-18) Unaweza kutumaini kabisa ahadi zote katika Biblia, kwa kuwa Chanzo chake ni “Yehova Mungu wa ukweli.”—Zaburi 31:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona Insight on the Scriptures, buku la 1, ukurasa wa 911-912, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.”—YOSHUA 23:14

[Picha katika ukurasa wa 4 and 5]

Yehova alitimiza ahadi zake kwa Waisraeli kwenye Bahari Nyekundu na nyikani

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova alitimiza ahadi yake kwa Abrahamu. Yesu Kristo, ambaye ni Uzao wake, atawaletea wanadamu baraka