Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Kutoka Kitabu cha Mwanzo—II

Mambo Makuu Kutoka Kitabu cha Mwanzo—II

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Kutoka Kitabu cha Mwanzo—II

KITABU cha Mwanzo kinazungumzia miaka 2,369 ya historia ya binadamu tangu kuumbwa kwa mwanadamu wa kwanza Adamu, hadi kifo cha Yosefu, mwana wa Yakobo. Makala iliyotangulia ya gazeti hili ilizungumzia sura za kwanza 10 na pia mistari 9 ya sura ya 11, zinazotia ndani habari za tangu uumbaji hadi kujengwa kwa mnara wa Babeli. * Makala hii inazungumzia mambo makuu ya sura zinazobaki za kitabu cha Mwanzo, kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu.

ABRAHAMU AWA RAFIKI YA MUNGU

(Mwanzo 11:10–23:20)

Miaka 350 hivi baada ya Gharika, mtu anayekuja kuwa wa pekee sana kwa Mungu anazaliwa katika ukoo wa Shemu, mwana wa Noa. Jina lake ni Abramu, ambalo baadaye linabadilishwa kuwa Abrahamu. Kwa amri ya Mungu, Abramu anaondoka jiji la Uru la Wakaldayo na kuwa mkaaji wa mahema katika nchi ambayo Yehova anamwahidi angempa yeye na wazao wake. Kwa sababu ya imani na utii wake, Abrahamu anakuja kuitwa “rafiki ya Yehova.”—Yakobo 2:23.

Yehova anachukua hatua dhidi ya wakaaji wa Sodoma na majiji yaliyo karibu, huku akimhifadhi Loti na binti zake. Ahadi ya Mungu inatimizwa wakati Isaka mwana wa Abrahamu anapozaliwa. Miaka kadhaa baadaye, imani ya Abrahamu inajaribiwa wakati Yehova anapomwagiza amtoe mwana wake kuwa dhabihu. Abrahamu yu tayari kutii lakini malaika anamzuia. Bila shaka, Abrahamu ni mtu mwenye imani, naye anahakikishiwa kwamba kupitia uzao wake mataifa yote yatajibariki. Abrahamu anahuzunishwa sana na kifo cha Sara mke wake mpendwa.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

12:1-3—Agano la Abrahamu lilianza kufanya kazi wakati gani, na lingedumu kwa muda gani? Yaonekana agano la Yehova na Abramu kwamba “familia zote za nchi zitajibariki kupitia kwa [Abramu]” lilianza kufanya kazi Abramu alipovuka Efrati akielekea Kanaani. Bila shaka, hiyo ilikuwa Nisani 14, 1943 K.W.K., yaani, miaka 430 kabla Waisraeli hawajakombolewa kutoka Misri. (Kutoka 12:2, 6, 7, 40, 41) Agano la Abrahamu ni “agano la mpaka wakati usio na kipimo.” Litaendelea kufanya kazi mpaka familia za dunia zibarikiwe na maadui wote wa Mungu waangamizwe.—Mwanzo 17:7; 1 Wakorintho 15:23-26.

15:13—Unabii kuhusu mateso ya miaka 400 ya uzao wa Abramu ulitimizwa wakati gani? Kipindi hicho cha mateso kilianza 1913 K.W.K. wakati Isaka mwana wa Abrahamu alipoachishwa kunyonya akiwa na umri wa miaka 5 hivi na ndugu yake wa kambo Ishmaeli, mwenye umri wa miaka 19, alipokuwa ‘akimdhihaki.’ (Mwanzo 21:8-14; Wagalatia 4:29) Kilimalizika Waisraeli walipokombolewa utumwani Misri mwaka wa 1513 K.W.K.

16:2—Je, ilifaa kwa Sarai kumpa Abramu kijakazi wake Hagari kuwa mke? Jambo ambalo Sarai alifanya lilipatana na desturi ya wakati huo, kwamba mke aliye tasa alipaswa kumpa mume wake suria ili amzalie mrithi. Zoea la kuoa wake wengi lilianza katika ukoo wa Kaini. Mwishowe, zoea hilo likawa desturi na baadhi ya watumishi wa Yehova wakaanza kuifuata. (Mwanzo 4:17-19; 16:1-3; 29:21-28) Hata hivyo, Yehova hakuacha kiwango chake cha awali cha ndoa ya mke mmoja. (Mwanzo 2:21, 22) Ni wazi kwamba Noa na wana wake, ambao walipewa tena amri ya ‘kuzaa wawe wengi na kuijaza dunia,’ walikuwa wameoa kila mmoja mke mmoja. (Mwanzo 7:7; 9:1; 2 Petro 2:5) Yesu Kristo alikazia tena kiwango hicho cha ndoa ya mke mmoja.—Mathayo 19:4-8; 1 Timotheo 3:2, 12.

19:8—Je, ilikuwa kosa kwa Loti kuwatoa binti zake kwa Wasodoma? Kulingana na kanuni za watu wa Mashariki, mkaribishaji alikuwa na daraka la kuwalinda wageni walio nyumbani mwake, hata kama hiyo ingemaanisha kupoteza uhai wake. Loti alikuwa tayari kufanya hivyo. Alitoka nje, akafunga mlango, na kukabiliana na genge hilo kwa ujasiri akiwa peke yake. Wakati alipowatoa binti zake, yaelekea Loti alikuwa ametambua kwamba wageni wake walikuwa wajumbe wa Mungu, na huenda aliona kwamba Mungu angeweza kuwalinda binti zake kama Alivyomlinda shangazi yake Sara huko Misri. (Mwanzo 12:17-20) Naam, mwishowe Loti na binti zake waliokolewa.

19:30-38—Je, Yehova alipuuza tendo la Loti la kulewa na kuzaa wana na binti zake wawili? Yehova hapuuzi ngono kati ya watu wa familia wala ulevi. (Mambo ya Walawi 18:6, 7, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10) Kwa kweli, Loti alichukizwa na ‘vitendo vya kuasi sheria’ vya wakaaji wa Sodoma. (2 Petro 2:6-8) Binti za Loti walimlewesha baba yao kwa sababu walitambua kwamba hangekubali kufanya ngono nao kama hangekuwa amelewa. Lakini kwa kuwa walikuwa wageni katika nchi hiyo, binti zake walihisi kwamba hiyo ndiyo iliyokuwa njia pekee ya kuzuia familia ya Loti isitoweke. Masimulizi hayo yaliandikwa katika Biblia ili kuonyesha uhusiano kati ya Wamoabu (kupitia Moabu) na Waamoni (kupitia Benami) na wazao wa Abrahamu, yaani Waisraeli.

Mambo Tunayojifunza:

13:8, 9. Abrahamu anatuwekea kielelezo kizuri sana cha kutatua matatizo. Hatupaswi kamwe kuharibu uhusiano wenye amani ili kujinufaisha kifedha, au kwa sababu ya mapendezi yetu ya kibinafsi, au kiburi.

15:5, 6. Abrahamu alipoanza kuzeeka na bado hakuwa na mwana, alizungumza na Mungu wake kuhusu jambo hilo. Yehova naye akamhakikishia kwamba atakuwa na uzao. Matokeo yakawaje? Abrahamu “akawa na imani katika Yehova.” Imani yetu itaimarishwa tukisali kwa Yehova na kumweleza yaliyo moyoni mwetu, tukikubali uhakikisho wake kutoka katika Biblia, na kumtii.

15:16. Yehova hakutekeleza hukumu yake juu ya Waamori (au, Wakanaani) kwa vizazi vinne. Kwa nini? Kwa sababu yeye ni Mungu mvumilivu. Alingoja hadi wakati ambapo hakukuwa na tumaini lolote kwa watu hao kubadilika. Tunapaswa kuwa wavumilivu kama Yehova.

18:23-33. Yehova haharibu watu kiholela. Yeye huwalinda waadilifu.

19:16. Loti “alipoendelea kukawia,” malaika walikuwa karibu kumkokota yeye na familia yake na kumtoa nje ya jiji la Sodoma. Tunakuwa wenye hekima tunapotambua uharaka wa nyakati huku tukingojea mwisho wa ulimwengu mwovu.

19:26. Lingekuwa jambo la upumbavu kama nini kukengeushwa fikira au kutamani vitu tulivyoacha katika ulimwengu!

YAKOBO ANA WANA 12

(Mwanzo 24:1–36:43)

Abrahamu anapanga ndoa ya Isaka na Rebeka, mwanamke ambaye anamwamini Yehova. Anazaa mapacha, Esau na Yakobo. Esau anadharau haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza na kuiuza kwa Yakobo, ambaye baadaye anapokea baraka ya baba yake. Yakobo anakimbilia Padan-aramu, ambako anaoa Lea na Raheli na kuchunga makundi ya wanyama wa baba yao kwa miaka 20 kabla ya kuondoka pamoja na familia yake. Kupitia Lea, Raheli, na wajakazi wake wawili, Yakobo ana wana 12 na binti mmoja. Yakobo anapigana mweleka na malaika naye anabarikiwa, na jina lake linabadilishwa kuwa Israeli.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

28:12, 13—Ndoto ya Yakobo iliyohusisha “ngazi” ilimaanisha nini? “Ngazi” hiyo ambayo huenda ilifanana na mawe yaliyokuwa yamepangwa kama ngazi, ilionyesha kwamba kuna mawasiliano kati ya dunia na mbingu. Kupanda na kushuka kwa malaika wa Mungu kulionyesha kwamba malaika huhudumu kwa njia fulani ya pekee kati ya Yehova na wanadamu walio na kibali chake.—Yohana 1:51.

30:14, 15—Kwa nini Raheli aliachilia nafasi ya kulala na mume wake kwa kubadilishana na baadhi ya dudai? Nyakati za kale, dudai zilitumiwa kama dawa ya kulevya na ya kuzuia au kupunguza mkazo wa ghafula wa misuli. Pia tunda hilo lilidhaniwa kwamba lilikuwa na uwezo wa kuchochea tamaa ya ngono na kuongeza uwezo wa mwanadamu wa kuzaa au lilisaidia katika kupata mimba. (Wimbo wa Sulemani 7:13) Ingawa Biblia haifunui nia ya Raheli ya kufanya hivyo, huenda alifikiri kwamba dudai hizo zingemsaidia kupata mimba na hivyo kuondoa aibu yake ya kuwa tasa. Hata hivyo, Yehova “alifungua tumbo lake la uzazi” baada ya miaka kadhaa kupita.—Mwanzo 30:22-24.

Mambo Tunayojifunza:

25:23. Yehova anaweza kutambua chembe za urithi zinazofanyiza mtoto ambaye hajazaliwa na kutumia uwezo wake wa kujua mambo kabla hayajatokea na hivyo kumchagua kimbele mtu atakayetimiza makusudi yake. Hata hivyo, yeye hapangi kimbele jinsi maisha ya watu yatakavyokuwa mwishowe.—Hosea 12:3; Waroma 9:10-12.

25:32, 33; 32:24-29. Hangaiko la Yakobo la kupata haki ya mzaliwa wa kwanza na kupigana mweleka usiku kucha na malaika ili kupata baraka linaonyesha kwamba alithamini kwelikweli mambo ya kiroho. Yehova ametupatia mambo mengi ya kiroho, kama vile uhusiano wetu pamoja naye, tengenezo lake, fidia, Biblia, na tumaini la Ufalme. Na tuwe kama Yakobo kwa kuthamini mambo hayo.

34:1, 30. Tatizo ‘lililofanya Yakobo atengwe’ lilianza kwa sababu Dina alifanya urafiki na watu wasiompenda Yehova. Tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima.

YEHOVA AMBARIKI YOSEFU HUKO MISRI

(Mwanzo 37:1–50:26)

Wivu unafanya wana wa Yakobo wamuuze ndugu yao Yosefu kuwa mtumwa. Akiwa Misri, Yosefu anatiwa gerezani kwa sababu anadumisha viwango vya Mungu vya maadili kwa ujasiri na kwa uaminifu. Baada ya muda, anatolewa gerezani ili kumfasiria Farao ndoto zake, ambazo zinatabiri miaka saba ya shibe na miaka saba ya njaa. Baadaye, Yosefu anawekwa kuwa msimamizi wa chakula wa Misri. Ndugu zake wanakuja Misri kutafuta chakula kwa sababu ya njaa. Familia hiyo inaungana tena na kuishi katika nchi yenye rutuba ya Gosheni. Kabla tu ya kufa, Yakobo anawabariki wana wake na kutamka unabii unaotoa tumaini hakika la baraka nyingi za wakati ujao. Mwili wa Yakobo unapelekwa Kanaani ukazikwe. Yosefu anapokufa akiwa na umri wa miaka 110, mwili wake unatiwa dawa, ili mwishowe usafirishwe hadi Nchi ya Ahadi.—Kutoka 13:19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

43:32—Kwa nini lilikuwa chukizo kwa Wamisri kula chakula pamoja na Waebrania? Huenda sababu kuu ilikuwa hasa ubaguzi wa kidini au kiburi cha kijamii. Wamisri pia walichukia wachungaji. (Mwanzo 46:34) Kwa nini? Huenda wachungaji walikuwa karibu na tabaka la chini katika mfumo wa matabaka wa Wamisri. Au labda kwa kuwa hakukuwa na ardhi ya kutosha ya kulima, Wamisri waliwachukia watu waliotafuta malisho kwa ajili ya wanyama wao.

44:5—Je, kweli Yosefu alitumia kikombe kusoma ishara za bahati? Yaonekana kikombe cha fedha na mambo yaliyosemwa kukihusu yalikuwa tu sehemu ya mpango fulani wa ujanja. Yosefu alikuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova. Ni kweli kwamba, hakutumia kikombe hicho kusoma ishara za bahati, kama vile tu Benyamini hakuwa kwa kweli amekiiba.

49:10—“Fimbo ya enzi” na “fimbo ya kiongozi” inamaanisha nini? Fimbo ya enzi ni kirungu kinachobebwa na mtawala kama ishara ya mamlaka. Fimbo ya kiongozi ni bakora ndefu inayoonyesha uwezo wake wa kuongoza. Yakobo alitaja vitu hivyo kuonyesha kwamba kabila la Yuda lingepewa uwezo na mamlaka makubwa hadi Shilo afike. Mzao huyo wa Yuda ni Yesu Kristo, ambaye Yehova amempa utawala wa kimbingu. Kristo ana mamlaka ya kifalme na uwezo wa kuongoza.—Zaburi 2:8, 9; Isaya 55:4; Danieli 7:13, 14.

Mambo Tunayojifunza:

38:26. Yuda alimtendea kimakosa binti-mkwe wake Tamari, aliyekuwa mjane. Hata hivyo, alipoelezwa kwamba yeye ndiye aliyekuwa amemtunga mimba, Yuda alikubali kosa lake kwa unyenyekevu. Sisi pia tunapaswa kuwa tayari kukubali makosa yetu.

39:9. Jibu la Yosefu kwa mke wa Potifa linaonyesha kwamba alikuwa na maoni sawa na ya Mungu kuhusu maadili na kwamba dhamiri yake iliongozwa na kanuni za kimungu. Je, sisi pia hatupaswi kujitahidi kufanya vivyo hivyo tunapozidi kupata ujuzi sahihi wa ile kweli?

41:14-16, 39, 40. Yehova anaweza kubadili hali za wale wanaomwogopa. Maafa yanapotokea, ni jambo la hekima kumtumaini Yehova na kuendelea kuwa waaminifu kwake.

Walikuwa na Imani Thabiti

Bila shaka, Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu walikuwa watu wenye imani ambao walimwogopa Mungu. Masimulizi katika kitabu cha Mwanzo kuhusu maisha yao, yanaimarisha imani kwelikweli na hutufunza mambo mengi yenye thamani.

Unaweza kunufaika na masimulizi hayo unapoendelea na usomaji wako wa Biblia wa kila juma kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kutafakari mambo hayo makuu kutafanya masimulizi hayo yawe yenye kupendeza.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona makala “Neno la Yehova Liko Hai—Mambo Makuu Kutoka Kitabu cha Mwanzo—I” katika toleo la Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 2004.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Abrahamu alikuwa mtu mwenye imani

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yehova ambariki Yosefu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Loti mwadilifu na binti zake walihifadhiwa

[Picha katika ukurasa wa 29]

Yakobo alithamini mambo matakatifu. Je, wewe unayathamini?