Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni hali gani zilizosababisha Yuda afanye ngono na mwanamke ambaye alifikiria kuwa ni kahaba, kama inavyoelezwa katika Mwanzo 38:15, 16?

Ingawa Yuda alifanya ngono na mwanamke aliyemfikiria kuwa kahaba, ukweli ni kwamba mwanamke huyo hakuwa kahaba. Kulingana na Mwanzo sura ya 38, hivi ndivyo ilivyotukia.

Kabla ya mwana wa kwanza wa Yuda kupata watoto wowote wa kiume kupitia mke wake Tamari, mwana huyo aliuawa kwa sababu “alikuwa mbaya machoni pa Yehova.” (Mwanzo 38:7) Wakati huo, desturi ya ndoa ya ndugu-mkwe ilifuatwa. Kulingana na desturi hiyo mwanamume alipokufa bila mrithi, ndugu yake alipaswa kumuoa mjane aliyeachwa na kulala naye ili azae mrithi. Lakini Onani, mwana wa pili wa Yuda, alikataa kutimiza daraka hilo. Kwa hiyo, alikufa kutokana na hukumu ya Mungu. Kisha, Yuda akamrudisha Tamari, binti-mkwe wake kwa baba yake hadi wakati ambapo Shela, mwana wake wa tatu, angekuwa na umri wa kutosha ili kumuoa Tamari. Hata hivyo, muda ulipita, lakini Yuda hakumruhusu Shela amuoe Tamari. Kwa hiyo, mke wa Yuda alipokufa, Tamari alitumia njia fulani ya werevu ya kupata mrithi kupitia Yuda, Mwisraeli aliyekuwa baba-mkwe wake. Alijifanya kahaba wa hekalu na kuketi kando ya barabara ambayo alijua kwamba Yuda angepitia.

Kwa kuwa Yuda hakumtambua Tamari, alifanya ngono naye. Kwa werevu, Tamari alimwomba Yuda ampe vitu fulani ili akubali kulala naye, na baadaye akavitumia kuthibitisha kwamba mimba hiyo ilikuwa ya Yuda. Ukweli ulipojulikana, Yuda hakumlaumu Tamari bali alisema hivi kwa unyenyekevu: “Yeye ni mwadilifu kuliko mimi, kwa sababu sikumpa Shela mwanangu awe mke wake.” Na jambo linalofaa zaidi ni kwamba “hakulala naye tena baada ya hayo.”—Mwanzo 38:26.

Yuda alikosea kwa sababu hakumtoa Shela kwa Tamari awe mume wake kama alivyoahidi. Pia alifanya ngono na mwanamke ambaye alifikiri kwamba ni kahaba wa hekalu. Jambo hilo lilipingana na kusudi la Mungu kwamba, mwanamume afanye ngono katika ndoa tu. (Mwanzo 2:24) Kwa kweli, Yuda hakufanya ngono na kahaba. Badala yake, alitimiza bila kujua daraka la mwana wake Shela kwa kufanya ndoa ya ndugu-mkwe na hivyo akawa baba ya mrithi halali.

Lakini Tamari hakuwa na mwenendo mbaya kiadili. Wana wake wawili mapacha hawakuonwa kuwa wana wa uasherati. Wakati Boazi wa Bethlehemu alipomuoa Ruthu Mmoabu katika ndoa ya ndugu-mkwe, wazee wa Bethlehemu walimsifu Perezi mwana wa Tamari na kumwambia Boazi hivi: “Nyumba yako na iwe kama nyumba ya Perezi, ambaye Tamari alimzalia Yuda, kutokana na uzao ambao Yehova atakupa kutoka kwa huyu mwanamke kijana.” (Ruthu 4:12) Pia Perezi anatajwa katika orodha ya mababu wa Yesu Kristo.—Mathayo 1:1-3; Luka 3:23-33.