Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtukuze Mungu, Si Mwanadamu

Mtukuze Mungu, Si Mwanadamu

Mtukuze Mungu, Si Mwanadamu

KATIKA miezi ya hivi karibuni, watu wanaopenda uadilifu duniani walijifunza jinsi ya kumtukuza Mungu kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya “Mtukuzeni Mungu.” Na tupitie programu yenye kuelimisha ya kusanyiko hilo.

Kwa wahudhuriaji walio wengi programu hiyo iliyotegemea Biblia iliendelea kwa siku tatu mfululizo, lakini kwa wale waliohudhuria makusanyiko ya pekee ya kimataifa, programu hiyo ilichukua siku nne. Kwa ujumla, wahudhuriaji walisikiliza hotuba za Kimaandiko zaidi ya 30, na baadhi ya hotuba hizo ziliwasaidia wathamini zaidi mambo ya kiroho. Mambo yaliyoonwa yaliwaimarisha imani, maonyesho yakakazia jinsi ya kutumia kanuni za Biblia, nayo drama iliyoigizwa kwa mavazi maalumu ikaonyesha magumu ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walikabili. Ikiwa ulihudhuria mojawapo ya makusanyiko hayo, kwa nini usipitie maandishi yako unaposoma makala hii? Tuna hakika kwamba ukifanya hivyo utakumbuka mambo mengi mazuri ya kiroho ambayo pia ni yenye kuelimisha.

Kichwa cha Siku ya Kwanza: “Wewe Wastahili, Yehova, . . . Kupokea Utukufu”

Baada ya wimbo na sala ya kufungua, msemaji wa kwanza aliwakaribisha wote kwa uchangamfu kupitia hotuba iliyokazia sababu kuu ya kusanyiko hilo: “Tumekusanyika ili Kumtukuza Mungu.” Akinukuu Ufunuo 4:11, msemaji alikazia kichwa kikuu cha kusanyiko. Baada ya hapo alifafanua maana ya kumtukuza Mungu. Akitumia kitabu cha Zaburi, alikazia kwamba kumtukuza Mungu kunatia ndani “ibada,” ‘utoaji shukrani,’ na “sifa.”—Zaburi 95:6; 100:4, 5; 111:1, 2.

Hotuba iliyofuata ilikuwa na kichwa “Wanaomtukuza Mungu Hubarikiwa.” Msemaji alitaja jambo fulani lenye kupendeza. Kwa kuwa kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita katika nchi 234 duniani, tunaweza kusema kwamba wanamtukuza Yehova mchana na usiku. (Ufunuo 7:15) Wasikilizaji walitiwa moyo wakati ndugu na dada kadhaa Wakristo walio katika aina fulani ya utumishi wa pekee walipohojiwa.

Hotuba iliyofuata ilikuwa na kichwa “Uumbaji Unatangaza Utukufu wa Mungu.” Ingawa mbingu halisi hazisemi chochote, zinautukuza ukuu wa Mungu na kutusaidia tuthamini zaidi utunzaji wake wenye upendo. Jambo hilo lilifafanuliwa kwa undani zaidi.—Isaya 40:26.

Mateso, upinzani, uvutano wa ulimwengu, na maelekeo yenye dhambi hujaribu uaminifu wa maadili wa Wakristo wa kweli. Hivyo, wasikilizaji walihitaji kusikiliza kwa makini hotuba yenye kichwa “Tembea kwa Uaminifu wa Maadili.” Msemaji alizungumzia Zaburi ya 26 mstari kwa mstari na kuwahoji wanashule wawili Mashahidi. Mmoja wao alidumisha msimamo imara wa maadili na yule mwingine alikuwa akitumia wakati mwingi kwenye vitumbuizo visivyofaa lakini akachukua hatua kushinda tatizo hilo.

Kichwa cha hotuba ya msingi kilikuwa, “Maono Matukufu ya Kinabii Hutuchochea!” Msemaji alitaja vielelezo vya nabii Danieli na mitume Yohana na Petro kuwa watu ambao imani yao ilitiwa nguvu na maono matukufu ya kinabii yaliyohusu kusimamishwa na kuanza kufanya kazi kwa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Msemaji alisema hivi kuhusu mtu yeyote ambaye huenda amesahau uthibitisho ulio wazi kwamba tunaishi wakati wa mwisho: “Tunatumaini kwa unyofu kwamba watu hao watakaza tena macho yao kwenye uhalisi wa kuwapo kwa Kristo katika utukufu wa Ufalme nao watasaidiwa wapate tena nguvu za kiroho.” Programu ya asubuhi kwenye makusanyiko ya Kiswahili imalizika kwa hotuba yenye kichwa, “Hatua Muhimu ya Kiroho!” ambapo Biblia nzima ya New World Translation ilitolewa katika Kiswahili.

Programu ya alasiri ilianza kwa hotuba yenye kichwa “Yehova Huwafunulia Wanyenyekevu Utukufu Wake.” Msemaji alionyesha jinsi Yehova anavyoweka kielelezo cha unyenyekevu, ingawa yeye ndiye Mkuu zaidi katika ulimwengu wote. (Zaburi 18:35) Wale walio wanyenyekevu kikweli hupata kibali cha Yehova, lakini yeye huwapinga wale ambao hujifanya kuwa wanyenyekevu wanaposhughulika na watu wa umri wao au wakubwa wao huku wakiwatendea kwa ukali wale walio chini ya uongozi wao.—Zaburi 138:6.

Halafu, unabii wa Biblia ukazungumziwa katika mfululizo wa hotuba zilizokazia mambo mbalimbali kuhusu kichwa kikuu: “Unabii wa Amosi—Ujumbe Wake kwa Ajili ya Siku Zetu.” Msemaji wa kwanza alitaja kielelezo cha Amosi na kuonyesha daraka letu la kuwaonya watu kuhusu hukumu ya Yehova inayokuja. Kichwa cha hotuba yake kilikuwa “Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri.” Msemaji wa pili aliuliza hivi: “Je, Yehova atakuja kukomesha uovu na mateso katika dunia hii?” Hotuba yake yenye kichwa, “Hukumu ya Mungu Juu ya Waovu,” ilionyesha kwamba sikuzote hukumu ya Mungu ni ya haki, haiepukiki, nayo huchagua. Msemaji wa mwisho katika mfululizo huo alikazia kichwa “Yehova Huuchunguza Moyo.” Wale wanaotamani kumpendeza Yehova watatii maneno haya ya Amosi 5:15: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.”

Vileo, kama vile divai ambayo hufurahisha moyo, vinaweza kutumiwa vibaya. Katika hotuba yake “Epuka Mtego wa Kutumia Kileo Kupita Kiasi,” msemaji alitaja hatari za kimwili na za kiroho za kutumia kileo kupita kiasi, hata kama mtu hatalewa. Alitaja kanuni inayotoa mwongozo: Kwa kuwa watu wana uwezo mbalimbali wa kustahimili kileo, kiasi chochote cha kileo kinachokufanya usiwe na “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri” kimepita kiasi.—Methali 3:21, 22.

Kwa kuwa tunaishi katika nyakati za hatari, hotuba iliyofuata, “Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu,’” ilikuwa yenye kufariji. Sala, roho takatifu, na Wakristo wenzetu wanaweza kutusaidia kuvumilia.

Hotuba ya mwisho siku hiyo, “Nchi Nzuri—Mwonjo wa Paradiso,” ilimalizika kwa jambo lililowasisimua na kuwafurahisha wote, yaani, kutolewa kwa kichapo kipya chenye ramani nyingi za Biblia! Kina kichwa, Ona Nchi Nzuri.

Kichwa cha Siku ya Pili: “Wahubirini Mataifa Habari za Utukufu Wake”

Baada ya kuchunguza andiko la siku, mfululizo wa pili kwenye kusanyiko ulitolewa nao ulikuwa na kichwa, ‘Tutoe Kama Vioo Mrudisho wa Utukufu wa Yehova.’ Hotuba ya kwanza ilizungumzia jinsi tunavyoweza ‘Kueneza Habari Njema Kila Mahali’ nayo ilitia ndani maigizo ya mambo halisi yaliyoonwa katika utumishi wa shambani. Katika hotuba ya pili iliyokuwa na onyesho kuhusu ziara ya kurudia, msemaji alizungumzia kichwa, “Kuondoa Shela Kutoka kwa Wale Waliopofushwa.” Mahojiano yenye kuvutia kuhusu mambo yaliyoonwa katika utumishi yalifanya hotuba ya mwisho ya mfululizo huo ambayo ilikuwa na kichwa “Tufanye Hivyo kwa Ukamili Zaidi Katika Huduma Yetu,” iwe yenye kupendeza.

Hotuba iliyofuata kwenye programu ilikuwa na kichwa “Wanachukiwa Bila Sababu.” Ilikuwa na mahojiano yenye kutia moyo ya watu waaminifu ambao kwa nguvu za Mungu walidumisha uaminifu-maadili chini ya upinzani.

Baada ya hotuba ya ubatizo ambayo hungojewa kwa hamu sana, wote wanaostahili hubatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji. Ubatizo wa maji huonyesha kwamba mtu amejiweka wakfu kabisa kwa Yehova. Hivyo, kichwa cha hotuba hiyo kilifaa sana: “Kuishi Kulingana na Wakfu Wetu Humtukuza Mungu.”

Programu ya alasiri ilianza kwa hotuba iliyowatia moyo wasikilizaji wajichunguze, “Kusitawisha Maoni ya Kristo Kuhusu Umashuhuri.” Msemaji alitaja jambo hili lenye kupendeza: Tunapata umashuhuri kwa kuiga unyenyekevu wa Kristo. Hivyo, Mkristo hapaswi kutafuta madaraka ili kutosheleza tamaa ya kibinafsi. Anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi niko tayari kufanya kazi zenye kusaidia wengine ambazo hazitatambuliwa kwa urahisi?’

Je, wewe huchoka? Jibu ni wazi. Wote walifurahia hotuba “Kuchoka Kimwili Wala Si Kiroho.” Mahojiano na Mashahidi waliotumikia kwa muda mrefu yalionyesha kwamba Yehova anaweza kutufanya ‘tuwe na uwezo kupitia roho yake.’—Waefeso 3:16.

Tunaweza kujizoeza sifa ya ukarimu ingawa hatuzaliwi nayo. Jambo hilo muhimu lilikaziwa katika hotuba “Tuwe Wakarimu, Tayari Kushiriki.” Kisha swali hili lenye kuamsha fikira likaulizwa: “Je, sisi tuko tayari kutumia dakika kadhaa kwa siku tukiwa pamoja na ndugu na dada walio wazee, wagonjwa, walioshuka moyo, au walio wapweke?”

Wasikilizaji walivutiwa na hotuba “Jihadhari na ‘Sauti ya Wageni.’” Hotuba hii iliwalinganisha wafuasi wa Yesu na kondoo ambao husikiliza sauti yake tu akiwa “mchungaji mwema” na ambao hawaisikilizi “sauti ya wageni” inayotokana na vyanzo vingi vya kibinadamu vyenye uvutano wa Ibilisi.—Yohana 10:5, 14, 27.

Lazima waimbaji wa kwaya waimbe kwa upatano ili waeleweke. Ili kumtukuza Mungu, ni lazima waabudu wa kweli duniani pote wawe na umoja. Hivyo, hotuba “Kumtukuza Mungu ‘kwa Kinywa Kimoja’” ilitoa maagizo yenye manufaa kuhusu jinsi sote tunavyoweza kusema “lugha safi” na kumtumikia Yehova “bega kwa bega.”—Sefania 3:9.

Wazazi, hasa wale walio na watoto wadogo walifurahia sana hotuba ya mwisho ya siku hiyo, “Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani.” Wasikilizaji walifurahi na kushangaa wakati kitabu kipya chenye kurasa 256 kilipotolewa. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kitawasaidia wazazi watumie wakati kwa njia yenye kunufaisha kiroho pamoja na watoto ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu.

Kichwa cha Siku ya Tatu: “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”

Siku ya mwisho ya kusanyiko ilianza kwa wazo la kiroho kupitia vikumbusho vya andiko la siku. Sehemu ya kwanza ya programu ya siku hiyo ilikazia fikira zaidi familia. Hotuba ya kwanza, “Enyi Wazazi, Jengeni Familia Zenu,” iliwatayarisha wasikilizaji. Baada ya kuzungumzia madaraka ya wazazi ya kuandaa mahitaji ya kimwili ya familia zao, msemaji alithibitisha kwamba daraka kuu la wazazi ni kuwaandalia watoto wao mahitaji ya kiroho.

Msemaji aliyefuata alizungumza kuhusu watoto katika hotuba yenye kichwa “Jinsi Vijana Wanavyomsifu Yehova.” Alisema kwamba vijana ni kama “matone ya umande” kwa sababu ni wengi na nguvu yao ya ujana huburudisha. Watu wazima hufurahi kumtumikia Yehova pamoja na vijana. (Zaburi 110:3) Hotuba hiyo ilikuwa na mahojiano yenye kuvutia ya vijana wenye mfano mzuri.

Sikuzote drama za Biblia ambazo huigizwa kwa mavazi maalumu, ni sehemu yenye kuvutia ya makusanyiko ya wilaya. Kusanyiko hilo lilikuwa na drama kama hiyo. Drama yenye kichwa “Kuhubiri kwa Ujasiri Licha ya Upinzani” iliigiza wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza. Drama hiyo ilikuwa yenye kufurahisha, na hasa yenye kufundisha. Hotuba iliyofuata drama hiyo, “Tangaza Habari Njema ‘Bila Kuacha,’” ilikazia mambo makuu ya drama hiyo.

Wahudhuriaji wote walitazamia kwa hamu jambo kuu katika programu ya Jumapili, yaani hotuba ya watu wote “Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?” Msemaji alithibitisha jinsi wanasayansi na wanadini kwa ujumla hawamtukuzi Mungu. Watu wanaoitwa kwa jina lake tu, ambao wanahubiri na kufundisha kweli kumhusu Yehova, ndio wanaotukuza kikweli jina lake leo.

Hotuba ya watu wote ilifuatwa na muhtasari wa funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo. Kisha ikafuata hotuba ya mwisho, “‘Endeleeni Kuzaa Matunda Mengi’ ili Kumtukuza Yehova.” Msemaji aliwasomea wasikilizaji azimio lenye mambo kumi yaliyokazia njia mbalimbali za kumtukuza Yehova, Muumba, na kuwaomba walikubali. Wote katika makusanyiko yote duniani waliitikia kwa kusema “Ndiyo.”

Hivyo, kusanyiko lilipomalizika kila mtu aliyehudhuria alikuwa akikumbuka kichwa “Mtukuzeni Mungu.” Sikuzote na tujitahidi kumtukuza Mungu wala si wanadamu kwa msaada wa roho ya Yehova na tengenezo lake linaloonekana.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Makusanyiko ya Kimataifa

Makusanyiko ya kimataifa ya siku nne yalifanywa huko Afrika, Asia, Australia, Ulaya, na Amerika Kaskazini na Kusini. Mashahidi kutoka sehemu mbalimbali za dunia walialikwa kuhudhuria makusanyiko hayo. Hivyo, kulikuwa na “ubadilishanaji wa kitia-moyo” kati ya wageni na wenyeji. (Waroma 1:12) Marafiki wa zamani walikutana na kuimarisha urafiki wao, na wengine wakapata marafiki wapya. Sehemu ya pekee ya makusanyiko hayo ya kimataifa ilikuwa hotuba yenye kichwa “Ripoti Kutoka Nchi Nyingine.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

Vichapo Vipya Vinavyomtukuza Mungu

Kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Kiswahili ya “Mtukuzeni Mungu,” Biblia ya New World Translation ilitolewa katika Kiswahili pamoja na vichapo vingine vipya viwili. Atlasi ya Biblia Ona Nchi Nzuri ina jalada ya kudumu na kurasa 36 zenye ramani na picha za maeneo ya Biblia. Atlasi hiyo ina ramani za milki ya Ashuru, Babiloni, Umedi-Uajemi, Ugiriki, na Roma na kila ukurasa una rangi kamili. Kuna ramani mbalimbali zinazoonyesha huduma ya Yesu na kuenea kwa Ukristo.

Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kina kurasa 256 na picha 230 hivi. Tunaweza kutumia vipindi vingi vyenye kufurahisha pamoja na watoto kwa kutazama tu picha na kujibu maswali yenye kuamsha fikira yaliyo katika kitabu hicho. Kitabu hiki kipya kimekusudiwa kupinga mashambulizi ya Shetani dhidi ya vijana wetu, ambayo yana lengo la kupotosha maadili yao.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mishonari walisimulia mambo yaliyoonwa yenye kuimarisha imani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ubatizo ulikuwa sehemu muhimu katika makusanyiko ya “Mtukuzeni Mungu”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Vijana kwa wazee hufurahia drama za Biblia