Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mungu Hakai Katika Mahekalu Yaliyofanywa kwa Mikono’

‘Mungu Hakai Katika Mahekalu Yaliyofanywa kwa Mikono’

‘Mungu Hakai Katika Mahekalu Yaliyofanywa kwa Mikono’

BILA shaka, mtume Paulo aliyajua mahekalu ya Athena kwa kuwa yalijengwa katika majiji mengi aliyoyatembelea katika safari zake za umishonari. Kichapo The Encyclopædia Britannica, kinasema kwamba Athena alikuwa mungu maarufu wa vita, hekima, na pia “mungu wa sanaa na kazi za ustadi ambazo kwa ujumla watu walifanya wakati wa amani.”

Hekalu maarufu zaidi la Athena lilikuwa Parthenon, ambalo lilikuwa limejengwa huko Athene, jiji lililopewa jina la mungu huyo wa kike. Hekalu hilo lililokuwa mojawapo ya mahekalu makubwa zaidi katika ulimwengu wa kale, lilikuwa na sanamu ya Athena yenye urefu wa meta 12, ambayo ilitengenezwa kwa dhahabu na pembe za tembo. Paulo alipotembelea Athene, hekalu hilo lililojengwa kwa mawe meupe ya marumaru tayari lilikuwa mashuhuri kwa miaka 500 hivi.

Paulo alipokuwa akihubiria kikundi cha Waathene kuhusu ‘Mungu ambaye hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono,’ walikuwa mahali ambapo hekalu la Parthenon lilikuwa linaonekana. (Matendo 17:23, 24) Labda fahari ya mahekalu ya Athena au utukufu wa sanamu zake ulifanya baadhi ya wasikilizaji wa Paulo wamwone Athena kuwa mashuhuri zaidi kuliko Mungu asiyeonekana ambaye hawakumjua. Hata hivyo, kama Paulo alivyosema, hatupaswi kuwazia kwamba Muumba wa wanadamu “ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa na . . . mwanadamu.”—Matendo 17:29.

Miungu ya kiume na ya kike, kama vile Athena ambayo utukufu wake ulitegemea mahekalu na sanamu, imetokea na kutoweka. Sanamu ya Athena ilitoweka kutoka Parthenon katika karne ya tano W.K., na ni magofu ya mahekalu yake machache tu ambayo yamebaki. Leo, hakuna mtu anayetafuta hekima na mwongozo wa Athena.

Yehova, yule “Mungu anayedumu milele,” ambaye hakuna mtu amewahi kumwona, ni tofauti sana. (Waroma 16:26; 1 Yohana 4:12) Wana wa Kora waliandika hivi: “Mungu huyu ni Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Yeye mwenyewe atatuongoza.” (Zaburi 48:14) Njia moja ya kupata mwongozo wa Yehova Mungu ni kujifunza Neno lake, Biblia, na kutumia shauri lake katika maisha yetu.