Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kutumaini Ahadi za Nani?

Unaweza Kutumaini Ahadi za Nani?

Unaweza Kutumaini Ahadi za Nani?

“AHADI zake zilikuwa zenye nguvu, jinsi yeye alivyokuwa mwenye nguvu, lakini hakufanya chochote kuzitimiza, kama vile asivyokuwa chochote leo.”—Kitabu Mfalme Henry wa Nane, cha William Shakespeare.

Ahadi hizo zenye nguvu zinazotajwa na Shakespeare ni za kadinali Mwingereza, Thomas Wolsey, aliyekuwa na mamlaka kubwa sana ya kisiasa nchini Uingereza katika karne ya 16. Huenda wengine wakasema kwamba maneno ya Shakespeare pia ni ya kweli kuhusiana na ahadi nyingi wanazozisikia leo. Mara nyingi watu huahidiwa mambo mengi lakini ni mambo machache sana hutimizwa. Kwa hiyo, si vigumu kuelewa ni kwa nini wao hutilia shaka kila ahadi.

Wengi Wamekatishwa Tamaa

Kwa mfano, katika vita vibaya sana vya nchi za Balkani vya miaka ya 1990, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilitangaza mji wa Bosnia wa Srebrenica kuwa “eneo la usalama.” Ahadi hiyo ya wanachama wa Umoja wa Mataifa ilionekana kuwa yenye kuaminika. Maelfu ya wakimbizi Waislamu huko Srebrenica waliamini hivyo. Hata hivyo, mwishowe ahadi ya mahali pa usalama haikutimizwa kabisa. (Zaburi 146:3) Mnamo Julai 1995, majeshi yenye kushambulia yaliyapuuza majeshi ya Umoja wa Mataifa na kuuvamia mji huo. Zaidi ya raia Waislamu 6,000 walitoweka, na wengine 1,200 hivi wakauawa.

Katika kila sehemu ya maisha ahadi huvunjwa. Watu huhisi kwamba wamedanganywa na “matangazo mengi sana ya kibiashara yasiyo ya kweli na yenye kupotosha” leo. Wanakata tamaa kwa sababu ya “kuvunjwa kwa ahadi zinazotolewa na wanasiasa wengi sana wakati wa kampeni.” (The New Encyclopædia Britannica, Buku la 15, ukurasa wa 37) Viongozi wa kidini wenye kutumainika ambao huahidi kuwatunza wafuasi wao huwadhulumu kwa njia yenye kuchukiza sana. Hata baadhi ya wale wanaofanya kazi kama ya ualimu na udaktari, ambao hutarajiwa kuwahurumia na kuwajali wengine, wamewasaliti na hata kuwaua watu ambao wao wanapaswa kuwatunza. Haishangazi kwamba Biblia hutuonya tusiamini kila neno!—Methali 14:15.

Ahadi Ambazo Hutimizwa

Bila shaka, watu wengi hutimiza ahadi zao, wakati mwingine wakilazimika kujidhabihu ili kufanya hivyo. (Zaburi 15:4) Wao huona ahadi zao kuwa jambo zito, nao huzitimiza. Wengine hutaka kwa unyoofu kutimiza ahadi wanazotoa wakiwa na nia nzuri. Wako tayari na wanatamani kutimiza ahadi zao lakini hawawezi kufanya hivyo. Hali zinaweza kuvuruga hata mipango mizuri kabisa.—Mhubiri 9:11.

Hata sababu iwe nini, watu wengi huona ni vigumu sana kuamini ahadi ya mtu yeyote. Hivyo, swali hili linatokea: Je, kuna ahadi zozote tunazoweza kuamini? Ndiyo. Tunaweza kuamini ahadi za Neno la Mungu, Biblia. Tunakualika uchunguze yale ambayo makala inayofuata inasema kuhusu habari hiyo. Huenda ukakata kauli kwamba kwa kweli tunaweza kuamini ahadi za Mungu, kama vile tayari mamilioni ya watu wamejionea.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

AP Photo/Amel Emric