Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mkuu Katika Upendo Mshikamanifu

Yehova Ni Mkuu Katika Upendo Mshikamanifu

Yehova Ni Mkuu Katika Upendo Mshikamanifu

“Yehova ni . . . mkuu katika fadhili zenye upendo.”—ZABURI 145:8.

1. Upendo wa Mungu ni mwingi kadiri gani?

“MUNGU ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Maneno hayo yenye kuchangamsha huthibitisha kwamba njia ya Yehova ya kutawala hutegemea upendo. Hata wanadamu ambao hawamtii hunufaika na jua na mvua anayonyesha kwa upendo! (Mathayo 5:44, 45) Kwa sababu Mungu anawapenda wanadamu, hata adui zake wanaweza kutubu, kumgeukia, na kupata uzima. (Yohana 3:16) Hata hivyo, hivi karibuni Yehova atawaharibu waovu wasiotaka kubadilika ili wanadamu wanaompenda wafurahie uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu.—Zaburi 37:9-11, 29; 2 Petro 3:13.

2. Ni aina gani ya upendo wa pekee ambao Yehova huwaonyesha wale waliojiweka wakfu kwake?

2 Yehova huwaonyesha upendo waabudu wake wa kweli kwa njia nzuri na yenye kudumu. Upendo huo unadokezwa na neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili zenye upendo” au “upendo mshikamanifu.” Mfalme Daudi wa Israeli la kale alithamini sana fadhili zenye upendo za Mungu. Kwa sababu ya mambo yaliyompata na kutafakari jinsi Mungu alivyoshughulika na wengine, Daudi angeweza kuimba hivi kwa uhakika: “Yehova ni . . . mkuu katika fadhili zenye upendo [au, “upendo mshikamanifu”].”—Zaburi 145:8.

Kuwatambua Washikamanifu wa Mungu

3, 4. (a) Zaburi ya 145 hutusaidiaje kuwatambua washikamanifu wa Yehova? (b) Washikamanifu wa Mungu ‘humbarikije’?

3 Hana, mama ya nabii Samweli alisema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Yeye hulinda miguu ya washikamanifu wake.” (1 Samweli 2:9) “Washikamanifu” hao ni nani? Mfalme Daudi anajibu swali hilo. Baada ya kutukuza sifa nzuri za Yehova Daudi anasema: “Washikamanifu wako watakusifu [“watakubariki,” Zaire Swahili Bible].” (Zaburi 145:10) Huenda ukajiuliza jinsi wanadamu wanavyoweza kumbariki Mungu. Wanafanya hivyo hasa kwa kumsifu.

4 Washikamanifu wa Yehova wanaweza kutambuliwa kuwa wale wanaotumia vinywa vyao kumsifu. Wao huzungumzia nini hasa wanapokuwa katika vikusanyiko vya kirafiki na kwenye mikutano ya Kikristo? Bila shaka, wao huzungumzia Ufalme wa Yehova! Watumishi wa Mungu wana hisia kama za Daudi aliyeimba: “Wataongea juu ya utukufu wa ufalme [wa Yehova], nao watasema juu ya nguvu zako.”—Zaburi 145:11.

5. Tunajuaje kwamba Yehova husikiliza washikamanifu wake wanapomsifu?

5 Je, Yehova husikiliza waaminifu wake wanapomsifu? Ndiyo, yeye husikiliza wanayosema. Katika unabii unaohusu ibada ya kweli leo, Malaki aliandika hivi: “Wakati huo wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.” (Malaki 3:16) Yehova hufurahi sana washikamanifu wake wanapomsifu, naye huwakumbuka.

6. Ni utendaji gani unaotusaidia kuwatambua washikamanifu wa Mungu?

6 Watumishi washikamanifu wa Yehova wanaweza kutambuliwa pia kwa sababu wanatumia kwa ujasiri na kwa ukamili nafasi wanazopata kuzungumza na watu ambao si waabudu wa Mungu wa kweli. Kwa kweli, washikamanifu wa Mungu ‘huwajulisha wana wa binadamu matendo yake yenye nguvu na utukufu wa fahari ya ufalme wake.’ (Zaburi 145:12) Je, wewe hutafuta na kutumia vizuri nafasi unazopata kuzungumza kuhusu ufalme wa Yehova pamoja na wasioamini? Tofauti na serikali za kibinadamu ambazo karibuni zitapitilia mbali, ufalme wake ni wa milele. (1 Timotheo 1:17) Ni jambo la haraka kwamba watu wajifunze kuhusu ufalme wa milele wa Yehova na kuuunga mkono. Daudi aliimba: “Ufalme wako ni ufalme kwa nyakati zote zisizo na kipimo, na mamlaka yako ni ya kuendelea mpaka vizazi vyote vinavyofuata.”—Zaburi 145:13.

7, 8. Ni nini kilichotukia mwaka wa 1914, na kuna uthibitisho gani kwamba sasa Mungu anatawala kupitia Ufalme wa Mwana wake?

7 Tangu 1914, kumekuwa na sababu nyingine ya kuzungumza kuhusu ufalme wa Yehova. Mwaka huo, Mungu alisimamisha Ufalme wa Kimasihi wa mbinguni, na kumtawaza Yesu Kristo, Mwana wa Daudi, kuwa Mfalme. Hivyo, Yehova alitimiza ahadi yake kwamba ufalme wa Daudi ungefanywa kuwa imara hadi wakati usio na kipimo.—2 Samweli 7:12, 13; Luka 1:32, 33.

8 Kuendelea kutimizwa kwa ishara ya kuwapo kwa Yesu Kristo kunathibitisha kwamba Yehova sasa anatawala kupitia Ufalme wa Mwana wake. Jambo kuu zaidi kuhusu ishara hiyo ni ile kazi ambayo Yesu alitabiri kwamba washikamanifu wote wa Mungu wangefanya aliposema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:3-14) Kwa kuwa washikamanifu wa Mungu wanatimiza unabii huo kwa bidii, sasa wanaume, wanawake, na watoto zaidi ya milioni sita wanashiriki katika kazi hii tukufu ambayo haitarudiwa kamwe. Hivi karibuni wapinzani wote wa Ufalme wa Yehova wataharibiwa.—Ufunuo 11:15, 18.

Kunufaika na Enzi Kuu ya Yehova

9, 10. Kuna tofauti gani kati ya Yehova na watawala wa wanadamu?

9 Ikiwa sisi ni Wakristo waliojiweka wakfu, uhusiano wetu na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hutunufaisha sana. (Zaburi 71:5; 116:12) Kwa mfano, kwa kuwa tunamwogopa Mungu na kushika uadilifu, tunapata kibali chake na tunakuwa karibu naye kiroho. (Matendo 10:34, 35; Yakobo 4:8) Tofauti na Yehova, mara nyingi watawala wa wanadamu huonekana wakishirikiana na watu mashuhuri, kama vile viongozi wa kijeshi, wafanyabiashara matajiri, au wanamichezo na watumbuizaji maarufu. Kulingana na gazeti moja la Afrika, Sowetan, ofisa mmoja mashuhuri wa serikali alisema hivi kuhusu maeneo yenye umaskini katika nchi yake: “Ninaelewa ni kwa nini wengi wetu hatutaki kwenda katika maeneo hayo. Hiyo ni kwa sababu tu tunataka kupuuza uhakika wa kwamba kuna hali kama hizo. Hali hizo hutusumbua dhamiri nasi huaibika kwa sababu tunaendesha [magari] ya bei ya juu.”

10 Bila shaka, watawala fulani wa wanadamu hujali kikweli hali ya raia zao. Lakini hata watawala walio wazuri zaidi kati yao hawawajui vizuri raia zao. Kwa kweli, huenda tukauliza: Je, kuna mtawala yeyote ambaye huwajali sana raia zake wote hivi kwamba humsaidia kwa haraka raia yeyote aliye na shida? Naam, yupo. Daudi aliandika: “Yehova anawategemeza wote wanaoanguka, naye anawainua wote ambao wameinama chini.”—Zaburi 145:14.

11. Washikamanifu wa Mungu hupatwa na majaribu gani, nao wana msaada gani?

11 Washikamanifu wa Yehova Mungu hupatwa na majaribu na misiba mingi kwa sababu wao si wakamilifu na wanaishi katika ulimwengu unaokaa katika nguvu za Shetani, “yule mwovu.” (1 Yohana 5:19; Zaburi 34:19) Wakristo hupatwa na mateso. Baadhi yao huteseka kwa sababu ya magonjwa ya kudumu au kwa sababu ya kufiwa. Nyakati nyingine, makosa ya washikamanifu wa Yehova yanaweza kuwafanya ‘wainame chini’ kwa kuvunjika moyo. Lakini, hata wapatwe na majaribu gani, sikuzote Yehova huwa tayari kufariji na kuimarisha kila mmoja wao kiroho. Mfalme Yesu Kristo anapendezwa pia na raia zake washikamanifu.—Zaburi 72:12-14.

Chakula Chenye Kutosheleza kwa Wakati Unaofaa

12, 13. Yehova hutoshelezaje kabisa mahitaji ya “kila kitu kilicho hai”?

12 Yehova huwatoshelezea watumishi wake mahitaji yao yote kwa sababu ya fadhili zake kuu zenye upendo. Hiyo hutia ndani kuwatosheleza kwa chakula kinachofaa. Mfalme Daudi aliandika: “Macho ya wote yanakutazama [wewe Yehova] yakiwa na tumaini, nawe unawapa chakula chao katika majira yake. Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:15, 16) Hata nyakati za misiba, Yehova anaweza kuelekeza mambo ili washikamanifu wake wapate ‘mkate kwa ajili ya siku.’—Luka 11:3; 12:29, 30.

13 Daudi alitaja kwamba “kila kitu kilicho hai” hutoshelezwa. Kila kilicho hai kinatia ndani wanyama. Viumbe wa baharini, ndege, na wanyama wa nchi kavu hawangepata hewa na chakula kama hakungekuwa na mimea baharini na kwenye nchi kavu. (Zaburi 104:14) Hata hivyo, Yehova huhakikisha kwamba mahitaji yao yote yanatoshelezwa.

14, 15. Chakula cha kiroho huandaliwaje leo?

14 Tofauti na wanyama, wanadamu wana uhitaji wa kiroho. (Mathayo 5:3) Yehova hutosheleza kwa njia nzuri kama nini mahitaji ya kiroho ya washikamanifu wake! Kabla ya kifo chake, Yesu aliahidi kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” angewaandalia wafuasi wake ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mathayo 24:45) Mabaki ya wale 144,000 ambao wametiwa mafuta hufanyiza jamii ya mtumwa huyo leo. Kupitia jamii hiyo, Yehova kwa kweli ameandaa chakula cha kiroho kwa wingi.

15 Kwa mfano, leo watu wengi wa Yehova hunufaika na tafsiri ya Biblia iliyo mpya na sahihi katika lugha yao. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imekuwa baraka iliyoje! Isitoshe, mamilioni ya vifaa vinavyotusaidia kujifunza Biblia vinaendelea kutolewa katika lugha zaidi ya 300. Chakula hicho chote cha kiroho kimekuwa baraka kwa waabudu wa kweli duniani pote. Ni nani anayestahili sifa kwa hayo yote? Ni Yehova Mungu. Kupitia fadhili zake kuu zenye upendo, ameiwezesha jamii ya mtumwa kuandaa ‘chakula katika majira yake.’ Kupitia maandalizi hayo, “tamaa ya kila kitu kilicho hai” katika paradiso ya kiroho ya sasa hutoshelezwa. Watumishi wa Yehova hufurahia sana tumaini la kuona dunia ikigeuzwa kuwa paradiso hivi karibuni.—Luka 23:42, 43.

16, 17. (a) Kuna mifano gani kuhusu chakula cha kiroho kilichofika katika majira yanayofaa? (b) Zaburi ya 145 huelezaje hisia za washikamanifu wa Mungu kuhusu suala kuu lililozushwa na Shetani?

16 Fikiria mfano wa kipekee kuhusu chakula cha kiroho kilichopokewa katika majira yanayofaa. Mnamo 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza huko Ulaya. Mwaka huohuo, toleo la Novemba 1 la Mnara wa Mlinzi lilikuwa na makala yenye kichwa “Msimamo wa Kutokuwamo.” Kwa kuwa makala hiyo ilieleza mambo waziwazi, Mashahidi wa Yehova duniani pote waliona uhitaji wa kudumisha msimamo thabiti wa kutokuwamo katika vita vya mataifa. Msimamo huo ulifanya wakasirikiwe sana na serikali zilizopigana vita hivyo vilivyodumu kwa miaka sita. Hata hivyo, ingawa walipigwa marufuku na kuteswa, washikamanifu hao wa Mungu waliendelea kuhubiri habari njema za Ufalme. Kuanzia 1939 hadi 1946, walipata ongezeko la kustaajabisha la asilimia 157. Isitoshe, kudumisha kwao utimilifu kwa njia yenye kutokeza wakati wa vita hivyo kunaendelea kuwasaidia watu watambue dini ya kweli.—Isaya 2:2-4.

17 Chakula cha kiroho ambacho Yehova huandaa ni cha wakati unaofaa na pia hutosheleza sana. Mataifa yalipokuwa yamezama kabisa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu wa Yehova walisaidiwa kukazia fikira jambo fulani muhimu zaidi kuliko wokovu wao. Yehova aliwasaidia waelewe kwamba suala kuu, ambalo linahusu ulimwengu wote, linahusiana na haki yake ya kuwa mtawala. Inaridhisha kama nini kujua kwamba kupitia ushikamanifu wao Mashahidi wote wa Yehova walishiriki kwa sehemu ndogo kutetea enzi kuu ya Yehova na kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo! (Methali 27:11) Tofauti na Shetani ambaye humchongea Yehova na njia yake ya kutawala, washikamanifu wa Yehova huendelea kutangaza hivi hadharani: “Yehova ni mwadilifu katika njia zake zote.”—Zaburi 145:17.

18. Kuna mfano gani wa hivi karibuni kuhusu chakula cha kiroho cha wakati unaofaa, na chenye kutosheleza sana?

18 Mfano mwingine kuhusu chakula cha kiroho cha wakati unaofaa na cha kutosheleza ni kitabu Mkaribie Yehova, kilichotolewa kwenye mamia ya Makusanyiko ya Wilaya ya “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” yaliyofanywa duniani pote mwaka wa 2002/2003. Kitabu hiki kilichotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova hukazia sifa nzuri za Yehova Mungu, kutia ndani zile zinazotajwa katika Zaburi ya 145. Bila shaka, kitabu hiki kizuri kitawasaidia sana washikamanifu wa Mungu wamkaribie zaidi.

Wakati wa Kumkaribia Yehova Zaidi

19. Ni kipindi gani muhimu kinachokaribia, na tunawezaje kukabiliana nacho?

19 Kipindi muhimu ambapo suala la enzi kuu ya Yehova litatatuliwa kinakaribia. Kama ilivyotabiriwa katika Ezekieli sura ya 38, hivi karibuni Shetani atakamilisha wajibu wake akiwa “Gogu wa nchi ya Magogu.” Hilo litatia ndani shambulio dhidi ya watu wa Yehova duniani pote. Litakuwa jaribio la Shetani la kufa na kupona la kuvunja utimilifu wa washikamanifu wa Mungu. Wakati huo hasa, waabudu wa Yehova watahitaji kusali kwake kwa bidii, hata kumlilia awasaidie. Je, upendo wao kwa Mungu na woga wao wenye heshima utakuwa wa bure? La, kwa kuwa Zaburi ya 145 inasema: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli. Atawatimizia wale wanaomwogopa tamaa yao, naye atakisikia kilio chao cha kuomba msaada, naye atawaokoa. Yehova anawalinda wale wote wanaompenda, lakini atawaangamiza waovu wote.”—Zaburi 145:18-20.

20. Maneno ya Zaburi 145:18-20 yatathibitikaje kuwa ya kweli hivi karibuni?

20 Litakuwa jambo lenye kufurahisha kama nini kuona jinsi Yehova alivyo karibu nasi na kuona nguvu zake za kuokoa atakapoangamiza waovu wote! Wakati huo muhimu ambao unakaribia sana, Yehova atawasikiliza tu wale “wanaomwitia yeye katika ukweli.” Bila shaka, hatawasikiliza wanafiki. Neno la Mungu huonyesha waziwazi kwamba sikuzote imekuwa kazi bure kwa waovu kuliitia jina lake dakika za mwisho-mwisho.—Methali 1:28, 29; Mika 3:4; Luka 13:24, 25.

21. Washikamanifu wa Yehova huonyeshaje kwamba wao hufurahi kulitumia jina la Mungu?

21 Huu hasa ndio wakati kwa wale wanaomwogopa Yehova ‘kumwitia yeye katika ukweli.’ Washikamanifu wake hufurahia kulitumia jina lake katika sala na katika maelezo yao kwenye mikutano. Wao hulitumia jina la Mungu katika mazungumzo yao ya kibinafsi. Nao hutangaza jina la Yehova kwa ujasiri katika huduma yao ya hadharani.—Waroma 10:10, 13-15.

22. Kwa nini ni muhimu kuendelea kukataa mitazamo na tamaa za ulimwengu?

22 Ili tuendelee kunufaika na uhusiano wetu wa karibu na Yehova Mungu, ni muhimu pia tuendelee kukataa mambo yanayodhuru kiroho kama ufuatiaji wa vitu vya kimwili, vitumbuizo visivyofaa, roho ya kutosamehe, au kutowajali wenye uhitaji. (1 Yohana 2:15-17; 3:15-17) Tusipoacha tabia hizo na pia kuacha kufuatia mambo hayo, tunaweza kuzoea dhambi nzito na mwishowe tupoteze kibali cha Yehova. (1 Yohana 2:1, 2; 3:6) Ni jambo la hekima kukumbuka kwamba Yehova ataendelea kutuonyesha fadhili zenye upendo, au upendo mshikamanifu, tukiendelea kuwa waaminifu kwake.—2 Samweli 22:26.

23. Washikamanifu wote wa Mungu wanatazamia wakati gani ujao mtukufu?

23 Kwa hiyo, acheni tukazie fikira wakati ujao mtukufu ambao washikamanifu wote wa Yehova wanautazamia. Kwa kufanya hivyo, tunakuwa na tazamio zuri la kuwa kati ya wale watakaomtukuza, kumbariki, na kumsifu Yehova “mchana kutwa . . . naam milele.” (Zaburi 145:1, 2) Kwa hiyo, na ‘tujitunze katika upendo wa Mungu, huku tukitazamia uzima wa milele.’ (Yuda 20, 21) Tunapoendelea kunufaika na sifa nzuri za Baba yetu wa mbinguni, zinazotia ndani fadhili zake kuu zenye upendo anazowaonyesha wampendao, sikuzote na tuonyeshe hisia ambazo Daudi alionyesha katika Zaburi ya 145: “Kinywa changu kitasema sifa za Yehova; na wote wenye mwili na walibariki jina lake takatifu mpaka wakati usio na kipimo, hata milele.”

Ungejibuje?

Zaburi ya 145 hutusaidiaje kuwatambua washikamanifu wa Mungu?

• Yehova ‘hutoshelezaje tamaa ya kila kitu kilicho hai’?

• Kwa nini tunahitaji kumkaribia Yehova zaidi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Washikamanifu wa Mungu hufurahi kuzungumzia matendo yake makuu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watumishi wa Yehova huwasaidia kwa ujasiri wale wasioamini wajifunze utukufu wa ufalme wake

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yehova huandaa chakula kwa “kila kitu kilicho hai”

[Hisani]

Animals: Parque de la Naturaleza de Cabárceno

[Picha katika ukurasa wa 19]

Yehova huwatia nguvu na kuwaongoza washikamanifu wanaotafuta msaada wake kupitia sala